Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wakristo Wapaswa Kutazamia Ulinzi wa Mungu?

Je, Wakristo Wapaswa Kutazamia Ulinzi wa Mungu?

Maoni ya Biblia

Je, Wakristo Wapaswa Kutazamia Ulinzi wa Mungu?

Mara nyingi Biblia hurejezea uwezo wa Mungu wa kuwalinda waabudu wake kutokana na madhara. Mfalme Daudi alisema: “Ee BWANA, uniokoe na mtu mbaya, unihifadhi na mtu wa jeuri.” (Zaburi 140:1) Leo waabudu wengi wa Mungu wameponyoka kifo au majeraha baada ya kukabiliana na jeuri, uhalifu, au misiba ya asili. Wengine wamewaza ikiwa Mungu aliwalinda kimuujiza pindi hizo, hasa kwa sababu katika pindi nyingine watu wanaomhofu Mungu wamepatwa na misiba mikubwa, hata kufa kikatili.

JE, YEHOVA Mungu huwalinda watu fulani wasipatwe na madhara na kukosa kuwalinda wengine? Je, twapaswa kutazamia kuokolewa kimuujiza kutokana na jeuri na misiba ya wakati huu?

Masimulizi ya Biblia Kuhusu Ulinzi wa Kimuujiza

Biblia ina masimulizi mengi yanayoonyesha jinsi Mungu alivyoingilia mambo kwa niaba ya waabudu wake. (Isaya 38:1-8; Matendo 12:1-11; 16:25, 26) Pia, Maandiko yanasimulia pindi fulani ambazo Yehova hakuwakomboa watumishi wake kutokana na misiba. (1 Wafalme 21:1-16; Matendo 12:1, 2; Waebrania 11:35-38) Bila shaka, Yehova aweza kuamua kuandaa ulinzi kwa sababu fulani au kwa kusudi fulani wakati wowote atakapo. Kwa hivyo, wakati ambapo Wakristo mmoja-mmoja hawakombolewi kutokana na majaribu, wasifikiri kwamba Mungu amewaacha. Ni lazima tukubali uhakika wa kwamba mambo mabaya yatatokea, hata kwa watumishi waaminifu wa Yehova. Kwa sababu gani?

Kwa Nini Mabaya Huwapata Watumishi Waaminifu wa Mungu

Sababu moja ni kwamba sote tulirithi dhambi na kutokamilika kutoka kwa Adamu na Hawa. Hivyo, tunatazamia maumivu, kuteseka, na kifo. (Waroma 5:12; 6:23) Pia, tunaishi katika siku za mwisho. Biblia hutaja watu wa siku zetu kuwa “wasio na shauku ya kiasili, wasiotaka upatano wowote, wachongezi, wasio na hali ya kujidhibiti, wakali, wasio na upendo wa wema.” (2 Timotheo 3:1-5) Kuongezeka kwa ubakaji, utekaji nyara, mauaji, na uhalifu mbalimbali wa kikatili kunathibitisha maneno hayo.

Watumishi wengi waaminifu wa Mungu wanaishi na kufanya kazi miongoni mwa watu wajeuri na mara nyingine wanakuwa shabaha yao. Huenda maisha yetu yakawa hatarini wakati mwingine kwa sababu tu ya kuwa mahali pasipofaa kwa wakati usiofaa. Isitoshe, tunaona uhakika wa maneno ya Solomoni aliposema kwamba “wakati na tukio lisilotazamiwa huwapata wote.”—Mhubiri 9:11, NW.

Kwa kuongezea, mtume Paulo alieleza kwamba Wakristo wangekuwa vitu vya kunyanyaswa kwa sababu wanamwabudu Mungu. Alisema: “Kwa kweli, wote wale wanaotamani kuishi kwa ujitoaji-kimungu katika ushirika na Kristo Yesu watanyanyaswa pia.” (2 Timotheo 3:12) Katika nchi kadhaa jambo hilo limethibitika kuwa kweli hivi majuzi.

Kwa hivyo, watu wanaomhofu Mungu huathiriwa na jeuri, uhalifu, misiba ya asili, au kifo kisichotazamiwa. Shetani amejaribu kudai kwamba Yehova amewawekea watu Wake ukigo pande zote ili wasipatwe na madhara maishani. (Ayubu 1:9, 10) Lakini sivyo hata kidogo. Tunaweza kuwa na hakika kwamba hata wakati ambapo Yehova hatoi ukombozi wa kimuujiza kutokana na hali fulani, yeye huwalinda watu wake.

Jinsi Ambavyo Yehova Hulinda Watu Wake Leo

Kupitia Neno lake, Yehova hutoa mwongozo unaowalinda watu wake. Hali nzuri ya kiroho na ujuzi wa Biblia waweza kutusaidia kuwa na maoni yanayofaa na kuwa na utimamu wa akili ili kufanya maamuzi kwa hekima na kuepuka makosa ya kipumbavu. (Zaburi 38:4; Mithali 3:21; 22:3) Kwa mfano, kutii shauri la Biblia kuhusu maadili katika ngono, pupa, hasira, na jeuri kumewasaidia Wakristo kuepuka misiba mingi. Pia, kwa kutokuwa na uhusiano wa karibu sana na watu wabaya, tutaepuka kuwa mahali ambapo huenda msiba ukatokea, yaani mahali pasipofaa kwa wakati usiofaa. (Zaburi 26:4, 5; Mithali 4:14) Wale wanaoishi kulingana na kanuni za Biblia wanafurahia maisha bora yanayotokeza afya njema ya kiakili na kimwili.

Inatia moyo sana kujua kwamba hata Mungu akiruhusu mabaya yatendeke, atawapa watumishi wake nguvu wanazohitaji ili waweze kuyahimili. Mtume Paulo atuhakikishia hivi: “Mungu ni mwaminifu, naye hatawaacha nyinyi mshawishwe kupita vile mwezavyo kuhimili, bali pamoja na hicho kishawishi ataifanya pia njia ya kutokea kusudi mweze kuvumilia hilo.” (1 Wakorintho 10:13) Biblia inaahidi pia “nguvu ipitayo iliyo ya kawaida” itakayotusaidia kuvumilia misiba.—2 Wakorintho 4:7.

Mungu Hutenda Kulingana na Mapenzi Yake

Je, Wakristo wapaswa kumtazamia Mungu awaokoe kimuujiza wakati wote msiba unapokaribia kutokea? Biblia haiungi mkono tazamio la aina hiyo.

Bila shaka, Yehova Mungu aweza kuchagua kuingilia mambo moja kwa moja kwa niaba ya watumishi wake wowote. Mtu yeyote hapaswi kuchambuliwa iwapo aamini kwamba ameponyoka madhara kwa sababu Mungu aliingilia mambo. Lakini wakati Yehova anapoamua kutoingilia mambo, hatupaswi kufikiri kwamba hapendezwi nasi.

Na tuwe na hakika kwamba hata tukipatwa na jaribu au hali yoyote ile, Yehova atawalinda watumishi wake waaminifu, ama kwa kuondoa hali hiyo, au kwa kutupatia nguvu ya kuivumilia, na hata tukifa, atatufufua tupate uhai udumuo milele katika ulimwengu wake mpya.—Zaburi 37:10, 11, 29; Yohana 5:28, 29.