Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Chakula Chenye Kujenga Afya kwa Wote

Chakula Chenye Kujenga Afya kwa Wote

Chakula Chenye Kujenga Afya kwa Wote

KULA vyakula vyenye afya hupendeza sana. Lakini kama vile tulivyoona, si rahisi kupata vyakula hivyo. Jambo linalosikitisha hata zaidi ni kwamba inawabidi mamilioni ya watu kula vyakula vyovyote wanavyoweza kupata bila kujali ikiwa vitawadhuru. Wanapambana kupata chakula cha kutosha. Je, hayo ni mapenzi ya Mungu?

Ebu fikiria. Mungu alipomwumba mwanamume na mwanamke duniani, je, walikuwa na sababu yoyote ya kuwa na wasiwasi juu ya chakula? Hata kidogo! Simulizi katika kitabu cha Biblia cha Mwanzo linasema: “BWANA Mungu akachipusha katika ardhi kila mti unaotamanika kwa macho na kufaa kwa kuliwa.” (Mwanzo 2:9) Kwa hiyo, Adamu na Hawa walikuwa na vyakula vingi mbalimbali. Mungu aliyewaumba alijua virutubishi walivyohitaji; na alijua pia kile ambacho kingewafurahisha. Bila shaka, hatumo katika shamba la Edeni leo. Lakini je, kusudi la Mungu kuhusiana na mwanadamu na dunia limebadilika?

Tuna sababu nzuri kutarajia kwamba hivi karibuni kila mtu duniani atakuwa na chakula kingi chenye kujenga afya! Tumaini hilo linaweza kutusaidia sana kuwa na maoni yanayofaa juu ya chakula leo. Tukiwa na tumaini hilo, hatutahangaika kupita kiasi.

Kwa nini tunaweza kuamini kwamba maisha yatabadilika hivi karibuni? Watu wanaojifunza Neno la Mungu kwa makini wanajua kwamba tunaishi katika “siku za mwisho” za ulimwengu huu. Ulimwengu huu unaongozwa kwa hekima ya wanadamu, ambayo mara nyingi haiaminiki wala haijathibitishwa kuwa yenye manufaa. Kufikia sasa haijathibitishwa kikamili kama vyakula vinavyotayarishwa viwandani vinadhuru afya ama la. Kutokuwa na uhakika na jambo hilo husababisha wasiwasi na mabishano.—2 Timotheo 3:1-5.

Muumba wa wanadamu ameahidi kwamba ataondoa ulimwengu huu na kuleta ulimwengu mpya. Kusudi lake la awali kwa dunia litatimia—dunia yote itakuwa paradiso kama bustani ya Edeni, nayo itakaliwa na watu wenye furaha na afya njema. Hekima ya Mungu inayounganisha wanadamu itaenea kotekote. (Isaya 11:9) Hekima isiyoaminika ya wanadamu haitaongoza mambo tena. Katika ulimwengu huo mpya, utakaofanyizwa na Mungu, wanadamu hawatakuwa na wasiwasi tena kuhusu chakula. Kwa hakika, Mungu aliyetuumba anajua vyakula tunavyohitaji.

Muumba Ataandaa Chakula Kisichodhuru

Katika Biblia kuna unabii mbalimbali kuhusu maisha katika ulimwengu unaokuja. Nabii Isaya aliandika hivi: “[Mungu] atatoa mvua juu ya mbegu zako, upate kuipanda nchi hii; na mkate wa mazao ya nchi, nayo itasitawi na kuzaa tele; katika siku hiyo ng’ombe zako watakula katika malisho mapana. Ng’ombe pia na wana-punda wailimao nchi watakula chakula kilichokolea, kilichopepetwa kwa ungo na kwa pepeo.”

Unabii wa Isaya pia unasema: “Katika mlima huu BWANA wa majeshi atawafanyia mataifa yote karamu ya vitu vinono, karamu ya divai iliyokaa juu ya urojorojo wake, karamu ya vinono vilivyojaa mafuta, karamu ya divai iliyokaa juu ya urojorojo wake, iliyochujwa sana.” Biblia Habari Njema inatafsiri sehemu ya mwisho hivi, “karamu ya vinono na divai nzuri, nyama tamu na mafuta, pamoja na divai safi.”—Isaya 25:6; 30:23, 24.

Je, hali hiyo inakuvutia? Unabii wa Isaya unatuhakikishia kwamba kila mtu atakayeishi katika ulimwengu mpya wa Mungu atakuwa na chakula cha kutosha. Je, chakula hicho kitakuwa chenye kujenga afya? Bila shaka. Unabii mwingine hutuhakikishia kwamba watu wa Mungu “wataketi kila mtu chini ya mzabibu wake, na chini ya mtini wake; wala hapana mtu atakayewatia hofu.” (Mika 4:4) Usalama huo utaletwa na Ufalme wa Mungu wa Kimesiya ambao utaanza kuitawala dunia yote hivi karibuni.—Isaya 9:6, 7.

Watu hawatakuwa na wasiwasi tena kamwe juu ya chakula. Badala yake, tutafurahia tunapoambiwa: “Karibu chakula.”

[Blabu katika ukurasa wa 12]

Hivi karibuni kila mtu duniani atakuwa na chakula kingi chenye kujenga afya

[Picha katika ukurasa wa 10]

Mungu amewaahidi watu wote chakula kisichodhuru na chenye afya