Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ualimu Huleta Uradhi na Shangwe

Ualimu Huleta Uradhi na Shangwe

Ualimu Huleta Uradhi na Shangwe

‘Ijapokuwa ualimu ni kazi ngumu na yenye kuchosha ninaendelea kufanya kazi hiyo ninapowaona watoto wakisisimuka wanapojifunza, na kuona maendeleo yao.’—Leemarys, mwalimu huko New York City.

LICHA ya magumu, vizuizi, na kukata tamaa, mamilioni ya walimu kotekote duniani huendelea na kazi yao. Na ni nini kinachowasukuma maelfu ya wanafunzi kujitahidi kustahili kuwa walimu huku wakijua kwamba huenda kazi yao isithaminiwe sana? Ni nini kinachowachochea kuendelea?

Inna, mwalimu mmoja huko Urusi alieleza hivi: ‘Ninafurahi sana ninapokutana na watu wazima waliokuwa wanafunzi wangu, na kusikia kwamba wamenufaishwa maishani mwao na kile nilichowafundisha. Ninatiwa moyo wanaponiambia jinsi walivyofurahia kufundishwa nami kwa miaka kadhaa.’

Giuliano, mwalimu aliyenukuliwa katika sehemu zilizotangulia, alisema hivi: ‘Mimi ninafurahi sana ninapotambua kwamba nimefaulu kuwafanya wanafunzi wapendezwe na somo fulani. Kwa mfano, baada ya kueleza tukio fulani la historia wanafunzi wengine walisema: “Endelea. Tueleze zaidi!” Maneno kama hayo yanayotoka moyoni hufurahisha kwa sababu yanaonyesha kwamba nimefaulu kuwavutia wanafunzi na jambo jipya. Ninafurahi sana ninapoona macho yao yaking’aa kwa sababu wameelewa somo.’

Elena, aliye mwalimu huko Italia, alisema hivi: ‘Mafanikio makubwa ni haba sana, kwa hiyo, naona kwamba maendeleo madogo na mafanikio ya kila siku ya wanafunzi ndiyo yanayoniletea uradhi hasa.’

Connie, ambaye ni Mwaustralia mwenye umri wa miaka 30 hivi, alisema: “Ninafurahi sana wakati mwanafunzi fulani ambaye nilikuwa na uhusiano mzuri pamoja naye shuleni anaponiandikia barua na kunishukuru kwa jitihada zangu.”

Oscar, anayeishi Mendoza, Argentina, alikubaliana naye: “Mimi huhisi kwamba jitihada zangu si za bure ninapokutana na wanafunzi wangu barabarani au kwingineko, nao wananishukuru kwa kile nilichowafundisha.” Angel, anayeishi Madrid, Hispania, alisema hivi: ‘Bila shaka, licha ya magumu ya ualimu, ninafurahi sana ninapoona kwamba nimeweza kuwasaidia watoto kwa kiasi fulani kuwa wanaume na wanawake waadilifu.’

Leemarys, aliyenukuliwa mwanzoni, alisema: ‘Kwa kweli ninahisi kwamba walimu ni watu wa pekee, la sivyo hatungekubali majukumu hayo yote. Lakini, iwe nimewasaidia watoto kumi au mtoto mmoja, nimetimiza lengo langu, na jambo hilo huridhisha sana. Ninafanya kazi yangu kwa furaha.’

Je, Umewashukuru Walimu Wako?

Je, wewe mwanafunzi au mzazi, umewahi kumshukuru mwalimu fulani kwa sababu ya ufundishaji wake, jitihada zake, na kujali kwake? Au hata kumtumia barua au kadi ili kumshukuru? Arthur, anayeishi Nairobi, Kenya, alitaja jambo la maana: “Hata walimu hupenda pongezi. Serikali, wazazi, na wanafunzi wanapaswa kuwaheshimu sana walimu kwa kazi yao.”

LouAnne Johnson, aliye mwandishi na mwalimu aliandika hivi: ‘Kwa kila barua moja ninayopokea ya kuwashutumu walimu ninapokea mia moja za kuwasifu. Kwa hiyo, nimesadikishwa kwamba walimu wazuri ni wengi kuliko walimu wabaya.’ Jambo la kupendeza ni kwamba watu wengi huajiri mpelelezi ili “kumtafuta mwalimu fulani aliyewafundisha. Watu hao wanawatafuta walimu wao ili waweze kuwashukuru.”

Walimu huweka msingi muhimu wa elimu ya mtu. Hata maprofesa kwenye vyuo vikuu maarufu wanapaswa kuwashukuru walimu waliotumia wakati, waliojitahidi kuwachochea, na kujenga ndani yao hamu ya kupata elimu, maarifa, na ufahamu. Arthur, huko Nairobi, anasema hivi: “Maafisa wote wakuu wa serikali na wasio wa serikali wamefundishwa na mwalimu wakati fulani maishani mwao.”

Tunapaswa kuwashukuru sana wale wanawake na wanaume walioamsha udadisi wetu, waliochochea akili na moyo wetu, na waliotuonyesha jinsi ya kutosheleza hamu yetu ya maarifa na ufahamu!

Tunapaswa kumshukuru hata zaidi Mwelimishaji Mkuu, Yehova Mungu, aliyeongoza kuandikwa kwa Mithali 2:1-6: “Mwanangu, kama ukiyakubali maneno yangu, na kuyaweka akiba maagizo yangu; hata ukatega sikio lako kusikia hekima, ukauelekeza moyo wako upate kufahamu; naam, ukiita busara, na kupaza sauti yako upate ufahamu; ukiutafuta kama fedha, na kuutafutia kama hazina iliyositirika; ndipo utakapofahamu kumcha BWANA, na kupata kumjua Mungu. Kwa kuwa BWANA huwapa watu hekima; kinywani mwake hutoka maarifa na ufahamu.”

Ona maneno yanayoonyesha sharti katika andiko hilo, “ukiyakubali,” “ukiita,” na “ukiutafuta.” Hebu wazia, tukiwa tayari kufanya bidii, tutaweza “kupata kumjua Mungu”! Hiyo ndiyo elimu bora kupita zote.

[Sanduku katika ukurasa wa 13]

Mzazi Mwenye Furaha

Mwalimu mmoja huko New York City alipokea barua hii:

“Ninataka kukushukuru kwa moyo wangu wote kwa jinsi ulivyowasaidia watoto wangu. Uliwajali, uliwaonyesha fadhili, na kuwafundisha kwa ustadi. Bila msaada wako hawangaliweza kufanikiwa kwa kadiri ambavyo wamefanikiwa. Ninawaonea watoto wangu fahari kwa sababu ya ualimu wako—sitasahau jambo hilo kamwe. Wako mwaminifu, S. B.”

Je, unamjua mwalimu fulani ambaye ungeweza kumtia moyo?

[Picha katika ukurasa wa 12]

‘Ninafurahi sana ninapoona macho ya wanafunzi yaking’aa kwa sababu wameelewa somo.’—GIULIANO, ITALIA

[Picha katika ukurasa wa 13]

‘Ninafurahi sana mwanafunzi anaponiandikia barua na kunishukuru kwa jitihada zangu.’—CONNIE, AUSTRALIA