Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Tunahitaji Walimu?

Kwa Nini Tunahitaji Walimu?

Kwa Nini Tunahitaji Walimu?

“Siku moja pamoja na mwalimu stadi ni bora kuliko siku elfu za kusoma kwa bidii.”—Methali ya Japani.

JE, UNAMKUMBUKA mwalimu fulani aliyekuvutia ulipokuwa shuleni? Au, kama ungali mwanafunzi, je, unampenda sana mwalimu fulani? Kwa nini walimu fulani huvutia au hupendwa?

Mwalimu bora huwafanya wanafunzi wajiamini na kufanya masomo yapendeze. Mwingereza mmoja mwenye umri wa miaka 70 anasema hivi kumhusu mwalimu mpendwa aliyemfundisha Kiingereza katika shule aliyosomea huko Birmingham: “Bw. Clewley alinisaidia kutambua vipawa ambavyo sikujua nilikuwa navyo. Ingawa nilikuwa mwenye haya na mnyamavu, alinitia moyo nishiriki katika mashindano ya mchezo wa kuigiza. Nilishinda tuzo ya mchezo wa kuigiza katika mwaka wangu wa mwisho shuleni. Kama hangalinitia moyo, singalipata tuzo hiyo. Nasikitika kwamba sikukutana naye katika miaka ya baadaye ili nimshukuru kwa jitihada zake za kuwasaidia wanafunzi.”

Margit, mwanamke mchangamfu mwenye umri wa miaka 50 na kitu, anayeishi Munich, Ujerumani, anasema hivi: “Nilimpenda hasa mwalimu mmoja. Alieleza mambo magumu kwa njia rahisi. Alitutia moyo kuuliza maswali wakati ambapo hatukuelewa jambo fulani. Hakuwa mkali, bali mwenye urafiki. Kwa sababu hiyo, tulifurahia masomo sana.”

Peter, anayeishi Australia, anamkumbuka mwalimu wake wa hesabu na anasema hivi kumhusu: ‘Alitusaidia kuelewa umuhimu wa yale tuliyojifunza kwa kutupatia mifano. Tulipojifunza trigonometria (elimu kuhusu uhusiano kati ya pembe na pande tatu za pembetatu) alituonyesha jinsi ya kupima urefu wa jengo hata bila kuligusa, kwa kutumia tu kanuni za trigonometria. Ninakumbuka kwamba nilivutiwa sana na jambo hilo.’

Pauline, anayeishi kaskazini mwa Uingereza, alimwambia mwalimu wake hivi: “Sielewi hesabu vizuri.” Mwalimu alimwuliza: “Je, ungetaka kufanya maendeleo? Naweza kukusaidia.” Pauline anaongeza hivi: “Katika miezi michache iliyofuata alinisaidia sana, hata baada ya shule. Nilijua kwamba alitaka nifaulu na kwamba alinijali. Kwa sababu hiyo, nilijitahidi hata zaidi na kufanya maendeleo.”

Angie, mwenye umri wa miaka 30 na kitu, anayeishi Scotland, anamkumbuka Bw. Graham, mwalimu wake wa historia. “Alifanya somo la historia livutie! Alisimulia kila tukio kana kwamba lilikuwa hadithi na alikuwa na shauku kuhusu kila somo. Tuliweza kuelewa matukio hayo yote vizuri.” Anamkumbuka pia Bi. Hewitt, mwalimu wake mpendwa mzee wa darasa la kwanza. “Alikuwa mwenye fadhili na aliwajali wanafunzi. Siku moja nilipomwendea ili kumwuliza swali alinikumbatia papo hapo. Nilihisi kwamba alinijali kwelikweli.”

Timothy, anayeishi kusini mwa Ugiriki, alisema hivi kwa uthamini: “Bado nakumbuka mwalimu wangu wa sayansi. Alibadili kabisa maoni yangu juu ya mazingira na maisha. Aliwafanya wanafunzi wastaajabie masomo. Alifanya tuwe na hamu sana ya kupata maarifa na kuelewa mambo.”

Ramona, anayeishi California, Marekani, anaandika hivi: “Mwalimu wangu wa sekondari alipenda Kiingereza sana. Shauku yake ilitusisimua! Alifanya mambo magumu yawe rahisi kuelewa.”

Jane, anayeishi Kanada, alitaja kwa shauku mwalimu wake wa michezo, ambaye “alikuwa na mbinu mpya za tafrija na masomo. Alitupeleka nje na kutufundisha kuteleza kwenye theluji na kuvua samaki kwenye ziwa lililofunikwa kwa barafu. Hata tulitengeneza mkate jinsi Wahindi Wekundu wanavyofanya kwenye moto ambao sisi wenyewe tulikuwa tumewasha. Hayo yote yalinifurahisha sana kwa sababu mara nyingi nilikaa ndani ya nyumba nikisoma!”

Helen, mwanamke mwenye haya aliyezaliwa Shanghai na kwenda shule Hong Kong, anasema hivi: “Nilipokuwa katika darasa la tano, Bw. Chan alikuwa mwalimu wetu wa michezo na uchoraji. Nilikuwa mdogo na sikuweza kucheza mpira wa wavu wala mpira wa kikapu vizuri. Hakuniaibisha. Aliniruhusu kucheza mpira wa vinyoya na michezo mingine iliyonifaa. Alikuwa mwenye huruma na fadhili.

“Vilevile, sikuwa na kipawa cha kuchora picha za watu wala vitu. Kwa hiyo, aliniruhusu kuchora mapambo na miundo, ambayo niliweza kuchora vizuri. Kwa sababu nilikuwa na umri mdogo kuliko wale wanafunzi wengine, alinishawishi kurudia darasa la tano. Hilo lilinisaidia sana katika masomo yangu. Nilianza kujiamini na kufanya maendeleo. Mimi huthamini sana msaada wake.”

Ni walimu wenye sifa zipi walio na matokeo zaidi? William Ayers anajibu hivi katika kitabu chake To Teach—The Journey of a Teacher: “Mwalimu bora ni mwalimu mwenye huruma anayewajali wanafunzi, na anayejitahidi sana kuwasaidia. . . . Mwalimu bora si yule ambaye hufuata mbinu, mitindo, mipango, au njia maalumu za ualimu. . . . Ualimu huchochewa na upendo.” Basi, ni mwalimu yupi atakayekuwa na matokeo mazuri? Ayers anasema hivi: “Mwalimu anayekuvutia, mwalimu anayekuelewa au anayekujali, mwalimu aliye na shauku juu ya jambo fulani, kama vile muziki, hesabu, Kilatini, vishada, na vilevile mwalimu anayewasisimua wanafunzi, na aliye na kipawa cha kuchochea.”

Bila shaka, walimu wengi wamesifiwa na wanafunzi na hata wazazi, na hivyo wametiwa moyo kuendelea na kazi yao licha ya magumu. Wanafunzi na wazazi wanamthamini hasa mwalimu anayemjali mwanafunzi na kumtendea kwa fadhili.

Bila shaka si walimu wote walio na sifa hizo. Lakini hatupaswi kusahau kwamba kuna magumu mengi yanayoweza kuwazuia walimu wasiwasaidie wanafunzi wao ifaavyo. Basi, swali hili linazuka, Kwa nini watu huchagua kufanya kazi hiyo ngumu?

[Picha katika ukurasa wa 4]

“Ualimu huchochewa na upendo”