Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wakristo Washerehekee Mwaka Mpya?

Je, Wakristo Washerehekee Mwaka Mpya?

Maoni ya Biblia

Je, Wakristo Washerehekee Mwaka Mpya?

DAKTARI anayeitwa Fernando huko Brazili anasema kwamba “kwa kawaida hatuna kazi nyingi alasiri ya kabla ya Mkesha wa Mwaka Mpya. Lakini, saa tano hivi za usiku, watu wengi huanza kuwasili—watu waliochomwa visu au kupigwa risasi, vijana waliojeruhiwa katika aksidenti za magari, na wanawake waliopigwa na waume wao. Karibu kila mara matatizo hayo husababishwa na ulevi.”

Hivyo, si ajabu gazeti moja la Brazili lilisema kwamba siku ya kwanza ya mwaka mpya ni siku mbaya sana katika mataifa yote kwa sababu ya sherehe hizo za kupindukia. Shirika moja la habari huko Ulaya lasema kwamba ‘sherehe za Mwaka Mpya ni sherehe za watu wanaopenda raha, na ni pambano jingine kati ya wanadamu na vileo.’

Ni kweli kwamba si watu wote wanaosherehekea Mwaka Mpya wanaofanya hivyo kwa kunywa kupindukia au kwa kufanya matendo ya ujeuri. Wengi hukumbuka sherehe hizo kwa furaha. Fernando aliyenukuliwa juu asema: “Tulipokuwa watoto tulitarajia Mkesha wa Mwaka Mpya kwa hamu sana. Tulicheza michezo mbalimbali, kulikuwa na chakula na vinywaji vingi. Usiku wa manane tulikumbatiana na kubusiana, na kutakiana heri ya ‘Mwaka Mpya!’”

Wengi leo, wanaona kwamba wao husherehekea Mwaka Mpya bila kupita kiasi. Hata hivyo, Wakristo wanapaswa kuchunguza chanzo na maana ya sherehe hiyo maarufu. Je, mafundisho ya Biblia yanapinga sherehe za Mwaka Mpya?

Sherehe za Kale

Sherehe za Mwaka Mpya zimekuwapo kwa muda mrefu. Maandishi ya kale yaliyochongwa yaonyesha kwamba Wababiloni waliadhimisha sherehe hizo katika milenia ya tatu K.W.K. Walifanya sherehe kuu ya mwaka mpya katikati ya mwezi wa Machi. Kitabu cha The World Book Encyclopedia chasema kwamba “wakati huo mungu Marduki aliamua mambo ya mwaka uliofuata.” Sherehe za mwaka mpya za Wababiloni ziliendelea kwa siku 11 na zilitia ndani maandamano, kutolewa kwa sadaka, na ibada ya kuomba mvua na mazao.

Mwaka mpya wa Waroma ulianza pia mwezi wa Machi katika kipindi fulani. Lakini mnamo mwaka wa 46 K.W.K., Maliki Juliasi Kaisari aliamua uanze Januari mosi. Hapo mbeleni Januari mosi ilikuwa siku ya Janus mungu wa mianzo na mwaka wa 46 siku hiyo ikawa pia siku ya kwanza ya mwaka wa Waroma. Tarehe hiyo ilibadilika lakini sherehe haikubadilika. Kitabu cha marejeo cha Cyclopedia cha McClintock na Strong kinasema kwamba katika Januari mosi watu “walijiingiza katika sherehe zenye fujo na ulevi, na ushirikina mbalimbali wa kipagani.”

Hata leo, sherehe za Mwaka Mpya zatia ndani ushirikina mbalimbali. Kwa mfano, katika maeneo kadhaa ya Amerika Kusini, wengi hukaribisha Mwaka Mpya huku wakisimama kwa mguu wao wa kulia tu. Wengine hupiga mbiu na kufyatua fataki. Watu wa Jamhuri ya Cheki wana desturi ya kula dengu wakati wa Mkesha wa Mwaka Mpya, lakini siku hiyo Waslovakia huweka fedha au magamba ya samaki chini ya kitambaa cha meza. Desturi kama hizo ambazo hufanywa ili kukinga bahati mbaya na kuhakikisha ufanisi huendeleza imani ya kale kwamba mambo yatakayokuja huamuliwa siku ya kwanza ya mwaka.

Maoni ya Biblia

Biblia yashauri Wakristo ‘wajiendeshe kwa adabu, si katika sherehe zenye makelele ya ulevi.’ * (Waroma 13:12-14; Wagalatia 5:19-21; 1 Petro 4:3) Wakristo hawashiriki katika sherehe za Mwaka Mpya kwa sababu mara nyingi sherehe hizo ndizo zenye ulevi na mambo mengine ya kupita kiasi yanayokatazwa na Biblia. Jambo hilo halimaanishi kwamba Wakristo wanataka kuzuia wengine wasifurahie mambo. Badala yake, wanajua kwamba Biblia huwaambia mara nyingi waabudu wa Mungu wa kweli washangilie, na kuna sababu nyingi za kufanya hivyo. (Kumbukumbu la Torati 26:10, 11; Zaburi 32:11; Mithali 5:15-19; Mhubiri 3:22; 11:9) Biblia pia yakubali kwamba kula na kunywa hufurahisha mara nyingi.—Zaburi 104:15; Mhubiri 9:7a.

Hata hivyo, tumeona kwamba sherehe za Mwaka Mpya hutokana na mila za kipagani. Dini za uwongo ni chafu na zenye kuchukiza mbele ya Yehova Mungu, na Wakristo wanakataa katakata desturi zilizo na uhusiano wowote nazo. (Kumbukumbu la Torati 18:9-12; Ezekieli 22:3, 4) Mtume Paulo aliandika hivi: “Uadilifu na uasi-sheria vina ushirika gani? Au nuru ina ushiriki gani na giza? Na zaidi, kuna upatano gani kati ya Kristo na Beliali?” Kwa kufaa, Paulo aliongeza hivi: “Komeni kugusa kitu kisicho safi.”—2 Wakorintho 6:14-17a.

Wakristo wanajua vilevile kwamba kushiriki katika desturi za ushirikina hakutawaletea furaha na ufanisi—hasa kwa sababu kushiriki sherehe hizo kunaweza kufanya wakataliwe na Mungu. (Mhubiri 9:11; Isaya 65:11, 12) Isitoshe, Biblia yawashauri Wakristo wawe wenye kiasi na wenye kujidhibiti. (1 Timotheo 3:2, 11) Bila shaka, mtu anayedai kufuata mafundisho ya Kristo hawezi kushiriki sherehe yenye fujo na ulevi.

Hata sherehe za Mwaka Mpya ziwe zenye kuvutia kadiri gani, Biblia yatuambia ‘tukome kugusa kitu kisicho safi’ na “tujisafishe wenyewe kila unajisi wa mwili na wa roho.” Yehova anawapa wale wanaotii ahadi hii yenye kutia moyo: “Nitawakaribisha ndani. . . . Nitakuwa baba kwenu, na nyinyi mtakuwa wana na mabinti kwangu.” (2 Wakorintho 6:17b–7:1) Ndiyo, Mungu anawaahidi wale wanaodumisha uaminifu kwake ufanisi na baraka za milele.—Zaburi 37:18, 28; Ufunuo 21:3, 4, 7.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 12 Huenda Paulo alifikiria sherehe za Mwaka Mpya alipotaja “sherehe zenye makelele ya ulevi,” kwa kuwa hizo zilikuwa za kawaida huko Roma katika karne ya kwanza.