Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuna Hatari Gani Kujihusisha Kidogo Tu na Mambo ya Mizungu?

Kuna Hatari Gani Kujihusisha Kidogo Tu na Mambo ya Mizungu?

Vijana Huuliza . . .

Kuna Hatari Gani Kujihusisha Kidogo Tu na Mambo ya Mizungu?

JE, VIJANA wanapenda mambo ya mizungu? Kikundi cha watafiti kiliwahoji wanafunzi wa shule 115 za msingi na za sekondari ili kupata jibu. Uchunguzi huo ulifunua mambo haya: Zaidi ya nusu ya wale waliohojiwa (asilimia 54) walisema kwamba wanapendezwa na mambo ya mizungu na ya roho, na robo moja (asilimia 26) walisema kwamba “wanapendezwa sana” na mambo hayo.

Watafiti wa Chuo Kikuu cha Alaska huko Anchorage wanaandika hivi: ‘Katika miaka ya karibuni kumekuwa na habari nyingi katika magazeti kuhusu ongezeko kubwa la ibada ya Shetani.’ Wataalamu wanasema kwamba hakuna uthibitisho wa kutosha kuonyesha kwamba vijana wengi wanajihusisha na ibada ya Shetani. Hata hivyo, hapana shaka kwamba vijana wengi wanapendezwa na mambo fulani ya ibada ya Shetani na mizungu, hata ingawa upendezi wao ni wa kijuujuu tu.

Hivyo, huenda vijana fulani wakauliza hivi: ‘Kuna hatari gani kujihusisha kidogo na mambo ya mizungu?’ Ili kujibu swali hilo, na tuchunguze jinsi ambavyo vijana hujihusisha na mambo ya mizungu.

Mtego wa Kujihusisha na Mizungu

Makala moja katika gazeti la U.S.News & World Report inasema kwamba ‘watoto na vijana leo hupata na huona picha na habari nyingi mbaya za kushtua, ambazo hazingekubaliwa hata miaka 20 iliyopita.’ Kwa sababu wanachochewa na udadisi, vijana wengi husoma vitabu na magazeti, hutazama video, au kuchunguza-chunguza vituo vya Internet vyenye mambo ya mizungu.

Ripoti moja kwenye kituo cha Internet cha Shirika la Utangazaji la BBC ilisema kwamba vipindi maarufu vya televisheni vinavyoonyesha uchawi na watu wanaonyonya damu ya watu wengine “husemwa kuwa vinawachochea watoto kupenda uchawi.” Maneno ya muziki fulani wenye mdundo mzito huzungumza pia kuhusu ujeuri na mambo ya mashetani. Mwandishi wa habari Tom Harpur aliandika hivi katika gazeti la The Sunday Star la Toronto: ‘Ni lazima nitoe onyo kali kuhusu [muziki]. . . . Sijawahi kamwe kuona kitu kingine chochote kilicho kichafu hivyo. Nyimbo hizo huzungumza hasa juu ya mambo ya kichaa, kupagawa, mashetani, umwagaji-damu, laana, ujeuri wa namna zote, kutia ndani ubakaji, kujikatakata, mauaji, na kujiua. Habari kuu za nyimbo hizo huwa juu ya kifo na uharibifu, utabiri wa maangamizi, kupinga yaliyo mema na kukubali mambo yote machafu na maovu.’

Je, kusikiliza muziki wa aina hiyo huchangia matendo ya ujeuri? Ilikuwa hivyo katika kisa kimoja. Kijana mwenye umri wa miaka 14 huko Marekani alimwua mamake kwa kumchoma kisu, kisha akajiua. Kijana huyo alikuwa amebandika picha za wanamuziki wa mdundo mzito kwenye kuta za chumba chake. Baadaye, babake alisihi hivi: “Waambieni wazazi wachunguze muziki ambao watoto wao husikiliza.” Alisema kwamba juma moja kabla ya mwanawe kumwua mamake, alikuwa akiimba wimbo wa roki “juu ya kumwaga-damu na kumwua mama yako.”

Kisha kuna michezo ya wahusika-wakuu. Katika baadhi ya michezo hiyo, wachezaji hujisingizia kuwa wachawi au kufanya mambo ya mizungu. Michezo mingi kama hiyo huwa na ujeuri mwingi wa kishetani. *

Hata hivyo, shirika la utafiti la Mediascope laripoti hivi: “Uchunguzi huonyesha kwamba kupenda muziki wenye mdundo mzito kwaweza kuwa sababu kuu ya kujitenga, matumizi ya dawa za kulevya, magonjwa ya akili, kujaribu kujiua . . . au kufanya mambo ya kuhatarisha uhai wakati wa kipindi cha kubalehe, lakini muziki hausababishi tabia hizo. Yasemekana kwamba huenda vijana walio na matatizo hayo wakavutiwa na muziki wenye mdundo mzito, kwa sababu maneno yake huzungumzia mahangaiko yao.”

Huenda watafiti wakakosa kukubaliana kuhusu hatari za kusikiliza muziki wa kishetani. Lakini ni wazi kwamba ni hatari kusikiliza muziki, kutazama video, au kucheza michezo inayohusisha ujeuri au kujiua. Hata hivyo, kuna hatari kubwa zaidi wakati Wakristo wanapojihusisha na mambo ya mizungu.

Maoni ya Mungu Kuhusu Mizungu

Kwenye 1 Wakorintho 10:20, mtume Paulo aliwaonya Wakristo hivi: “Sitaki nyinyi mwe washiriki pamoja na roho waovu.” Roho waovu ni nani, na kwa nini ni hatari sana kujihusisha nao? Kwa ufupi, roho waovu walikuwa malaika hapo zamani, lakini wakachagua kumfuata Shetani Ibilisi. Neno Shetani humaanisha “Mpinzani” na Ibilisi humaanisha “Mchongezi.” Kulingana na Biblia, malaika huyo wa zamani aliyekuwa mwana wa Mungu alijifanya kuwa mpinzani na mchongezi alipochagua kumwasi Mungu. Baadaye, aliwachochea malaika wengine kuasi. Hivyo, malaika hao wakawa roho waovu.—Mwanzo 3:1-15; 6:1-4; Yuda 6.

Yesu alimwita Shetani “mtawala wa ulimwengu huu.” (Yohana 12:31) Shetani na roho wake waovu wana “hasira kubwa” kwa sababu uharibifu wao unakaribia. (Ufunuo 12:9-12) Haishangazi kwamba wale ambao wamejihusisha na roho waovu wameona kwamba roho hao ni wakatili. Mwanamke mmoja huko Suriname aliyelelewa katika familia iliyowasiliana na roho waovu alijionea jinsi roho waovu ‘wanavyofurahia kuwatesa-tesa watu wasiotaka kuwaabudu.’ * Kwa hiyo, ni hatari sana kujihusisha kwa njia yoyote ile na viumbe hao wa roho wakatili!

Kwa sababu hiyo, Mungu aliwaamuru watu wake wa kale, Waisraeli, waepuke mazoea yote ya mizungu. “Mtu atendaye hayo ni chukizo kwa BWANA,” ndivyo andiko la Kumbukumbu la Torati 18:10-12 linavyoonya. Wakristo pia walionywa kwamba “wale wanaozoea kuwasiliana na roho” wataharibiwa na Mungu. (Ufunuo 21:8) Mungu hushutumu pia kujihusisha kidogo na mambo ya mizungu. Biblia huamuru hivi: “Komeni kugusa kitu kisicho safi.”—2 Wakorintho 6:17.

Kuacha Mazoea ya Mizungu

Je, umejihusisha kidogo na mambo ya mizungu? Basi fikiria yaliyotukia katika jiji la Efeso la karne ya kwanza. Watu wengi huko ‘walizoea kufanya ufundi wa kimzungu.’ Lakini baadhi yao walivutiwa na kazi zenye nguvu ambazo mtume Paulo alifanya kwa msaada wa roho takatifu. Matokeo yakawa nini? “Idadi kubwa ya wale waliozoea kufanya ufundi wa kimzungu wakaleta pamoja vitabu vyao wakavichoma kabisa mbele ya kila mtu. Nao wakapiga pamoja hesabu za bei zavyo na kukuta vikiwa na thamani ya vipande elfu hamsini vya fedha. Hivyo katika njia yenye uweza neno la Yehova likafuliza kukua na kuweza.”—Matendo 19:11-20.

Jambo hilo laonyesha nini? Kwamba ikiwa mtu anataka kuachana na roho waovu, anapaswa kuharibu vitu vyote vinavyohusiana na ibada ya Shetani! Hivyo vyatia ndani vitabu, magazeti, picha za kubandika ukutani, vitabu vya katuni, video, hirizi (vitu vinavyovaliwa “kujikinga”), na habari kuhusu roho waovu zinazotolewa kwenye Internet. (Kumbukumbu la Torati 7:25, 26) Tupa vitu vyovyote vinavyotumiwa katika uaguzi, kama vile matufe ya vioo au bao za uaguzi. Pia, haribu kaseti za muziki au za video ambazo zina mambo ya kishetani.

Ujasiri unahitajiwa ili kuchukua hatua hizo madhubuti. Lakini kuna faida nyingi. Mwanamke mmoja Mkristo anayeitwa Jean * alinunua mchezo wa kompyuta ambao ulionekana kuwa mzuri hapo kwanza. Alipoendelea kuucheza, aligundua kwamba mchezo huo ulikuwa na mambo fulani ya roho waovu. Baada ya muda, akaanza kuota ndoto za kutisha! Jean asema hivi: “Niliamka usiku wa manane na kuharibu CD zote za mchezo huo.” Matokeo yalikuwa nini? “Sijapata matatizo yoyote tangu wakati huo.”

Ukiazimia kabisa kuacha mazoea hayo, utafanikiwa. Kumbuka jinsi Yesu alivyoazimia kwa ujasiri kumkinza Ibilisi wakati alipojaribu kumshawishi Yesu amwabudu. “Yesu akamwambia: ‘Enda zako, Shetani! Kwa maana imeandikwa, “Ni Yehova Mungu wako ambaye lazima uabudu, na ni kwake peke yake lazima utoe utumishi mtakatifu.”’ Ndipo Ibilisi akamwacha.”—Mathayo 4:8-11.

Usiwapinge Roho Waovu Ukiwa Peke Yako

Mtume Paulo anatukumbusha kwamba Wakristo wote ‘wana kushindana mwereka dhidi ya majeshi ya roho waovu katika mahali pa kimbingu.’ (Waefeso 6:12) Lakini usijaribu kumpinga Ibilisi na roho wake waovu ukiwa peke yako. Omba msaada wa wazazi wako wanaomhofu Mungu na wa wazee katika kutaniko la Kikristo. Huenda ukaona haya kufunua kwamba umejihusisha na mambo ya mizungu, lakini ukitubu utategemezwa sana.—Yakobo 5:14, 15.

Pia, kumbuka kwamba Biblia husema hivi: “Mpingeni Ibilisi, naye atawakimbia. Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia.” (Yakobo 4:7, 8) Naam, Yehova Mungu atakutegemeza! Atakusaidia kuacha kabisa mambo ya mizungu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Ona makala “Vijana Huuliza . . . Je, Kuna Hatari Yoyote Katika Michezo Inayokufanya Uwe Mhusika-Mkuu?,” katika toleo la Amkeni! la Agosti 22, 1999.

^ fu. 15 Ona makala “Kukung’uta Lile Kongwa la Kuwasiliana na Ulimwengu wa Roho” katika toleo la Septemba 1, 1987 la gazeti letu jenzi, Mnara wa Mlinzi, linalochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 20 Jina limebadilishwa.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Haribu vitu vyote vinavyohusiana na ibada ya Shetani

[Picha katika ukurasa wa 26]

Jihadhari na vituo vya Internet vinavyoendeleza zoea la kuwasiliana na roho waovu