Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Udugu Wenye Umoja Usioweza Kuvunjwa

Udugu Wenye Umoja Usioweza Kuvunjwa

Udugu Wenye Umoja Usioweza Kuvunjwa

Na Mwandishi Wa Amkeni! Nchini El Salvador

MNAMO JANUARI 13, 2001, SAA 5:34 ASUBUHI, TETEMEKO LA ARDHI LENYE KIPIMO CHA RICHTER CHA 7.6 LILITINGISHA NCHI YA EL SALVADOR NA LILIENEA HADI PANAMA NA MEXICO. HAKUNA ATAKAYESAHAU ALICHOKUWA AKIFANYA TETEMEKO HILO LILIPOTOKEA.

“WAKATI tetemeko hilo lenye kishindo lilipotulia, tulitazama mlimani, kilele chake kilikuwa kimegawanyika na ni kana kwamba kiliganda kwa sekunde chache,” akumbuka Miriam Quezada. “Binti yangu alilia kwa sauti, ‘Mama! Kimbia! Kimbia!’” Kisha sehemu ya juu ya mlima ikaanguka kuwaelekea. Karibu watu 500 walipoteza maisha yao katika jumuiya ya Las Colinas ya Nueva San Salvador, au Santa Tecla, na nyumba zipatazo 300 ziliharibiwa kabisa.

“Nilikuwa nimetoka tu nyumbani na nilikuwa kwenye kituo cha basi wakati tetemeko lilipotokea,” asimulia Roxana Sánchez. “Tetemeko lilipokoma, nilimsaidia mwanamke mmoja kubeba mifuko yake na nikaamua kurudi nyumbani kwa sababu familia yangu wangekuwa na wasiwasi kunihusu.’” Roxana alipopiga kona, aliona kwamba barabara yao iliishia ghafula chini ya rundo la mchanga. Nyumba yao ilikuwa imetoweka!

Kuandaa Msaada wa Haraka

Kuna Mashahidi wa Yehova 28,000 nchini El Salvador na wengi wao wanaishi katika sehemu iliyokumbwa na msiba—sehemu iliyo karibu na pwani ya Salvador. Ingawa wengi bado waliteseka kutokana na mfadhaiko, upesi walianza kufikiria mahitaji ya wengine. Mario Suarez, mwangalizi asafiriye wa Mashahidi wa Yehova anayetumikia huko Santa Tecla, asimulia: “Saa moja hivi baada ya tetemeko la ardhi kutukia, niliitwa ili kusaidia. Ilisemekana kwamba baadhi ya akina ndugu na dada Wakristo walikuwa wamenaswa ndani ya nyumba zao. Mara moja kikundi cha wajitoleaji kilifanyizwa.

“Tulifikiri kwamba huenda kuta fulani zilikuwa zimeanguka na kwamba ilihitaji tu kuondoa vifusi na kufanyiza njia ili walionaswa waweze kutoka nje. Kumbe hatukujua kwamba ulikuwa msiba mkubwa sana. Tulipofika mahali hapo tuliuliza nyumba zilipokuwa. Tulishtuka tulipoambiwa kwamba zilikuwa zimefukiwa mahali tuliposimama! Nyumba zilifukiwa kabisa kufikia orofa ya pili kwa meta tatu ya udongo. Lilikuwa jambo lenye kufadhaisha!”

Kufikia mchana, Mashahidi wapatao 250 kutoka kwa makutaniko jirani walimiminika katika eneo hili ili kusaidia. Wajitoleaji walijaribu sana kuwaokoa manusura kwa kutumia sururu, sepetu, sinia za plastiki na mikono bila vifaa. Hata hivyo ni wachache tu waliookolewa huko Santa Tecla. Mashahidi wa Yehova watano walikuwa miongoni mwa mamia ya watu waliokufa kwa kukosa hewa au kwa kufukiwa.

Kutoa Msaada kwa Utaratibu

Makutaniko yote ya Mashahidi nchini yalishiriki katika kazi hii ya kutoa msaada. Mashahidi wengi katika Comasagua, Ozatlán, Santa Elena, Santiago de María, na Usulután, walipoteza makao yao. Majumba ya Ufalme na nyumba za faragha zilifanywa kuwa vituo vya misaada. “Ulikuwa msaada mkubwa sana,” asema mwangalizi asafiriye Edwin Hernández. “Akina ndugu walifika wakiwa na chakula, mavazi, magodoro, dawa na hata pesa za kugharimia mazishi.”

Halmashauri ya kuandaa msaada, iliyoteuliwa na ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova ya El Salvador, ilipanga makutaniko ambayo hayakuathiriwa sana yashughulikie mahitaji ya makutaniko yaliyoathiriwa zaidi. Vikundi vya wafanyakazi vilifanyizwa vikiwa na Mashahidi kati ya 10 hadi 20 walioshughulikia marekebisho yaliyohitajiwa.

Kwa kuongezea, Halmashauri ya Ujenzi ya Mkoa ya Mashahidi wa Yehova, ambayo hupanga ujenzi wa Majumba ya Ufalme, ilipanga vikundi vya akina ndugu kuwajengea makao ya muda wale ambao nyumba zao ziliharibiwa kabisa. Kwa kuwa bei ya mabati ilipanda sana nchini El Salvador, ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova ya Guatemala ilichanga mabati mengi sana. Ofisi za tawi za Marekani na Honduras zilichanga mbao zilizotumiwa kwa ujenzi wa vibanda.

Pamoja na hekaheka hizo zote, matetemeko ya ardhi yaliendelea. Watu wote walilala barabarani wakiwa wamejifunika maturubai na mashiti yaliyochakaa. Kukawa na makelele na ugomvi mwingi. Kufikia Februari 12, jumla ya matetemeko madogo 3,486 yalikuwa yamerekodiwa.

Tetemeko la Pili Kubwa

Katika Februari 13, 2001, saa 2:22 asubuhi, mwezi mmoja baada ya lile tetemeko la ardhi la kwanza, tetemeko la ardhi lilitikisa kitovu cha El Salvador kwa mara ya pili, likiwa na ukubwa wa kipimo cha Richter cha 6.6. Kwa mara nyingine tena, Mashahidi wa Yehova wakajitolea upesi kuandaa misaada na uokoaji. Mzee mmoja wa kutaniko aitwaye Noé Iraheta alieleza hivi: “Kila kiongozi wa Funzo la Kitabu la Kutaniko alienda kutafuta Mashahidi wa kikundi chake kuhakikisha kwamba wote walikuwa salama.”

Majiji ya San Vicente na Cojutepeque na vitongoji vyake yaliathiriwa zaidi. Miji ya San Pedro Nonualco, San Miguel Tepezontes, na San Juan Tepezontes yalikuwa magofu. Katika Candelaria, Cuscatlán ambapo uharibifu ulienea karibu kila mahali, shule moja ya parokia iliporomoka na watoto 20 wakafa. Salvador Trejo, Shahidi anayeishi huko aeleza: “Saa moja hivi baadaye, nilisikia mtu akiniita, ‘Ndugu Trejo!’ Mwanzoni, sikuweza kuona kwa sababu ya vumbi. Halafu, ghafula, Mashahidi kutoka Cojutepeque wakatokea. Walikuja kutuona!”

Makutaniko jirani yalipanga tena kuandaa mahitaji ya lazima kwa wahasiriwa wa huu msiba wa pili. Walifuata mfano wa Wakristo wa Makedonia katika karne ya kwanza waliofurahia pendeleo la kutoa, ingawaje wao pia walikuwa na uhitaji. Kwa mfano, wale wa makutaniko ya jiji la Santiago Texacuangos, waliopoteza vitu vingi wakati wa tetemeko la ardhi la kwanza, walipika vyakula na kuwapelekea ndugu zao katika mji wa karibu wa San Miguel Tepezontes.

Kwa jumla, inakadiriwa kwamba zaidi ya watu 1,200 walikufa kutokana na tetemeko la ardhi huko El Salvador, na wengine wanane wakaripotiwa kufa katika nchi jirani ya Guatemala.

Juhudi Zao Zilithaminiwa

Juhudi za pamoja za Mashahidi kusaidia wahasiriwa zilithaminiwa na vikundi vingine vya kutoa misaada. Gari la Kamati ya Kitaifa ya Mambo ya Dharura lilipeleka maandalizi ya dharura kwenye Jumba la Ufalme lililotumiwa kama makao ya wahasiriwa. Mwakilishi mmoja mwanamke alisema kwa mshangao: “Kati ya makao yote ya wahasiriwa tuliyotembelea, haya tu ndiyo ya kwanza yenye utaratibu. Nawapongeza!” Watu hawakusongamana wala kusukumana, wakati gari lilipofika kama ilivyokuwa katika vituo vingine. Watu wenye umri mkubwa zaidi walishughulikiwa kwanza.

Katika juhudi zao za kuandaa misaada, Mashahidi waliwasaidia wengine mbali na waamini wenzao. Kwa mfano, katika San Vicente, majirani wengi wasio Mashahidi walikimbilia kwenye maeneo ya Jumba la Ufalme. Regina Durán de Cañas alisema hivi: “Watu walio hapa katika Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova ni wakarimu sana. Walifungua milango yao na kusema, ‘Karibuni!’ Hata wana zamu ya kutulinda wakati wa usiku tunapolala.”

Mipango ya Ujenzi wa Nyumba

Baada ya kuchanganua uharibifu huo, mapendekezo yalifanywa kwa ofisi ya tawi ili kujenga nyumba zilizohitajiwa. Nyumba za muda zilijengwa kwa wale waliopoteza makao yao. Marekebisho yalifanywa pia kwa nyumba ambazo hazikuharibika sana. Wengi walivutiwa na bidii na ustadi wa wafanyakazi wa ujenzi kwani hata majirani walikuja kuwatazama wakifanya kazi.

Mwanamke mmoja akifikiri kwamba wafanyakazi hao walikuwa wale waliotarajiwa kutoka mjini ili kuwasaidia, alilalamika kwamba hakuna aliyemsaidia katika kazi yake ya kufagia vifusi. “La, mama, hawa hawatoki mjini. Ni watu wa Ufalme!” wakaeleza watoto majirani. Moisés Antonio Díaz ambaye si Shahidi pia alisema: “Ni jambo zuri kuona jinsi Mashahidi wa Yehova wanavyowasaidia walio na uhitaji. Tengenezo hili lina umoja sana, na tunamshukuru Mungu kwamba wana nia ya kutusaidia sisi tulio maskini. Nimefanya kazi pamoja nao na ninanuia kuendelea kufanya hivyo.”

Dada mmoja Mkristo aliyejengewa nyumba alisema hivi kwa machozi: “Mimi na mume wangu tumekosa maneno yafaayo ya kueleza shukrani zetu—kwanza kwa Yehova kisha kwa hawa akina ndugu ambao ijapokuwa hawakutujua walifika bila kukawia ili kutusaidia.”

Kufikia katikati ya mwezi wa Aprili, Mashahidi walikuwa wamewajengea wahasiriwa wa tetemeko la ardhi nyumba 567 na kuandalia karibu familia 100 vifaa vya kurekebisha nyumba zao zilizokuwa zimeharibiwa. Mara tu familia zenye uhitaji zilipopata makao salama, Mashahidi walielekeza uangalifu kwa yale Majumba ya Ufalme 92 yaliyohitaji kurekebishwa au kujengwa upya.

Maisha Mapya

Mbali na ujenzi wa majengo na makao, wengi hasa walishukuru kwa kuimarishwa kiroho na kihisia-moyo.

“Chini ya hali hizo, na kwa sababu matetemeko yaliendelea, wakati mwingine nilihofu sana, lakini akina ndugu walikuwa chanzo cha kitia-moyo,” akasema Miriam aliyetajwa awali. “Tungekuwa wapi bila ndugu hawa?”

Utunzaji wa upendo ambao Yehova ameandaa kupitia kwa mpango wa kutaniko umewachochea wahasiriwa wa tetemeko la ardhi kwa njia zenye kustaajabisha sana. Tetemeko la kwanza lilibomoa au kuharibu karibu nyumba zote za Mashahidi katika mji wa Comasagua. Hata hivyo, Mashahidi 12 kati ya 17 wanaoishi huko, walijiandikisha kushiriki katika huduma ya wakati wote miezi ya Aprili na Mei, na tangu wakati huo 2 kati yao ni wahudumu wa kawaida wa wakati wote.

Makutaniko yaliyo katika jimbo la Cuscatlán, mmojawapo ya maeneo yaliyoathiriwa sana na tetemeko la pili, walifanya siku ya kusanyiko la pekee katika mwezi wa Machi. Kulikuwa na kilele cha wahudhuriaji 1,535, na watu 22 wakabatizwa. Wasimamizi wa kusanyiko walistaajabu kuona kwamba ijapokuwa wengi wa wahudhuriaji walikuwa wamepoteza makao yao, walichanga kiasi kikubwa cha pesa kwa ajili ya Jumba la Kusanyiko.

Akielezea shukrani za kutoka moyoni za wengi, Shahidi mmoja kutoka San Vicente alisema: “Niliwahi kusoma jinsi tengenezo linavyotenda msiba unapotokea, lakini sasa nimejionea mwenyewe na kuhisi utegemezo wa akina ndugu. Tumeona upendo wa Kikristo kwa njia iliyo halisi. Ni pendeleo lililoje kuwa miongoni mwa watu hawa wenye umoja!”

[Picha katika ukurasa wa 23]

Poromoko la ardhi lililosababishwa na tetemeko lililofukia zaidi ya nyumba 300 huko Las Colinas

[Hisani]

Sehemu ya chini ya ukurasa wa 23-25: Courtesy El Diario de Hoy

[Picha katika ukurasa wa 24]

Wanakijiji walitumia sururu, sepetu na ndoo katika kazi yao ya uokoaji

[Hisani]

Courtesy of La Prensa Gráfica (photograph by Milton Flores/Alberto Morales/Félix Amaya)

[Picha katika ukurasa wa 25]

Magofu ya Jumba la Ufalme katika mji wa Tepecoyo

[Picha katika ukurasa wa 26]

Ndugu katika mji wa Tepecoyo walijenga kibanda kwa ajili ya mikutano yao bila kukawia

[Picha katika ukurasa wa 26]

Mashahidi walijenga upya Majumba ya Ufalme bila kukawia na kujenga zaidi ya nyumba 500

[Picha katika ukurasa wa 26]

Mama mmoja mwenye shukrani asiye na mume atazama na bintiye nyumba yao iliyoharibiwa ikijengwa upya