Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuna Hatari Gani Mvulana na Msichana Wanapokutana Kirafiki?

Kuna Hatari Gani Mvulana na Msichana Wanapokutana Kirafiki?

Vijana Huuliza . . .

Kuna Hatari Gani Mvulana na Msichana Wanapokutana Kirafiki?

“Hivi majuzi, wavulana fulani shuleni wametaka tukutane kirafiki au niwe rafiki yao.”—Becky, mwenye umri wa miaka 11. *

“Wavulana na wasichana wengi shuleni hukutana kirafiki. Ni jambo la kawaida kuwaona wavulana na wasichana wakipigana mabusu kwenye kumbi za shule.”—Liana, mwanafunzi wa shule ya sekondari.

VIJANA wengi huanza kupanga kukutana kirafiki na watu wa jinsia tofauti wakiwa wachanga sana. Vyombo vya habari hufanya jambo hilo lionekane kuwa la kawaida—kana kwamba ni tafrija isiyodhuru. Oneyda, mwenye umri wa miaka 12 asema hivi: “Karibu kila kijana shuleni ana rafiki wa jinsia tofauti.” Mwanamke mmoja kijana anayeitwa Jenifer akumbuka hivi: “Nakumbuka watoto wa darasa la tatu ambao walikuwa wakikutana kirafiki na watoto wa jinsia tofauti.” Anaongezea hivi: “Nilishawishiwa nikutane kirafiki na mtu wa jinsia tofauti tangu nilipokuwa na umri wa miaka 11.”

Hivyo basi, usipokutana kirafiki na mtu wa jinsia tofauti huenda ukaonekana kuwa tofauti. Kwa kweli, huenda ukadhihakiwa usipofanya hivyo. Kwa kuwa Jenifer alijua kwamba alikuwa mchanga sana kukutana kirafiki na wavulana, yeye alikataa walipomwomba kufanya hivyo. Wavulana hao walifanya nini? Jenifer akumbuka hivi: “Walinicheka na kunifanyia mzaha.” Hakuna anayependa kudhihakiwa. Lakini je, wapaswa kukutana kirafiki na mtu wa jinsia tofauti kwa sababu tu wengine wanafanya hivyo? Kukutana kirafiki na mtu wa jinsia tofauti kwamaanisha nini? Kusudi la kufanya hivyo ni nini?

Kukutana Kirafiki na Mtu wa Jinsia Tofauti

‘Hatufanyi mikutano ya kirafiki. Sisi ni marafiki tu.’ Vijana wengi husema hivyo, hata ingawa wanatumia muda mwingi pamoja na mtu fulani wa jinsia tofauti. Lakini vyovyote utakavyofafanua hali hiyo—iwe ni kukutana kirafiki, kutembea pamoja, au kuonana tu—wakati mvulana na msichana wanapofikiriana sana na kuanza kutumia wakati pamoja kirafiki hawawezi kuwa marafiki tu. Na watu wanaweza kukutana kirafiki bila kuonana. Kukutana kirafiki kwaweza kuhusisha kupiga gumzo kwenye Internet, kuwasiliana kwa simu, kwa barua, au kwa kompyuta (E-mail).

Swali ni hili, Kuna hatari gani kutumia wakati mwingi pamoja na mtu mmoja tu wa jinsia tofauti?

Hatari za Kukutana Kirafiki na Mtu wa Jinsia Tofauti

Kwenye Mithali 30:19, Biblia husema kuhusu “mwendo wa mtu pamoja na msichana.” Usemi huo hudokeza kwamba mahusiano kati ya wanaume na wanawake hufuata mwelekeo maalumu. Ikiwa watu wawili wa jinsia tofauti ni wakomavu na wanafuata kabisa maadili waliyopewa na Mungu, kukutana kirafiki kwaweza kuwafanya wapendane na hatimaye kuwa na ndoa yenye kuheshimika. Kwani, Mungu aliumba mwanamume na mwanamke ili kila mmoja avutiwe na mwenzake. Lakini vipi ikiwa wewe ni mchanga mno kufunga ndoa? Kuanza kukutana kirafiki na mtu wa jinsia tofauti kabla ya wakati barabara ni kujiwekea mtego.

Kwa nini? Kwa sababu ukitumia wakati mwingi pamoja na mtu wa jinsia tofauti, hapana shaka hisia zako zitasisimuka. Bila kujua, unajikuta ukitarajia kumwona mtu huyo. Wakati hamko pamoja, unajikuta ukimfikiria. Hata hivyo, mara nyingi mtu mmoja ndiye anayehisi hivyo—na hatimaye mtu huyo ataumia moyoni. Hata ikiwa wote wawili wanapendana, iwapo mmoja wao bado ni mchanga mno kufunga ndoa au hajakomaa, watafadhaika na kuvunjika moyo. Je, kweli uhusiano huo unaweza kudumu? Mithali moja ya Biblia husema hivi: “Je! mtu aweza kuua [“kuweka,” BHN] moto kifuani pake, na nguo zake zisiteketezwe?”—Mithali 6:27.

Fikiria kijana anayeitwa Nina. Yeye asema hivi: “Nilijuana na mvulana mmoja kupitia Internet. Tulizungumza kwa saa nyingi kila siku kwenye kituo cha kupiga gumzo. Nilimpenda sana na nilifikiria kuhusu yeye tu. Uhusiano huo haukudumu kwa muda mrefu. Ulipovunjika nilishuka moyo sana. Kisha mvulana huyo alinipigia simu akaniambia kwamba atajiua kwa sababu uhusiano wetu ulivunjika. Nilishuka moyo hata zaidi.” Nina anapofikiria yaliyopita, yeye anakata kauli hii: “Uhusiano huo haukuwa na faida yoyote! Uhusiano huo ulivunjika miaka miwili iliyopita, na bado nimeshuka moyo.” Nina alikuwa mchanga mno kuwa na uhusiano na mtu wa jinsia tofauti.

Huenda Biblia inarejezea ngono inapozungumza kuhusu “mwendo wa mtu pamoja na msichana.” Katika ulimwengu wa sasa, mara nyingi watu wa jinsia tofauti wanapokutana kirafiki, hiyo huongoza kwenye ngono. Huenda wakaanza bila kuwa na nia mbaya, kwa kushikana mikono tu. Kisha, huenda kumbatio na busu likafuata. Matendo hayo ya kimapenzi yakifanywa na watu wawili waliokomaa ambao wameamua kufunga ndoa, hiyo ni tofauti. Lakini kwa watu wawili ambao ni wachanga mno kufunga ndoa, matendo hayo yataamsha tu hamu ya kufanya ngono. Matendo ya “kimapenzi” yanaweza kuzidi kuwa machafu. Yanaweza kuongoza mtu kufanya aina fulani ya uasherati. *

Matokeo ya uasherati huumiza sana. Watu fulani wanaofanya uasherati hupata magonjwa yanayoambukizwa kingono. Wengine hukosa kujistahi na dhamiri zao huwasumbua. Wasichana fulani hupata mimba. Ndiyo sababu Biblia huamuru hivi: “Ukimbieni uasherati”! (1 Wakorintho 6:13, 18; 1 Wathesalonike 4:3) Ukiepuka kukutana kirafiki na mtu wa jinsia tofauti ukiwa mchanga, utaweza kutii amri hiyo.

Wakati Unaofaa Kukutana Kirafiki na Mtu wa Jinsia Tofauti

Hiyo haimaanishi kwamba hutakutana kirafiki na mtu wa jinsia tofauti kamwe. Lakini iwapo wewe ni tineja, huenda u katika ule “mchanuko wa ujana” unaotajwa na Biblia. (1 Wakorintho 7:36) Ndio umeanza tu kuwa mwanamume au mwanamke. Katika kipindi hiki, unaanza kukomaa kimwili, kihisia, na kingono. Hisia zako—kutia ndani tamaa ya ngono—zaweza kuwa nyingi zaidi ya wakati mwingine wowote. Hata hivyo, hisia hizo zaweza pia kubadilika haraka. Ndiyo sababu mara nyingi uhusiano kati ya matineja wa jinsia tofauti huvunjika haraka. Msichana mmoja tineja anasema hivi: “Nilipokutana kirafiki na wavulana, uhusiano wetu ulikuwa ukivunjika baada ya juma moja tu.”

Kwa wazi, si jambo la busara kukutana kirafiki na mtu wa jinsia tofauti wakati wa “mchanuko wa ujana.” Ni afadhali kusubiri hadi utakapojijua vizuri, kujua mambo unayopenda na usiyopenda, na miradi yako. Pia, unapaswa kuwa na umri wa kutosha kutimiza madaraka ya ndoa. Kwa mfano, Yehova anamtazamia mume aandalie familia yake kimwili na kiroho. Iwapo wewe ni mvulana tineja, je, uko tayari kutafuta kazi na kutunza mke na hata labda watoto? Je, unaweza kuwasaidia kudumisha hali ya kiroho? Na vipi ikiwa wewe ni msichana mchanga? Mke apaswa kumpenda na kumheshimu mumewe; apaswa kuunga mkono maamuzi yake. Je, uko tayari kufanya hivyo kwa muda mrefu? Je, uko tayari pia kutunza nyumba kila siku, kutayarisha chakula na kutunza watoto?—Waefeso 5:22-25, 28-31; 1 Timotheo 5:8.

Kwa mfano: Katika nchi za Magharibi, vijana hutamani sana kuendesha gari la familia. Lakini kijana anapaswa kufanya nini kabla ya kuruhusiwa kuliendesha? Katika nchi nyingi ni lazima uzoezwe na kufanya mtihani kwanza kabla ya kupata leseni. Kwa nini? Kwa sababu kuendesha gari ni daraka zito. Maisha yako na ya wengine yatakuwa mikononi mwako unapoendesha gari. Naam, ndoa pia ni daraka zito sana! Ukiwa tineja, huenda huko tayari kufunga ndoa. Basi, litakuwa jambo la busara kuepuka kukutana kirafiki na mtu wa jinsia tofauti kwani hiyo ni hatua inayochukuliwa wakati mtu anapotafuta mwenzi wa ndoa. Kwa ufupi: Iwapo huko tayari kufunga ndoa, hupaswi kukutana kirafiki na mtu wa jinsia tofauti.

Ili ufanye uamuzi unaofaa kuhusu jambo hilo, unahitaji “maarifa na hadhari” kama Biblia inavyosema. (Mithali 1:4) Basi, lingekuwa jambo la busara kuomba maoni ya mtu mwenye umri mkubwa. Kwa kawaida, wazazi Wakristo ndio wanaoweza kukusaidia kuona iwapo uko tayari kufunga ndoa. Huenda ungependa pia kutafuta mashauri ya Wakristo wakomavu kutanikoni. Iwapo wazazi wako hawataki utumie wakati pamoja na mtu wa jinsia tofauti, itafaa ufuate mashauri yao. Wanataka kukusaidia ‘ujikinge.’—Mhubiri 11:10, BHN.

Iwapo wanaona kwamba u mchanga sana kukutana kirafiki na mtu wa jinsia tofauti, huenda wakakushauri uwe na marafiki wengi kwa sasa, badala ya kufikiria tu kuhusu mtu mmoja. Kushirikiana na waseja na watu waliofunga ndoa, wazee na vijana, na vilevile marika wako, kwaweza kukusaidia kuboresha utu wako kabisa na kuwa na maoni yanayofaa kuhusu maisha na ndoa.

Haitakuwa rahisi kusubiri hadi wakati unaofaa ili upange kukutana kirafiki na mtu wa jinsia tofauti. Lakini kuna faida kusubiri. Ukitumia kipindi cha “mchanuko wa ujana” kukomaa, utaepuka matatizo mengi. Utakuwa unajipa muda wa kukomaa ili uweze kushughulikia matatizo na madaraka ya ndoa. Pia, utakuwa unajipa muda ili uwe mtu wa kiroho. Kwa njia hiyo, utakapokuwa tayari kukutana kirafiki na mtu wa jinsia tofauti, huenda wengine watapendezwa kukujua vizuri zaidi.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

^ fu. 14 Neno la awali la Kigiriki la uasherati ni por neiʹa. Neno hilo humaanisha matendo ya ngono yanayohusisha kutumia viungo vya uzazi ambayo hufanywa na watu wasiofunga ndoa. Hilo latia ndani kushika-shika viungo vya uzazi vya mtu mwingine na ngono inayohusisha mdomo.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Mara nyingi matendo ya kimapenzi huleta matatizo