Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Matukio ya Kuogopesha Matendo ya Kutumainisha

Matukio ya Kuogopesha Matendo ya Kutumainisha

Matukio ya Kuogopesha Matendo ya Kutumainisha

“MAJENGO YALITIKISIKA NA MIALE YA MOTO ILIWAKA KOTEKOTE. NILIPOKUWA NIKIKIMBIA NILISIKIA WATU KOTEKOTE WAKILIA, WAKISALI NA KUOMBA MSAADA. NILIFIKIRI MWISHO WA DUNIA ULIKUWA UMEFIKA.”—G. R., MWOKOKAJI WA TETEMEKO LA ARDHI.

Kila mwaka mamilioni ya matetemeko ya ardhi hutokea katika tabaka la nje la dunia linalosongasonga. Kwa wazi, hatuwezi kusikia mengi ya matetemeko hayo. * Hata hivyo, kwa wastani, karibu matetemeko ya ardhi 140 yenye nguvu sana hutokea kila mwaka. Kuna matetemeko “yenye nguvu,” matetemeko “makubwa,” na “makubwa zaidi.” Tangu zamani, matetemeko hayo yamesababisha vifo vya mamilioni ya watu na kuharibu mali nyingi sana.

Waokokaji wa matetemeko ya ardhi huathiriwa sana kihisia. Kwa mfano, matetemeko mawili ya ardhi yalipotokea nchini El Salvador mapema katika mwaka wa 2001, mratibu wa kamati ya ushauri wa tiba ya akili ya wizara ya afya ya nchi hiyo, alisema hivi: “Watu wanakumbwa na matatizo mengi sana ya akili yanayosababisha huzuni, mfadhaiko na hasira.” Basi haishangazi kwamba wafanyakazi wa huduma za afya nchini El Salvador waliripoti kwamba watu walioshuka moyo na wenye wasiwasi waliongezeka kwa asilimia 73. Kwa kweli, uchunguzi mbalimbali ulionyesha kwamba uhitaji mkubwa wa watu katika kambi za msaada ulikuwa maji, kisha matibabu ya magonjwa ya akili.

Lakini habari za matetemeko ya ardhi hazihusishi kifo, uharibifu, na mfadhaiko tu. Katika visa vingi, misiba hiyo imewachochea watu kusaidia sana na kujitoa mhanga. Kwa kweli, watu fulani wamefanya kazi kwa bidii kurekebisha majengo yaliyoharibiwa na kuwatia moyo watu waliofadhaika. Kama tutakavyoona, matendo hayo yamewapa watu tumaini hata wakati wa matukio ya kuogopesha sana.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Hiyo inatia ndani matetemeko madogo sana ya ardhi. Maelfu ya matetemeko hayo hutokea kila siku.

[Picha katika ukurasa wa 3]

Ukurasa wa 2 na wa 3: Huko Athens, Ugiriki, msichana mmoja aliyefadhaika atambua kwamba mamake hawezi kutoka katika jengo lililoporomoka. Wakati huohuo, baba mmoja afurahi kuona kwamba msichana wake mwenye umri wa miaka mitano ameokolewa

[Hisani]

AP Photos/Dimitri Messinis