Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Maji Ule mfululizo wenye kichwa “Je, Kutakuwa na Maji ya Kutosha?” (Juni 22, 2001) ulikuwa wenye kuelimisha sana. Hata hivyo, mlisema kwamba “utengenezaji wa tani moja ya feleji waweza kutumia tani 280 za maji.” Hapo pana kasoro. Mimi ni mtaalamu wa maji na ninajua kwamba viwanda fulani vya kutengeneza feleji hapa India hutumia tani 20 hadi 23 tu za maji.

N.K.K., India

“Amkeni!” linajibu: Takwimu tuliyoandika inaonyesha kiasi cha maji yanayotumiwa kutengeneza feleji. Imebainika kwamba kiasi kikubwa cha maji yanayotumiwa kutengeneza feleji hayamaliziki bali yanatumiwa tena. Tunaomba radhi kwa hitilafu hiyo.

Biblia ya Dalmatin Nilipokuwa nikisoma makala yenye kichwa “Biblia ya Dalmatin—Haipatikani Sana Lakini Haijasahaulika” (Juni 22, 2001), nilishangaa kusoma hivi kwenye ukurasa wa 15: “Yaonekana kwamba [Dalmatin] alitafsiri kutokana na lugha za awali huku akirejezea kwa ukaribu tafsiri ya Kijerumani ya Biblia ya Kilatini ya Vulgate ya Martin Luther.” Nilifikiri kuwa Luther alitafsiri kutokana na lugha za awali za Biblia.

R. S., Ujerumani

“Amkeni!” linajibu: Hatukukusudia kuonyesha kwamba Luther alitumia “Vulgate” peke yake alipokuwa akitafsiri Maandiko ya Kiebrania. Japo mambo mengi kuhusu tafsiri ya Kijerumani ya Luther hayajulikani, wengi hukubali kwamba “Vulgate” ni mojawapo ya vichapo ambavyo Luther alitumia ili kuelewa maandishi ya lugha ya awali. Hapana shaka kwamba Luther alitumia vichapo vingine vilivyokuwepo katika siku yake, kama vile tafsiri ya Kigiriki inayoitwa “Septuagint.”

Mnavajo Ninataka kuwashukuru kwa ile makala nzuri na yenye kutia moyo yenye kichwa “Jina la Mungu Lilibadili Maisha Yangu!” (Julai 8, 2001), iliyosimuliwa na yule mwanamke Mnavajo aitwaye Sandy Yazzie Tsosie. Maneno yake yalinichochea sana hata nikalia. Nilipata tumaini niliposoma mambo aliyopata maishani na jinsi alivyoshinda huzuni kabla ya kupata furaha na upendo. Ninatambua jinsi Yehova Mungu anavyotupenda sote!

A. S., Marekani

Msiba Mbaya Sana Sikufikiri kuwa mambo mabaya jinsi hiyo yanaweza kutokea kihalisi. Hivyo nilishtuka sana niliposoma simulizi lenye kichwa “Kukabiliana na Msiba Mbaya Sana.” (Julai 22, 2001) Mara tu nilipomaliza kulisoma, nilisali na nikamwomba Yehova amtegemeze Jonathan, Oscar, na babu na nyanya ya Oscar. Masimulizi kama hayo hutuchochea kujitoa kabisa kwa Yehova kabla “wakati na tukio lisilotazamiwa” halijatupata. —Mhubiri 9:11, NW.

E. P., Italia

Niliguswa sana kihisia niliposoma simulizi lenye kutisha kuhusu msiba uliomkumba Theresa na familia yake. Ninataka familia yake ijue kwamba mimi pia ninataka sana kumkumbatia Theresa katika ulimwengu mpya ulioahidiwa na Yehova.

L. T., Italia

Nilisita kufanya uamuzi wa kubatizwa kwa miaka sita. Sikuwa nimeamua kufanya mabadiliko fulani. Lakini simulizi hilo juu ya Theresa lilifanya nitafakari. Niling’amua kwamba siwezi kuishi bila kumtegemea Yehova, na nilisali kwa moyo wote. Japo familia hiyo ilikumbwa na msiba mbaya sana, simulizi hilo lilinitia moyo.

M. L., Jamhuri ya Cheki

Nilishangaa kujua kwamba tendo baya kama hilo linaweza kumpata Shahidi wa Yehova, lakini makala hiyo ilinisaidia kutambua kwamba Yehova hatulindi kimuujiza. Sijui nitakumbwa na msiba lini, lakini familia ya Theresa ilikuwa na imani yenye nguvu na hiyo imenifanya niazimie kusimama imara katika jaribu lolote.

S. O., Japani