Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Matumaini Yangu Yalivyotimizwa

Jinsi Matumaini Yangu Yalivyotimizwa

Jinsi Matumaini Yangu Yalivyotimizwa

IMESIMULIWA NA ALENA Z̆ITNÍKOVÁ

Nilipolelewa nchini Chekoslovakia, iliyokuwa chini ya utawala wa Sovieti, familia yetu ilitamani kuona ulimwengu wa amani ulioahidiwa na Ukomunisti. Hata hivyo, lengo la Wakomunisti la kuleta maisha yenye furaha na umoja lilikoma wakati Muungano wa Sovieti ulipovunjika mwaka wa 1991. Acha nieleze jinsi matazamio yangu yalivyotimizwa kwa njia tofauti sana.

NILIZALIWA Septemba 12, 1962. Wazazi wangu walikuwa Wakomunisti thabiti na tuliishi katika kijiji cha Horní Benešov, umbali wa kilometa 290 hivi kutoka Prague. Baba yangu aliamini kabisa malengo ya Ukomunisti naye aliishi kulingana nayo. Alinilea mimi na ndugu zangu wawili na dada yangu kulingana na malengo hayo. Alitufundisha kwamba kama tungefanya kazi kwa bidii na kuwa na mwenendo mzuri maishani, tungeweza kusaidia kujenga jamii bora. Aliona Ukomunisti kuwa utawala bora na aliuunga mkono kabisa.

Mara nyingi Baba alihudhuria mikutano iliyotukuza Ukomunisti. Alidharau dini kwa sababu ya unafiki wa makanisa, nasi tulifundishwa na tukaamini kwamba hakuna Mungu. Baba aliamini kwamba iwapo watu wote wangepewa chakula cha kutosha na makao, wangekuwa watu bora na wangeishi kwa amani. Nilisikia mengi kuhusu tumaini hilo zuri nilipokuwa mtoto. Niliamini yote ambayo Baba alitufundisha, nami pia niliazimia kuunga mkono Ukomunisti.

Nilipokuwa msichana mdogo, nilijitayarisha kuwa mshiriki wa shirika maarufu la vijana Wakomunisti. Washiriki walihimizwa wakuze sifa nzuri na wawe wazalendo. Nilipokuwa na umri wa miaka tisa, nilikula kiapo, na nilipewa kitambaa chekundu. Niliruhusiwa pia kuvaa mavazi rasmi ya shirika hilo wakati wa sherehe za pekee. Nilijaribu sana kuwa mshiriki bora. Niliposikia wanafunzi wenzangu wakitumia matusi, niliwakemea na kuwakumbusha kwamba wasichana wa shirika letu hawapaswi kutumia maneno hayo.

Hata hivyo, punde si punde, nilianza kuona kwamba wengi waliojidai kuwa Wakomunisti hawakuunga mkono malengo ya Ukomunisti. Hawakujaribu kushinda sifa zao mbaya za pupa na wivu, bali waliiba mali za umma. Ijapokuwa wengi waliwatia wengine moyo wajitolee kufanya kazi ya maendeleo, wao wenyewe walikataa kufanya kazi hiyo. Usemi huu ukawa maarufu: “Mtu asiyeiba, hunyima familia yake.” Nilianza kujiuliza, ‘Kwa nini kuna unafiki mwingi hivyo? Kwa nini ni watu wachache sana wanaofanya kazi ili kuendeleza malengo mazuri ya Ukomunisti? Kwa nini hakuna maendeleo?’

Kujifunza Mambo Mapya

Nilipokuwa na umri wa kati ya miaka 14 na 17 hivi, nilikuwa nikimtembelea mwanafunzi mwenzangu, Alena, kila mwaka wakati wa likizo. Rafiki mmoja wa Alena anayeitwa Tanya alikuja kututembelea usiku mmoja. Alisema hivi: “Ninataka kuongea nanyi juu ya jambo muhimu sana. Nimesadikishwa kwamba kuna Mungu.” Tulishangaa kusikia kwamba amefikia uamuzi huo. Baada ya kutulia, tulimuuliza maswali mengi sana. “Je, unaweza kuthibitisha jambo hilo?” “Ana umbo la aina gani?” “Anaishi wapi?” “Kwa nini huyo Mungu hawasaidii wanadamu?”

Tanya alijibu maswali yetu yote. Alieleza kuhusu kusudi la awali la Mungu la kufanya dunia iwe makao ya kiparadiso kwa wanadamu na jinsi kusudi hilo litakavyotimizwa hatimaye. Alipotuonyesha ahadi za Biblia kuhusu dunia safi itakayokaliwa na watu wanaopendana, wenye mwenendo bora na afya nzuri, nilitambua kwamba ahadi hizo zilifanana na ahadi zile nilizoamini. Lakini nilijua kwamba Baba hangefurahi iwapo angeambiwa kwamba ni Ufalme wa Mungu utakaoleta hali hizo wala si Ukomunisti.

Nilipokuwa na umri wa miaka saba hivi, msichana jirani alinipeleka kanisani bila wazazi wangu kujua. Padri alisimulia hadithi moja ya Biblia, nami niliipenda sana hivi kwamba nilitaka kujua zaidi. Hata nilipata vichapo vingine vya kidini. Nilipowaambia wazazi wangu, walinikataza katakata nisiende kanisani tena na waliharibu vichapo vyote ambavyo nilikuwa nimeleta nyumbani. Ili kuhakikisha kwamba nimeelewa, Baba alinichapa viboko.

Baada ya hapo, Mungu hakutajwa kamwe nyumbani kwetu. Nikaamini kuwa ni watu wa hali ya chini wasio na elimu wanaomwamini Mungu na kwamba dini ilibuniwa na mwanadamu. Huko shuleni tulifundishwa kwamba wanadamu wamebuni Mungu kwa sababu kuna mambo mengi ambayo hatuwezi kuelewa. Lakini kumbe, Tanya, mwanamke mwenye akili—tena mwalimu—alimwamini Mungu! Nikajua kwamba huo hauwezi kuwa uwongo mtupu.

Tanya aliongea kwa usadikisho hivi kwamba tuliona kuwa aliamini kile alichotuambia. Kwa hiyo, tukamwuliza hivi: “Tanya, ni nini kilichokusadikisha kwamba kuna Mungu?”

“Biblia,” akajibu. “Maswali yote ambayo mmeniuliza yanajibiwa katika Biblia. Je, mngependa kuielewa vizuri zaidi?”

Nilijua kwamba wazazi wangu hawangefurahia iwapo ningeanza kujifunza Biblia. Hata hivyo, nilitamani sana kujua mengi zaidi. Kwa hiyo, Tanya alinipa anwani ya Ludmila, mmoja wa Mashahidi wa Yehova aliyeishi karibu na kwetu huko Horní Benešov. Nilipochunguza ahadi za Mungu kuhusu dunia-paradiso pamoja na Ludmila nilikuwa nikijiuliza, ‘Ni nini kinachonithibitishia kwamba hayo yote yatatimizwa?’

Ludmila alisema kwamba nilihitaji kujifunza zaidi kumhusu Mungu ili kumwamini yeye na ahadi zake. Nilipoendelea kujifunza nilisadikishwa kwamba dunia, na mimea na viumbe wote duniani hawakutokea tu. Ilinibidi kukubali kwamba kuna Muumba mwenye akili nyingi sana. Nilitambua ukweli wa maneno haya ya Biblia: “Kila nyumba imejengwa na mtu fulani, lakini yeye aliyejenga vitu vyote ni Mungu.”—Waebrania 3:4.

Nilitaka watu wa familia yangu wajue hayo yote. Lakini, niliwaza kwamba hawangependezwa, kwa hiyo niliahirisha kuwaeleza. Kisha siku moja, miongoni mwa vitu vyangu, mama yangu akapata ukurasa mmoja wa Biblia kuukuu niliyokuwa nimepewa. Wazazi wangu walifadhaishwa sana.

Mazungumzo Pamoja na Baba

Baada ya kujua kwamba nilikuwa nikishirikiana na Mashahidi wa Yehova, Baba alinialika twende matembezi. Alinihimiza hivi: “Ni lazima uache kushirikiana na watu hao mara moja. Usipofanya hivyo, sitaweza kuendelea kuwa meya wa kijiji chetu. Itanibidi kuacha kazi. Nitalazimika kuacha kazi ya ofisi na kurudia kazi niliyofanya hapo awali katika kiwanda. Utaaibisha familia yetu.”

“Lakini, Baba, Biblia ni kitabu chenye hekima, na kina ushauri mzuri sana kuhusu maisha,” nikamsihi.

Baba alisema, “La, Alenka, sijahitaji kamwe Biblia wala Mungu ili niwe na furaha. Mimi mwenyewe nimefanya yote kwa mikono yangu. Hakuna aliyenisaidia. Nashangaa kwamba unaweza kuamini upuuzi huo! Kwanza, ni lazima uishi maisha halisi, uolewe, na uwe na watoto, kisha utaona kwamba huhitaji Mungu ili uwe na furaha.”

Msimamo wa Baba usioyumbayumba uliniathiri. Nilianza kuwa na shaka kwa kuwa imani yangu haikuwa thabiti bado. Nilikuwa nimemjua baba yangu kwa muda mrefu kuliko nilivyokuwa nimewajua Mashahidi wa Yehova, na sikuzote nilikuwa salama nyumbani. Nilijua Baba hakuwa na nia mbaya. Nilijua alinipenda, kwa hiyo nilimwahidi ningeacha kujifunza Biblia. Punde baadaye, nilipokuwa na umri wa miaka 18, nilimaliza shule na nilikwenda kufanya kazi huko Prague, mji mkuu wa nchi yetu.

Maisha Yangu Jijini Prague

Nilipata kazi katika benki, na nilitarajia kwa hamu kuishi yale maisha halisi ambayo Baba alisema Ukomunisti ungetuletea. Hata hivyo, punde si punde niligundua kwamba watu wa mjini hawakuwa na furaha zaidi ya wale wa kijijini. Badala yake, ukosefu wa maadili, unafiki, ubinafsi, na ulevi yalikuwa mambo ya kawaida.

Hatimaye, Shahidi mmoja, aliyeishi karibu na kwetu huko Horní Benešov, alitembelea Prague naye alipanga Mashahidi wanitembelee. Kwa hiyo, nilianza tena kujifunza Biblia huko Prague pamoja na mwanamke aliyeitwa Eva. Baada ya kila kipindi cha funzo Eva aliniuliza, “Je, unataka nije juma lijalo?” Hakunilazimisha kamwe kukubali maoni yake, ijapokuwa mara nyingine nilimuuliza angefanya nini kama angekuwa mimi.

“Siwezi kukuambia jambo la kufanya,” alisema. Alinionyesha jambo fulani katika Biblia lililonisaidia kufanya uamuzi. Uhusiano wangu pamoja na wazazi wangu ulinihangaisha sana, kwa hiyo nilimwuliza Eva kama ingekuwa afadhali niache kushirikiana nao. Alinionyesha andiko la Biblia la Kutoka 20:12, linalosema kwamba ni lazima tuwaheshimu wazazi wetu. Kisha akaniuliza, “Hata hivyo, je, kuna yeyote ambaye tunapaswa kumheshimu zaidi ya wazazi wetu?”

Kwa kuwa sikujua jibu, alifungua Biblia na kunionyesha maneno haya ya Yesu Kristo: “Yeye aliye na shauku kubwa zaidi kwa baba au mama kuliko kwangu hanistahili mimi.” (Mathayo 10:37) Kwa hiyo, nikaelewa kwamba ijapokuwa wazazi wangu wanastahili heshima, Yesu, na vilevile Baba yake wa mbinguni, wanastahili upendo mwingi hata zaidi. Eva alijaribu sikuzote kunionyesha kanuni ya Biblia, kisha akaniacha nijiamulie mwenyewe.

Miradi Isiyopatana

Hatimaye, mnamo Septemba 1982, nilikubaliwa kuwa mwanafunzi wa masomo ya kilimo kwenye chuo kimoja cha Prague. Hata hivyo, punde niligundua kwamba singeweza kukaza fikira ifaavyo kwa masomo yangu chuoni na wakati huohuo kujifunza Biblia kwa kadiri nilivyotaka. Kwa hiyo, nilimwambia profesa mmoja kwamba nilitaka kuacha chuo. “Nitakutuma kwa mtu ambaye anaweza kukuelewa na kukusaidia,” akasema. Alipanga mshauri wa wanafunzi wa chuo azungumze nami.

Mshauri huyo alinikaribisha na kuniuliza: “Ni kwa nini mwanafunzi wetu bora anataka kuacha shule?”

“Kwa sababu sina wakati wa kufanya mambo mengine ambayo ninapendezwa nayo,” nikajibu. Kwa kuwa Mashahidi wa Yehova walikuwa wamepigwa marufuku nchini Chekoslovakia, sikutaka kumwambia sababu yenyewe. Lakini baada ya kuongea naye kwa muda wa saa mbili hivi, nilidhani anaaminika. Kwa hiyo, nilimwambia kwamba nilikuwa nikijifunza Biblia.

Alisema: ‘Jifunze Biblia na Umaksi, kisha ufanye uamuzi.’ Ilionekana kana kwamba alinitia moyo nijifunze Biblia!

Njama Ilishindwa

Hata hivyo, kesho yake, yeye na yule profesa walisafiri hadi katika kijiji chetu ili kuwatembelea wazazi wangu. Waliwaonya wazazi wangu kwamba nilikuwa mshiriki wa madhehebu hatari ambayo imepigwa marufuku, na kuwaambia kwamba nilitaka kuacha chuo. Mshauri wa chuo alimwahidi Baba hivi: “Iwapo binti yako ataamua kuacha shule, tutahakikisha kwamba hatapata kazi huko Prague, kisha atalazimika kurudi kwako na kuacha kushiriki na madhehebu hiyo.”

Niliacha shule mnamo Januari 1983. Rafiki yangu mmoja aliyejifunza Biblia pia, alinisaidia kukodi chumba cha mwanamke mmoja mzee. Sikujua kwamba mshauri huyo aliwatembelea wazazi wangu wala alichomwahidi Baba, kwa hiyo sikuelewa ni kwa nini nilishindwa kupata kazi. Mwanamke huyo mwenye nyumba pia hakuelewa jambo hilo. Kwa hiyo, bila kuniambia, alimwendea yule mshauri wa chuo na kumwuliza ni kwa nini niliacha shule.

“Jihadhari!” alimwonya. “Yeye ni mshiriki wa madhehebu hatari ya Mashahidi wa Yehova. Ndiyo sababu alilazimika kuacha shule. Lazima arudi nyumbani na aache kushirikiana na watu hao. Nitahakikisha hatapata kazi hapa Prague!”

Mwenye nyumba aliporudi nyumbani usiku huo, aliniita na kuniambia hivi: “Alenka, leo nilitembelea chuo chako.” Nilifikiri ningelazimika kufunga virago na kuhama usiku huohuo. Lakini aliniambia hivi: “Sikubaliani na mshauri huyo. Una haki ya kuwa na imani yako; jambo la maana ni mwenendo wako. Nitakusaidia kupata kazi.” Usiku huo, nilimshukuru Yehova kwa msaada wake.

Punde baadaye, Baba akaja Prague ili anipeleke nyumbani. Lakini wakati huo hakuweza kunisadikisha. Imani yangu katika Yehova na ahadi zake ilikuwa thabiti. Mwishowe, Baba alirudi nyumbani peke yake, na kwa mara ya kwanza maishani mwangu nilimwona akilia machozi. Tukio hilo lilinisaidia kumkaribia Yehova zaidi ijapokuwa nilichomwa moyoni. Nilitaka kuwa mali ya Yehova na kumtumikia. Kwa hiyo, katika Novemba 19, 1983, ili kuonyesha kwamba nimejiweka wakfu kwa Yehova nilibatizwa katika bafu ya nyumba moja huko Prague.

Uamuzi Wangu Ulibarikiwa

Punde si punde, nilianza kusaidia kutengeneza vichapo vya Mashahidi wa Yehova vilivyopigwa marufuku. Tulichukua hatua madhubuti za usalama, kwa kuwa tayari wengine walikuwa wamefungwa kwa sababu ya kufanya kazi hiyo. Kazi yangu ya kwanza ilikuwa kutengeneza nakala za Mnara wa Mlinzi za Kicheki kwa kutumia taipureta. Kisha nakala hizo ziligawiwa Mashahidi ili zitumiwe katika funzo la Biblia.

Baadaye, nilialikwa kujiunga na watu wengine kadhaa waliotengeneza vitabu katika nyumba fulani huko Prague. Karibu vitu vyote viliondolewa katika chumba kimoja, kisha tukaweka meza ndefu katikati ya chumba na kuitumia tulipokusanya kurasa za vichapo. Baadaye, kurasa hizo ziliunganishwa kwa gundi au kushonwa pamoja ziwe kitabu kimoja. Nilitamani kufanya kazi hiyo wakati wote.

Nilipokuwa mshiriki wa shirika la vijana Wakomunisti, nilijaribu kuwafundisha watoto wawe watu bora. Sasa ninaendelea kuwasaidia vijana, na nimewasaidia vijana kadhaa wawe watumishi wa Yehova waliobatizwa. Ijapokuwa hakuna yeyote bado katika familia yetu ambaye amekuwa Shahidi, nimepata baba na mama na ndugu na dada wengi wa kiroho, kama vile Biblia inavyoahidi.—Marko 10:29, 30.

Mnamo mwaka wa 1989, serikali ya kidemokrasia ilianza kutawala nchi yetu badala ya ile ya Kikomunisti. Kwa sababu ya badiliko hilo Mashahidi wa Yehova wamepata uhuru. Sasa tunaweza kukutana ili kujifunza Biblia bila kujificha, kuhubiri nyumba hadi nyumba bila kuhofu kukamatwa, na kusafiri ng’ambo ili kuhudhuria mikusanyiko ya kimataifa. Isitoshe, hatuhojiwi tena na polisi, hatukamatwi, wala hatutishwi!

Kutumikia Pamoja na Mume Wangu

Mwaka wa 1990, niliolewa na Mkristo mwenzangu, Petr. Mnamo Aprili 1992, tulitimiza lengo la kuwa mapainia, kama Mashahidi wanaohubiri wakati wote wanavyoitwa. Hatimaye, mnamo Juni 1994, tulialikwa kufanya kazi katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huku Prague. Siku hizi, kazi yetu ya kutengeneza vichapo vya Biblia na kuwasaidia watu kiroho hufanywa waziwazi katika sehemu zote za Jamhuri ya Cheki.

Miaka michache iliyopita, mimi na Petr tulifurahi mno wakati wazazi wangu walipotembelea ofisi yetu ya tawi, mahali ambapo sisi na watu wengine 60 huishi na kufanya kazi pamoja. Baada ya kuchunguza makao na ofisi zetu, Baba alisema hivi: “Naam, ninahisi kuna upendo wa kweli miongoni mwenu.” Nilifurahi sana kusikia maneno hayo.

Matumaini Yangu Yametimizwa

Tumaini letu la kupata maisha bora kupitia Ukomunisti lilikuwa tu ndoto za mchana. Historia ya wanadamu inaonyesha kwamba hata jitihada zinazofanywa kwa unyofu zimeshindwa kuleta maisha maadilifu duniani. Ninaamini kwamba bado kuna watu wengine wengi ambao wataelewa kuwa mwanadamu hawezi kuishi kwa furaha bila msaada wa Mungu.—Yeremia 10:23.

Mara nyingi, mimi hukumbuka jinsi Baba alivyonitakia “maisha halisi,” ambayo alitufundisha yataletwa na Ukomunisti. Hata hivyo, nimejifunza katika Biblia kwamba “uhai ulio halisi”—maisha katika ulimwengu mpya wa Mungu—ndiyo ahadi pekee ambayo wanadamu wanaweza kuitumaini. (1 Timotheo 6:19) Ninasema hivyo kwa kuwa, licha ya kuwa wenye dhambi na wasiokamilika, wale ambao wamejaribu kwa moyo wote kufuata mafundisho ya Biblia maishani mwao wamefaulu kuishi pamoja kwa amani. Wameshinda majaribio yote ya kuvunja umoja wao au uaminifu wao kwa Yehova, Mungu wao.

Nilitambua jambo hilo hasa wakati mimi na mume wangu tulipoalikwa kuhudhuria kuwekwa wakfu kwa ofisi mpya ya tawi ya Mashahidi wa Yehova karibu na Lviv, Ukrainia, mnamo Mei 19, 2001. Nilikutana na Mashahidi wengine huko, ambao walikuwa washiriki wa lile shirika la vijana Wakomunisti hapo awali. Hao walikuwa wameamini, kama mimi, kwamba Ukomunisti ungeleta amani ya kweli na umoja kwa wanadamu. Vladimir Grigoriev, anayetumikia katika ofisi ya tawi nchini Urusi pamoja na mke wake, alikuwa pia mshiriki wa shirika hilo hapo awali.

Sasa kuna ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova mahali ambapo shirika hilo lilikuwa na kambi. Kwa sababu hakukuwa na nafasi ya kutosha, ni watu 839 tu kutoka nchi 35 ndio walioweza kuhudhuria kuwekwa wakfu kwa ofisi hiyo ya tawi. Hata hivyo, watu 30,881 walikusanyika kwenye uwanja wa mpira huko Lviv, ili kusikiliza programu hiyo iliyorudiwa asubuhi iliyofuata. * Baadhi yao walitoka sehemu za mbali sana na walikuwa wamesafiri muda wa saa sita au zaidi ili wahudhurie.

Hata hivyo, watu hao waliposikia kwamba wangeweza kutembelea ofisi mpya ya tawi, walipanda mabasi, na waliwasili kwenye ofisi ya tawi alasiri ili kutembelea majengo hayo mapya. Mimi na mume wangu tulikuwa na pendeleo la kulala hapo. Zaidi ya waamini wenzetu wapendwa 16,000 walitembelea ofisi ya tawi siku hiyo, na kufikia jioni, wote walikuwa wameingia katika mabasi yao na kuanza safari ya kurudi makwao!

Huko Ukrainia, kama vile katika nchi nyingine za Ulaya Mashariki, mamilioni ya watu waliamini kwamba Ukomunisti ulikuwa njia bora ya kuleta jamii mpya yenye amani. Hata hivyo, leo, kuna zaidi ya watu 120,000 nchini Ukrainia wanaohubiri Ufalme wa Mungu. Wengi wetu tuliokuwa Wakomunisti hapo awali tumekuja kuamini kwamba serikali hiyo ya Mungu ndiyo itakayoleta udugu wa kweli na amani miongoni mwa watu wote!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 51 Watu wengine 41,143 walikusanyika wakati huohuo katika uwanja fulani huko Kiev—umbali wa kilometa 500 hivi—na kusikiliza programu ya kuweka wakfu ofisi ya tawi. Jumla ya idadi ya wahudhuriaji ilikuwa 72,024. Mashahidi wa Yehova hawajawahi kamwe kuwa na kusanyiko kubwa namna hiyo nchini Ukrainia.

[Picha katika ukurasa wa 12]

Nilipokuwa na umri wa miaka kumi, muda mfupi baada ya kujiunga na shirika la vijana Wakomunisti

[Picha katika ukurasa wa 16]

Mimi na mume wangu, Petr

[Picha katika ukurasa wa 16]

Vladimir, mshiriki wa shirika la vijana Wakomunisti hapo awali, niliyekutana naye wakati wa kuwekwa wakfu kwa ofisi ya tawi ya Ukrainia

[Picha katika ukurasa wa 16, 17]

Zaidi ya watu 30,000 walisikiliza pitio la programu ya kuweka wakfu siku iliyofuata

[Picha katika ukurasa wa 17]

Zaidi ya watu 16,000 walitembelea ofisi ya tawi