Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Matetemeko ya Ardhi, Unabii wa Biblia, na Wewe

Matetemeko ya Ardhi, Unabii wa Biblia, na Wewe

Matetemeko ya Ardhi, Unabii wa Biblia, na Wewe

Kabla ya kifo chake, Yesu alitabiri matukio na hali ambazo zingeonyesha kwamba ulimwengu ulikuwa katika “umalizio wa mfumo wa mambo.” Yeye alisema kwamba magonjwa ya kuambukiza, upungufu wa chakula, na vita kila mahala ni mambo ambayo yangetukia katika kipindi hicho. Pia alisema kuhusu “matetemeko makubwa ya dunia” ambayo yangetokea “katika mahali pamoja baada ya pengine.” (Mathayo 24:3, 7; Luka 21:10, 11) Je, Yesu alikuwa anatabiri kuhusu siku zetu?

Watu wengi hupinga jambo hilo. Wanasema kwamba matetemeko ya ardhi hayajaongezeka sana katika miaka ya karibuni. Kituo cha Taifa cha Habari za Matetemeko ya Ardhi cha Marekani kinaripoti kwamba matetemeko ya ardhi ya ukubwa wa 7.0 au zaidi kwenye kipimo cha Richter “hayakuongezeka sana” katika karne yote ya 20. *

Hata hivyo, tambua kwamba si lazima utimizo wa unabii wa Yesu uhusishe ongezeko la idadi au la nguvu za matetemeko ya ardhi. Yesu alisema tu kungekuwapo na matetemeko makubwa ya ardhi mahali pamoja baada ya pengine. Kwa kuongezea, alisema kwamba matukio hayo yangeonyesha “mwanzo wa maumivu makali ya ghafula ya taabu.” (Mathayo 24:8) Taabu huonyeshwa kwa jinsi ambavyo watu huathiriwa wala si na idadi wala ukubwa wa matetemeko ya ardhi kwenye kipimo cha Richter.

Matetemeko ya ardhi huwataabisha watu sana siku hizi. Katika karne ya 20, mamilioni ya watu walikufa au kupoteza makao kwa sababu ya matetemeko ya ardhi. Wataalamu wanasema kwamba vifo vingi vingaliweza kuzuiwa. Shirika la Utangazaji la BBC laripoti hivi: “Katika nchi zinazoendelea, mara nyingi sheria za ujenzi hupuuzwa ili kujenga nyumba za bei rahisi haraka-haraka kwa minajili ya kuwawezesha watu wengi wanaohamia mijini kupata makao.” Ben Wisner, mtaalamu wa misiba inayotokea mijini alisema hivi alipozungumzia misiba miwili ya hivi majuzi: “Watu hao hawakufa kwa sababu ya matetemeko ya ardhi. Vifo vyao vilisababishwa na makosa ya wanadamu, kutojali, ufisadi, na pupa.”

Naam, tetemeko la ardhi linapotokea, nyakati nyingine watu hufa kwa sababu ya ubinafsi na uzembe. Sifa hizo zinaonyeshwa wazi katika unabii mwingine wa Biblia unaohusu “siku za mwisho” za mfumo huu. Biblia yasema kwamba katika kipindi hicho watu wangekuwa na “ubinafsi, wenye tamaa ya fedha,” na “wasio na upendo moyoni.” (2 Timotheo 3:1-5, Biblia Habari Njema) Unabii huo pamoja na maneno ya Yesu kuhusu umalizio wa mfumo wa mambo unaonyesha wazi kwamba tumekaribia wakati ambapo Mungu ataondoa visababishi vya maumivu na kuteseka—kutia ndani matetemeko ya ardhi.—Zaburi 37:11.

Je, unataka kujifunza mengi zaidi kuhusu tumaini hilo linalopatikana katika Biblia? Wasiliana na Mashahidi wa Yehova mahala unapoishi, au utume barua yako kwa kutumia anwani ifaayo iliyoorodheshwa kwenye ukurasa wa 5.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Watu fulani wanasema kwamba ripoti za kuongezeka kwa matetemeko ya ardhi zimetokana tu na maendeleo ya kitekinolojia yanayofanya iwe rahisi kutambua matetemeko mengi zaidi.