Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Naweza Kuwahubiria Wanashule Wenzangu Vipi?

Naweza Kuwahubiria Wanashule Wenzangu Vipi?

Vijana Huuliza . . .

Naweza Kuwahubiria Wanashule Wenzangu Vipi?

“Nilikuwa nikihubiri kisha kwa ghafula nikakutana na mtu fulani niliyemjua. Nilishtuka sana! Mhubiri tuliyekuwa naye alilazimika kuzungumza kwa niaba yangu.”—Alberto.

“Kwa kuwa nilijua kwamba mwanafunzi mwenzangu aliishi katika mtaa huo, nilimwomba ndugu yangu azungumze kwenye nyumba zote. Baada ya muda fulani alichoka na akaniomba nizungumze kwenye nyumba iliyofuata. Nilibisha hodi, na kumbe, ilikuwa nyumba ya mwanafunzi mwenzangu! Nilibabaika sana!”—James.

MARA nyingi vijana huona kwamba ni ushamba kuzungumza kuhusu dini. Hata hivyo, vijana ambao ni Wakristo wa kweli huthamini pendeleo walilopewa na Mungu la kuwaelezea wengine kuhusu imani yao. Hivyo, maelfu ya vijana walio Mashahidi wa Yehova hushiriki katika kazi ya kuhubiri nyumba hadi nyumba. Lakini baadhi yao hufanya kazi hiyo wakihofu kwamba watakutana na mwanashule fulani wanayemjua. Hata ingawa Jennifer alimaliza shule ya sekondari miaka kadhaa iliyopita, asema hivi: “Bado mimi hubabaika ninapokutana na watu niliosoma nao shuleni.”

Iwapo wewe ni kijana Mkristo, huenda ukahisi hivyo nyakati nyingine. Kwa wazi, hakuna mtu anayependa kukataliwa. Hivyo, ni jambo la kawaida kabisa kwa mtu kuwa na wasiwasi fulani wakati anapozungumza na mwanashule mwenzake kuhusu dini. * Lakini hakuna haja ya kuogopa. Je, wamkumbuka “Yosefu kutoka Arimathea,” anayetajwa katika Biblia? Aliamini mafundisho ya Yesu. Hata hivyo, Biblia humfafanua Yosefu kuwa “mwanafunzi wa Yesu lakini wa siri kutokana na kuhofu kwake Wayahudi.” (Yohana 19:38) Wewe ungemwonaje rafiki ambaye angetaka kuficha urafiki wenu? (Luka 12:8, 9) Basi, haishangazi kwamba Mungu anawataka Wakristo wote wafanye “tangazo la hadharani” la imani yao. (Waroma 10:10) Hiyo inatia ndani kuwahubiria vijana wenzako shuleni.

Yosefu wa Arimathea alishinda hofu yake hivi kwamba aliomba ruhusa kuzika mwili wa Yesu. Waweza kushinda hofu yako jinsi gani?

Kusitawisha Hamu ya Kuhubiri

Kwa wazi, mtume Paulo hakuaibika kuwaeleza wengine kuhusu imani yake. Kwenye Waroma 1:15, Paulo anasema kwamba alikuwa na hamu ya kutangaza ujumbe wa Biblia. Alipataje hamu hiyo? Anasema hivi, kama ilivyoandikwa katika mstari wa 16: “Siaibikii habari njema; kwa kweli, hiyo ni nguvu ya Mungu kwa ajili ya wokovu kwa kila mtu mwenye imani.” Vipi wewe? Je, umejithibitishia ukweli? (Waroma 12:2) Je, unasadiki kabisa kwamba ujumbe wa Biblia ni “nguvu ya Mungu kwa ajili ya wokovu”?

Haitoshi tu kuhudhuria mikutano ya Kikristo pamoja na wazazi wako. Kijana mmoja anayeitwa Deborah asema hivi: “Unaweza tu kwenda mikutanoni kwa sababu wazazi wako wamekuambia uende. Lakini watu waliponiuliza maswali ya Biblia, nilishindwa kuyajibu.” Kijana mwingine anayeitwa Mi Young anasema hivi pia: “Twapaswa kujithibitishia kwamba huu ndio ukweli.”

Ni nini kinachoweza kukuchochea kuwaeleza wengine kuhusu Biblia? Ni kujifunza Biblia kibinafsi. Kijana anayeitwa Sean anasema hivi: “Unapoanza kujifunza Biblia kibinafsi, unaanza kufanya ukweli uwe mali yako. Unajifunza kwa faida yako.” Ni kweli kwamba si kila mtu anapenda kujifunza. Shevon anakiri hivi: “Sipendi kusoma. Kwa hiyo, hapo mwanzoni niliona ni vigumu kusoma magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! au kusoma Biblia kila siku. Lakini muda si muda, nilianza kufanya hivyo.”

Ni nini matokeo ya kujifunza kwa bidii? Mtume Paulo asema hivi: “Imani hufuata jambo lisikiwalo.” (Waroma 10:17) Imani na usadikisho wako ukiongezeka, mtazamo wako utabadilika. Elisângela, kijana mmoja kutoka Brazili, alikata kauli hii: “Kuwa Mkristo ni pendeleo kubwa, na si jambo la kuaibikia.” Pasina shaka, imani yako ikiongezeka, utasukumwa kuzungumza na wengine—kutia ndani wanafunzi wenzako. Paulo alisema hivi: “Sisi . . . hudhihirisha imani na kwa hiyo twasema.” (2 Wakorintho 4:13) Isitoshe, utakuwaje “safi kutokana na damu” ya watu wengine ukiwanyima vijana unaowaona kila siku ujuzi unaoleta uhai?—Matendo 20:26, 27.

Hata hivyo, vijana fulani Wakristo huona kwamba hawana ustadi wa kutosha kuzungumza na wengine kuhusu Biblia. Kijana anayeitwa Joshua asema hivi: “Usipojua la kusema, hutafurahia sana kuhubiri.” Kuelewa Biblia kwa undani kutakuwezesha kuitumia kwa ustadi. (2 Timotheo 2:15) Katika makutaniko ya Mashahidi wa Yehova, vijana wanaweza kuwaendea wazee wa kutaniko na kuwaomba wawasaidie kusitawisha ustadi wa kufundisha. Kijana mmoja Mjerumani anayeitwa Matthias asema hivi: “Nilipoanza kuzungumza na watu—badala tu ya kuwatolea vichapo vya Biblia—nilianza kufurahia kuhubiri.”

Hatimaye, waweza kumwomba Mungu akusaidie kuzungumza kwa ujasiri. (Matendo 4:29) Mtume Paulo alisaidiwa na Mungu kwa habari hiyo. Kwenye 1 Wathesalonike 2:2, Paulo asema hivi: “Tulijipa ujasiri kwa njia ya Mungu wetu kusema nanyi habari njema ya Mungu kwa kushindana sana.” Kitabu kimoja cha marejeo chasema kwamba maneno hayo yaweza kutafsiriwa hivi, “Mungu aliondoa hofu mioyoni mwetu.” Basi, mbona usimwombe Mungu aondoe hofu moyoni mwako?

Kujitambulisha

Baada ya kusali, unaweza kuchukua hatua madhubuti. Kijana mmoja Mwingereza anayeitwa Chic ashauri hivi: “Waambie wanashule wenzako kwamba wewe ni Mkristo.” Hungependa kuwa ‘mwanafunzi wa siri.’ Kijana anayeitwa Rebecca anakubali kwamba hapo awali aliogopa kukutana na mtu aliyemjua alipokuwa akihubiri. Lakini yeye anasema aligundua kwamba “ukiwaambia kuwa wewe ni Mkristo na kwamba wewe huenda nyumba hadi nyumba, nyakati nyingine wao huuliza hivi, ‘Basi, utakuja kwetu siku moja?’”

Lakini hakuna haja ya kungoja hadi mkutane pasipo kutarajia. Tafuta njia za kuwaeleza wengine shuleni kuhusu imani yako. Kumbuka maswali ambayo mtume Paulo aliuliza: “Watawekaje imani katika yeye ambaye hawajasikia? Nao watasikiaje bila mtu fulani kuhubiri?” (Waroma 10:14) Ni wewe hasa unayeweza kuwasaidia wanafunzi wenzako kusikia habari njema. Kijana mmoja anayeitwa Iraida anasema hivi: “Shule ni eneo la kuhubiri na ni sisi wanafunzi tu tunaoweza kulihubiri.” Hivyo, vijana wengi wametumia vizuri hali yao kwa kuhubiri kivivi hivi.

Nyakati nyingine kazi unayopewa darasani yaweza kukupa nafasi ya kueleza kweli za Biblia. Msichana mmoja Mwingereza anayeitwa Jaimie anasema hivi: “Tulikuwa tukizungumza kuhusu mageuzi katika somo la sayansi, na nilieleza yale ninayoamini. Mvulana mmoja alinidhihaki na akasema kwamba Mashahidi wa Yehova hawana akili na hawastahili kuwa shuleni. Hata hivyo, vijana wengine darasani walinitetea mara moja.” Yaelekea mwenendo wake bora wa Kikristo ulimsaidia. Jaimie aongeza hivi: “Kwa sababu hiyo, mwanafunzi mmoja alikubali kupokea nakala ya kitabu Je, Kweli Kuna Muumba Anayetujali? *

Msichana mmoja mwenye umri wa miaka 14 huko Rumania anayeitwa Roxana asimulia kisa kama hicho: “Mwalimu wangu alitangaza kwamba kungekuwa na mazungumzo darasani kuhusu kileo, tumbaku, na dawa za kulevya. Hivyo, nilibeba toleo la Amkeni! la Machi 22, 2000 lenye kichwa ‘Jinsi Unavyoweza Kuacha Kuvuta Sigareti.’ Mwanafunzi mwenzangu aliona gazeti hilo, akalichukua, na akakataa kulirudisha. Baada ya kulisoma, alisema kwamba alikuwa ameazimia kuacha kuvuta sigara.”

Huenda hutapata matokeo mazuri hivyo sikuzote. Lakini Mhubiri 11:6 hutusihi hivi: “Asubuhi panda mbegu zako, wala jioni usiuzuie mkono wako. Kwa maana wewe hujui ni zipi zitakazofanikiwa.” Hata matokeo yasipokuwa mazuri, ukiwaeleza wengine shuleni kuhusu imani yako utaweka msingi kwa ajili ya mazungumzo mazuri endapo utakutana na mwanashule mwenzako katika huduma ya nyumba hadi nyumba. Kijana mmoja Mwingereza anayeitwa Jessica asema hivi: “Kuwahubiria wanashule wenzako ni rahisi kwani tayari unawajua.” Huenda ukashangaa kujua kwamba baadhi ya wanashule wenzako wangependa sana kujua yale unayoamini.

Ni kweli kwamba si wote watakaoitikia vizuri. Lakini Yesu alitoa ushauri huu unaofaa: “Popote pale ambapo yeyote hawakaribishi nyinyi au hasikilizi maneno yenu, mnapoenda kutoka katika nyumba hiyo . . . yakung’uteni mavumbi kutoka kwenye miguu yenu.” (Mathayo 10:14) Yaani, hupaswi kuudhika. Ondoka hapo kwa amani na umtafute mtu mwingine anayetaka kusikiliza. Muda si muda utawapata watu wanaotaka kujua ukweli na wanaotaka kusikiliza. Je, hungefurahi iwapo mmojawapo wa watu hao angekuwa mwanafunzi mwenzako? Ikiwa ndivyo, utafurahi kwamba ulishinda hofu ya kuwaeleza wanafunzi wenzako kuhusu imani yako.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Ona makala ya “Vijana Huuliza . . . Nifanye Nini Nikikutana na Mwanafunzi Mwenzangu?,” katika toleo letu la Februari 22, 2002.

^ fu. 18 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Blabu katika ukurasa wa 12]

“Unapoanza kujifunza Biblia kibinafsi, unaanza kufanya ukweli uwe mali yako.”—Sean.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Usiogope kujitambulisha kuwa Mkristo

[Picha katika ukurasa wa 10]

Mara nyingi, kazi unayopewa darasani hutoa nafasi za kuwaeleza wengine kweli za Biblia