Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Uhamishoni Huko Siberia Nilithamini sana simulizi la Fyodor Kalin katika mfululizo “Dini Nchini Urusi—Zitapatwa na Nini?” (Aprili 22, 2001) Nilivutiwa sana kusoma jinsi yeye na familia yake walivyohamishwa Siberia na jinsi walivyoendelea kuwa waaminifu na wenye furaha hata katika hali ngumu sana. Miaka michache iliyopita, nilikuwa na pendeleo la kutembelea baadhi ya ndugu zetu Wakristo huko Moldova, na sitasahau kamwe masimulizi yao kuhusu uhamisho wao huko Siberia. Imani na tumaini lao katika Yehova lilinitia moyo kuendelea kuwa mwaminifu.

G. F., Sweden

Kiziwi na Kipofu Asanteni kwa simulizi la maisha la Janice Adams, “Nilipata Usalama Nijapokuwa Kiziwi na Kipofu.” (Aprili 22, 2001) Sikufikiri kamwe kwamba mtu aliye kiziwi na vilevile kipofu angeweza kunitia moyo hivyo. Mimi na mume wangu tumekuwa wagonjwa mara nyingi, kimwili na vilevile kihisia. Masimulizi kama hayo yanatutia moyo kuwa waaminifu na kuvumilia hadi mwisho.

P. G., Marekani

Mara nyingi hatuthamini kile tulicho nacho, hata tunaweza kukosa kuhudhuria mkutano wa Kikristo kwa sababu tu tunaumwa na kichwa. Lakini ijapokuwa Janice alikuwa na sababu ya kubaki nyumbani—kwa sababu alikuwa ameshuka moyo na kutendwa vibaya—alimtegemea Yehova ili amtie nguvu ya kuendelea na utendaji wa kiroho.

C. D., Italia

Mimi nina afya nzuri, kwa hiyo hali yangu hailingani na ya Janice. Lakini kwa sababu nilikandamizwa shuleni, mara nyingi ninashuka moyo. Mimi hulia mara nyingi na kuwa na uchungu moyoni. Wakristo wenzangu hunitia moyo na wazazi wangu pia hunisaidia. Hata hivyo, ninawashukuru kwa moyo wangu wote kwa simulizi la Janice Adam. Lilinitia moyo sana.

M. T., Japani

Babu na Nyanya Asanteni kwa sehemu ya “Vijana Huuliza . . . Kwa Nini Niwajue Vyema Babu na Nyanya?” (Aprili 22, 2001) Nilikuwa na uhusiano wa kipekee na nyanya yangu. Wazazi wangu walipotalikiana nilichanganyikiwa sana na nililia mara nyingi. Nyanya yangu alinisaidia sikuzote. Tulihubiri pamoja, naye alifanya nipende huduma. Nilifuata mfano wake kwa kuanza utumishi wa wakati wote miaka minne iliyopita. Hata alipopata ugonjwa wa Alzheimer na hakunitambua tena, macho yake yaling’aa kwa furaha nilipomsomea maandiko kuhusu Paradiso. Alikufa Septemba 2000. Asanteni sana kwa kufundisha vijana jinsi babu na nyanya zetu walivyo muhimu kwetu.

C. R., Marekani

Wazazi wangu walitalikiana miaka kumi iliyopita. Niliacha kushirikiana na jamaa ya babangu kwa kuwa nilitaka kumwunga mkono mama yangu. Lakini baada ya kusoma makala hizo ninaona umuhimu na faida za kuwa na uhusiano mzuri pamoja na babu na nyanya yangu. Madokezo ya Biblia katika makala hizo yatanisaidia kukuza uhusiano huo.

G. V., Marekani

Ijapokuwa babu na nyanya zangu si Wakristo, nina uhusiano mzuri pamoja na wote wanne. Pia nina “nyanya” kutanikoni—dada Mkristo anayekaribia umri wa miaka 70. Ninapokuwa na tatizo, yeye hunisomea Biblia na kunitia moyo. Mara nyingine yeye hushika tu mkono wangu au kuweka mkono wake begani mwangu. Nyakati nyingine ninahisi kana kwamba sisi ni wa rika moja.

M. K., Japani