Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tumaini kwa Wale Wanaougua Yabisi-Kavu

Tumaini kwa Wale Wanaougua Yabisi-Kavu

Tumaini kwa Wale Wanaougua Yabisi-Kavu

“UGONJWA wa yabisi-kavu hauui mara nyingi kama vile maradhi ya moyo na kansa yanavyofanya, hata hivyo, unaathiri sana hali ya maisha,” Dakt. Fatima Mili anasema. Ugonjwa huo unaweza kuathiri kila jambo maishani. Wagonjwa wa yabisi-kavu wanakabili matatizo gani hasa? Je, inawezekana kuvumilia?

Huko Italia, mtu mmoja anayeitwa Katia, * mwenye umri wa miaka 28, anasema hivi: “Maisha yangu yote yalibadilika nilipokuwa na umri wa miaka 20 nilipojua kwamba nilikuwa na ugonjwa wa yabisi-kavu. Ilinibidi kuacha kazi na utumishi wa wakati wote kwa sababu ya maumivu.” Kila mtu anayeugua yabisi-kavu huwa na maumivu. Huko Uingereza, mtu mmoja mwenye umri wa miaka 63 anayeitwa Alan anasema hivi: “Sikuzote, sehemu fulani ya mwili wangu inauma, ijapokuwa huenda maumivu yasiwe makali sana.” Uchovu ni tatizo jingine. Sarah, mwenye umri wa miaka 21, anasema: ‘Ni vigumu zaidi kuvumilia ule uchovu kuliko kuvumilia maumivu na uvimbe.’

Uchungu wa Moyoni

Huko Japani, Setsuko, mwenye umri wa miaka 61, anasema kwamba kupambana kila siku na maumivu ya kudumu “kunachosha mtu kiakili na kihisia.” Hata kushika kalamu au simu ni vigumu! Kazumi, mwenye umri wa miaka 47, analalamika: “Nimeshindwa kufanya hata mambo ya kawaida ambayo mtoto anaweza kufanya.” Janice, mwenye umri wa miaka 60, ambaye hawezi kusimama wala kutembea kwa muda mrefu, anasema hivi: “Ninavunjika moyo kwa sababu siwezi kufanya yale ambayo nilikuwa nimezoea kufanya.”

Hali kama hizo zinaweza kufanya mtu akate tamaa na ajione kuwa asiyefaa. Gaku, mwenye umri wa miaka 27, ambaye ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova anasema hivi: “Ninahisi kwamba sifai kitu, kwa sababu siwezi kushiriki kikamili katika kazi ya kuhubiri habari njema wala kutimiza madaraka yangu kutanikoni. Francesca, ambaye amepambana na yabisi-kavu tangu alipokuwa na umri wa miaka miwili, anasema kwamba ‘anaendelea kushuka moyo zaidi na zaidi.’ Mtu anayeshuka moyo hivyo, anaweza kuathiriwa kiroho. Joyce, ambaye ni Shahidi huko Afrika Kusini, anakiri kwamba aliacha kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Anasema: “Sikutaka kumwona mtu yeyote.”

Huenda mgonjwa akawa na wasiwasi mwingi kuhusu wakati wake ujao—wasiwasi kwamba atakuwa mlemavu asiyejiweza, wasiwasi kwamba ataachwa bila mtu wa kumtunza, wasiwasi kwamba ataanguka na kuvunjika mifupa, wasiwasi kwamba hataweza kuruzuku familia yake. Yoko, aliye na umri wa miaka 52, anasema: “Nilipoona jinsi mwili wangu ulivyoharibika umbo, nilikuwa na wasiwasi kwamba hali hiyo ingezidi.”

Huenda watu wa familia wakahuzunika pia wanapowaona wapendwa wao wakiteseka kila siku. Wenzi wa ndoa hata wanaweza kupata matatizo makubwa ya ndoa. Mwanamke mmoja huko Uingereza anayeitwa Denise anasema hivi: “Baada ya miaka 15 ya ndoa yetu, mume wangu alisema, ‘Siwezi tena kuvumilia ugonjwa wako wa yabisi-kavu!’ Aliniacha na binti yetu mwenye umri wa miaka 5.”

Kwa hiyo, wagonjwa wanaougua yabisi-kavu na hali kadhalika familia zao wanakabili hali ngumu. Hata hivyo, wengi wanapambana na hali hiyo kwa mafanikio! Tusikie maoni ya wengine.

Ishi kwa Kupatana na Hali Yako

Kupumzika vya kutosha ni muhimu iwapo unaugua yabisi-kavu; kunaweza kupunguza uchovu. Hata hivyo, hupaswi kukaa kitako tu. Timothy anasema hivi: ‘Lazima ufanye mambo mbalimbali, la sivyo ugonjwa huo utakushinda, nawe utakaa tu huku ukihisi maumivu.’ Tabibu wa Ugonjwa wa Baridi-Yabisi, William Ginsburg wa Kituo cha Afya cha Mayo, anasema hivi: “Mgonjwa hapaswi kufanya mengi mno, wala kidogo mno. Nyakati nyingine, inatubidi kuwakumbusha wagonjwa wapunguze shughuli na kuishi kwa kupatana na hali yao.”

Huenda jambo hilo likamaanisha kubadili maoni yako juu ya hali yako. Daphne anayeishi huko Afrika Kusini, anasema hivi: “Imenibidi kusawazisha maoni yangu na kutambua kwamba sijapoteza uwezo wangu wa kufanya mambo mbalimbali; ninahitaji tu kuyafanya polepole. Badala ya kuhangaika au kuvunjika moyo, ninafanya kidogo-kidogo tu.”

Pia inafaa kuelewa vifaa mbalimbali vinavyopatikana. Huenda ukaweza kuzungumzia jinsi vinavyoweza kukusaidia pamoja na daktari wako au tabibu fulani wa maungo. Keiko anasema: “Sisi tumeweka kifaa cha kunipandisha kwenye ngazi. Vifundo vya milango viliumiza mikono yangu kwa hiyo tumevirekebisha. Sasa ninaweza kufungua milango yote kwa kuisukuma kwa kichwa changu. Tuliweka kifaa cha kurahisisha kufungua mfereji wa maji ili niweze kufanya angalau kazi fulani za nyumbani.” Mgonjwa mwingine wa yabisi-kavu anayeitwa Gail anasema hivi: “Funguo za gari langu na nyumba yangu zimeunganishwa na mpini mrefu ili kurahisisha kufungua milango hiyo. Chanuo changu na burashi vina mipini mirefu pia na vinaweza kupindwa ili niweze kuchanua nywele zangu pande zote.”

Familia Wanaweza Kutia Moyo Sana

Carla anayeishi huko Brazili, anasema hivi: “Mume wangu amenisaidia na kunitia moyo sana. Nilitiwa moyo alipoambatana nami kumwona daktari. Tulijifunza pamoja jinsi ugonjwa huo unavyoathiri mwili wangu, dalili zake, na matibabu ambayo ningehitaji. Ilinisaidia kujua kwamba alielewa magumu yangu.” Ndiyo, waume na wake wanaotambua udhaifu wa wenzi wao na walio tayari kujifunza juu ya hali yao wanaweza kusaidia sana na kutia moyo.

Kwa mfano, Bette, alifanya kazi ya usafi, mume wake aliposhindwa kufanya kazi yake ya ujenzi kwa sababu ya yabisi-kavu. Mume wa Kazumi alimtunza na alifanya kazi ya nyumbani ambayo Kazumi hakuweza kufanya. Isitoshe, aliwazoeza watoto wao kufanya kazi mbalimbali. Kazumi anasema hivi: “Mume wangu amenitia moyo sana. Bila msaada wake ningekuwa katika hali mbaya sana.”

Mwanamke mmoja anayeitwa Carol, huko Australia, anaonya hivi: “Usifanye mengi mno. Nisipoweza kufanya yote ambayo wengine wa familia wanafanya ninahisi kana kwamba nimeshindwa.” Watu wa familia wanaowaelewa wagonjwa na kuwajali wanaweza kuwasaidia sana na kuwatia moyo.

Msaada wa Kiroho

Katia anasema: “Mtu anapougua ugonjwa huu, anaamini kabisa kwamba hakuna mtu yeyote anayeelewa hali yake. Kwa hiyo, ni muhimu sana kumwendea Yehova Mungu, kwa kuwa yeye anaelewa kabisa hali yetu ya afya na hisia zetu za moyoni. (Zaburi 31:7) Kwa sababu nina uhusiano mzuri pamoja na Yehova, nimepata amani ya akili kiasi cha kwamba sihangaishwi tena na ugonjwa wangu.” Kwa kufaa Biblia yamwita Yehova, “Mungu wa faraja yote, ambaye hutufariji katika dhiki yetu yote.”—2 Wakorintho 1:3, 4.

Kwa hiyo, sala inaweza kuwa chanzo kikubwa cha faraja kwa wale wenye maumivu ya kudumu. Kazumi anaeleza: “Ninaposhindwa kupata usingizi kwa sababu ya maumivu, ninamtolea Yehova sala za moyoni huku nikilia machozi na kumwomba nguvu ya kuvumilia maumivu hayo, na hekima ya kukabili matatizo yangu yote. Yehova amejibu sala zangu.” Mungu amemsaidia Francesca pia. Anasema hivi: “Nimeona utimizo wa maneno ya Wafilipi 4:13: ‘Kwa mambo yote ninayo nguvu kwa njia ya yeye anipaye nguvu.’”

Mara nyingi, Yehova Mungu hutoa msaada kwa kutumia kutaniko la Kikristo. Kwa mfano, Gail anasema kwamba ndugu na dada zake wa kiroho katika kutaniko la Mashahidi wa Yehova walimsaidia. Gail anasema: “Upendo walionionyesha ulinisaidia nisishuke moyo.” Hali kadhalika, Keiko alipoulizwa: “Je, unaweza kutaja jambo lolote ambalo limekufurahisha maishani mwako?,” alijibu: “Ndiyo, upendo na huruma za washiriki wote wa kutaniko!”

Katika makutaniko ya Mashahidi wa Yehova, waangalizi hasa wana daraka la kusaidia na kutia moyo. Setsuko anasema hivi: “Siwezi kueleza jinsi mgonjwa anavyonufaishwa wazee wanapomsikiliza na kumfariji.” Hata hivyo, Daniel anayeugua yabisi-kavu anatukumbusha kwamba, “ndugu na dada zetu wa kiroho wanaweza kutusaidia tu iwapo tutawaruhusu.” Kwa hiyo, ni muhimu kwa wagonjwa kushirikiana na Wakristo wenzao kwa kuhudhuria mikutano kwa kadiri wanavyoweza. (Waebrania 10:24, 25) Wanapohudhuria mikutano wanatiwa moyo kiroho ili waweze kuvumilia.

Maumivu Yatakwisha

Wagonjwa wanaougua yabisi-kavu wanashukuru wataalamu wa kitiba kwa ajili ya maendeleo ya kitiba ambayo yamefanywa hadi leo. Lakini, hata matibabu bora si tiba kamili. Kwa hiyo, wagonjwa wanafarijika hasa wanapokubali ahadi za Mungu za ulimwengu mpya. * (Isaya 33:24; Ufunuo 21:3, 4) Katika ulimwengu huo “kilema ataruka-ruka kama kulungu.” (Isaya 35:6) Ugonjwa wa yabisi-kavu na magonjwa mengine yote yatakuwa yametoweka milele! Kwa hiyo, Peter, anayeugua yabisi-kavu ya uti wa mgongo, anasema: ‘Nina tumaini la kuishi maisha mazuri wakati ujao.’ Hali kadhalika, mwanamke Mkristo anayeitwa Giuliana anasema hivi: ‘Kila siku inayopita inapunguza muda wa kuvumilia kabla ya mwisho!’ Ndiyo, wakati ambapo ugonjwa wa yabisi-kavu na mateso mengine yote yatakapokuwa yamekwisha u karibu!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

^ fu. 24 Ukitaka mmoja wa Mashahidi wa Yehova akutembelee ili akueleze ahadi za Biblia, wasiliana na Mashahidi wa Yehova wa eneo lako au uandikie wachapishaji wa gazeti hili.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Kuna vifaa vingi vinavyoweza kuwasaidia wagonjwa kufanya kazi mbalimbali

[Picha katika ukurasa wa 12]

Wagonjwa wanatiwa moyo kwenye mikutano ya Kikristo