Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Huenda Akabadalika”

“Huenda Akabadalika”

Huenda Akabadalika

ROXANA * ni mwanamke mchangamfu, mama mwenye kuvutia wa watoto wanne na mke wa daktari-mpasuaji anayeheshimiwa sana huko Amerika Kusini. Yeye asema, “mume wangu huwavutia sana wanawake na hupendwa sana na wanaume.” Hata hivyo mume huyu hutenda mambo yenye kuchukiza ambayo hata marafiki wake wa karibu hawajui. “Yeye ni mtu katili nyumbani. Ana wivu mbaya sana.”

Roxana anaonekana mwenye woga anapoendelea kusimulia yanayompata. “Matatizo yalianza majuma machache tu baada ya kuolewa. Ndugu zangu na mama yangu walipotutembelea, nilifurahi sana kuzungumza na kucheka pamoja nao. Lakini walipoondoka, mume wangu alinibwaga kwenye sofa akiwa amepandwa na hasira kali. Sikuweza kamwe kuamini yaliyokuwa yakitendeka.”

Huo ulikuwa mwanzo tu wa mateso ya Roxana, kwani kwa miaka mingi amepigwa sana na mume wake. Yaelekea mashambulizi hayo hufuata utaratibu fulani. Kwanza yeye humpiga, kisha anaomba msamaha na kuahidi kwamba hatarudia tena. Yeye huacha kumshambulia angalau kwa muda fulani. Halafu anaanza tena kumshambulia kwa ukatili. “Mimi hufikiri tena na tena kwamba huenda akabadilika wakati huu,” asema Roxana. “Hata nikitoroka mimi bado humrudia.”

Roxana anahofu kwamba ukatili wa mume wake huenda ukaongezeka. Yeye asema, “alitisha kuniua, kuua watoto na kisha kujiua. Siku moja aliniwekea makasi kooni. Wakati mwingine alielekeza bunduki kwenye sikio langu na kuifyatua! Jambo zuri ni kwamba haikuwa na risasi, lakini nilishtuka, karibu nife.”

Wameamua Kunyamaza

Kama Roxana, mamilioni ya wanawake ulimwenguni pote wameteswa na wanaume wenye jeuri. * Wengi wao hunyamaza wakisababu kwamba hata wakiripoti mambo hayo huenda wasisaidiwe. Kwani wanaume wengi wakatili hukataa madai hayo kwa kusema “Mke wangu hubabaika-babaika tu” au “Yeye hufanya mambo madogo yaonekane kuwa makubwa mno.”

Inasikitisha kwamba wanawake wengi wanaishi wakiwa na hofu ya kushambuliwa nyumbani, mahali ambapo wanapaswa kuhisi wakiwa salama zaidi. Tena, mara nyingi mkosaji huhurumiwa badala ya aliyekosewa. Inakuwa vigumu kwa wengi kuamini kwamba mwanamume anayeonekana kuwa raia mwenye kuheshimika anaweza kumpiga mwenzi wake. Fikiria kisa cha Anita, mwanamke aliyezungumza waziwazi kuhusu jinsi alivyotendewa kikatili na mume wake aliyeheshimiwa sana. “Mtu tunayefahamiana aliniambia hivi: ‘Unawezaje kumlaumu mwanamume huyu mwenye kuheshimiwa sana?’ Mwingine alisema kwamba haikosi mimi ndiye ninayemchokoza! Hata baada ya ukatili wa mume wangu kujulikana wazi, baadhi ya marafiki wangu walianza kuniepuka. Walihisi kwamba nilipaswa kuvumilia ‘eti kwa sababu hivyo ndivyo wanaume walivyo.’”

Kama simulizi la Anita linavyoonyesha, wengi hawaelewi jinsi mtu anavyoweza kumtendea mwenzi wake wa ndoa kwa ukatili. Ni nini humfanya mwanamume anayedai kumpenda mke wake kuwa katili sana? Je wale wanaotendewa kwa jeuri wanaweza kusaidiwa?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Majina yamebadilishwa katika mfululizo huu.

^ fu. 7 Ni kweli kwamba hata wanaume wengi pia hupigwa. Lakini uchunguzi unaonyesha kwamba wanawake wengi huelekea kujeruhiwa vibaya zaidi. Kwa hivyo, makala hii itazungumzia ukatili kuelekea wanawake.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 4]

Kuenea kwa Jeuri Nyumbani

Kulingana na Azimio la Umoja wa Mataifa la Kukomesha Jeuri Dhidi ya Wanawake, maneno “jeuri dhidi ya wanawake” yaweza kurejezea “tendo lolote la jeuri ya kijinsia ambalo huenda likatokeza maumivu ya kimwili, kiakili na kingono, au kuteseka kwa wanawake kutokana na kutishwa kutendewa kwa jeuri. Inatia ndani pia kukandamizwa, kuonewa na kunyimwa uhuru, iwe ni faraghani au peupe.” Pamoja na mambo mengine, jeuri hii hutia ndani “kujeruhiwa kimwili, kingono na kiakili, mambo ambayo hutokea katika familia na katika jumuiya kwa ujumla, kutia ndani kupigwa, watoto wa kike kutendewa vibaya kingono, jeuri inayohusiana na malipo ya mahari, wake kubakwa na waume zao, kutahiriwa kwa wanawake na mazoea mengineyo ya kidesturi yanayowadhuru wanawake.”