Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Kazi Yetu Ilivyosifiwa Huko Moscow

Jinsi Kazi Yetu Ilivyosifiwa Huko Moscow

Jinsi Kazi Yetu Ilivyosifiwa Huko Moscow

MNAMO mwaka wa 1998, kesi ya kupiga marufuku kazi ya Mashahidi wa Yehova iliwasilishwa kwenye mahakama ya manispaa katika wilaya ya Golovinsky huko Moscow. Hivyo, huenda ukashangaa kusikia kwamba wenye mamlaka wa Wilaya ya Golovinsky waliwasifu Mashahidi hivi majuzi.

Ilikuwaje kwamba Mashahidi walisifiwa na wenye mamlaka wa Moscow na wakati huohuo watu fulani walikuwa wakijaribu kuwaondosha jijini? Simulizi hili fupi kuhusu kazi ya Mashahidi huko, litajibu swali hilo.

Mashahidi Huko Moscow

Katikati ya miaka ya 1950, Moscow lilikuwa mojawapo ya majiji makuu ulimwenguni ambapo Mashahidi wa Yehova hawakupatikana. Kwa nini? Kwa sababu Mashahidi waliokuwa Moscow walikuwa wamehamishwa, kama vile maelfu ya Mashahidi wengine walivyohamishwa kutoka sehemu nyingine za Muungano wa Sovieti. Walipelekwa wapi? Wengi walipelekwa kwenye kambi za kazi ngumu huko Siberia.

Miaka ilipopita, wenyeji wachache wa jiji la Moscow walianza kujifunza Biblia kwa kutumia vichapo vya Mashahidi ambavyo vilikuwa vimepigwa marufuku wakati huo nchini Urusi. Katikati ya miaka ya 1970, wenyeji wachache ambao kufikia wakati huo walikuwa Mashahidi, walikutana kujifunza Biblia kwenye nyumba ya Murat Shakirov huko Moscow. Katika miaka ya 1980, washiriki wa kikundi hicho kidogo waliwashawishi wengine wengi wajifunze Biblia.

Kazi ya Mashahidi wa Yehova ilipohalalishwa katika Muungano wa Sovieti mnamo Machi 1991, kutaniko kubwa la Mashahidi huko Moscow lilianza kufanya kazi waziwazi. Maelfu ya watu walitaka sana kujua mafundisho ya kweli ya Biblia na kwa nini Mashahidi walikuwa wamenyanyaswa. Hivyo basi, mnamo Agosti 1991, zaidi ya watu 2,000 kutoka Moscow walisafiri kilometa 890 hivi ili kuhudhuria mkusanyiko huko Kiev, Ukrainia. Wengi wao walikuwa kati ya wale 1,843 waliobatizwa huko.

Katika 1993, watu 23,743 kutoka nchi zaidi ya 30 walihudhuria mkusanyiko mkubwa wa kimataifa wa Mashahidi wa Yehova kwenye Uwanja wa Michezo wa Locomotive huko Moscow. Kufikia mwishoni mwa mwaka huo, idadi ya makutaniko jijini Moscow iliongezeka kuwa 21. Leo, miaka minane baadaye, kuna makutaniko 104 katika eneo hilo.

Katika mwezi wa Juni na Julai mwaka huu, watu 18,292 walihudhuria mikusanyiko minne ya wilaya ya Mashahidi wa Yehova huko Moscow, na 546 walibatizwa. Kwa sababu ya ongezeko kubwa la idadi ya watu wanaojifunza Biblia na Mashahidi, viongozi wa Kanisa la Othodoksi la Urusi wamejaribu kuwachochea wenye mamlaka wa Moscow wapige marufuku kazi yao.

Mapema katika mwaka wa 1998, kesi ya kupiga marufuku kazi ya Mashahidi iliwasilishwa mbele ya mahakama ya Golovinsky. Mwishowe, mnamo Februari 23, 2001, hakimu aliamua kwamba Mashahidi hawakuwa na hatia yoyote. Hata hivyo, waendesha mashtaka walipokata rufani kwenye mahakama nyingine kuu ya Moscow, kesi hiyo ilirudishwa tena kwenye mahakama ile ya awali ili ichunguzwe upya.

Lakini, ni kwa nini wenye mamlaka wa Wilaya ya Golovinsky huko Moscow waliwasifu Mashahidi, japo watu fulani walijaribu kupiga marufuku kazi yao?

Jumba Jipya la Mikutano Lilihusika

Mnamo Desemba 1998, Mashahidi walinunua jengo kubwa la orofa mbili kando ya Bustani ya Mikhalkovsky. Hapo mbeleni jengo hilo lilikuwa kituo cha utamaduni. Muda fulani uliopita, Mashahidi walianza kurekebisha jengo hilo. Kuna Majumba matano ya Ufalme katika jengo hilo, au majumba ya kukutania, kwa ajili ya makutaniko 22 ya Mashahidi wa Yehova.

Mnamo Aprili 15 mwaka huu, msimamizi mmoja wa wilaya ya Golovinsky aliwaomba Mashahidi wasafishe Bustani ya Mikhalkovsky siku ya Aprili 21. Ni jambo la kawaida kwa wakazi na vikundi nchini Urusi kusafisha bustani na barabara kuu baada ya majira ya baridi kali. Mashahidi walikutana mnamo Aprili 17 ili kupanga kazi hiyo. Kwenye mkutano huo, iliamuliwa kwamba wafanyakazi 700 hivi wangehitajiwa.

Jinsi Kazi Hiyo Ilivyofanywa

Mnamo Aprili 18, wakati Mashahidi walipowaeleza wenye mamlaka wa wilaya ya Golovinsky idadi ya vifaa ambavyo vingehitajiwa, maafisa hao hawakudhani wafanyakazi 700 wangekuja. Hata hivyo, kufikia saa 3:30 asubuhi mnamo Aprili 21, wakati wafanyakazi wa usimamizi wa jiji walipofika kwenye bustani hiyo, mamia ya Mashahidi tayari walikuwepo, lakini kulikuwa vifaa 200 tu. Punde si punde, vifaa 200 viliongezwa. Wale wasiokuwa na vifaa walifanya kazi mikono mitupu wakikusanya takataka na kuziweka ndani ya mifuko ya plastiki. Mashahidi walileta pia mabuti marefu na mashua ili kusafisha kidimbwi kikubwa.

Wawakilishi wa wasimamizi wa jiji walishangazwa na kazi iliyofanywa. Walisema kwamba watu hao walifanya kazi kwa furaha na shauku kana kwamba walikuwa wanasafisha bustani zao. Kwa ujumla, Mashahidi wa Yehova elfu moja hivi walifanya kazi kwenye Bustani ya Mikhalkovsky, na zaidi ya tani 250 za takataka ziliondolewa. Wakazi wa eneo hilo walisema kwamba bustani hiyo haijawahi kusafishwa hivyo kwa muda mrefu.

Kama ilivyotajwa mwanzoni, wenye mamlaka hao walifurahishwa sana na kazi hiyo na walishukuru sana. Afisa mmoja wa wilaya ya Golovinsky aliandika hivi: “Wasimamizi wa Wilaya ya Golovinsky wa Jimbo la Kaskazini la Moscow wanashukuru jamii ya kidini ya Mashahidi wa Yehova kwa ajili ya kazi yao ya kusafisha Bustani ya Mikhalkovsky.” Vivyo hivyo, afisa mwingine alitoa shukrani zake na kumalizia hivi: “Kazi hiyo nzuri na muhimu itawafaidi na kuwafurahisha watu wote wanaotembelea bustani hii.”

Ingawa Mashahidi wa Yehova wanapenda kurembesha bustani zao—na kushiriki katika miradi kama hii—kazi yao muhimu leo ni kuwahubiria wengine habari njema ya Ufalme wa Mungu, yaani, serikali itakayoleta Paradiso duniani pote. (Mathayo 24:14) Walipokuwa wakisafisha Bustani ya Mikhalkovsky, baadhi ya Mashahidi walisema kwamba yale waliyokuwa wakifanya yaliwazoeza kwa ajili ya kazi ya kurembesha dunia yote itakayofanywa baada ya Har–Magedoni.—Ufunuo 16:14, 16.

Naam, wote wanaopenda Biblia wanatarajia wakati dunia yote itakapokuwa bustani maridadi, kama vile Mungu alivyokusudia alipowaumba wale wenzi wawili wa kwanza.—Mwanzo 1:28; 2:8, 9, 15; Ufunuo 21:3, 4.

[Picha katika ukurasa wa 15]

Wale waliokuwa wakikutanika kwenye nyumba ya Murat Shakirov katikati ya miaka ya 1970, wakutana tena

[Picha katika ukurasa wa 16]

Watu 18,292 walihudhuria mikusanyiko minne iliyofanywa mwaka huu huko Moscow

[Picha katika ukurasa wa 17]

Jengo hili, ambalo hapo awali lilikuwa kituo cha utamaduni, lilirekebishwa ili liwe na Majumba matano ya Ufalme

[Picha katika ukurasa wa 18]

Zaidi ya tani 250 za takataka ziliondolewa