Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nilitegemezwa kwa Kumwamini Mungu Kabisa

Nilitegemezwa kwa Kumwamini Mungu Kabisa

Nilitegemezwa kwa Kumwamini Mungu Kabisa

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA RACHEL SACKSIONI-LEVEE

WAKATI ASKARI JELA MMOJA ALIPONIPIGA USONI MARA NYINGI KWA SABABU NILIKATAA KUTENGENEZA SPEA ZA NDEGE ZA WANAZI ZA KURUSHIA MABOMU, ASKARI MWINGINE ALIMWAMBIA: “NI AFADHALI UMWACHE. HAO ‘BIBELFORSCHER’ WATAKUBALI KUPIGWA HADI KIFO KWA SABABU YA MUNGU WAO.”

JAMBO hilo lilitokea mnamo Desemba 1944 katika Beendorff, kambi ya kazi ngumu ya wanawake karibu na migodi ya chumvi huko kaskazini mwa Ujerumani. Nitawaeleza jinsi nilivyofika huko na nilivyookoka miezi ya kumalizia Vita ya Pili ya Ulimwengu.

Nilizaliwa mwaka wa 1908 katika familia ya Wayahudi huko Amsterdam, Uholanzi. Tulikuwa wasichana watatu, mimi nikiwa mtoto wa pili. Baba yangu alifanya kazi ya kung’arisha almasi. Wayahudi wengi walifanya kazi hiyo huko Amsterdam kabla ya Vita ya Pili ya Ulimwengu. Baba alikufa nilipokuwa na umri wa miaka 12, na baadaye babu alikuja kuishi nasi. Babu alifuata sana dini ya Kiyahudi, na alihakikisha kwamba tulilelewa kulingana na desturi za Wayahudi.

Kwa kufuata nyayo za babangu, nilijifunza kazi ya kukata almasi, na katika mwaka wa 1930, niliolewa na mfanyakazi mwenzangu. Tulipata watoto wawili—Silvain, mvulana machachari mwenye shauku, na Carry, msichana mzuri mtulivu. Kwa kusikitisha, ndoa yetu haikudumu kwa muda mrefu. Mnamo mwaka wa 1938, muda mfupi baada ya kupata talaka, niliolewa na Louis Sacksioni, ambaye pia alifanya kazi ya kung’arisha almasi. Msichana wetu Johanna alizaliwa mnamo Februari 1940.

Japo Louis alikuwa Myahudi, hakufuata sana dini yake. Hivyo, hatukusherehekea miadhimisho ya Kiyahudi ambayo niliipenda sana nilipokuwa mtoto. Nilikosa sherehe hizo sana, lakini niliendelea kumwamini Mungu moyoni.

Kubadili Dini

Mapema katika mwaka wa 1940, wakati Wajerumani walianza kumiliki Uholanzi, mwanamke mmoja alifika nyumbani kwetu na akanieleza kuhusu Biblia. Sikuelewa mambo mengi aliyosema, lakini nilikubali vichapo alivyoacha kila mara alipokuja. Hata hivyo, sikusoma vichapo hivyo kwani sikutaka kujua mambo yoyote kuhusu Yesu. Nilikuwa nimefundishwa kwamba Yesu alikuwa Myahudi aliyeasi imani.

Kisha, siku moja mwanamume mmoja akaja nyumbani. Nilimuuliza maswali haya, “Kwa nini Mungu hakuwaumba watu wengine baada ya Adamu na Hawa kufanya dhambi? Kwa nini kuna matatizo mengi? Kwa nini watu huchukiana na kupigana?” Alinihakikishia kwamba nikiwa na subira, angejibu maswali yangu yote kupitia Biblia. Basi funzo la Biblia likaanzishwa.

Hata hivyo, nilipinga lile wazo la kwamba Yesu alikuwa Mesiya. Lakini baada ya kusali kuhusu jambo hilo nilianza kusoma unabii mbalimbali kuhusu Mesiya katika Biblia, na kuuelewa kwa njia tofauti. (Zaburi 22:7, 8, 18; Isaya 53:1-12) Yehova alinisaidia kuona kwamba Yesu alitimiza unabii huo mbalimbali. Mume wangu hakupendezwa na yale niliyojifunza, lakini hakunikataza nisiwe Shahidi wa Yehova.

Kuhubiri Tukiwa Tumejificha

Maisha yangu yalikuwa hatarini Wajerumani walipomiliki Uholanzi. Hiyo ni kwa sababu mbali na kuwa Myahudi, ambao Wajerumani walikuwa wakiwapeleka kwenye kambi za mateso, nilikuwa pia mmoja wa Mashahidi wa Yehova, tengenezo la kidini ambalo Wanazi walitaka kulikomesha. Hata hivyo, niliendelea kuhubiri, nikitumia saa 60 kwa wastani kila mwezi nikiwaeleza wengine kuhusu tumaini langu jipya la Kikristo.—Mathayo 24:14.

Mume wangu hakurudi kutoka kazini jioni moja ya Desemba 1942. Alikuwa amekamatwa kazini pamoja na wafanyakazi wengine. Sikumwona tena. Mashahidi wenzangu walinishauri nijifiche pamoja na watoto wangu. Nilikaa pamoja na dada mwingine Mkristo upande ule mwingine wa Amsterdam. Kwa kuwa ilikuwa hatari sote wanne kuishi pamoja, nililazimika kuwaachia watu wengine watoto wangu.

Mara nyingi niliponea chupuchupu kukamatwa. Jioni moja, Shahidi fulani alinipeleka kwenye maficho mengine kwa baiskeli yake. Hata hivyo, taa ya baiskeli yake ilikuwa imeharibika, na tulisimamishwa na polisi wawili Waholanzi. Walinimulika usoni kwa tochi zao na wakatambua kwamba nilikuwa Myahudi. Kwa kustaajabisha, walisema hivi: “Ondokeni hapa haraka—lakini kwa miguu.”

Kukamatwa na Kufungwa

Nilipokuwa nikitaka kuanza huduma yangu asubuhi moja ya Mei 1944, nilikamatwa—si kwa sababu nilikuwa Shahidi bali kwa sababu nilikuwa Myahudi. Nilipelekwa kwenye gereza moja huko Amsterdam, na nikakaa huko kwa siku kumi. Kisha nilisafirishwa kwa gari-moshi, pamoja na Wayahudi wengine hadi kwenye kambi ya muda ya Westerbork, kaskazini-mashariki mwa Uholanzi. Wayahudi walisafirishwa kutoka hapo hadi Ujerumani.

Huko Westerbork, nilikutana na shemeji wangu wa kiume na mwanawe, ambao pia walikuwa wamekamatwa. Ni mimi tu niliyekuwa Shahidi kati ya Wayahudi, na niliendelea kumwomba Yehova anitegemeze. Siku mbili baadaye, mimi, shemeji wangu wa kiume, na mwanawe tuliketi katika gari-moshi la kubeba mifugo ambalo lilikuwa linaenda ama kwenye kambi ya kifo ya Auschwitz au ya Sobibor huko Poland. Kwa ghafula, niliitwa na kupelekwa kwenye gari-moshi jingine—gari-moshi la kubeba abiria wa kawaida.

Ndani ya gari-moshi hilo mlikuwemo watu waliokuwa wamefanya kazi ya kung’arisha almasi pamoja nami zamani. Wafanyakazi mia moja hivi wa kung’arisha almasi walipelekwa Bergen-Belsen, kaskazini mwa Ujerumani. Baadaye, nilifahamu kwamba kazi yangu iliokoa uhai wangu, kwani kwa kawaida Wayahudi waliopelekwa Auschwitz na Sobibor walikuwa wakiingizwa moja kwa moja kwenye vyumba vya kuua watu kwa gesi. Mume wangu, watoto wangu wawili, na watu wengine wa jamaa waliuawa kwa njia hiyo. Hata hivyo, wakati huo sikuwa nimepata habari hiyo.

Huko Bergen-Belsen, sisi wakataji wa almasi tuliishi katika vibanda vya pekee. Ili kutuwezesha kufanya kazi hiyo ngumu, hatukupaswa kufanya kazi nyingine. Ni mimi tu niliyekuwa Shahidi katika kikundi chetu, na niliwaeleza Wayahudi wenzangu kwa ujasiri kuhusu imani yangu mpya. Hata hivyo, waliniona kuwa mwasi-imani, kama vile mtume Paulo alivyoonwa katika karne ya kwanza.

Japo nilitamani sana chakula cha kiroho, sikuwa na Biblia. Daktari mmoja Myahudi kambini alikuwa na Biblia, na alinipa Biblia hiyo kwa kubadilishana na vipande vichache vya mkate na siagi. Nilikaa miezi saba pamoja na kikundi hicho cha wakataji almasi huko Bergen-Belsen. Tulitendewa vizuri kwa kiasi fulani, hivi kwamba wafungwa wengine Wayahudi walituchukia. Hata hivyo, mwishowe madini ya almasi yaliisha. Hivyo, mnamo Desemba 5, 1944, tukiwa wanawake 70 hivi Wayahudi, tulipelekwa kwenye kambi ya kazi ngumu ya wanawake huko Beendorff.

Kukataa Kuunda Silaha

Meta 400 hivi chini ya ardhi katika migodi iliyo karibu na kambi hiyo, wafungwa walipewa kazi ya kutengeneza spea za ndege za kurushia mabomu. Nilipokataa kufanya kazi hiyo, nilipigwa ngumi kadhaa. (Isaya 2:4) Askari jela aliniambia kwa ukali kwamba nilipaswa kujitayarisha kufanya kazi hiyo siku iliyofuata.

Asubuhi iliyofuata, sikwenda kuandikisha jina, nilibaki chumbani. Nilifikiri nitapigwa risasi, hivyo nilimwomba Yehova anithawabishe kwa ajili ya imani yangu. Nilirudia-rudia ile zaburi ya Biblia inayosema: “Nimemtumaini Mungu, sitaogopa; mwanadamu atanitenda nini?”—Zaburi 56:11.

Kambi zilisakwa, na nilipelekwa nje. Wakati huo ndipo askari jela mmoja aliponipiga sana, akisema: “Ni nani aliyekukataza usifanye kazi?” Kila mara alipouliza, nilijibu kwamba ni Mungu. Ndipo askari mwingine akamwambia: “Ni afadhali umwache. Hao Bibelforscher * watakubali kupigwa hadi kifo kwa sababu ya Mungu wao.” Maneno yake yaliniimarisha sana.

Kwa sababu kulikuwa na adhabu ya kusafisha vyoo ambavyo vilikuwa vichafu sana, nilijitolea kuifanya. Nilifurahi kugawiwa kazi hiyo kwani ilikuwa kazi ambayo ningefanya kwa dhamiri safi. Asubuhi moja, kamanda wa kambi, ambaye aliogopwa na kila mtu, alikuja. Alisimama mbele yangu na kusema hivi: “Wewe ndiwe yule Myahudi anayekataa kufanya kazi?”

Nikamjibu hivi: “Unaweza kuona ninafanya kazi.”

“Lakini hutaki kufanya kazi ili kuendeleza vita, sivyo?”

“Naam,” nikamjibu. “Mungu hapendi jambo hilo.”

“Lakini huwezi kumwua mtu yeyote ukifanya kazi hiyo.”

Nilimweleza kwamba kwa kutengeneza silaha, ningekuwa nikitenda kinyume cha dhamiri yangu ya Kikristo.

Akachukua ufagio wangu na kusema hivi: “Naweza kukuua kwa ufagio huu, sivyo?”

“Naam, bila shaka,” nikamjibu, “lakini ufagio haukutengenezwa kwa kusudi hilo. Bunduki huundwa kwa kusudi hilo.”

Tulizungumza kuhusu maisha ya Yesu akiwa Myahudi, na kwamba licha ya mimi kuwa Myahudi nilibadili dini nikawa Shahidi wa Yehova. Alipoondoka, wafungwa wenzangu walinijia, wakishangaa jinsi nilivyopata ujasiri wa kuzungumza kwa utulivu na kamanda wa kambi. Niliwaambia kwamba nilikuwa mtulivu kwa sababu nilipewa nguvu na Mungu wangu wala si kwa sababu nilikuwa jasiri.

Kuokoka Mwishoni mwa Vita

Mnamo Aprili 10, 1945, wakati Majeshi ya Muungano yalipokaribia Beendorff, tulilazimika kusimama kwenye ua karibu siku nzima ili kuandikishwa. Baadaye, tukiwa wanawake 150 hivi tulijazwa ndani ya magari-moshi ya kubeba mifugo, bila kupewa chakula wala maji. Magari-moshi hayo yalielekea mahala pasipojulikana, na tulisafiri kwa siku nyingi katikati ya maeneo ambapo vita ilikuwa imechacha. Wafungwa fulani waliwanyonga wenzao ili kupata nafasi katika mabehewa, na hilo likawafanya wanawake wengi waharibike akili. Nilivumilia yote hayo kwa kuamini kabisa kwamba Yehova angenitunza.

Siku moja, gari-moshi letu lilisimama karibu na kambi ya wanaume, na tukaruhusiwa tutoke. Baadhi yetu tulipewa ndoo ili kuchota maji kwenye kambi hiyo. Nilipofika mferejini, nilikunywa maji mengi kisha nikajaza ndoo yangu. Niliporudi, wanawake walinivamia kama wanyama-pori. Maji yote yalimwagika. Askari wa SS (washiriki wa kikosi maalumu cha Hitler) walicheka tu. Siku 11 baadaye, tulifika kwenye kambi ya Eidelstedt, nje ya mji wa Hamburg. Karibu nusu ya wafungwa wa kundi letu walikufa kwa sababu ya ugumu wa safari.

Siku moja nilipokuwa Eidelstedt, nilikuwa nikiwasomea wanawake kadhaa Biblia. Kwa ghafula, tulimwona kamanda wa kambi dirishani. Tulihofu sana kwa kuwa Biblia ilikuwa imepigwa marufuku kambini. Kamanda huyo aliingia, akachukua Biblia na kusema hivi: “Kumbe hii ndiyo Biblia?” Nilitulia sana alipoirudisha na kusema: “Mwanamke yeyote akifa, uwasomee wengine jambo fulani kutoka kwenye Biblia.”

Kukutana Tena na Mashahidi Wenzangu

Baada ya kuachiliwa siku 14 baadaye, Shirika la Msalaba Mwekundu lilitupeleka kwenye shule fulani karibu na Malmö, Sweden. Tukiwa huko tulitengwa na watu wengine kwa muda. Nilimwomba mtunzaji mmoja awajulishe Mashahidi wa Yehova kwamba nilikuwa kwenye makao hayo ya wakimbizi. Siku chache baadaye, mwanamke fulani aliniita. Nilipomwambia mwanamke huyo kwamba nilikuwa Shahidi, alilia sana. Alikuwa Shahidi pia! Alipotulia, aliniambia kwamba sikuzote Mashahidi nchini Sweden walikuwa wakisali kwa ajili ya ndugu na dada zao Wakristo waliokuwa katika kambi za Nazi.

Kuanzia siku hiyo, dada mmoja aliniletea kahawa na kitu kitamu kila siku. Nilipotoka kwenye makao hayo ya wakimbizi nilipelekwa mahala fulani karibu na Göteborg. Huko, Mashahidi walipanga sherehe kwa ajili yangu alasiri moja. Japo sikuweza kuelewa waliyosema, nilitiwa moyo kuwa pamoja na ndugu na dada zangu tena.

Nilipokuwa Göteborg, nilipata barua kutoka kwa Shahidi mmoja huko Amsterdam aliyenieleza kuwa watoto wangu Silvain na Carry na watu wote wa jamaa walikuwa wamekamatwa na hawakurudi. Ni msichana wangu Johanna na dadangu mdogo tu waliookoka. Hivi majuzi niliona majina ya mwanangu na binti yangu katika kitabu cha rekodi cha Wayahudi waliouawa kwa gesi huko Auschwitz na Sobibor.

Matukio Baada ya Vita

Niliporudi Amsterdam na kuungana na Johanna, ambaye alikuwa na umri wa miaka mitano, nilianza tena kuhubiri. Nyakati nyingine nilikutana na wanachama wa NSB, Chama cha Taifa cha Kisoshalisti cha Uholanzi. Chama hicho cha kisiasa ndicho kilichoshirikiana na Wajerumani. Watu hao walihusika kuwaua karibu watu wote wa familia yangu. Ilinibidi nishinde uhasama ili niweze kuwahubiria watu hao habari njema kuhusu Ufalme wa Mungu. Niliendelea kujikumbusha kwamba Yehova ndiye anayetazama moyo na kwamba yeye ndiye atakayefanya hukumu hatimaye, wala si mimi. Na nilibarikiwa sana kwa kufanya hivyo!

Nilianza kujifunza Biblia na mwanamke ambaye mume wake alifungwa gerezani kwa sababu ya kushirikiana na Wanazi. Nilipopanda ngazi kuelekea kwenye nyumba yao, nilikuwa nikiwasikia majirani wakisema hivi: “Angalieni! Yule Myahudi anawatembelea watu wa NSB tena.” Lakini licha ya kupingwa sana na mumewe aliyekuwa gerezani, ambaye aliwachukia sana Wayahudi, mwanamke huyo na binti zake watatu wakawa Mashahidi wa Yehova.

Nilifurahi wakati binti yangu Johanna alipojiweka wakfu kwa Yehova baadaye. Mimi na yeye tulihamia mahala ambapo palikuwa na uhitaji mkubwa wa watangazaji wa Ufalme. Tulipata baraka nyingi za kiroho. Sasa ninaishi katika mji mdogo kusini mwa Uholanzi, ambapo ninahubiri pamoja na wahubiri wengine kutanikoni mara nyingi iwezekanavyo. Ninapofikiria yaliyopita, ninaweza kusema kwamba Yehova hajaniacha kamwe. Sikuzote nimehisi kwamba Yehova na Mwanawe mpendwa, Yesu, wako pamoja nami hata wakati wa hali ngumu.

Nilipoteza mume wangu, watoto wangu wawili, na watu wengi wa jamaa yangu katika vita. Hata hivyo, ninatumaini kuwaona wote tena hivi karibuni katika ulimwengu mpya wa Mungu. Ninapokuwa peke yangu na kukumbuka mambo yaliyonipata, ninatafakari kwa furaha na shukrani maneno haya ya mtunga-zaburi: “Malaika wa BWANA hufanya kituo, akiwazungukia wamchao na kuwaokoa.”—Zaburi 34:7.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 25 Jinsi Mashahidi wa Yehova walivyojulikana siku hizo huko Ujerumani.

[Picha katika ukurasa wa 20]

Wayahudi wakihamishwa kutoka kwenye kambi ya Westerbork hadi Ujerumani

[Hisani]

Herinneringscentrum kamp Westerbork

[Picha katika ukurasa wa 21]

Nikiwa na watoto wangu Carry na Silvain ambao walikufa katika yale Maangamizi Makubwa

[Picha katika ukurasa wa 22]

Tulipotengwa na watu wengine huko Sweden

[Picha katika ukurasa wa 22]

Kitambulisho cha muda cha kurudishwa nyumbani

[Picha katika ukurasa wa 23]

Nikiwa na binti yangu Johanna leo