Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Ibilisi Ni Kiumbe Halisi?

Je, Ibilisi Ni Kiumbe Halisi?

Je, Ibilisi Ni Kiumbe Halisi?

WATU wengi wa dini wamekuja kumwona Ibilisi kuwa tu ushirikina wa kale, na kwamba alibuniwa na wanadamu. Kwa hiyo, Dionigi Tettamanzi, askofu mkuu wa Genoa—mmojawapo wa maaskofu wenye cheo cha juu huko Italia—alisababisha ubishi mkali kwa kuandika barua yake yenye kurasa 40 inayoonyesha jinsi ya kumpinga Ibilisi. Katika barua hiyo aliorodhesha “amri 10.”

Ya kwanza: “Usisahau kamwe kwamba ibilisi ni kiumbe halisi,” kwa kuwa “udanganyifu wake mkuu” ni “kutufanya tusiamini kwamba yeye ni kiumbe halisi.”

Ya pili: “Usisahau kwamba ibilisi ni mshawishi. . . . Usifikiri kwamba hataweza kukushawishi au kukudhuru.”

Ya tatu: “Usisahau kwamba ibilisi ana akili nyingi na ni mwerevu. Anaendelea kuwadhuru watu kwa kuwashawishi, kama alivyofanya na mwanadamu wa kwanza.”

Ya nne: “Kaa macho: kihalisi na moyoni. Na uwe imara: katika azimio na uadilifu.”

Ya tano: “Amini kabisa kwamba Kristo atamshinda mshawishi” kwa kuwa ukiamini “utakuwa thabiti na mtulivu hata ukishambuliwa vikali sana.”

Ya sita: “Kumbuka kwamba utashiriki katika ushindi wa Kristo.”

Ya saba: “Endelea kusikiliza Neno la Mungu.”

Ya nane: “Uwe mnyenyekevu na ukubali kuaibishwa.”

Ya tisa: “Sali sikuzote, bila kuchoka,” ili kushinda kishawishi.

Ya kumi: “Mpende Bwana Mungu wako na umwabudu yeye pekee.”

Barua hiyo ilikuwa na matokeo gani? Ushauri huo haukupendwa na watu wa Kituo cha Masomo ya Theolojia huko Milan. Kituo hicho kilibisha kwamba ‘hayo ni mambo ambayo watu waliamini zamani za kale.’ Kulingana na msemaji mmoja, “kumlaumu ibilisi kunaweza kuwafanya watu wasijilaumu [wenyewe] wanapofanya makosa.”

Ijapokuwa Biblia haiwaondolei watu lawama, inaonyesha wazi kwamba Shetani Ibilisi ndiye “mungu wa huu mfumo wa mambo,” aliyemshawishi Yesu. Inafunua pia mamlaka ya Shetani na lengo lake la ‘kupofusha akili za wasioamini.’—2 Wakorintho 4:4; Mathayo 4:1-11.

Naam, kama vile mtume Petro alivyoandika, Shetani ni “kama simba anayenguruma, akitafuta sana kunyafua mtu fulani.” (1 Petro 5:8) Si ajabu kwamba mtume Yohana aliwakumbusha waamini hivi: “Ulimwengu mzima unakaa katika nguvu ya mwovu.” (1 Yohana 5:19) Tukiwa watu wenye busara hatutapuuza maonyo hayo ya Maandiko.