Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ugiriki Yaunga Mkono Haki za Dini

Ugiriki Yaunga Mkono Haki za Dini

Ugiriki Yaunga Mkono Haki za Dini

KWA MARA YA KWANZA, serikali ya Ugiriki iliwaruhusu Mashahidi wa Yehova watumie mojawapo ya nyanja zake za kipekee kwa ajili ya mkusanyiko mkubwa mwaka jana. Uwanja huo uliofunikwa huitwa Olympic Sportshall, na unaweza kutoshea watu 20,000. Uwanja huo ni sehemu ya majengo yatakayotumiwa wakati wa Michezo ya Olimpiki ya mwaka wa 2004 huko Athens.

Mnamo mwaka wa 1963 na 1988, Mashahidi walipanga kutumia nyanja kubwa za michezo za Athens kwa ajili ya mikusanyiko yao. Hata hivyo, wenye mamlaka walitishwa na Kanisa Othodoksi la Ugiriki na hawakuwaruhusu Mashahidi kuzitumia.

Mambo Yabadilika

Mnamo Februari 2001, Mashahidi waliomba watumie uwanja wa Olympic Sportshall—mojawapo ya nyanja zilizofunikwa ambazo zina nafasi ya kutosha. Lakini walihofia kwamba wangenyimwa ruhusa kama ilivyokuwa hapo mbeleni. Kama ilivyohofiwa, hapo kwanza wenye mamlaka walikataa ombi lao.

Hata hivyo, maafisa wa ngazi za juu, ambao hufanya mambo bila ubaguzi, walipelekewa ombi hilo mara moja. Je, wangekubali kutetea uhuru wa ibada na uhuru wa kufanya kusanyiko la amani? Je, wangekinza misongo ya viongozi wa dini? Walifanya hivyo, na uamuzi wao ukabatilisha ule wa kwanza. Hilo liliwawezesha Mashahidi wapange kufanya kusanyiko lao kwenye uwanja wa Sportshall mnamo Julai 27-29, 2001.

Wakati huohuo, wenye mamlaka waliwaruhusu Mashahidi watumie uwanja mwingine uliofunikwa huko Thessalonica ambao unadumishwa na serikali. Uwanja huo unaitwa Palais de Sport.

Msongo Mkali Haukufaulu

Siku ya kwanza ya mkusanyiko wa Athens ilipokaribia, kulikuwa na mahangaiko haya: Je, wenye mamlaka wangetimiza ahadi yao licha ya msongo wa makasisi wa Kanisa Othodoksi? Na je, Mashahidi wangeweza kufurahia mkusanyiko wao bila kusumbuliwa na watu wajeuri?

Kama kawaida, Kanisa Othodoksi lilijaribu kutumia uvutano wake ili kukatiza mkusanyiko huo. Vituo vya televisheni vilitangaza kwamba makasisi wa Kanisa Othodoksi hawakutaka habari zozote za kusanyiko zitangazwe. Hata hivyo, jitihada za kanisa hilo hazikufua dafu.

Jambo la kushangaza ni kwamba Kanisa Othodoksi limewashutumu Mashahidi kuwa dini ya siri. Lakini kanisa hilo ndilo lililojaribu kuwazuia watu wasijue kilichokuwa kikiendelea katika uwanja huo. Kwa kupendeza, waandishi wa habari wenye ujasiri walikinza msongo wa makasisi. Walitangaza waziwazi yale yaliyotukia mkusanyikoni bila ubaguzi.

Isitoshe, maelfu ya wahudhuriaji waliwaeleza watu kuhusu mkusanyiko huo na kuhusu imani yao. Kokote walikokwenda, wahudhuriaji hao walitambuliwa kwa beji zao za mkusanyiko za rangi ya manjano. Watu wengi ambao si Mashahidi wa Yehova walialikwa kwenye mkusanyiko na walihudhuria, hivi kwamba kwenye siku ya mwisho ya mkusanyiko kulikuwa na watu 15,760 katika uwanja wa Sportshall. Kwenye miisho-juma miwili ya mwisho ya Julai, watu 13,173 walihudhuria mikusanyiko iliyofanywa kwenye uwanja wa Palais de Sport huko Thessalonica.

Watazamaji Walivutiwa

Mashahidi wa Yehova 2,604 waliojitolea walipofurika kwenye uwanja wa Sportshall ili kusafisha, kupaka rangi, na kufanya matayarisho ya mkusanyiko, wasimamizi wa uwanja huo walisema hivi: “Tulikuja kujionea jambo ambalo halijawahi kamwe kutukia mahala hapa.” Mtu mmoja alisema hivi: “Mwapaswa kutumia uwanja huo kila mwaka ili urekebishwe kabisa.”

Andreas Vardakis, mkurugenzi anayeshughulikia mambo ya umma kwenye uwanja wa Sportshall, alivutiwa. Alisema hivi: “Nyinyi watu mmerembesha uwanja huu. Tuna wafanyakazi wanaotunza uwanja huu. Lakini jitihada zenu ndizo zimewezesha mkusanyiko huo kufanikiwa.”

Mkuu mmoja wa polisi alipotambua kwamba hakuhitaji kuwatuma maafisa wake ili kudhibiti umati huo wenye amani wakati wa mkusanyiko, alisema hivi: “Sijawahi kamwe kuona utulivu na utaratibu kama huo!”

Jambo Kuu Mkusanyikoni

Katika hotuba ya mwisho ya mkusanyiko, ilitangazwa kwamba Wizara ya Elimu ya Taifa na Dini huko Ugiriki ilisema kwamba Mashahidi wa Yehova ni “dini inayojulikana.” Isitoshe, Wizara hiyo ilikubali rasmi kuwepo kwa makao makuu ya Mashahidi wa Yehova huko Athens. Hati ya serikali ilisema hivi kwa sehemu:

‘Serikali inawaona Mashahidi wa Yehova kuwa dini inayojulikana hivyo watapata manufaa zote zinazotolewa na sheria. Kifungu cha Katiba kilichotajwa hapo juu kinatetea uhuru wa ibada, uhuru wa mbinu za kuabudu na kutumia mali zilizotengwa kwa kusudi hilo, na uhuru wa kuchagua jinsi ya kusimamia na kupanga kila kanisa au mkutano wa kidini. Kinatambua majengo ya shirika hilo huko Marousi [ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova kuwa] mahala patakatifu na palipowekwa wakfu kwa ajili ya kumwabudu Mungu. Majengo hayo yanaitwa Betheli, yaani, “Nyumba ya Mungu.”’

Mashahidi wa Yehova, na watu wengine wanaounga mkono uhuru wa dini, wanafurahia maendeleo hayo. Kwa sababu hiyo, wao husali kwamba watu wataweza kuishi maisha ya Kikristo “yaliyo shwari na matulivu pamoja na ujitoaji-kimungu kamili na uchukuaji-mambo kwa uzito.”—1 Timotheo 2:1, 2.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Mashahidi wakusanyika kwenye uwanja wa Olympic Sportshall

[Hisani]

Harry Bilios