Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ndoa Inapaswa Kuwa Muungano wa Kudumu

Ndoa Inapaswa Kuwa Muungano wa Kudumu

Ndoa Inapaswa Kuwa Muungano wa Kudumu

KUTOKANA na jinsi sinema nyingi zinavyomalizika hatuna budi kukata kauli kwamba ndoa ni lengo linalotamanika. Sinema nyingi humalizika mwanamume na mwanamke wanapopatana hatimaye, wanafunga ndoa, na kuishi ‘raha mustarehe’ baada ya hapo. Kwa kawaida, huo ndio mwisho wa hadithi.

Katika maisha halisi, ndoa si mwisho, bali ni mwanzo wa maisha mapya pamoja. Na yatumainiwa kwamba maneno haya ya Mhubiri 7:8 yatatimizwa: “Heri mwisho wa neno kuliko mwanzo wake.”

Muungano wa Kudumu

Busara inahitajika katika ndoa. Ni lazima ndoa iwe na msingi imara ili idumu na ifurahishe. La sivyo, mfadhaiko wa baada ya arusi utazidi ule wa kabla ya arusi. Mkristo hawezi kufunga ndoa na kufikiri: ‘Tusipofaulu, nitamtaliki.’ Anapaswa kuiona ndoa kuwa muungano wa kudumu.

Yesu alionyesha wazi kwamba ndoa ni muungano wa kudumu alipojibu swali moja kuhusu talaka. Alisema hivi: “Je, hamkusoma kwamba [Mungu] aliyewaumba wao kutoka mwanzo aliwafanya wa kiume na wa kike na kusema, ‘Kwa sababu hiyo mtu ataacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake, na hao wawili watakuwa mwili mmoja’? Hivi kwamba wao si wawili tena, bali mwili mmoja. Kwa hiyo, kile ambacho Mungu amefunga nira pamoja msiache mtu yeyote akitenganishe.”—Mathayo 19:4-6.

Baada ya Arusi

Katika maisha ya Mkristo, kujiweka wakfu kwa Mungu ndiyo hatua muhimu, kisha ndoa. Mtu anapojiweka wakfu kwa Mungu anamwahidi Muumba kwamba atashikamana naye kwa umilele wote, na ubatizo ni tangazo la hadharani la jambo hilo. Ndoa ni tangazo la hadharani kwamba mtu ameahidi kushikamana na mwenzi wake wa ndoa—kwa umilele wote. Haiwezekani kujiweka wakfu kwa Mungu wala kufunga ndoa huku mtu akiwa na mashaka makubwa. Kwa hiyo, ni muhimu kuchunguza vizuri imani, miradi, mitazamo, na mwelekeo wa yule unayetaka kufunga ndoa naye.

Arusi inapopangwa, ni muhimu kuonyesha fadhili, kuwafikiria wengine, na kuonyesha roho ya ushirikiano. Sifa hizo ni muhimu hata zaidi baada ya arusi ili kufanikisha ndoa. Wenzi waliofunga ndoa karibuni hupendana, lakini baadaye katika maisha yao ya ndoa wanapaswa kukumbuka sikuzote kwamba upendo “hautafuti masilahi yao wenyewe.” Upendo unapoonyeshwa mwaka baada ya mwaka “haushindwi kamwe.” (1 Wakorintho 13:5, 8) Upendo usioshindwa ukiwepo itakuwa rahisi kuonyesha matunda ya roho ya Mungu, yaani, ustahimilivu, fadhili, wema, upole, kujidhibiti, na kadhalika. Sifa hizo ni za lazima ili kufanikisha ndoa.—Wagalatia 5:22, 23.

Jambo gumu ni kuendelea kuonyesha sifa hizo baada ya arusi. Hata hivyo, utafaulu kuonyesha sifa hizo nzuri ukimpenda mwenzi wako wa ndoa, na ukiwa tayari kujitolea kwa niaba yake.

Yesu alisema kwamba amri kuu kwa wanadamu ni kumpenda Yehova, na amri ya pili ni, “Umpende jirani yako kama wewe mwenyewe.” (Mathayo 22:39) Jirani wa karibu zaidi wa mtu aliyefunga ndoa ni mwenzi wake wa ndoa, kwa kuwa hakuna jambo jingine lolote duniani linaloweza kuunganisha watu wawili kama ndoa.

Hata hivyo, muungano wa miili pekee hauwezi kuleta upatano wa kihisia. Muungano wa miili haufanyi watu wawili wapatane kimawazo. Ili uhusiano wa kingono ufurahishe kikamili, lazima kuwe na upendo wa moyoni na nia moja. Mara nyingi, kujitolea kwa niaba ya mwenzi wa ndoa ni jambo la lazima ili kufanikisha ndoa. Ni nani anayepaswa kujitolea kwa niaba ya mwingine? Je, ni mume au mke?

Kuonyesha Upendo na Heshima

Neno la Mungu linaamuru: “Katika kuonyeshana heshima iweni wenye kuongoza.” (Waroma 12:10) Ikiwezekana, jitolee kabla ya mwenzi wako kukuomba. Kwani, mwenzi wako hatathamini sana kile unachomfanyia unapokifanya tu baada ya kuombwa mara nyingi. Badala yake, wenzi wa ndoa wanapaswa kuzoea kuchukua hatua ya kwanza kuwaonyesha wenzi wao heshima.

Kwa mfano, mume ameamuriwa ‘ampe mke heshima kama chombo dhaifu zaidi, kile cha kike, kusudi sala zake zisizuiwe.’ (1 Petro 3:7) Mume asipomheshimu mke, hata sala zake kwa Mungu zitaathiriwa sana. Lakini, kumheshimu mke kunamaanisha nini? Maana yake ni kumfikiria kila wakati, kusikiliza maoni yake, na kumpa uchaguzi wa kwanza mara nyingi katika mambo mbalimbali. Na mke anaweza kumheshimu mume kwa njia iyo hiyo akijitahidi kuwa msaidizi anayemuunga mkono mume wake.—Mwanzo 21:12; Mithali 31:10-31.

Neno la Mungu linasema: “Waume wapaswa kuwa wakiwapenda wake zao kama miili yao wenyewe. Yeye apendaye mke wake ajipenda mwenyewe, kwa maana hakuna mtu aliyepata wakati wowote kuuchukia mwili wake mwenyewe; bali huulisha na kuutunza sana, kama vile Kristo pia alifanyiavyo kutaniko.” Kristo aliwapenda wafuasi wake kwa kadiri gani? Alikuwa tayari kufa kwa ajili yao. Biblia inasema pia: “Acheni kila mtu mmoja-mmoja kati yenu [waume] ampende hivyo mke wake kama yeye mwenyewe.” (Waefeso 5:28-33) Na Neno la Mungu linawaamuru wake ‘wawapende waume zao, . . . wakijitiisha wenyewe kwa waume zao wenyewe, ili neno la Mungu lisipate kusemewa kwa maneno yenye kuudhi.’—Tito 2:4, 5.

Vumilia Makosa

Watu wote hufanya makosa, kwa kuwa wote ni wasiokamilika. (Waroma 3:23; 5:12; 1 Yohana 1:8-10) Lakini badala ya kukazia makosa, tii ushauri huu wa Biblia: “Juu ya mambo yote, iweni na upendo wenye juhudi nyingi nyinyi kwa nyinyi, kwa sababu upendo hufunika wingi wa dhambi.” (1 Petro 4:8) Ni heri kusamehe na kusahau makosa madogo-madogo. Hata makosa mazito yanaweza kushughulikiwa hivyo. Andiko la Wakolosai 3:12-14 linasema hivi: “Jivikeni wenyewe shauku nyororo za huruma, fadhili, hali ya akili ya kujishusha chini, upole, na ustahimilivu. Endeleeni kuchukuliana mtu na mwenzake na kusameheana kwa hiari mtu na mwenzake ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika dhidi ya mwingine. Kama vile Yehova alivyowasamehe nyinyi kwa hiari, fanyeni hivyo nyinyi pia. Lakini, zaidi ya mambo haya yote, jivikeni wenyewe upendo, kwa maana huo ni kifungo kikamilifu cha muungano.”

Tusamehe makosa ya kawaida ya mwenzi wetu wa ndoa mara ngapi? Petro alimwuliza Yesu hivi: “‘Bwana, ni mara ngapi ndugu yangu atafanya dhambi dhidi yangu nami nimsamehe? Mpaka mara saba?’ Yesu akamwambia: ‘Nakuambia, si, Mpaka mara saba, bali, Mpaka mara sabini na saba.’” (Mathayo 18:21, 22) Kwa kuwa Yesu alisema maneno hayo kuwahusu watu wasiokuwa wenzi wa ndoa, msamaha ni muhimu hata zaidi kati ya wenzi wa ndoa.

Ijapokuwa mpango wa ndoa umeshambuliwa katika miaka ya karibuni, hautakoma kamwe kwa kuwa ni mpango wa Mungu na kila kitu anachoanzisha ni “chema sana.” (Mwanzo 1:31) Mpango wa ndoa hautaondolewa kana kwamba haufai tena. Na ndoa inaweza kufanikishwa, hasa ndoa za wale wanaoziheshimu na kuzitii amri za Mungu. Lakini swali ni: Je, wale watu wawili walioahidi kwamba watapendana na kutunzana, watatimiza ahadi hiyo waliyotoa siku ya arusi? Huenda ukahitaji kupambana sana ili utimize ahadi hiyo. Lakini ukijitahidi sana ndoa yako itakuwa yenye furaha!

[Sanduku katika ukurasa wa 10]

Talaka na Kutengana

Mungu aliye mwanzilishi wa ndoa alikusudia ndoa iwe muungano wa kudumu. Lakini, je, Maandiko yanamruhusu mtu kumtaliki mwenzi wake wa ndoa, na baadaye kuoa au kuolewa na mtu mwingine? Yesu alijibu swali hilo kwa kusema: “Nawaambia kwamba yeyote yule atalikiye mke wake, ila kwa sababu ya uasherati, na kuoa mwingine afanya uzinzi.” (Mathayo 19:9) Kukosa uaminifu katika ndoa ni msingi pekee wa talaka unaomweka mwenzi asiye na hatia huru kuoa au kuolewa na mtu mwingine.

Isitoshe, licha ya kuwatia moyo wenzi wa ndoa wasitengane, maneno ya Biblia katika 1 Wakorintho 7:10-16 yanataja mambo yanayoweza kusababisha watengane. Baada ya kujaribu sana kuokoa ndoa yao, wengine wamehisi kwamba hakuna namna isipokuwa kutengana. Maandiko yanakubali kutengana katika hali gani?

Hali moja ni kukataa kimakusudi kuandaa riziki. Mwanamume anapooa, anakubali daraka la kuwaruzuku mke na watoto wake. Mwanamume anayekataa kimakusudi kuruzuku familia yake “ameikana imani naye ni mbaya zaidi kuliko mtu asiye na imani.” (1 Timotheo 5:8) Kwa hiyo, kutengana kunawezekana.

Hali nyingine ni kutendewa kikatili. Kwa hiyo, ikiwa mwenzi mmoja humtendea mwenzi mwingine kwa ukatili, mwenzi anayeumizwa anaweza kuamua kutengana na mwenzi wake. (Wagalatia 5:19-21; Tito 1:7) “[Mungu] humchukia asiye haki, na mwenye kupenda udhalimu.”—Zaburi 11:5.

Mwamini anaweza kuamua kutengana na mwenzi wake pia ikiwa hali yake ya kiroho imo hatarini, yaani, uhusiano wake pamoja na Mungu. Nyakati nyingine upinzani wa mwenzi wa ndoa, labda kutia ndani kunyimwa uhuru, umemzuia mwamini asiweze kuendelea na ibada ya kweli. Kwa hiyo, baadhi ya waamini wameamua kutengana na wenzi wao kwa sababu hali yao ya kiroho ilihatarishwa. *Mathayo 22:37; Matendo 5:27-32.

Hata hivyo, iwapo mtu atamtaliki mwenzi wake kwa sababu ya hali hizo, hatakuwa huru kufunga ndoa na mtu mwingine. Biblia inasema kwamba msingi pekee wa talaka inayomweka mtu huru kuoa au kuolewa na mtu mwingine ni uzinzi au “uasherati.”—Mathayo 5:32.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 27 Soma kuhusu kutengana katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Novemba 1, 1988, ukurasa wa 22-23.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Ndoa inapaswa kuonwa kuwa muungano wa kudumu

[Picha katika ukurasa wa 10]

Yesu alisema tunapaswa kusamehe “mara sabini na saba”