Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Chakula Kinaweza Kukudhuru?

Je, Chakula Kinaweza Kukudhuru?

Je, Chakula Kinaweza Kukudhuru?

JE, UNAKULA mara tatu kwa siku? Ikiwa ndivyo, utakapofikia umri wa miaka 70 utakuwa umekula zaidi ya mara 75,000. Hiyo inamaanisha kwamba Mzungu wa kawaida, atakuwa amekula mayai 10,000, mikate 5,000, magunia 100 ya viazi, ng’ombe 3, na kondoo 2, mbali na vyakula vingine. Je, inachosha kula vyakula hivyo vyote? La hasha! Tunafurahia kuambiwa maneno kama “karibu chakula.” Mkuu mmoja wa shule ya upishi alisema hivi: “Chakula ndicho jambo muhimu maishani.”

Kwa kawaida tunaamini kwamba chakula tunachokula ni chenye kujenga afya. Lakini ikiwa mlo mmoja tu kati ya ile milo 75,000 ungekuwa na kitu kinachodhuru, tungeweza kuwa wagonjwa mahututi. Je, tunaweza kuwa na uhakika kwamba chakula tunachokula hakitatudhuru? Siku hizi watu wengi hawana uhakika juu ya jambo hilo. Katika nchi kadhaa watu wameanza kuwa na wasiwasi mwingi kuhusu chakula. Kwa nini?

Kwa Nini Wana Wasiwasi?

Kila mwaka, asilimia 15 hivi ya wakazi wa Ulaya wanapata magonjwa yanayosababishwa na chakula. Kwa mfano, mapema katika miaka ya 1980, mafuta ya kupikia yenye sumu yaliua watu 1,000 huko Hispania na kufanya watu 20,000 wawe wagonjwa mahututi. Katika mwaka wa 1999, Wabelgiji walishtuka walipojua kwamba chakula kama vile mayai, kuku, jibini, na siagi huenda kikawa na sumu inayoitwa dioxin. Hivi majuzi, Waingereza walishtuka sana—na biashara ya nyama ya ng’ombe ikaharibika—ng’ombe walipoambukizwa ugonjwa wa kichaa cha ng’ombe. Kisha ugonjwa wa midomo na miguu ulienea, na mamilioni ya ng’ombe, kondoo, nguruwe, na mbuzi wakachinjwa na kutupwa.

Hata ingawa mambo hayo yanaogopesha, kuna matisho mengine pia kuhusiana na vyakula. Mbinu mpya za kukuza na kutengeneza vyakula huwatia watu wasiwasi. Tume ya Ulaya ilitaarifu hivi mwaka wa 1998: “Tekinolojia mpya ya kunururisha vyakula na kurekebisha maumbile ya mbegu kwa kuingiza chembe tofauti za urithi imesababisha mabishano mengi.” Je, mbinu hizo za kisayansi huboresha chakula chetu au hukiharibu? Na tunaweza kufanya nini ili kuhakikisha kwamba chakula tunachokula hakitatudhuru?