Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mimba Yangu Iliharibika

Mimba Yangu Iliharibika

Mimba Yangu Iliharibika

JUMATATU, Aprili 10, 2000, ilikuwa siku nzuri yenye joto na jua, kwa hiyo niliazimia kufanya shughuli mbalimbali. Nilikuwa na mimba ya miezi minne hivi, na ingawa sikuwa na nguvu nyingi, nilifurahia kutoka nje. Lakini, nilipokuwa nimepanga foleni dukani nikingoja kulipa, nilihisi kana kwamba nilikuwa mgonjwa.

Nilipofika nyumbani niligundua kwamba nilikuwa nikitokwa na damu. Nilishtuka sana, kwa kuwa jambo hilo halikuwa limetukia nilipokuwa mjamzito mara mbili hapo awali. Nilimpigia simu daktari wangu, lakini yeye alipendekeza ningoje hadi siku iliyofuata kwa kuwa nilikuwa nimeorodheshwa kumwona wakati huo. Kabla ya kulaza watoto wetu wawili usiku huo, mimi na mume wangu tulitoa sala pamoja tukimwomba Yehova atupe nguvu kukabili hali zozote. Hatimaye, nilishikwa na usingizi.

Lakini saa nane usiku, niliamka nikiwa na maumivu makali. Maumivu yalipungua polepole, lakini nilipoanza kusinzia maumivu yalianza tena, na wakati huo yalikuwa yakitokea na kupungua tena na tena. Nilizidi kutokwa na damu, na nilitambua kwamba hayo yalikuwa maumivu ya kuzaa. Niliwaza na kuwazua ili nitambue kama nilitenda jambo lolote ambalo lingeweza kusababisha hali hiyo. Lakini sikuweza kufikiria jambo lolote lisilofaa ambalo nilifanya.

Saa kumi na moja asubuhi nilitambua kwamba nilihitaji kwenda hospitalini. Mimi na mume wangu tulitulia tulipofika kwenye idara ya dharura hospitalini kwa sababu tulishughulikiwa na watu wenye huruma sana, waliojali, na waliokuwa tayari kutusaidia. Kisha, muda wa saa mbili baadaye, daktari alitupa habari mbaya ambayo tulihofia tungepata: Mimba yangu ilikuwa imeharibika.

Sikushtuka sana nilipopata habari hiyo kwa sababu nilikuwa nimejua kwamba dalili zangu zingeweza kuleta matokeo hayo. Isitoshe, mume wangu alikuwa pamoja nami, naye alinitegemeza sana. Lakini sasa kwa kuwa tungerudi nyumbani bila mtoto tulijiuliza, tungewaambia watoto wetu nini? Binti yetu Kaitlyn alikuwa na umri wa miaka sita, na David, alikuwa na umri wa miaka minne.

Tuwaambie Watoto Wetu Nini?

Watoto walikuwa wamekwenda kulala wakijua kwamba kulikuwa na tatizo fulani, lakini tungewaeleza jinsi gani kwamba ndugu au dada yao alikuwa amekufa? Tuliamua kwamba tungewaeleza waziwazi bila kuficha. Mama yangu alitusaidia kwa kuwaambia watoto kwamba mtoto huyo hangerudi nyumbani pamoja nasi. Tulipofika nyumbani, walitukimbilia, na kutukumbatia na kutubusu. Swali lao la kwanza lilikuwa, “Je, mtoto yu mzima?” Nilishindwa kuwajibu, lakini mume wangu alitukumbatia sisi sote akisema: “Mtoto amekufa.” Tulikumbatiana na kulia, na huzuni yetu ilianza kupungua polepole.

Hata hivyo, tulishtuka kuona jinsi watoto wetu walivyoathiriwa baadaye. Kwa mfano, majuma mawili baada ya mimba yangu kuharibika, kwenye kutaniko letu la Mashahidi wa Yehova, tulitangaziwa kwamba Shahidi mmoja mzee, aliyekuwa rafiki wa karibu wa familia yetu, alikuwa amekufa. David, mwenye umri wa miaka minne, alilia sana hivi kwamba mume wangu alimpeleka nje. Baada ya kutulia, David aliuliza kwa nini rafiki yake alikufa. Kisha aliuliza kwa nini mtoto alikufa. Baadaye alimwuliza babake: “Je, wewe pia utakufa?” Pia alitaka kujua kwa nini Yehova Mungu hajamwangamiza Shetani bado na kuanza “kurekebisha mambo.” Tulishangaa kuona jinsi alivyofikiria mambo mazito licha ya kuwa mchanga sana.

Kaitlyn pia aliuliza maswali mengi. Alipocheza na wanasesere wake, mara nyingi alisingizia kwamba mwanasesere mmoja alikuwa mgonjwa, na wale wanasesere wengine walikuwa wauguzi au watu wa familia. Alitengeneza hospitali ya wanasesere kwa karatasi, na mara kwa mara alisingizia kwamba mmojawapo wa wanasesere wake alikuwa amekufa. Michezo na maswali ya watoto wetu yalitupatia nafasi nyingi za kuwafundisha masomo muhimu kuhusu maisha na jinsi Biblia inavyoweza kutusaidia kukabili majaribu. Tuliwakumbusha pia juu ya kusudi la Mungu la kufanya dunia iwe paradiso yenye kupendeza, bila mateso, uchungu, wala kifo.—Ufunuo 21:3, 4.

Jinsi Nilivyoikabili Hali Hiyo

Nilipotoka hospitalini, mwanzoni nilikuwa nimevurugika na nilihisi kana kwamba moyo wangu ulikuwa umekufa ganzi. Nilikuwa na kazi nyingi za nyumbani, lakini nilishindwa nianzie wapi. Niliamua kuwapigia simu marafiki kadhaa waliokuwa wamepatwa na hali hiyohiyo, nao walinifariji sana. Rafiki mmoja mpendwa alitutumia maua na kujitolea kutunza watoto alasiri moja. Nilithamini sana msaada wake!

Niliweka picha za familia katika vitabu vya picha. Nilitazama na kushikashika nguo za mtoto niliyempoteza, kwa kuwa sikuwa na kitu kingine cha kunikumbusha mtoto huyo aliyekufa. Kwa majuma kadhaa, hisia zangu zilibadilika-badilika. Siku fulani sikuweza kuacha kulia licha ya kutiwa moyo na familia na marafiki. Nyakati nyingine nilifikiri nimerukwa na akili. Nilihuzunika hasa nilipowaona marafiki wangu waliokuwa wajawazito. Mbeleni nilikuwa nikifikiri kwamba wanawake walioharibikiwa mimba hawakuathiriwa sana. Nilifikiri huzuni yao huisha tu bila matatizo mengi. Lakini nilikosea. *

Upendo Ni Dawa Bora

Kadiri wakati ulivyopita nilianza kupata nafuu, na upendo wa mume wangu na Wakristo wenzangu ulinisaidia vilevile. Shahidi mmoja alitengeneza chakula cha jioni na kutuletea nyumbani. Mzee mmoja wa kutaniko na mke wake walitutembelea jioni moja na kuniletea maua na kadi yenye maneno ya kufariji. Tulijua kwamba walikuwa na shughuli nyingi, kwa hiyo tulithamini sana upendo wao. Marafiki wengine wengi walitutumia kadi na maua. Kujua kwamba walikuwa wakitufikiria kulitutia nguvu! Mshiriki mmoja wa kutaniko aliandika hivi: “Yehova anaona uhai kuwa wenye thamani kubwa, na ndivyo tunavyouona. Iwapo yeye anajua wakati shore anapoanguka chini, bila shaka anajua kijusi kinapokufa.” Binamu yangu aliandika hivi: “Tunastaajabishwa na mwujiza wa uzazi na uhai, na tunastaajabishwa vivyo hivyo mwujiza huo unapokosa kutimia.”

Nilipokuwa kwenye Jumba la Ufalme majuma kadhaa baadaye, nilitaka kulia, kwa hiyo nilitoka nje kabla ya mkutano kuanza. Marafiki wawili wapendwa waliponiona nikitoka nje, walikaa nami katika gari, wakanishika mkono, na kufanya nicheke. Punde si punde tulirudi ndani. Ni jambo lenye kufurahisha kama nini kuwa na “marafiki waaminifu kuliko ndugu”!—Mithali 18:24, Biblia Habari Njema.

Mashahidi wenzetu walipojulishwa kuhusu msiba wangu, nilishangaa kujua kwamba wengi kati yao walikuwa wamepatwa na hali kama hiyo. Hata wengine wasiokuwa marafiki wa karibu hapo mbeleni walinifariji kwa njia ya pekee na kunitia moyo. Kwa sababu walinisaidia nilipokuwa taabani, nilikumbushwa maneno haya ya Biblia: “Rafiki hupenda sikuzote; na ndugu amezaliwa kwa siku ya taabu.”—Mithali 17:17.

Faraja Kutoka kwa Neno la Mungu

Ukumbusho wa kifo cha Kristo uliadhimishwa juma moja baada ya mimba yangu kuharibika. Jioni moja tulipokuwa tukisoma masimulizi ya Biblia juu ya siku za mwisho za maisha ya Yesu, kwa ghafula nilitambua kwamba: Yehova anaelewa uchungu unaosababishwa na kifo. Mwana wake alikufa! Kwa sababu Yehova ni Baba yetu wa mbinguni, nyakati nyingine ninasahau kwamba anawaelewa kabisa na kuwahurumia sana watumishi wake, wanaume kwa wanawake. Mara nilitulia kabisa. Nilimkaribia Yehova kuliko wakati mwingine wowote.

Nilitiwa moyo pia kwa kusoma vichapo vya Biblia, na hasa matoleo mbalimbali ya gazeti la Mnara wa Mlinzi na Amkeni! yanayozungumzia kifo cha mpendwa. Kwa mfano, kichapo cha Mtu Fulani Umpendaye Anapokufa, na vilevile mfululizo wenye kichwa “Kuelekeana na Kifo cha Mtoto” katika toleo la Amkeni! la Julai 8, 1988 au Agosti 8, 1987, Kiingereza, ulinisaidia sana. *

Huzuni Itakoma

Muda si muda, nilijua kwamba nimeanza kupona nilipoweza kufurahia mambo bila kuwa na hisia ya hatia, na nilipoweza kuongea kuhusu mambo mengine bila kutaja mtoto wangu aliyekufa. Hata hivyo, bado nilihuzunika nilipokutana na marafiki ambao hawakujua juu ya msiba huo, au nilipomwona mtoto mchanga kwenye Jumba la Ufalme.

Kisha asubuhi moja niliamka na kujua kwamba huzuni yangu ilikuwa imetoweka. Hata kabla ya kufumbua macho, nilihisi utulivu na amani ambayo sikuwa nimehisi kwa miezi mingi. Lakini nilipopata mimba nyingine mwaka mmoja baada ya mtoto wangu kufa, nilihofia kwamba mimba hiyo itaharibika pia. Hata hivyo, nilijifungua mtoto wa kiume mwenye afya mnamo Oktoba 2001.

Bado mimi huhuzunika kwa sababu ya mtoto wangu aliyekufa. Lakini matukio hayo yote yamenifanya nithamini sana uhai, familia yangu, Wakristo wenzangu, na kumthamini Mungu anayetufariji. Msiba huo umekazia pia ukweli kwamba Mungu hachukui watoto wetu bali ‘wakati na tukio lisilotazamiwa hutupata sote.’—Mhubiri 9:11, NW.

Ninatarajia kwa hamu nyingi sana wakati ambapo Mungu atakomesha huzuni, kilio, na maumivu yote, kutia ndani uchungu wa kimwili na wa kihisia unaosababishwa na kuharibika kwa mimba. (Isaya 65:17-23) Wakati huo wanadamu wote watiifu wataweza kusema: “Kifo, ushindi wako uko wapi? Kifo, kichomeo chako kiko wapi?”—1 Wakorintho 15:55; Isaya 25:8.—Tulitumiwa makala hii.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 13 Uchunguzi unaonyesha kwamba kuharibika kwa mimba huathiri kila mwanamke kwa njia tofauti. Baadhi ya wanawake huvurugika, wengine hukata tamaa, na wengine huhuzunika sana. Watafiti wanasema kwamba kuharibika kwa mimba husababisha majonzi, na kuomboleza humsaidia mtu kurudia hali ya kawaida.

^ fu. 20 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Sanduku katika ukurasa wa 21]

Kwa Nini Mimba Huharibika?

Kitabu The World Book Encyclopedia kinasema hivi: “Uchunguzi unaonyesha kwamba asilimia 15 hadi 20 ya mimba zote huharibika. Lakini uwezekano wa mimba kuharibika ni mkubwa katika kipindi cha majuma mawili ya kwanza baada ya mimba kutungwa, wakati ambapo wanawake wengi hata hawajui kwamba wana mimba.” Kitabu kingine cha marejeo kinaonyesha kwamba zaidi ya “asilimia 80 ya mimba huharibika katika majuma 12 ya kwanza baada ya mimba kutungwa,” na angalau nusu ya visa hivyo huenda husababishwa na kasoro katika chembe za urithi za kijusi. Kasoro hizo hazitokei kwa sababu mama au baba ana kasoro za aina hiyo katika chembe zake za urithi.

Mimba inaweza kuharibika ikiwa mama ana ugonjwa fulani. Wataalamu wa tiba wanafikiri kwamba magonjwa ya mfumo wa kinga na wa homoni, maambukizo, na kasoro katika mlango wa kizazi au tumbo la uzazi la mama zinaweza kuwa visababishi. Visababishi vingine vinaweza kuwa magonjwa ya kudumu kama vile ugonjwa wa sukari (usipotibiwa vizuri) na shinikizo la damu linalopanda.

Wataalamu wanasema kwamba si lazima mimba iharibike mtu anapofanya mazoezi ya mwili, kuinua vitu vizito, au kufanya ngono. Haielekei kwamba kuanguka, kugongwa kidogo, au kutishwa kwa ghafula kutasababisha kuharibika kwa mimba. Kitabu kimoja kinasema hivi: ‘Yaelekea kijusi kitajeruhiwa tu ikiwa mama atapatwa na dhara linaloweza kusababisha kifo.’ Kwa kweli, muundo wa tumbo la uzazi unaonyesha kwamba Muumba ana hekima na upendo!—Zaburi 139:13, 14.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 23]

Jinsi Familia na Marafiki Wanavyoweza Kusaidia

Nyakati nyingine ni vigumu kujua la kusema au la kufanya wakati mimba inapoharibika, iwe hali hiyo imempata mtu wa familia au rafiki. Kwa sababu watu huathiriwa kwa njia mbalimbali na msiba huo, hakuna njia maalumu ya kuwafariji na kuwasaidia. Hata hivyo, fikiria madokezo yanayofuata. *

Kile unachoweza kufanya:

◆ Jitolee kuwatunza watoto wale wengine wenye umri mkubwa.

◆ Tayarishia familia hiyo chakula na kuwapelekea.

◆ Msaidie baba pia. Baba mmoja alisema hivi: “Kadi za kuwapa pole akina baba wanaopatwa na msiba huo hazichapishwi.”

Mambo mazuri unayoweza kusema:

“Nimesikitika sana kusikia kwamba mimba yako imeharibika.”

Maneno hayo yanafariji sana, na baadaye huenda yakafanya iwe rahisi kufariji kwa maneno mengine.

“Si vibaya kulia.”

Machozi hububujika kwa urahisi katika majuma ya kwanza au hata miezi ya kwanza baada ya mimba kuharibika. Mhakikishie mtu huyo kwamba bado unamthamini hata katika hali hiyo.

“Je, ninaweza kurudi juma lijalo ili nikujulie hali?”

Mwanzoni, huenda watu wengi wakawatembelea wanaoomboleza ili kuwapa pole, lakini kadiri muda unavyozidi kupita huku wangali wakihuzunika, huenda wakahisi kwamba wengine wamewasahau. Watafarijika kujua kwamba bado unawajali. Huzuni inaweza kuendelea kwa muda wa majuma au miezi kadhaa, na hata baada ya kuzaa mtoto mwingine bila matatizo.

“Sijui la kusema.”

Ni afadhali kusema maneno hayo kuliko kunyamaza tu. Unyofu wako na nia yako ya kutaka kusaidia inaonyesha kwamba unajali.

Usiseme:

“Usijali, utapata mtoto mwingine.”

Ijapokuwa hilo linaweza kuwa kweli, ukisema hivyo huenda ukaonekana kuwa huna huruma. Wazazi hawakutaka tu mtoto yeyote, walitaka mtoto yule aliyekufa. Bila shaka wanahitaji kuomboleza kifo cha yule aliyekufa kabla ya kuanza kufikiria kupata mtoto mwingine.

“Yaelekea kijusi hicho kilikuwa na kasoro fulani.”

Ijapokuwa jambo hilo linaweza kuwa kweli, maneno hayo hayafariji. Katika akili ya mama, mtoto huyo alikuwa mwenye afya.

“Kwa vyovyote, hukumjua huyo mtoto. Ingekuwa vibaya zaidi kama angekufa baada ya kuzaliwa.”

Wanawake wengi huanza kuwapenda watoto wao wasiozaliwa mimba inapokuwa ingali changa. Kwa hiyo, mtoto kama huyo akifa, mama huomboleza. Majonzi hayo huwa mengi zaidi kwa sababu ni mama tu “aliyemjua” huyo mtoto.

“Angalau, una watoto wengine.”

Jambo hilo ni sawa na kumwambia mtu aliyepoteza mguu: “Angalau una mguu ule mwingine.”

Bila shaka, nyakati nyingine hata watu wanaojali kwelikweli husema maneno yenye kuumiza bila kukusudia. (Yakobo 3:2) Kwa hiyo, wanawake wenye busara, ambao mimba zao zimeharibika, wataonyesha upendo wa Kikristo, nao hawataudhika wengine wanaposema maneno yenye kuumiza bila kukusudia.—Wakolosai 3:13.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 36 Madokezo haya yametolewa katika kitabu A Guide to Coping With Miscarriage, kilichotungwa na shirika la kuwasaidia wanawake ambao mimba zao zimeharibika huko Wellington, New Zealand.