Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Siku ya Arusi Ni Yenye Shangwe Licha ya Shughuli Nyingi

Siku ya Arusi Ni Yenye Shangwe Licha ya Shughuli Nyingi

Siku ya Arusi Ni Yenye Shangwe Licha ya Shughuli Nyingi

BIBLIA inaonyesha kwamba Ye- hova Mungu—anayewajua wana- damu vizuri kuliko mtu mwingi- ne yeyote—ndiye aliyefunganisha watu wawili wa kwanza katika ndoa. Alikusudia ndoa iwe msingi wa jamii ya wanadamu. (Mwanzo 2:18-24) Na katika Neno la Mungu, Biblia, kuna kanuni mbalimbali zinazoweza kutuongoza tunapopanga arusi.

Kwa mfano, Yesu alisema kwamba Wakristo wanapaswa ‘kumlipa Kaisari vitu vya Kaisari.’ (Mathayo 22:21) Kwa hiyo, wanapaswa kutii sheria ya nchi yao. Ndoa iliyohalalishwa inalinda haki za wale waliohusika, kama vile kuonyesha madaraka yanayohusu watoto (kutia ndani kuwaruzuku na kuwaelimisha) na haki za urithi. Hali kadhalika, kuna sheria zinazowalinda watu wasitendewe au wasitumiwe vibaya na wengine katika familia. *

Matayarisho

Watu wawili walioamua kufunga ndoa kulingana na sheria na kanuni za Biblia na vilevile sheria ya nchi, wanapaswa kufikiria mambo gani? Baadhi ya mambo yanayopasa kufikiriwa ni tarehe na sherehe ya arusi.

Kitabu kimoja kuhusu arusi kinasema: “Huenda maoni ya maarusi yasipatane na maoni ya wazazi wao na huenda wakasitasita kati ya kufuata mapendezi yao wenyewe au kufuata desturi za jamaa.” Suluhisho ni nini? “Hakuna suluhisho rahisi, bali ni muhimu kusikiliza wengine kwa busara, kuzungumzia matatizo, na kukubaliana. Watu huwa na hisia mbalimbali wakati kama huo, kwa hiyo kutumia busara na kuwafikiria wengine hurahisisha sana matayarisho.”—The Complete Wedding Organiser and Record.

Ijapokuwa wazazi wenye upendo wanaweza kuchangia sana shangwe ya siku ya arusi, wanapaswa kujihadhari wasiwalazimishe watoto wao kufuata mapendezi yao. Kwa upande mwingine, ijapokuwa maarusi ndio watakaofanya maamuzi ya mwisho, bado kuna faida kusikiliza ushauri unaofaa. Maarusi wanapoamua ni mapendekezo gani watakayofuata, inafaa wakumbuke ushauri huu wa Biblia: “Mambo yote yaruhusika kisheria; lakini si mambo yote yenye faida. Mambo yote yaruhusika kisheria; lakini si mambo yote yajengayo. Acheni kila mmoja afulize kutafuta sana, si faida yake mwenyewe, bali ya mtu yule mwingine.”—1 Wakorintho 10:23, 24.

Matayarisho yanahusisha mambo kama vile kutuma kadi za mwaliko na kupanga karamu. Katika kitabu chake Marriage for Moderns H. Bowman anasema hivi: “Matayarisho yakipangwa vizuri, kwa busara na kwa utaratibu, uchovu na mfadhaiko hautakuwa mwingi.” Anaonya hivi: “Hata kama matayarisho ni mazuri, bado watu watachoka kadiri fulani na ni jambo la busara kujitahidi iwezekanavyo kupunguza uchovu huo.”

Kutakuwa na kazi mbalimbali na ni lazima wageni washughulikiwe. Je, familia na marafiki wanaweza kusaidia? Je, maarusi wangeweza kuwaomba wengine wanaotegemeka wawasaidie na kazi mbalimbali ambazo si lazima wao wenyewe wafanye?

Gharama

Gharama zinapasa kukadiriwa kwa hekima. Si jambo la busara wala la upendo kutarajia maarusi au wazazi wao wajiingize katika deni ili kulipia gharama kubwa ya arusi. Wengi wanaoweza kufanya arusi kubwa wameamua kufanya arusi ya kiasi. Vyovyote vile, maarusi fulani wameona kuna faida kuandika orodha ya gharama iliyokadiriwa na orodha ya kiasi kilicholipwa. Pia, linaweza kuwa jambo zuri kuandika orodha ya tarehe ambazo shughuli mbalimbali zinapasa kuwa zimetekelezwa. Kujaribu kukumbuka mambo yote bila kuandika kunaweza kuleta wasiwasi.

Je, arusi itagharimu kiasi gani? Bei zinatofautiana mahali-mahali, lakini uwe unaishi wapi, ni jambo la hekima kujiuliza: ‘Je, tunaweza kulipa mambo yote ambayo tumepanga? Je, mambo hayo ni ya lazima?’ Tina, aliyeolewa karibuni, alisema hivi: “Mambo mengine yalionekana kuwa ‘ya lazima’ tulipopanga arusi, lakini baadaye tuliona kwamba hayakuwa ya lazima hata kidogo.” Fikiria ushauri huu wa Yesu: “Ni nani kati yenu atakaye kujenga mnara asiyeketi kwanza na kupiga hesabu ya gharama, ili aone kama ana kiasi cha kutosha kuukamilisha?” (Luka 14:28) Ikiwa huwezi kulipa mambo yote unayotaka, acha mengine. Hata kama una uwezo wa kufanya arusi kubwa, huenda ukaamua kufanya arusi ya kiasi.

Kiasi ambacho bibi-arusi huko Italia anakadiriwa kutumia kwa ajili ya arusi yake kilionyeshwa kwenye maonyesho ya bidhaa za arusi. Kupaka vipodozi na kutengeneza nywele, dola 450 za Marekani; kukodi gari la anasa, dola 300; kupiga picha ya video ya siku ya arusi, dola 600; kitabu cha kuwekea picha za arusi (bila picha), dola 125-500; maua, kuanzia dola 600; karamu, dola 45-90 kwa kila mtu; nguo ya arusi, kufikia dola 1,200. Kwa kuwa siku hiyo ni muhimu sana, si ajabu kwamba watu wanataka kuifanya iwe ya kipekee. Lakini hata uwe umeamua nini, mambo yote yanapasa kufanywa kwa busara.

Ijapokuwa baadhi ya watu hutumia fedha nyingi sana, wengine hufurahia kufanya arusi ya kiasi—au, hufanya hivyo kwa sababu hawana namna nyingine. Bibi-arusi mmoja alisema: “Tulikuwa mapainia [wahubiri wa wakati wote], nasi hatukuwa na fedha zozote, lakini hilo halikutusumbua. Mama-mkwe wangu alinunua kitambaa, na rafiki mmoja alinishonea nguo ya arusi. Mume wangu aliandika kadi za mwaliko kwa mkono, na rafiki Mkristo alituazima gari. Tulinunua vitu vilivyokuwa vya lazima kwa ajili ya karamu, na mtu fulani alitupatia divai. Arusi yetu haikuwa yenye mambo mengi lakini ilikuwa nzuri.” Bwana-arusi mmoja alisema kwamba familia na marafiki wanaposaidia, “gharama hupunguka sana.”

Hata hali yao ya uchumi iweje, wenzi wa ndoa Wakristo hujaribu kuepuka kupita kiasi, mtindo wa ulimwengu, au kujionyesha. (1 Yohana 2:15-17) Siku ya arusi inapasa kuwa ya shangwe. Ingehuzunisha kama nini, ikiwa mtu fulani angeshindwa kufuata kanuni za Maandiko zinazoonya kuhusu ulafi, ulevi; au, jambo jingine linaloweza kufanya ashindwe kuwa “asiyelaumika”!—Mithali 23:20, 21; 1 Timotheo 3:2.

Epuka mwelekeo wa kutaka kufanya arusi kubwa na bora kushinda arusi nyingine. Fikiria shela kubwa za bibi-arusi wawili katika nchi moja—shela moja ilikuwa na kipenyo cha meta 13 na uzito wa kilogramu 220; ile nyingine ilikuwa na urefu wa meta 300 na wasindikizaji 100 waliibeba. Je, kuiga majivuno kama hayo kungepatana na ushauri wa Biblia?—Wafilipi 4:5.

Je, Mila Zifuatwe?

Desturi za arusi hutofautiana katika nchi mbalimbali, kwa hiyo haiwezekani kuzungumzia zote. Maarusi wanapofanya uamuzi kuhusiana na desturi fulani, ingefaa wajiulize maswali haya: ‘Maana ya desturi hiyo ni nini? Je, inatokana na ushirikina wa kutakia mtu bahati nzuri au uwezo wa kuzaa—kama vile kuwarushia maarusi mchele? Je, inahusiana na dini ya uwongo au mazoea mengine yanayokatazwa katika Biblia? Je, inapita kiasi au inakosa upendo? Je, inaweza kuwaaibisha au kuwakwaza wengine? Je, ingetilia shaka madhumuni ya maarusi? Je, inaudhi?’ Ikiwa kuna shaka lolote kuhusiana na mambo hayo, ni heri kuepuka desturi hiyo inayotiliwa shaka na kuwajulisha wageni uamuzi huo.

Shangwe na Hisia za Moyoni

Katika siku ya arusi watu wanaweza kuwa na shangwe kuu au huzuni. Bibi-arusi mmoja alisema hivi: “Nilifurahi sana kwa kuwa matamanio yangu yote yalitimizwa.” Lakini bwana-arusi fulani anasema: “Ilikuwa siku mbaya na siku nzuri kupita zote maishani mwangu. Wakwe wangu walibubujika machozi kwa sababu nilichukua binti yao wa kwanza, na mke wangu alilia kwa sababu wazazi wake walilia, na mwishowe, hata mimi nililia kwa sababu sikuweza kuvumilia hayo yote.”

Usiwe na wasiwasi iwapo hali kama hizo zitatokea—hizo husababishwa na mfadhaiko. Wala haipasi kushangaza kwamba uhusiano kati ya watu wa familia, au hata kati ya maarusi, huathiriwa nyakati nyingine. Kitabu cha The Complete Wedding Organiser and Record kinasema: “Labda hiyo ni mara yao ya kwanza kupanga tukio kuu pamoja, na bila shaka hekaheka itaathiri uhusiano wao kwa njia moja au nyingine. Hakuna haja kuudhika ikiwa mambo hayatakuwa shwari; ni afadhali kuomba ushauri na msaada.”

Bwana-arusi mmoja alisema: ‘Ningalithamini sana kuwa na mtu wa kunishauri ambaye ningaliweza kumtumaini na kumweleza hisia zangu za moyoni.’ Mshauri mzuri ni rafiki mkomavu au mtu wa ukoo mkomavu, au mtu mwingine mwenye ujuzi katika kutaniko la Kikristo.

Wazazi wataona fahari na shangwe mtoto wao anapoondoka nyumbani, lakini huenda pia wakahisi wasiwasi. Hata hivyo, wanapaswa kutambua kwamba wakati umewadia kwa mtoto wao ‘kumwacha baba yake na mama yake,’ naye ataambatana na mwenzi wake, na hao wawili “watakuwa mwili mmoja,” kama vile Muumba alivyokusudia. (Mwanzo 2:24) Mama mmoja anaeleza jinsi alivyohisi wakati mwana wake wa kwanza alipooa: “Nililia machozi, lakini machozi yangu hayakuwa ya huzuni tu bali pia ya furaha kwa sababu nilipata binti mpendwa, yaani, mke wa mwanangu.”

Ili siku ya arusi iwe ya kupendeza na kujenga, ni lazima wazazi—na vilevile maarusi—waonyeshe sifa za Kikristo za ushirikiano, utulivu, uvumilivu, na kuwafikiria wengine.—1 Wakorintho 13:4-8; Wagalatia 5:22-24; Wafilipi 2:2-4.

Baadhi ya bibi-arusi wana wasiwasi mwingi sana kwamba mambo yatakwenda kombo katika siku yao ya arusi. Wanahofu kwamba gurudumu la gari litaishiwa pumzi na watachelewa, hali ya hewa itakuwa mbaya sana, au nguo ya arusi itaharibika kabisa dakika ya mwisho. Yaelekea mambo hayo hayatatukia. Hata hivyo, kumbuka kwamba mipango yote haiwezi kufanikiwa kikamili. Vikwazo vitakuwapo. (Mhubiri 9:11) Uwe na mtazamo unaofaa, na jambo fulani likienda kombo, usife moyo. Kumbuka kwamba, baada ya miaka mingi huenda ukacheka ukilisimulia. Usiruhusu hitilafu ndogo ziharibu shangwe ya arusi.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Sheria katika nchi mbalimbali inakataza ndoa ya wake au waume wengi, kufanya ngono na maharimu, ulaghai, ujeuri katika ndoa, na ndoa ya vijana ambao hawajafikia umri wa kisheria wa kufunga ndoa.

[Blabu katika ukurasa wa 7]

“Mambo mengine yalionekana kuwa ‘ya lazima’ tulipopanga arusi, lakini baadaye tuliona kwamba hayakuwa ya lazima hata kidogo.”—TINA, BIBI-ARUSI MMOJA

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 7]

ORODHA YA MATAYARISHO *

Miezi 6 au zaidi kabla ya arusi

Zungumzia mipango pamoja na yule unayetaka kufunga ndoa naye, wakwe, na wazazi

Amua aina ya arusi mnayotaka

Hesabu gharama

Chunguza matakwa ya kisheria

Weka nafasi mapema ya mahali pa karamu

Fanya mpango kuwe na mpiga picha

Miezi 4

Chagua (kati ya nguo ulizo nazo), ununue, au ushoneshe nguo za arusi

Agiza maua

Chagua na agiza kadi za mwaliko

Miezi 2

❑ Tuma kadi za mwaliko

❑ Nunua pete

❑ Tafuta vyeti vinavyohitajika

Mwezi 1

❑ Vaa nguo za arusi ili kuhakikisha zinafaa

❑ Hakikisha kwamba miadi na maagizo yataweza kutekelezwa

❑ Andika barua ili kushukuru kwa ajili ya zawadi ambazo mmepokea tayari

Majuma 2

❑ Anza kuvipeleka vitu vyako kwenye makazi mapya

Juma 1

❑ Hakikisha kwamba wasaidizi wote wanaelewa wajibu wao

❑ Panga jinsi vitu vyote vilivyoazimwa na kukodiwa vitakavyorudishwa

❑ Omba wengine wasaidie na kazi nyingi iwezekanavyo

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 31 Orodha hii inaweza kurekebishwa kulingana na matakwa ya kisheria na hali za kila mtu.

[Picha katika ukurasa wa 8]

“Kile ambacho Mungu amefunga nira pamoja msiache mtu yeyote akitenganishe”