Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kufanya Mahala Pako pa Kazi Pawe Salama

Kufanya Mahala Pako pa Kazi Pawe Salama

Kufanya Mahala Pako pa Kazi Pawe Salama

LICHA ya kuwepo kwa sheria zinazohusu afya na usalama wa wafanyakazi, bado watu wengi hufa na kujeruhiwa kazini. Hivyo basi, ni wazi kwamba sheria pekee haziwezi kuleta usalama kazini. Waajiri na waajiriwa wana jukumu la kujilinda na kuwalinda wengine.

Kwa hiyo, wafanyakazi wote wanapaswa kuchunguza kwa makini mazingira na mazoea yao ya kikazi. Kwa mfano, je, umewahi kuchunguza iwapo mahala pako pa kazi ni salama? Je, wewe hutumia kemikali zenye sumu kazini? Ikiwa ndivyo, je, wewe hujilinda kabisa? Je, wewe hukabili mfadhaiko sikuzote? Je, wewe hukubali kufanya kazi kwa muda mrefu kuliko vile sheria inavyoruhusu au kufanya kazi inayokiuka mipaka iliyowekwa?

Majibu yako kwa maswali hayo yataonyesha iwapo uko salama kazini.

Kufahamu Hatari

Ni hatari kuendelea kujaribu kufanya kazi kupindukia. Baada ya kuchunguza matokeo ya utafiti uliohusu wafanyakazi milioni 3.6 na mahala 37,200 pa kazi, Profesa Lawson Savery wa Chuo Kikuu cha Curtin huko Australia pamoja na mtafiti mmoja, walichapisha uchunguzi wao wenye kichwa “Je, Ni Hatari Kufanya Kazi kwa Muda Mrefu? na Je, Watu Hukubali Kufanya Hivyo kwa Hiari?” Jibu la maswali hayo ni, ndiyo.

Wafanyakazi waliochoka hufanya makosa mengi na hawawezi kufanya kazi vizuri. Profesa Savery alisema hivi, kama ilivyoripotiwa katika gazeti la The Sun-Herald la Australia: “Makampuni mengi yaliwatia watu moyo kufanya kazi kupindukia na yalitafuta sana wafanyakazi wa aina hiyo na kuwalipa vizuri.” Matokeo ya kufanya kazi kupindukia yaweza kudhuru sana. Jambo hilo linaonekana sana katika biashara ya usafiri. Madereva hutiwa moyo au hata hulazimishwa kuendesha magari kwa muda mrefu bila kupumzika—jambo ambalo ni kinyume cha sheria katika nchi fulani.

Mazoea mabaya ya kazi, ambayo yanaweza kutia ndani ukosefu wa utaratibu na usafi, hutokeza hatari nyingine. Majeraha au hata vifo husababishwa mara nyingi kwa kuacha vifaa ovyoovyo sakafuni au nyaya za stima zikiwa hazijafunikwa. Ni hatari pia kupuuza kanuni za usalama unapotumia vifaa na mashine za stima. Jambo jingine linalosababisha watu waumie na kufa, ni kutosafisha sehemu zilizomwagikiwa na umajimaji—hasa umajimaji wenye sumu. Wafanyakazi wengi wamejeruhiwa kwa kuteleza kwenye sakafu zenye maji au mafuta. Hivyo, hatua ya kwanza ya kuwa mfanyakazi bora ni kudumisha mahala pa kazi pakiwa safi na penye utaratibu.

Hata hivyo, watu wengi huwa na mwelekeo wa kupuuza kanuni za usalama. Jarida la Monthly Labor Review lilisema hivi: “Watu wanapokuwa na kazi nyingi huenda wakafikiri kwamba wanaweza kumaliza kazi haraka kwa kuacha kufuata utaratibu wa kawaida wa kufanya kazi.” Hivyo, huenda wengine wakafikiri kwamba kupuuza kanuni fulani kwafaa kwani hawajawahi kamwe kupata matatizo yoyote kwa kuipuuza. Mkurugenzi mmoja wa kiwanda mwenye ujuzi alisema hivi alipozungumzia jambo hilo: “Mojawapo ya mambo mabaya zaidi ambayo mtu anaweza kufanya kazini ni kupuuza tahadhari na asiumie!” Kwa nini? Kwa sababu mtu asipoumia, hiyo itamfanya awe na uhakika kupita kiasi na asiyejali, hivyo atasababisha misiba mingi zaidi.

Mlipuko uliotokea kwenye kiwanda cha Chernobyl huko Ukrainia mnamo mwaka wa 1986 husemekana kuwa “msiba mbaya zaidi wa nyukilia ulimwenguni.” Msiba huo ulisababishwa na nini? Ripoti moja kuhusu msiba huo inataja visababishi kama vile ‘kutofuata utaratibu mbalimbali’ na “mazoea ya kupuuza tahadhari.”

Waajiri na waajiriwa wanaweza kushirikiana kutambua hatari zinazoweza kutokea. Mithali moja yenye hekima katika Biblia, husema hivi: “Mwenye busara huyaona mabaya na kujificha.” (Mithali 22:3) Naam, mwenye hekima hutambua mambo yanayoweza kusababisha hatari na kutafuta njia za kujilinda na kuwalinda wengine.

Waajiri wanapofanya hivyo, wao na vilevile waajiriwa wao hunufaika. Kwa mfano, kampuni moja iliyorekebisha jengo lake la ofisi ili kuepuka magonjwa yanayosababishwa na kemikali zenye sumu kwenye majengo, iligundua kwamba muda si muda ilipata mapato mengi na wafanyakazi wengi walifurahi. Pia, ni wafanyakazi wachache tu waliokosa kufika kazini kwa sababu ya ugonjwa. Kufikiria afya ya wengine kwa njia hiyo hufanya waajiri na waajiriwa wawe na mazingira yenye kupendeza na vilevile hutokeza faida za kiuchumi kama vile mfano huo unavyoonyesha.

Kama ilivyotajwa katika makala iliyotangulia, ujeuri umeongezeka kazini. Unaweza kufanya nini ili kujilinda?

Hatua Unazoweza Kuchukua

Hata visa vidogo vya uchokozi kazini vimetokeza visa vibaya zaidi vya mnyanyaso. Gazeti la Harvard Business Review linatoa shauri hili: “Unapojaribu kutatua tatizo hilo la ujeuri kazini, fahamu kwamba mara nyingi watu wanaofanya matendo madogo ya ujeuri hufanya matendo makubwa zaidi kama hayo baadaye.”

Huenda mwanamke asinuie kuwavutia wafanyakazi wengine. Lakini iwapo mwenendo, usemi, na mavazi yake si ya kiasi, wengine wanaweza kufikiri kwamba ana maadili mabaya. Katika siku za karibuni, mwenendo ambao haukukusudiwa kuvutia kingono, nyakati nyingine umetokeza matatizo makubwa kama vile, kufuatwa-fuatwa, kubakwa, au hata kuuawa. Basi fikiria jinsi mavazi na mwenendo wako unavyowaathiri wengine. Tii shauri hili la Biblia: ‘Jirembeni katika mavazi yenye mpangilio mzuri, pamoja na kiasi na utimamu wa akili.’1 Timotheo 2:9.

Gazeti la Monthly Labor Review lilionyesha hali nyingine inayoweza kusababisha hatari, liliposema hivi: “Kuna mahangaiko kuhusu watu wanaofanya kazi peke yao usiku katika maeneo yasiyokuwa na watu.” Hivyo, fikiria hili: Je, ni jambo la hekima ujihatarishe kwa kufanya kazi ukiwa peke yako, hasa usiku sana? Je, kuna faida kujihatarisha ili kupata pesa?

Ni muhimu pia kufikiria jinsi tunavyotenda wakati tunapokabili tabia zenye kuudhi na za ukatili za wafanyakazi wenzetu waliofadhaika. Ni jambo gani linaloweza kufanywa ili kutuliza hali inayoweza kusababisha hatari? Mithali moja ya Biblia yashauri hivi: “Jawabu la upole hugeuza hasira; bali neno liumizalo huchochea ghadhabu.” (Mithali 15:1) Naam, ukiwa mwenye fadhili na mwenye heshima, utakomesha hali ya kutoelewana na kuepuka mgogoro.

Katika ulimwengu huu wenye misongo mingi, watu wengi hutenda mambo ya kuudhi na ya kikatili. Ingawa huenda tukadhania kwamba mtu fulani anataka kutuudhi, labda anafanya hivyo tu kwa sababu amefadhaika kwa muda mrefu. Huenda ikawa tumejikuta tu mahala pabaya wakati usiofaa. Basi, jinsi tunavyotenda katika hali hiyo ni muhimu. Matendo yetu yaweza kutuliza au kuzidisha mgogoro.

Hata hivyo, huenda maoni yakatofautiana. Kitabu Resolving Conflicts at Work chataja jambo hili: ‘Mara nyingi tunapohusika katika mgogoro, hatusemi wazi jinsi tunavyohisi.’ Sababu yaweza kuwa nini? Kitabu hicho kiliendelea kusema hivi: “Migogoro inaweza kutuchanganya na kutuvuruga sana, hivi kwamba tunafikiri kwamba suluhisho ni vita tu.”

Basi suluhisho ni nini? SIKILIZA! Kitabu kilichonukuliwa kwenye ukurasa uliotangulia chasema hivi: ‘Tukiwasikiliza kabisa watu tunaohitilafiana nao, twaweza kutulia, kuacha mgogoro, na kutafuta masuluhisho.’ Hilo ni shauri zuri la kuzuia kutoelewana kusisitawi na kusababisha mapambano.

Hivyo basi, tumia busara ili uwe salama. Hiyo yatia ndani kujitahidi kutii kanuni za usalama zilizowekwa. Jambo hilo laweza kusaidia sana kufanya mahala pako pa kazi pawe salama.

Pia, mtazamo wetu juu ya maisha, kazi, na wasaa wa kustarehe unaweza kuathiri uchaguzi wetu wa kazi na maoni yetu kuhusu usalama. Makala ifuatayo inaweza kutusaidia kufanya uchaguzi unaofaa kuhusiana na hilo.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Safisha kabisa sehemu zilizomwagikiwa mafuta

[Picha katika ukurasa wa 7]

Jawabu la upole laweza kukomesha hali ya kutoelewana