Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unaweza kupata Msaada

Unaweza kupata Msaada

Unaweza kupata Msaada

‘MNA tembe 49 za usingizi ndani ya kikombe. Je, nizimeze au nisizimeze?’ Hivyo ndivyo mwanamume mmoja mwenye umri wa miaka 28 nchini Uswisi alivyojiuliza. Mkewe na watoto walikuwa wamemwacha, na alikuwa ameshuka moyo sana. Hata hivyo, baada ya kumeza tembe hizo, alijiambia hivi: ‘La. Sitaki kufa!’ Jambo zuri ni kwamba hakufa. Nyakati nyingine watu wanaotaka kujiua hawafaulu.

Alex Crosby wa Vituo vya Marekani vya Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa alisema hivi kuhusu matineja waliojaribu kujiua: ‘Ukiwazuia hata kwa saa chache tu wasijiue, unaweza kukomesha nia hiyo. Unaweza kuwazuia wengi wasijiue kwa kuingilia kati. Unaweza kuokoa uhai wao.’

Profesa Hisashi Kurosawa alipokuwa akifanya kazi kwenye Kituo cha Dharura cha Kuokoa Uhai kwenye Chuo cha Mafunzo ya Tiba cha Japani, aliwasaidia mamia ya watu waliotaka kujiua watamani tena kuishi. Naam, nia hiyo ikizuiwa kwa njia fulani, uhai unaweza kuokolewa. Ni msaada gani unaohitajiwa?

Kushughulikia Matatizo Yasiyoonekana Wazi

Kama ilivyoonyeshwa katika makala iliyotangulia, watafiti wanasema kwamba asilimia 90 ya watu waliojiua walikuwa na magonjwa ya akili au walitumia vileo kupita kiasi au dawa za kulevya. Hivyo, Eve K. Mościcki wa Taasisi ya Kitaifa ya Marekani ya Masuala ya Akili, asema hivi: “Njia kuu ya kuzuia watu wa kila umri wasijiue ni kuzuia magonjwa ya akili na uraibu.”

Inahuzunisha kwamba wengi wanaougua magonjwa hayo hawataki kutafuta msaada. Kwa nini? ‘Ni kwa sababu watu wengi wana maoni mabaya,’ asema Yoshitomo Takahashi wa Taasisi ya Magonjwa ya Akili ya Mji wa Tokyo. Anaongezea kwamba kutokana na hilo, hata watu wanaohisi wanaugua kidogo husita kutafuta matibabu mara moja.

Hata hivyo, watu fulani hawaaibiki kutafuta msaada. Hiroshi Ogawa, mtangazaji maarufu wa televisheni ambaye ameendesha kipindi chake mwenyewe kwa miaka 17 nchini Japani, alikubali hadharani kwamba ameshuka moyo na kwamba alikuwa karibu kujiua. Ogawa alisema hivi: “Kushuka moyo ni kama mafua yanayoathiri akili.” Alieleza kwamba mtu yeyote anaweza kuambukizwa lakini anaweza kupona.

Zungumza na Mtu Fulani

Béla Buda, afisa wa afya wa Hungaria aliyenukuliwa hapo awali, asema hivi: “Mtu asipolitaja tatizo lake, kwa kawaida yeye huliona kuwa kubwa sana na lisiloweza kutatuliwa.” Maoni yake yanakazia hekima ya mithali ya kale ya Biblia: “Ajitengaye na wenzake hutafuta matakwa yake mwenyewe; hushindana na kila shauri jema.”—Mithali 18:1.

Zingatia maneno hayo ya hekima. Usiumie peke yako unapokumbwa na matatizo mengi ya kibinafsi yenye kulemea. Tafuta mtu anayeaminika unayeweza kumfunulia matatizo hayo. Huenda ukasema, ‘Lakini sina mtu yeyote ninayeweza kumfunulia matatizo.’ Dakt. Naoki Sato, mtaalamu wa magonjwa ya akili, alisema kwamba watu wengi huhisi hivyo. Sato alisema kwamba huenda wagonjwa wengi huepuka kuwaeleza wengine matatizo yao kwa kuwa hawataki kufunua udhaifu wao.

Mtu atapata wapi atakayemsikiliza? Katika sehemu nyingi anaweza kutafuta msaada kutoka kwa kituo kinachozuia watu kujiua au kuwapigia simu watu wanaoandaa msaada kwa matatizo ya kibinafsi au kumwona daktari anayeaminika ambaye hushughulikia matatizo ya kihisia. Lakini wataalamu fulani pia hung’amua kwamba kuna chanzo kingine cha msaada—dini. Dini yaweza kusaidiaje?

Kupata Msaada Unaohitajiwa

Mtu mmoja mlemavu huko Bulgaria anayeitwa Marin, alitaka sana kujiua. Siku moja aliliona gazeti la kidini la Mnara wa Mlinzi, linalochapishwa na Mashahidi wa Yehova. Alikubali mwaliko wa kutembelewa na Mashahidi wa Yehova uliotolewa katika gazeti hilo. Marin anaeleza matokeo: “Walinifundisha kwamba uhai ni zawadi kutoka kwa Baba yetu wa kimbingu na hatuna haki ya kujidhuru wala kujiua kimakusudi. Basi niliacha kutamani kujiua na nikapenda tena kuishi!” Marin pia alisaidiwa kwa upendo na kutaniko la Kikristo. Ijapokuwa bado yeye ni mlemavu, asema hivi: “Sasa siku zangu ni zenye shangwe na utulivu, na kuna mambo mengi ya kufanya yanayopendeza—mengi zaidi hata sina wakati wa kutosha! Yote hayo yamewezekana kwa sababu ya Yehova na Mashahidi wake.”

Yule mwanamume kijana Mswisi aliyetajwa hapo mwanzoni alisaidiwa pia na Mashahidi wa Yehova. Sasa anasimulia kuhusu “fadhili ya familia moja ya Kikristo” ambayo ilikubali kuishi naye. Aongezea hivi: “Baadaye, washiriki wa kutaniko [la Mashahidi wa Yehova] walinialika kwenye milo kwa siku nyingi. Kilichonisaidia hasa si tu kutendewa kwa ukarimu bali pia kuweza kuzungumza na mtu fulani.”

Mwanamume huyo alitiwa moyo sana na yale aliyojifunza katika Biblia, hasa alipojifunza kuhusu upendo ambao Mungu wa kweli, Yehova, anao kwa wanadamu. (Yohana 3:16) Kwa kweli, Yehova Mungu anakusikiliza ‘unapofunua moyo wako’ mbele zake. (Zaburi 62:8) ‘Macho yake hukimbia-kimbia duniani mwote,’ si ili atafute makosa ya wanadamu, bali “ili ajionyeshe mwenye nguvu kwa ajili ya hao, waliokamilika moyo kuelekea kwake.” (2 Mambo ya Nyakati 16:9) Yehova atuhakikishia hivi: “Usiogope, kwa maana mimi ni pamoja nawe; usifadhaike, kwa maana mimi ni Mungu wako; nitakutia nguvu, naam, nitakusaidia, naam, nitakushika kwa mkono wa kuume wa haki yangu.”—Isaya 41:10.

Mwanamume huyo Mswisi alisema hivi kuhusu ahadi ya Mungu ya ulimwengu mpya: “Imepunguza sana fadhaa yangu.” Tumaini hilo, linalofafanuliwa kuwa “nanga ya nafsi,” latia ndani ahadi ya uhai udumuo milele katika Paradiso duniani.—Waebrania 6:19; Zaburi 37:10, 11, 29.

Maisha Yako Ni Yenye Thamani kwa Wengine

Ni kweli kuwa unaweza kukabili hali zinazokufanya uhisi kwamba u peke yako kabisa na kwamba ukifa hakuna atakayejali. Lakini kumbuka: Kuna tofauti kubwa kati ya kuhisi u peke yako na kuwa peke yako. Katika nyakati za Biblia, nabii Eliya alifadhaika maishani mwake. Alimwambia Yehova hivi: ‘Wamewaua manabii wako kwa upanga; nami nimesalia, mimi peke yangu.’ Naam, Eliya alihisi kwamba alikuwa peke yake kabisa—na alihisi hivyo kwa sababu fulani. Manabii wenzake wengi walikuwa wameuawa. Alikuwa ametishwa kuuawa, na alikuwa anakimbia ili kujiokoa. Lakini je, kweli alikuwa peke yake? La. Yehova alimjulisha kwamba kulikuwa na watu 7,000 waaminifu ambao, kama yeye, walikuwa wanajitahidi kumtumikia Mungu wa kweli kwa uaminifu katika nyakati hizo za kuhuzunisha. (1 Wafalme 19:1-18) Lakini, vipi wewe? Je, yawezekana kwamba huko peke yako kama unavyohisi?

Kuna watu wanaokujali. Unaweza kufikiria wazazi wako, mwenzi wako, watoto wako, na rafiki zako. Lakini kuna wengi zaidi. Katika kutaniko la Mashahidi wa Yehova, unaweza kuwapata Wakristo wakomavu wanaopendezwa nawe, watakaokusikiliza kwa subira, na kusali pamoja nawe na kwa ajili yako. (Yakobo 5:14, 15) Na hata kila mtu asiyekamilika akikutupa, kuna Mmoja ambaye hatakuacha. Mfalme Daudi wa kale alisema hivi: “Baba yangu na mama yangu wameniacha, bali BWANA atanikaribisha kwake.” (Zaburi 27:10) Naam, Yehova ‘anakujali.’ (1 Petro 5:7) Katu usisahau kwamba una thamani machoni pa Yehova.

Uhai ni zawadi kutoka kwa Mungu. Ni kweli kwamba nyakati nyingine uhai unaweza kuonekana kuwa mzigo mzito badala ya zawadi. Hata hivyo, je unaweza kuwazia jinsi ungehisi iwapo ungempa mtu zawadi yenye thamani kisha aitupe hata kabla ya kuitumia? Sisi wanadamu wasiokamilika hatujatumia kikamili zawadi ya uhai. Kwa hakika, Biblia huonyesha kwamba machoni pa Mungu uhai tulio nao sasa hivi si “uhai ulio halisi.” (1 Timotheo 6:19) Naam, karibuni uhai wetu utakuwa kamili, wenye maana zaidi, na wenye kufurahisha zaidi. Jinsi gani?

Biblia yasema hivi: “[Mungu] atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.” (Ufunuo 21:3, 4) Hebu wazia jinsi uhai wako utakavyokuwa maneno hayo yatakapotimia. Tulia. Jaribu kupiga picha kamili yenye kuvutia akilini. Picha hiyo si ndoto tu isiyo na maana. Unapotafakari jinsi Yehova alivyoshughulika na watu wake zamani, utamwamini zaidi na utaona picha hiyo kihalisi zaidi.—Zaburi 136:1-26.

Huenda ikachukua muda fulani kabla hujawa tena na tamaa ya kuishi. Endelea kusali kwa “Mungu wa faraja yote, ambaye hutufariji katika dhiki yetu yote.” (2 Wakorintho 1:3, 4; Waroma 12:12; 1 Wathesalonike 5:17) Yehova atakupa nguvu unayohitaji. Atakufundisha kwamba uhai una thamani.—Isaya 40:29.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]

Utamsaidiaje Mtu Anayeonyesha Dalili za Kujiua?

Unapaswa kufanya nini mtu akikuambia kwamba anataka kujiua? Shauri la Vituo vya Marekani vya Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa (CDC) ni hili: “Sikiliza kwa makini.” Acha aeleze jinsi anavyohisi. Hata hivyo, katika visa vingi, mtu anayetaka kujiua hujitenga na kunyamaza. Tambua kwamba maumivu au hali ya kukosa tumaini inayomkumba ni halisi. Ukimtajia kwa upole mabadiliko fulani mahususi ambayo umeona katika tabia yake, huenda utamfanya akufunulie matatizo yake yote.

Onyesha huruma unapomsikiliza. “Ni muhimu kukazia kwamba uhai wake ni wenye thamani kwako na kwa wengine,” lasema shirika la CDC. Mjulishe jinsi kifo chake kitakavyokuumiza na kuwaumiza wengine vilevile. Msaidie mtu huyo atambue kwamba Muumba wake anamjali.—1 Petro 5:7.

Wataalamu pia wanadokeza kwamba vitu vyovyote ambavyo mtu huyo aweza kutumia kujiua viondolewe—hasa bunduki. Hali ikionekana kuwa hatari, huenda ukapenda kumtia moyo mtu huyo amwone daktari. Katika hali mbaya zaidi huenda wewe mwenyewe ukalazimika kuomba huduma ya kitiba ya dharura.

[Sanduku katika ukurasa wa 11]

‘Je, Mungu Atanisamehe kwa Kuhisi Hivi?’

Kushirikiana na Mashahidi wa Yehova kumewasaidia watu wengi kukomesha nia ya kujiua. Hata hivyo, leo hakuna mtu asiyeweza kukumbwa na mikazo au kushuka moyo. Mara nyingi, Wakristo waliofikiria kujiua hujilaumu sana kwa kufikiri hivyo. Kujilaumu huzidisha tu matatizo yao. Basi mtu anaweza kukabilianaje na hisia hizo?

Yafaa kung’amua kwamba wanaume na wanawake fulani waaminifu wa nyakati za Biblia walieleza juu ya hisia zao zisizofaa kuhusu uhai. Wakati mmoja Rebeka, mke wa yule mzee wa ukoo Isaka, alihuzunishwa sana na tatizo la familia kiasi cha kusema hivi: “Sina raha kabisa maishani.” (Mwanzo 27:46, Biblia Habari Njema) Yobu, aliyepoteza watoto wake, afya yake, mali yake, na hadhi yake ya kijamii, alisema hivi: “Nayachukia maisha yangu!” (Ayubu 10:1, BHN) Wakati fulani Musa alimlilia Mungu akisema: “Nakuomba uniulie mbali.” (Hesabu 11:15) Eliya, nabii wa Mungu, alisema hivi wakati fulani: “Imetosha! Siwezi tena. Ee Mwenyezi-Mungu, sasa utoe uhai wangu.” (1 Wafalme 19:4, BHN) Naye nabii Yona alirudia kusema hivi: “Ni afadhali nife mimi kuliko kuishi.”—Yona 4:8.

Je, Yehova aliwashutumu watu hao kwa kuhisi hivyo? La. Hata alihifadhi maneno yao katika Biblia. Hata hivyo, ni muhimu kutambua kwamba hakuna hata mmoja wa waaminifu hao aliyeruhusu hisia zake zimchochee kujiua. Yehova aliwathamini; alitaka waishi. Jambo la hakika ni kwamba, Mungu hujali hata uhai wa watu waovu. Anawasihi wabadilike ‘waendelee kuishi.’ (Ezekieli 33:11, NW) Jinsi angependa wale wanaohangaikia kupata kibali chake waendelee kuishi!

Mungu ameandaa dhabihu ya fidia ya Mwanawe, kutaniko la Kikristo, Biblia, na pendeleo la sala. Njia hiyo ya mawasiliano pamoja na Mungu—sala—yaweza kutumiwa nyakati zote. Mungu anaweza na atawasikiliza wote wanaomfikia wakiwa na moyo mweupe na mnyenyekevu. “Kwa hiyo, acheni tukaribie kwa uhuru wa usemi kwenye kiti cha ufalme cha fadhili isiyostahiliwa, ili tuweze kupokea rehema na kupata fadhili isiyostahiliwa kwa msaada katika wakati ufaao.”—Waebrania 4:16.

[Sanduku katika ukurasa wa 12]

Je, Mpendwa Wako Amejiua?

Mtu anapojiua, washiriki wa familia na rafiki wa karibu huumia sana kiakili. Wengi hujilaumu kwa msiba huo. Wanasema mambo kama vile: ‘Laiti ningalitumia wakati mwingi zaidi naye siku hiyo,’ ‘Laiti ningalizuia ulimi wangu wakati huo,’ ‘Laiti ningalimsaidia zaidi.’ Yaani wanamaanisha, ‘Laiti ningalifanya hivi au vile, mpendwa wangu bado angalikuwapo.’ Hata hivyo, je, yafaa kujilaumu mtu anapojiua?

Kumbuka kwamba ni rahisi sana kujua dalili za mtu anayenuia kujiua baada ya mtu huyo kujiua. Kabla ya hapo si rahisi kuzijua. Biblia husema: “Moyo waujua uchungu wake wenyewe, wala mgeni hawezi kushiriki furaha yake.” (Mithali 14:10, BHN) Nyakati nyingine, haiwezekani kujua mambo ambayo mtu mwingine anafikiri au kuhisi. Watu wengi wanaotaka kujiua hawawezi kuwaeleza wengine hisia zao za ndani vizuri, hata kama ni washiriki wa karibu wa familia.

Kitabu Giving Sorrow Words chasema hivi kuhusu dalili za mtu anayetaka kujiua: “Ukweli ni kwamba kwa kawaida si rahisi kutambua dalili hizo.” Kitabu hichohicho chaongezea kusema kwamba hata ikiwa ulitambua dalili fulani, hiyo haimaanishi kwamba ungemzuia mtu huyo asijiue. Badala ya kujiumiza, unaweza kufarijiwa na maneno haya ya Mfalme Solomoni mwenye hekima: “Walio hai wanajua ya kwamba watakufa; lakini wafu hawajui neno lo lote.” (Mhubiri 9:5) Mpendwa wako hateswi motoni. Na yale mateso ya kiakili au ya kihisia yaliyomfanya ajiue yamekwisha. Hateseki; anapumzika tu.

Kwa sasa, huenda ingefaa kuhangaikia hali ya walio hai, kutia ndani wewe. Solomoni aliendelea kusema hivi: “Lo lote mkono wako utakalolipata kulifanya, ulifanye kwa nguvu zako” ukiwa hai. (Mhubiri 9:10) Unaweza kuwa na hakika kwamba mataraja ya uhai ya wakati ujao kwa wale waliojiua yako mikononi mwa Yehova, “Baba ya rehema nyororo na Mungu wa faraja yote.”—2 Wakorintho 1:3. *

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 40 Utapata maoni yaliyosawazika kuhusu mataraja ya wakati ujao kwa wale waliojiua katika makala “Maoni ya Biblia: Kujiua—Kuna Ufufuo?” katika toleo la Amkeni! la Septemba 8, 1990.

[Picha katika ukurasa wa 8]

Zungumza na mtu fulani

[Picha katika ukurasa wa 10]

Uhai wako una thamani kwa wengine