Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni Nini Kitakachotokea Wakati Ujao?

Ni Nini Kitakachotokea Wakati Ujao?

Ni Nini Kitakachotokea Wakati Ujao?

MWANADAMU na viumbe vyote duniani wana sehemu yao kulingana na daraka walilopewa na Mungu. Sisi hufurahia vitu vingi pamoja na viumbe vingine vinavyotuzunguka—kitu cha maana zaidi kikiwa ni muujiza wa uhai. Kwa sababu hiyo, watu wengi huona wamepata hasara kubwa wakati kiumbe fulani kinapoangamia.

Mwanasayansi Anthony C. Janetos, aliandika hivi katika gazeti la Consequences: “Watu wengi watakubali kwamba tukiwa jamii tuna wajibu wa kimaadili wa kulinda dunia ili iweze kukalika, na kutunza unamna-namna wake wa viumbe kwa faida ya sasa ya wanadamu na ya wakati ujao. Ili tuweze kufanya hivyo twapaswa kuelewa umuhimu wa kuwa na aina mbalimbali za viumbe—jinsi zinavyonufaisha mazingira na jinsi tunavyoweza kuzitumia—na kujitoa mhanga kuzihifadhi.”

Ni Hatua Zipi Zinazochukuliwa?

Kwa hakika, hangaiko la ulimwenguni pote kuhusu kuangamia kwa viumbe liliwalazimu wawakilishi wa serikali na mashirika mengine kukutana ili kuunda Mkataba kuhusu Aina Mbalimbali za Viumbe. Mkataba huo wenye masuala mengi huonyesha kwamba watu wote wanahangaikia kuhifadhi aina mbalimbali za viumbe.

Ili kuelewa zaidi umuhimu wa kuwa na aina mbalimbali za viumbe, wanabiolojia, wanaekolojia, na wanasayansi wengine ulimwenguni kote wametangaza mwaka wa 2001-2002 kuwa Mwaka wa Kimataifa wa Kuchunguza Aina Mbalimbali za Viumbe (IBOY). Diana Wall, mwanabiolojia wa Chuo Kikuu cha Jimbo la Colorado aliye mwenyekiti wa IBOY, alisema hivi: “Kuchunguza aina mbalimbali za viumbe kutaleta faida nyingi kupitia uvumbuzi wa kemikali na chembe mpya za urithi ambazo zaweza kutumiwa kutengeneza dawa, kuboresha mazao au kurekebisha ardhi iliyochafuliwa.” Wall aliongezea kusema hivi: “Zaidi ya yote, ni muhimu kujua mahala ambapo aina mpya za viumbe zapatikana, jinsi aina hizo zinavyoendeleza hali bora ya mazingira na jinsi tunavyoweza kuzihifadhi, ili tufanye maamuzi mazuri kuhusu ardhi, mito, na bahari zetu.”

Mabadiliko Makubwa Yahitajiwa

Japo kumekuwa na maendeleo fulani, jitihada hizo zimeshughulikia matokeo badala ya visababishi. Kulingana na watafiti, sasa wanadamu hawana wakati wa kupoteza. Ruth Patrick, wa Chuo cha Philadelphia cha Sayansi ya Mambo ya Asili huko Pennsylvania, Marekani, alipochunguza kile alichotaja kuwa “uwezekano wa kuangamia kwa aina mbalimbali za viumbe,” alikata shauri kwamba “muda unazidi kupungua . . . Hatua madhubuti zapasa kuchukuliwa haraka.” Ili kuzuia kuangamia kwa viumbe, ni lazima mabadiliko ya haraka yafanywe kuhusiana na jinsi wanadamu wanavyoitendea dunia na viumbe vilivyomo. Jambo linalohitajiwa si kupunguza hasara tu. Taasisi ya Mali Asili za Ulimwengu ilisema hivi: ‘Hivyo, matatizo ya kuhifadhi aina mbalimbali za viumbe yanahusiana sana na masuala makubwa ya ustawi . . . wa jamii.’

Ili kufikia mradi huo, badiliko kubwa katika jamii ya wanadamu lingehitajiwa. Kitabu Caring for the Earth chakubali kwamba usimamizi mzuri unapaswa kuwa na “maadili, mifumo ya kiuchumi na jamii zilizo tofauti na nyingi kati ya zile zilizoko leo.”

Biblia huonyesha wazi kwamba wanadamu hawawezi kamwe kuleta mabadiliko hayo. Andiko la Yeremia 10:23 husema: “Ee BWANA, najua ya kuwa njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.” (Mithali 20:24) Pasipo shaka jambo hilo limeonekana wazi katika historia yote, na kwa kuwa wanadamu wamepuuza kanuni hiyo tumekabili “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo” zinazotajwa kwenye 2 Timotheo 3:1-5. Mistari hiyo pia hutuonyesha kwamba nyakati hizo za hatari husababishwa na mawazo mabaya ya wanadamu. Hivyo basi, isipokuwa watu wabadilike, utatuzi wowote kwa matatizo tunayokabili utakuwa wa muda tu.

Wakati mwanasayansi maarufu Dakt. Jane Goodall alipohojiwa, alisema kwamba uharibifu wa makao ya viumbe “unasababishwa mara nyingi na pupa ya kupata pesa na mali katika nchi zilizositawi.” Na mtaalamu wa elimu ya mimea Peter Raven, aliyekuwa katibu wa Chuo cha Kitaifa cha Sayansi cha Marekani, alionya kwamba “kutojua, kutokujali, umaskini na pupa hutokeza matatizo ambayo yanaelekea kusababisha madhara mengi sana katika Dunia.” Hivyo basi, baadhi ya maadili yanayopaswa kubadilika yanatia ndani ubinafsi, pupa, kutojua, na kutokupanga mambo kimbele.

Mlinzi Mkuu wa Aina Mbalimbali za Viumbe

Kwa kufaa, Muumba aliyetokeza uhai wenye unamna-namna unaostaajabisha anapendezwa sana na wakati ujao wa uumbaji wake. Biblia hutueleza kwamba Mungu atachukua hatua hivi punde kwa “kuwaleta kwenye uangamizi wale wanaoiangamiza dunia.”—Ufunuo 11:18.

Je, Mungu ataumba tena viumbe vilivyoangamia kwa sababu wanadamu wameharibu dunia? Iwapo Muumba anataka aina za wanyama zilizoangamia zitokee tena duniani, pasina shaka kwamba anaweza kuziumba tena wakati ujao. Vivyo hivyo pia kwa habari ya mimea iliyoangamia. Lakini kwa kuwa Biblia haituelezi, si jambo la hekima kukisia-kisia jambo hilo.

Utawala wa Mungu utahakikisha kwamba viumbe vyote duniani vitabarikiwa. Mtunga-zaburi alisema hivi: “Nchi na ishangilie, bahari na ivume na vyote viijazavyo, mashamba na yashangilie, na vyote vilivyomo, ndipo miti yote ya mwituni iimbe kwa furaha.”—Zaburi 96:11, 12.