Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maoni Yanayofaa Kuhusu Kazi

Maoni Yanayofaa Kuhusu Kazi

Maoni Yanayofaa Kuhusu Kazi

AFISA mmoja wa kijeshi aliyejitoa mhanga, alifanya kazi wakati wa chakula cha mchana ili amalize kazi iliyohitajiwa haraka na mkubwa wake. Wafanyakazi wenzake waliporudi baada ya chakula cha mchana, walimpata amelala juu ya dawati lake—akiwa amekufa.

Baada ya muda usiozidi saa mbili, maafisa wenzake walishtuka wakati mkubwa wao alipopiga simu na kusema: “Ninasikitika kuhusu yale yaliyompata———, lakini ninahitaji mtu wa kuchukua mahala pake kesho asubuhi!” Watu waliosikia maneno hayo walijiuliza hivi, Je, afisa huyo alithaminiwa na mkubwa wake kwa sababu tu ya kazi aliyofanya?

Kisa hicho cha kweli chaonyesha wazi jambo fulani—kwamba mara nyingi thamani ya mtu hupimwa tu kulingana na jinsi anavyomfaidi mwajiri wake. Hilo laweza kumfanya mtu ajiulize hivi: Je, kufanya kazi ndilo jambo la maana maishani mwangu ama mimi hufanya kazi ili nijiruzuku tu? Ni mambo gani ninayojinyima maishani kwa sababu ya kazi yangu?

Kufanya Uchaguzi Unaofaa

Mara nyingi, maamuzi mawili ambayo watu fulani huyaona kuwa muhimu zaidi maishani hufanywa bila kufikiri—uchaguzi wa mwenzi wa ndoa na uchaguzi wa kazi. Hapo zamani, kazi na ndoa zilionwa kuwa mambo ya kudumu. Hivyo, watu walifikiria sana kabla ya kufanya uchaguzi kuhusu mambo hayo. Mara nyingi, walitafuta ushauri wa wazazi na marafiki wenye umri mkubwa.

Hata hivyo, siku hizi watu wengi huchagua wenzi wa ndoa hasa kwa sababu ya sura inayovutia, huku wakiwaza kwamba ndoa hiyo isipofanikiwa, wanaweza kutafuta mwenzi mwingine. Vivyo hivyo, watu wengi huchagua kazi hasa kwa sababu ya mshahara mnono, bila kufikiria hatari zinazoweza kutokea. Au, wao hupuuza hatari hizo wakifikiri kwamba wataweza kuzishughulikia.

Inasikitisha kwamba wanawake katika nchi maskini mara nyingi hukubali kushawishiwa na matangazo yanayoahidi kazi na maisha ya kuvutia katika nchi nyingine. Hata hivyo, wanapofika katika nchi hizo, mara nyingi wao hupelekwa kwenye nyumba za makahaba ili wafanye kazi ya umalaya. Hivyo, maisha yao yanakuwa mabaya kuliko yalivyokuwa hapo awali. Makala moja ya gazeti la World Press Review yasema kwamba hali hiyo ya kulazimishwa kuwa malaya ‘haitaisha kamwe.’

Je, watu wanaweza kushawishiwa kwamba watapata kazi nzuri kisha wajihisi kuwa watumwa? Jambo hilo limetukia! Kwa mfano, makampuni fulani huwapa wafanyakazi mambo mengi ya anasa. Mambo hayo yaweza kutia ndani kuruhusiwa kutumia vyumba vya kula pamoja na familia na rafiki zao huko kazini, kuwasafirisha na kuwalipia huduma za dobi, kuwatolea huduma za madaktari wa meno, kutumia majumba ya mazoezi bila malipo, na kuwawezesha kula kwa bei nafuu katika mikahawa ya hali ya juu.

Mwandishi wa habari Richard Reeves anaripoti hivi: ‘Hata kampuni moja imelipia huduma za kuwatafutia wafanyakazi wake wapenzi.’ Lakini jihadhari! Reeves anasema hivi: ‘Wenye makampuni hayo huahidi mambo ya anasa ili kufanya maisha yako yawe rahisi maadamu utawaruhusu wakutawale; ufanye kazi kwa muda wa saa 18 kila siku kutia ndani miisho-juma, ule, ufanye mazoezi, ucheze, na hata ulale ofisini ili upatikane kwa urahisi ikiwa watakuhitaji.’

Kuchagua Kazi Inayofaa Zaidi

Mithali moja ya kale yasema hivi: “Afadhali mbwa aliye hai kuliko simba aliyekufa.” (Mhubiri 9:4) Mithali hiyo yatokeza swali hili, Je, inafaa nihatarishe uhai wangu au afya yangu kwa sababu ya kazi yangu? Watu wengi wamechunguza hali zao na wamepata njia ya kujiruzuku—na pia kuruzuku familia zao—na kuishi maisha yanayofurahisha na yenye kusudi.

Ili kufanya hivyo, mara nyingi mtu anahitaji kuwa na kiasi, na huenda ikambidi kufikiria yale ambayo anahitaji, badala ya mambo yasiyo ya lazima ambayo anataka. Huenda watu wanaotafuta cheo au ufanisi wakakataa kuchagua kazi ya hali ya chini na hata kuwadharau watu wanaochagua kazi ya aina hiyo. Lakini jambo la maana maishani ni nini? Je, umefikiria swali hilo hivi karibuni?

Mfalme Solomoni mwenye hekima, aliyeandika mithali iliyotajwa juu, alikuwa amefanikiwa kupata mali nyingi hata labda kuliko mwanadamu mwingine yeyote. Lakini alipoonyesha jambo la maana zaidi, yeye aliongozwa na Mungu kusema hivi: “Hii ndiyo jumla ya maneno; yote yamekwisha sikiwa; mche Mungu, nawe uzishike amri zake, maana kwa jumla ndiyo impasayo mtu.”—Mhubiri 12:13.

Kwa upande mwingine, Solomoni alithamini kazi. Alisema hivi: “Hakuna chema kimfaacho binadamu, isipokuwa kula na kunywa na kuifurahia kazi yake.” (Mhubiri 2:24, Biblia Habari Njema) Vivyo hivyo, Yesu Kristo, Solomoni Mkubwa Zaidi, anathamini kazi, na ndivyo ilivyo pia na Baba yake wa mbinguni. Yesu alisema hivi: “Baba yangu amefuliza kufanya kazi hadi sasa, na mimi nafuliza kufanya kazi.”—Yohana 5:17; Mathayo 12:42.

Hata hivyo, kwa sasa maisha ya mwanadamu ni mafupi. (Zaburi 90:10) Lakini Kristo alijua kwamba uhai wa milele duniani utawezekana chini ya utawala wa Ufalme, ambao aliwafundisha wanafunzi wake kuomba uje. Ndiyo sababu alisihi hivi katika Mahubiri yake maarufu ya Mlimani: “Basi, fulizeni kutafuta kwanza ufalme na uadilifu [wa Mungu], na vitu vingine vyote hivi mtaongezewa.”—Mathayo 6:9, 10, 33.

Biblia yaahidi hivi kuhusu maisha chini ya utawala wa Ufalme: “Watajenga nyumba, na kukaa ndani yake; watapanda mizabibu, na kula matunda yake. Hawatajenga, akakaa mtu mwingine ndani yake; . . . wateule wangu wataifurahia kazi ya mikono yao muda wa siku nyingi.”—Isaya 65:21, 22.

Ni taraja zuri kama nini—kufurahia kuishi milele pamoja na kuwa na kazi yenye kuridhisha na ya maana! Huenda tukichunguza hali zetu kwa uangalifu tutaona kwamba twahitaji kuzingatia mambo fulani kuhusu kazi yetu ili kuepuka hatari zinazoweza kutuzuia kufurahia “uhai ulio halisi”—uhai wa wakati ujao chini ya Ufalme wa Mungu. (1 Timotheo 6:19) Hivyo basi, tunapofanya kazi, au tunapofanya jambo jingine lolote, na tuonyeshe kwamba tunamheshimu Yule aliyetupatia uhai.—Wakolosai 3:23.

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Chini ya Ufalme wa Mungu, watu watafurahia kazi iliyo salama na yenye kuridhisha