Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nifanye Nini Nikikutana na Mwanafunzi Mwenzangu?

Nifanye Nini Nikikutana na Mwanafunzi Mwenzangu?

Vijana Huuliza . . .

Nifanye Nini Nikikutana na Mwanafunzi Mwenzangu?

“Sikutaka kurudi shuleni Jumatatu. Ikiwa mmoja wa rafiki zangu alikuwa ameniona, nilibuni hadithi fulani. Kwa mfano, nyakati nyingine niliwaeleza rafiki zangu kwamba nilikuwa nikiomba michango kwa ajili ya chama cha Labour Party.” —James, Uingereza.

“Nilidhihakiwa shuleni na vijana waliokuwa wameniona. Nilifadhaika sana.”—Débora, Brazili.

KWA nini vijana hao hawakutaka rafiki zao wawaone? Je, walikuwa wakifanya jambo lisilo halali? La, walikuwa wakifanya kazi njema iliyo muhimu zaidi duniani leo. Walikuwa wakifanya kazi iliyoamriwa na Yesu aliposema hivi: “Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, . . . kuwafundisha kushika mambo yote ambayo mimi nimewaamuru nyinyi.”—Mathayo 28:19, 20.

Kulingana na uchunguzi mmoja huko Marekani, zaidi ya asilimia 90 ya vijana wanamwamini Mungu. Karibu nusu ya vijana wote huenda kanisani kila juma. Lakini ijapokuwa vijana wengi hushiriki shughuli mbalimbali za kanisa, kama vile kuimba katika kwaya, ni wachache sana wanaoongea kumhusu Mungu pamoja na wanafunzi wenzao. Hata hivyo, Mashahidi wa Yehova wanajulikana ulimwenguni pote kwa kazi yao ya kuhubiri nyumba hadi nyumba. Maelfu ya Mashahidi wachanga hufanya kazi hiyo.

Ikiwa wewe ni Shahidi mchanga, bila shaka wewe pia hufanya kazi hiyo ya kuhubiri. Lakini huenda isiwe rahisi kwako kufanya hivyo. Kama vijana walionukuliwa hapa juu, huenda ukaogopa kukutana na mwanafunzi mwenzako unapohubiri nyumba hadi nyumba. Msichana mmoja Mwingereza anayeitwa Jennie anasema hivi: “Niliogopa sana kwamba mmoja wa wanafunzi wenzangu angeniona nikiwa nimebeba mkoba, nikiwa nadhifu kuliko nilivyovalia shuleni.”

Wakristo wengine wachanga wameogopa sana kukutana na mwanafunzi mwenzao hivi kwamba wametumia hila. Kijana anayeitwa Leon anasema hivi: ‘Ninamjua Shahidi mmoja mchanga anayefunika uso wake kwa ukaya wa koti yake akiwaona marafiki wa shule.’ Na vijana wengine hukataa kuhubiri katika mitaa fulani. Kijana anayeitwa Simon anasema hivi: “Ninakumbuka kwamba nilitoa sala na kuomba tusihubiri kwenye mtaa fulani kwa sababu wanafunzi wenzangu wengi waliishi huko.”

Ni jambo la kawaida kuona haya kidogo ukikutana na mtu unayemfahamu katika kazi ya kuhubiri. Hata hivyo, kuruhusu woga huo ukushinde, kwaweza kukuletea matokeo mabaya. Kijana mmoja Mjerumani anayeitwa Alicia anakiri hivi: “Nilikuwa na mtazamo mbaya sana kuhusu kuhubiri hivi kwamba hali yangu ya kiroho iliathiriwa.”

Hata hivyo, kwa nini ni lazima uhubiri ikiwa ni jambo gumu kwako? Tuone ni kwa nini Mungu ametuwekea wajibu huo. Baadaye tutazungumzia jinsi unavyoweza kushinda woga ukiamua na kujitahidi kufanya hivyo.

Wajibu wa Kuhubiri

Kwanza, huenda ukafaidika kujua kwamba si jambo jipya wala jambo geni kuongea na wengine kuhusu imani yako. Watu wanaomcha Mungu wamefanya hivyo tangu zamani. Kwa mfano, Noa anajulikana hasa kwa kujenga safina kubwa mno. (Mwanzo 6: 14-16) Lakini kulingana na 2 Petro 2:5, alikuwa pia “mhubiri wa uadilifu.” Noa aliona kwamba alikuwa na wajibu wa kuwaonya wengine kuhusu uharibifu uliokaribia.—Mathayo 24:37-39.

Baadaye, ijapokuwa Wayahudi hawakupewa amri ya kuwahubiria watu wa mataifa mengine, wengi wao waliongea na watu wengine kuhusu imani yao. Kwa hiyo, mwanamke wa taifa lingine aliyeitwa Ruthu alikuja kujifunza kumhusu Yehova. Ruthu alimshukuru Naomi, mama mkwe wake Myahudi, na kumwambia: “Watu wako watakuwa watu wangu, na Mungu wako atakuwa Mungu wangu.” (Ruthu 1:16) Baadaye, Mfalme Sulemani alionyesha kwamba watu wengi wasio Wayahudi wangekuja kusikia kuhusu ‘jina kuu’ la Yehova na kumwabudu katika hekalu Lake.—1 Wafalme 8:41, 42.

Watumishi hao wa kale wa Mungu walihubiri ijapokuwa hawakuamriwa kufanya hivyo. Basi, sisi Wakristo tunapaswa kuchukua kwa uzito wajibu wetu wa kuhubiri, kwa kuwa tumeamriwa kuhubiri ‘habari njema ya ufalme.’ (Mathayo 24:14) Sisi, kama vile mtume Paulo, tumewekewa sharti la kutangaza habari njema. (1 Wakorintho 9:16) Wokovu wetu unategemea jambo hilo. Andiko la Waroma 10:9, 10 linasema hivi: “Ukitangaza hadharani lile ‘neno katika kinywa chako mwenyewe,’ kwamba Yesu ni Bwana, . . . utaokolewa. Kwa maana kwa moyo mtu hudhihirisha imani kwa ajili ya uadilifu, lakini kwa kinywa mtu hufanya tangazo la hadharani kwa ajili ya wokovu.”

Unaweza kufanya “tangazo [hilo] la hadharani” wapi? Ijapokuwa inafaa kuhubiri vivi hivi, kuhubiri nyumba hadi nyumba bado ndiyo njia yenye matokeo zaidi ya kuwasaidia wengine. (Matendo 5:42; 20:20) Je, wewe umeondolewa wajibu wa kufanya kazi hiyo kwa sababu ya umri wako mdogo? Hata kidogo. Biblia inatoa amri hii katika Zaburi 148:12, 13: “Vijana waume, na wanawali, wazee, na watoto; na walisifu jina la BWANA.”

Ugumu wa Kuwahubiria Marika

Kukutana na mwanashule mwenzako unapohubiri kunaweza kukufanya uone aibu na kukutia wasiwasi, kwa kuwa kila mtu anataka kupendwa na wengine. Hakuna anayependa kuchokozwa, kudhihakiwa au kutukanwa. Kijana mmoja anayeitwa Tanya anasema: “Watoto shuleni wanaweza kuwa wakatili sana!” Kwa hiyo, huenda ukajiuliza, wanafunzi wenzako watasema nini wakikuona ukiwa nadhifu na ukibeba Biblia. Kuna uwezekano kwamba watakudhihaki. Kijana Mbrazili anayeitwa Felipe anakumbuka: “Mvulana mmoja wa darasa langu aliyeishi katika jengo letu alizoea kusema, ‘Wewe na Biblia yako! Unabeba nini katika mkoba wako?’”

Kudhihakiwa kwa njia hiyo hakufurahishi hata kidogo. Biblia inasimulia juu ya Isaka, mwana wa Abrahamu, aliyedhihakiwa vikali na ndugu yake wa kambo, Ishmaeli. (Mwanzo 21:9) Mtume Paulo aliiona dhihaka hiyo kuwa jambo zito. Katika Wagalatia 4:29 mtume huyo anasema kwamba tendo hilo lilikuwa ‘mnyanyaso.’

Vivyo hivyo, Yesu alionya kwamba baadhi ya watu wangewatenda wafuasi wake kwa uhasama. Alisema hivi: “Ikiwa ulimwengu wawachukia nyinyi, mwajua kwamba huo umenichukia mimi kabla ya huo kuwachukia nyinyi. Kama mngekuwa sehemu ya ulimwengu, ulimwengu ungependa sana kilicho chao wenyewe. Sasa kwa sababu nyinyi si sehemu ya ulimwengu, bali nimewachagua nyinyi kutoka ulimwenguni, kwa ajili ya hili ulimwengu huwachukia nyinyi.”—Yohana 15:18, 19.

Kwa hiyo, unapaswa kuwa tayari kunyanyaswa kwa kadiri fulani kwa kuwa wewe ni Mkristo. (2 Timotheo 3:12) Hata kama hungezungumza kamwe juu ya Biblia pamoja na marika wako, wengine wao bado wangekunyanyasa kwa sababu ya mwenendo wako mzuri na kwa sababu hujiungi nao katika mwenendo mpotovu. (1 Petro 4:4) Hata hivyo, Yesu anatufariji kwa maneno haya: “Wenye furaha ni nyinyi watu wawashutumupo na kuwanyanyasa nyinyi na kusema kwa uwongo kila namna ya jambo ovu dhidi yenu kwa ajili yangu.” (Mathayo 5:11) Kwa nini unaweza kuwa mwenye furaha ijapokuwa unadhihakiwa au kutukanwa? Kwa sababu unajua unafurahisha moyo wa Yehova Mungu! (Mithali 27:11) Na ukimpendeza Mungu, utakuwa na tumaini la kuishi milele!—Luka 10:25-28.

Hata hivyo, wengi wa wanafunzi wenzako hawataonyesha uhasama ukikutana nao katika kazi ya kuhubiri. Kijana Mwingereza anayeitwa Angela anatukumbusha hivi: “Unapokutana na mwanafunzi mwenzako mlangoni, mara nyingi yeye ana wasiwasi mwingi kuliko wewe!” Hata wengine huenda wakataka kukusikiliza. Kwa vyovyote vile, Wakristo wengi wachanga wanawahubiria wanafunzi wenzao kwa mafanikio. Makala ifuatayo ya “Vijana Huuliza” itazungumzia jinsi unavyoweza kufanya hivyo pia.

[Picha katika ukurasa wa 21]

Vijana wengi huogopa kwamba watakutana na mwanafunzi mwenzao wanapohubiri nyumba hadi nyumba

[Picha katika ukurasa wa 23]

Usiaibikie kamwe imani yako kwa sababu ya kudhihakiwa