Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kuhisi Hatia Ni Kubaya Sikuzote?

Je, Kuhisi Hatia Ni Kubaya Sikuzote?

Maoni ya Biblia

Je, Kuhisi Hatia Ni Kubaya Sikuzote?

WATU wengi leo huona kwamba hawapaswi kuhisi hatia. Wao wana maoni kama ya mwanafalsafa Mjerumani Friedrich Nietzsche, aliyesema hivi: ‘Sikuzote, udhaifu mkubwa wa wanadamu umekuwa kuhisi hatia.’

Lakini sasa wataalamu wengine wana maoni tofauti. Dakt. Susan Forward, mtaalamu maarufu wa tiba aliye pia mwandishi, anasema hivi: “Hisia ya hatia ni muhimu ili mtu awe mwenye huruma na mwenye kuwajibika. Ni sehemu ya dhamiri.” Hivyo basi, je, ni vibaya kuhisi hatia? Je, kuna wakati ambapo inafaa mtu ahisi hatia?

Hatia Ni Nini?

Sisi huhisi hatia tunapong’amua kwamba tumemuumiza mtu fulani tunayempenda au tusipotimiza viwango fulani tulivyojiwekea. Kitabu kimoja cha marejeo chasema kwamba, hatia huhusiana na ‘kuhisi kuwa unawajibika kwa sababu ya kutofaulu, kukosea, kutenda uhalifu, au dhambi.’

Maandiko ya Kiebrania yanaonyesha kwamba Mwisraeli ambaye hakutimiza Sheria ya Mungu alikuwa na hatia. Neno hatia limetajwa mara nyingi katika vitabu vya Biblia vya Mambo ya Walawi na Hesabu. Kwa kupendeza, neno hilo linapatikana mara chache sana katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Lakini mahala ambapo linaonekana, linahusiana na dhambi nzito dhidi ya Mungu.—Marko 3:29; 1 Wakorintho 11:27.

Kwa kusikitisha, twaweza kuhisi hatia ijapokuwa hatuna hatia. Kwa mfano, iwapo mtu anapenda kutenda mambo kikamilifu na anajiwekea viwango asivyoweza kufikia, huenda akahisi hatia kila anapokosa kufaulu kufikia viwango hivyo. (Mhubiri 7:16) Au huenda tukajutia kosa kupita kiasi na kufadhaika kwa kuaibika na mwishowe tukajiumiza bila sababu. Basi, je, kuna faida yoyote kuhisi hatia?

Kuna Faida Kuhisi Hatia

Kuna angalau faida tatu za kuhisi hatia. Kwanza, hiyo inaonyesha kwamba tunajua maadili yanayofaa. Inaonyesha kwamba dhamiri yetu inafanya kazi. (Waroma 2:15) Kitabu kimoja kilichochapishwa na Shirika la Marekani la Magonjwa ya Akili kinasema kwamba kutohisi hatia kwaweza kusababisha hatari katika jamii. Watu wenye dhamiri zilizotiwa unajisi au zisizofanya kazi wanaweza kushindwa kutambua tofauti kati ya lililo jema na lililo baya, na hiyo yaweza kuwa hatari.—Tito 1:15, 16.

Pili, dhamiri yenye hatia yaweza kutusaidia tusifanye mabaya. Kama vile maumivu ya mwili yanavyoweza kuonyesha kwamba tuna ugonjwa fulani, uchungu wa moyoni unaosababishwa na hatia hutuonyesha kwamba tuna tatizo la maadili au la kiroho tunalohitaji kushughulikia. Tukiisha tambua udhaifu huo, sisi hujaribu kuepuka kujiumiza, kuwaumiza wapendwa wetu, au kuwaumiza watu wengine wakati ujao.—Mathayo 7:12.

Hatimaye, kukubali hatia kwaweza kumsaidia mwenye hatia na vilevile mtu aliyekosewa. Kwa mfano, Mfalme Daudi alipokuwa na hatia aliumia sana moyoni. Aliandika hivi: “Niliponyamaza mifupa yangu ilichakaa kwa kuugua kwangu mchana kutwa.” Lakini alipotubu dhambi yake mbele za Mungu hatimaye, Daudi aliimba hivi kwa furaha: “Utanizungusha [“utanizunguka na,” Zaire Swahili Bible] nyimbo za wokovu.” (Zaburi 32:3, 7) Kutubu kwaweza hata kumfanya mtu aliyekosewa ahisi vizuri kwani kukubali hatia kwaweza kumhakikishia kuwa anapendwa na ndiyo sababu yule aliyemkosea amejuta jinsi alivyomuumiza.—2 Samweli 11:2-15.

Maoni Yanayofaa Kuhusu Hisia ya Hatia

Ili upate maoni yanayofaa kuhusu hisia ya hatia, ona tofauti kubwa iliyopo kati ya maoni ya Yesu na maoni ya Mafarisayo kuhusu dhambi na watenda dhambi. Kwenye Luka 7:36-50, twasoma kuhusu mwanamke mwasherati aliyeingia katika nyumba ya Farisayo ambamo Yesu alikuwa ameenda kula. Mwanamke huyo aliingia na kumkaribia Yesu, akasafisha miguu ya Yesu kwa machozi yake, na kuipaka mafuta ya marashi ya bei ghali.

Farisayo huyo mnafiki alimdharau mwanamke huyo na kuona kuwa hastahili uangalifu wake. Alisema hivi moyoni mwake: “Mtu huyu [Yesu], kama angekuwa ni nabii, angejua ni nani na ni wa aina gani mwanamke anayemgusa, kwamba ni mtenda-dhambi.” (Luka 7:39) Yesu alirekebisha mawazo ya mtu huyo upesi kwa kusema hivi: “Wewe hukupaka kichwa changu mafuta; lakini mwanamke huyu alipaka miguu yangu mafuta yenye marashi. Kwa msingi huu, mimi nakuambia wewe, dhambi zake, ingawa ni nyingi, zimesamehewa, kwa sababu alipenda sana.” Hapana shaka maneno hayo mazuri yalimtia moyo mwanamke huyo na kumchangamsha.—Luka 7:46, 47.

Yesu hakuwa akionyesha kwamba uasherati ni sawa. Badala yake, alikuwa akimfundisha Farisayo huyo mwenye kiburi kwamba upendo wapasa kuwa kichocheo kikuu cha kumtumikia Mungu. (Mathayo 22:36-40) Kwa wazi, ilifaa mwanamke huyo ahisi hatia kwa sababu ya uasherati aliofanya hapo kale. Na hapana shaka kwamba alitubu, kwani alilia, hakujaribu kutetea mwenendo wake mbaya, na alichukua hatua zinazofaa kumheshimu Yesu hadharani. Yesu alipoona hayo, alimwambia hivi: “Imani yako imekuokoa; shika njia yako uende kwa amani.”—Luka 7:50.

Kwa upande mwingine, yule Farisayo aliendelea kumdharau kuwa mtenda dhambi. Huenda alitaka kumfanya ajihisi kuwa ana hatia mbele za Mungu na kumwaibisha. Lakini si jambo la upendo kuendelea kuwafanya watu wahisi hatia eti kwa sababu nyakati nyingine hawafanyi mambo kama tunavyotaka, na muda si muda hiyo itawazuia kufanya vizuri. (2 Wakorintho 9:7) Matokeo mazuri hutokana na kumwiga Yesu—kwa kuweka mfano bora, kuwasifu wengine kwa unyofu, na kuwaamini hata ingawa nyakati nyingine huenda wakahitaji kukemewa na kushauriwa.—Mathayo 11:28-30; Waroma 12:10; Waefeso 4:29.

Hivyo basi, kuhisi hatia kwaweza kuwa jambo zuri, au hata la lazima, wakati ambapo mtu amekosa. Mithali 14:9 husema hivi: “Wapumbavu huidharau hatia.” Dhamiri yenye hatia yaweza na yapasa kutuchochea kukubali kosa na kuchukua hatua nyingine zinazofaa. Hata hivyo, sikuzote twapaswa kumtumikia Yehova kwa sababu tunampenda bali si kwa sababu ya kuhisi hatia. (Ayubu 1:9-11; 2:4, 5) Biblia hutuhakikishia kwamba watu wazuri wanapotiwa moyo na kukumbushwa jambo hilo, watafanya yote wawezayo. Zaidi ya hilo, watafurahi wanapofanya hivyo.