Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mikaeli Yule Malaika Mkuu Ni Nani?

Mikaeli Yule Malaika Mkuu Ni Nani?

Maoni ya Biblia

Mikaeli Yule Malaika Mkuu Ni Nani?

KULINGANA na Biblia, kuna mamilioni ya malaika wanaoishi katika makao ya kiroho. (Danieli 7:9, 10; Ufunuo 5:11) Kutoka mwanzo hadi mwisho, Maandiko mara nyingi hurejezea malaika walio waaminifu kwa Mungu. Hata hivyo, ni wawili tu kati ya viumbe hao wa kiroho wanaotajwa kwa majina. Mmoja wao ni malaika Gabrieli, aliyewapelekea watu watatu tofauti-tofauti ujumbe kutoka kwa Mungu kwa kipindi cha miaka 600 hivi. (Danieli 9:20-22; Luka 1:8-19, 26-28) Malaika mwingine anayetajwa kwa jina katika Biblia ni Mikaeli.

Bila shaka, Mikaeli ni malaika mwenye cheo cha pekee. Kwa mfano, katika kitabu cha Danieli, Mikaeli anatajwa kuwa anapigana na roho waovu kwa niaba ya watu wa Yehova. (Danieli 10:13; 12:1) Katika barua iliyopuliziwa ya Yuda, Mikaeli amshambulia Shetani katika bishano juu ya mwili wa Musa. (Yuda 9) Kitabu cha Ufunuo chaonyesha kwamba Mikaeli alipigana na Shetani na malaika zake na kuwavurumisha chini kutoka mbinguni. (Ufunuo 12:7-9) Hakuna malaika mwingine yeyote anayeonyeshwa kuwa mwenye uwezo na mwenye mamlaka kubwa kama hiyo juu ya maadui wa Mungu. Basi, si ajabu kwamba Biblia kwa kufaa inamtaja Mikaeli kama “yule malaika mkuu.”

Ubishi Kuhusu Mikaeli

Dini za Jumuiya ya Wakristo na vilevile dini ya Kiyahudi na ya Kiislamu, zina maoni yanayotofautiana kuhusu malaika. Baadhi ya maoni yao hayaeleweki. Kwa mfano, kamusi ya The Anchor Bible Dictionary inaeleza: “Huenda kuna malaika mmoja mkuu na/au kikundi kidogo cha malaika wakuu (kwa kawaida wanne au saba).” Kulingana na kamusi ya The Imperial Bible-Dictionary, Mikaeli ni “jina la kiumbe mwenye uwezo unaozidi ule wa wanadamu, ambaye watu wamekuwa na maoni mawili yanayopingana kumhusu, eti huenda yeye ni Bwana Yesu Kristo, Mwana wa Mungu, au kwamba yeye ndiye mmoja wa wale waitwao malaika wakuu saba.”

Katika desturi za Kiyahudi, malaika hao wakuu saba ni, Gabrieli, Yeremieli, Mikaeli, Ragueli, Rafaeli, Sarieli, na Urieli. Kwa upande mwingine, Waislamu wanaamini katika malaika wakuu wanne, Jibril, Mikal, Izrail, na Israfil. Wakatoliki pia wanaamini katika malaika wakuu wanne: Mikaeli, Gabrieli, Rafaeli, na Urieli. Biblia inasema nini? Je, kuna malaika wakuu wengi?

Jibu la Biblia

Katika Biblia, hakuna malaika mkuu mwingine anayetajwa ila Mikaeli, wala Maandiko hayatumii usemi “malaika mkuu” katika wingi. Biblia inamtaja Mikaeli kuwa yule malaika mkuu, kuonyesha kwamba ni yeye pekee aliye na cheo hicho. Kwa hivyo, inafaa kusema kwamba Yehova Mungu amempa mmoja tu wa viumbe wake wa mbinguni mamlaka yote juu ya malaika wengine wote.

Mbali na Muumba pekee, Yesu Kristo ndiye mtu mmoja tu mwaminifu anayetajwa kuwa na malaika wanaojitiisha chini yake. (Mathayo 13:41; 16:27; 24:31) Mtume Paulo alitaja wazi juu ya “Bwana Yesu” na “malaika zake wenye nguvu.” (2 Wathesalonike 1:7) Na Petro alisema hivi kumhusu Yesu aliyefufuliwa: “Yeye yuko kwenye mkono wa kuume wa Mungu, kwa maana alienda akishika njia yake kuelekea mbinguni; na malaika na mamlaka na nguvu vilifanywa kuwa vyenye kutiishwa kwake.”—1 Petro 3:22.

Ijapokuwa hakuna taarifa katika Biblia inayomtambulisha Yesu kwa wazi kuwa Mikaeli yule malaika mkuu, kuna andiko moja ambalo linamhusisha Yesu na cheo cha malaika mkuu. Katika barua yake kwa Wathesalonike, mtume Paulo alitabiri: “Bwana mwenyewe atashuka kutoka mbinguni akiwa na mwito wa kuamuru, akiwa na sauti ya malaika mkuu na kwa tarumbeta ya Mungu, na wale walio wafu katika muungano na Kristo watafufuliwa kwanza.” (1 Wathesalonike 4:16) Andiko hili linamtaja Yesu kama ambaye tayari amechukua mamlaka yake akiwa Mfalme wa Kimesiya wa Mungu. Hata hivyo, anazungumza kwa “sauti ya malaika mkuu.” Kumbuka pia kwamba, ana uwezo wa kufufua wafu.

Akiwa duniani kama mwanadamu, Yesu alifufua watu kadhaa. Kwa kufanya hivyo, alitumia mwito wa kuamuru. Kwa mfano, alipomfufua mwana wa mjane mmoja wa jiji la Naini, alisema: “Mwanamume kijana, nakuambia, Inuka!” (Luka 7:14, 15) Baadaye, kabla tu ya kumfufua rafiki yake Lazaro, Yesu ‘alipaaza kilio kwa sauti kubwa: “Lazaro, njoo huku nje!”’(Yohana 11:43) Lakini katika pindi hizi, Yesu alisema kwa sauti ya mwanadamu mkamilifu.

Baada ya Yesu kufufuliwa, alikwezwa kwenye “cheo cha juu zaidi” mbinguni akiwa kiumbe wa roho. (Wafilipi 2:9) Sasa ana sauti ya malaika mkuu kwani yeye si mwanadamu tena. Hivyo, wakati tarumbeta ya Mungu ilipowatolea mwito “wale walio wafu katika muungano na Kristo” wafufuliwe kwenda mbinguni, Yesu alitoa “mwito wa kuamuru,” lakini wakati huo “akiwa na sauti ya malaika mkuu.” Inafaa basi kufikia mkataa kwamba ni malaika mkuu pekee anayeweza kutoa mwito “akiwa na sauti ya malaika mkuu.”

Ni kweli kwamba kuna malaika wengine wenye vyeo vya juu, kama maserafi na makerubi. (Mwanzo 3:24; Isaya 6:2) Hata hivyo, Maandiko humrejezea Yesu Kristo aliyefufuliwa kuwa mkuu wa malaika wote—Mikaeli yule malaika mkuu.