Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutimiza Wajibu wa Mama

Kutimiza Wajibu wa Mama

Kutimiza Wajibu wa Mama

Ikiwa watoto huwakilisha kizazi kipya, basi mama zao wanastahili kusifiwa, kuheshimiwa, na kusaidiwa. Ijapokuwa ulimwengu hauna msimamo kuhusu wajibu wa mama, Biblia inasema kwamba watoto ni baraka kutoka kwa Mungu na wanaweza kuwafurahisha wazazi. (Zaburi 127:3-5) Hata hivyo, Maandiko hayapuuzi magumu ambayo akina mama hukabili. Biblia hutaja magumu mengi yanayowapata.

Maamuzi ambayo wazazi hufanya kuhusu kulea watoto na wajibu wa mama yatakuwa na matokeo makubwa na ya kudumu katika maisha na nyutu za watoto wao. Maamuzi hayo yanaweza kubadili sana maisha ya wazazi, kwa hiyo yanapaswa kufikiriwa kwa uzito. Maamuzi hayo hutia ndani maswali kama vile: Je, mama afanye kazi ya kuajiriwa? Ikiwa ndivyo, kwa muda wa saa ngapi kila siku? Ni nani atakayewatunza watoto mama akiwa kazini? Uamuzi ni wa wazazi, nao wanapaswa kuwafaidi watoto wao na kufanya yale ambayo Mungu anaona ni sawa.

Hata hivyo, akina mama hawahitaji kupambana kufanya maamuzi ya hekima peke yao. Maneno ya Isaya 40:11 yanaweza kuwafariji sana, kwa kuwa yanasema kwamba Mungu huwajali sana mama wenye watoto wachanga, naye ‘huwaongoza polepole.’ Mungu anaonyesha kwamba anajali kwa kutoa maagizo katika Biblia yanayoweza kuwasaidia akina mama wafurahie wajibu wao na kufanikiwa kuutimiza.

❖ Uwe mwenye kukubali sababu: Wakristo wanapaswa kujulikana kuwa watu wenye kukubali sababu. (Wafilipi 4:5) Janet Penley, aliye mwandishi na mama, aliona jinsi ambavyo kanuni hiyo ni yenye manufaa. Alisema hivi: ‘Nilipopata mtoto wa kwanza nilikuwa na matarajio mazuri. Niliazimia kuwa mama bora. Nilisoma vitabu vingi na kusikiliza wataalamu wengi. Lakini badala ya kuhisi kwamba nilikuwa nimefanikiwa na kwamba nilikuwa na ujuzi, nilifadhaika na kuhisi nimeshindwa.’ Anasema kwamba “kujaribu kutimiza matarajio ya wengine na kuwa mama ‘bora,’ huvunja moyo na kusababisha wasiwasi na hisia ya hatia.”

❖ Rahisisha maisha yako: Gazeti la Newsweek lilisema hivi: ‘Kwa sababu ya hekaheka za maisha, wengi hawatafurahia maisha mazuri ya utotoni au ya familia.’ Ndiyo sababu akina mama wengi wanataka kurahisisha maisha. Unaweza kurahisisha maisha jinsi gani? Kwanza, tanguliza “mambo yaliyo ya maana zaidi,” kutia ndani wakati na utunzaji ambao watoto wako huhitaji. (Wafilipi 1:10, 11) Pili, chunguza maisha yako. Huenda ukahitaji kuacha shughuli na vitu visivyo vya lazima.

Ni nini kilicho cha maana maishani mwako? Je, ni lazima upate kila kitu mara hii, au unaweza kuahirisha miradi fulani huku ukitimiza mingine? Carolyn, mama asiye na fedha nyingi, anataja jinsi anavyoshughulikia hali yake: “Mimi hurahisisha mambo na kupunguza gharama.” Gloria, aliye na watoto watatu, anasema hivi: “Hatukuwa na fedha za kununua nguo za mitindo maalumu, lakini niliwashonea watoto nguo, na kuwaambia kwamba nguo hizo zilikuwa za kipekee kwa sababu hakuna mwingine aliyekuwa na nguo kama hizo.”

Neno la Mungu linasema kwamba mtu “ashikaye ufahamu atapata mema.” (Mithali 19:8) Ufahamu huhitajika ili kuchunguza faida za tafrija, vifaa mbalimbali, na mitindo, zinazowalemea mama na watoto. Judith, mama anayeishi huko Afrika Kusini anasema hivi: “Tunatangaziwa sikuzote juu ya vitu vipya, tekinolojia bora, na huduma mpya!” Angela, mwenye watoto wanne anayeishi Ujerumani, anasema hivi: “Ni lazima uamue kilicho muhimu na kile kitakachokusaidia, na uwasaidie watoto wako wafanye vivyo hivyo.”

❖ Fanya mabadiliko yanayowezekana: Biblia inahimiza hivi: “Shika hekima kamili na busara.” (Mithali 3:21) Ikiwa unafanya kazi ya kuajiriwa, je, mshahara wa mume wako peke yake ungetosha kuiruzuku familia? Ili kujibu swali hilo, fikiria ni kiasi gani cha mshahara wako kinachobaki baada ya kulipa ushuru, kulipa utunzaji wa watoto, kulipa nauli ya kusafiri kazini, kununua nguo za kazi, kulipa milo kwenye mikahawa, na kutenga gharama nyinginezo. Pia, huenda mume wako akatozwa ushuru wa juu ikiwa mapato yenu yaliyounganishwa yatawaweka katika kundi la watu wanaopata mapato ya juu. Huenda ukashangaa kuona kwamba kiasi kilichosalia ni kidogo sana.

Wengine hufanya kazi kwa muda wa saa chache au karibu na mahali wanapokaa, ijapokuwa watachuma pesa kidogo, ili waweze kutumia wakati zaidi pamoja na watoto. Ikiwa utaamua kuacha kazi na ikiwa kazi yako ndiyo ilikufanya ujistahi na kuhisi kwamba umefanikiwa maishani, fikiria kwa uzito jinsi utakavyoweza kuendeleza hisia hizo za maana huku ukifanya kazi za nyumbani na kutunza watoto.

❖ Omba msaada: Neno la Mungu linasema tena na tena kwamba “kilio cha kuomba msaada” (NW) kinaweza kuleta matokeo. (Kutoka 2:23, 24; Zaburi 34:15) Kilio cha mama kinapaswa kumsukuma mume amsaidie. Akikusaidia huenda mkaweza kugawana kazi za nyumbani ili mweze kutimiza miradi yenu, kama vile kutumia wakati pamoja na watoto wenu. Ikiwezekana, mama anapaswa pia kuomba msaada wa watu wa familia na marafiki waaminifu walio na mapendezi na miradi kama yake.

Akina mama wengi hupata msaada kutoka kwa waamini wenzao katika kutaniko lao la Kikristo. María, aliye na watoto watatu, aliona kwamba “kuwakaribia Wakristo wenzake kutanikoni” ni mojawapo ya njia ambazo “Mungu huonyesha kuwa anatuhurumia, anatupenda, na kutujali.”

❖ Pumzika: Hata Yesu, mwanamume mkamilifu mwenye nguvu nyingi, aliwaambia wanafunzi wake waende ‘mahali pa upweke wapumzike kidogo.’ (Marko 6:30-32) Ukitaka kuwa mama mwenye mafanikio, ni lazima usawazishe mambo nyakati za taabu. Ni kweli kwamba watoto wako wanakuhitaji, lakini wanahitaji pia kuwa na mama mwenye furaha na aliyeridhika. Unahitaji kupumzika vya kutosha.

Angela, aliyetajwa mapema, amepanga kazi yake ili apate nafasi ya kupumzika: “Ninachukua angalau nusu saa kila asubuhi kupumzika. Na jioni moja au mbili kila juma mimi na mume wangu huwaomba watoto waende mahali pengine kufanya shughuli zao polepole. Kwa njia hiyo tunaweza kuwa na muda wa saa moja bila kusumbuliwa na watoto.”

❖ Tanguliza mambo ya kiroho: Inajulikana kwamba magumu huzidi wakati akina mama wanapokosa kutambua umuhimu wa kazi yao na kukosa miradi maalumu maishani. Familia za Wakristo hupata furaha zinapofanya kazi pamoja ili kutanguliza mapenzi ya Mungu maishani. Mtume Paulo aliandika hivi: “Ujitoaji-kimungu ni wenye manufaa kwa mambo yote, kwa kuwa una ahadi ya uhai wa sasa na ule utakaokuja.” (1 Timotheo 4:8) Familia inayoishi kwa ujitoaji-kimungu kulingana na miongozo ya Mungu katika Biblia itakuwa na furaha. Hata iwapo ni mtu mmoja tu wa familia anayeishi kwa kupatana na kanuni za Biblia, bado anaweza kuboresha hali.

Adele, mama Mkristo anayefanya kazi ya kuajiriwa wakati wote, ameona manufaa ya kuwa mtu wa kiroho. Anasema hivi: “Tuna miongozo na habari nyingi sana katika vichapo vya Biblia vinavyotueleza kile ambacho watoto wetu hukabili na jinsi tunavyoweza kuwasaidia. Inafurahisha sana kuona watoto wako wakikubali mafundisho ya kiroho. Unapoona wakirekebisha mambo fulani madogo katika mienendo yao na mitazamo yao, unajua kwamba wanaelewa mafundisho yako na jitihada zako si za bure.” *

Naam, akina mama wanaweza kufanikiwa kushinda magumu wanayokabili. Mungu mwenyewe anawahakikishia akina mama wanaomtumaini kwamba kujitolea kwao na jitihada zao hazitakuwa za bure. Akina mama walio na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu wanafarijiwa na ahadi yake ya ‘kuwapa nguvu wazimiao.’—Isaya 40:29.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 16 Mashahidi wa Yehova wamechapisha vichapo kadhaa vya Biblia vya kuwazoeza watoto. Hivyo vinatia ndani Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia, Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, na Siri ya Kupata Furaha ya Familia.

[Sanduku katika ukurasa wa 10]

Malezi ya Mama Huwa na Matokeo Gani?

Ukiwa mama, nyakati nyingine huenda ukajiuliza ikiwa malezi yako yatakuwa na matokeo mazuri katika maisha ya mtoto wako. Huenda ikaonekana kana kwamba uvutano wa marafiki, walimu, tafrija, michezo ya video, na muziki huwa na matokeo makubwa kuliko malezi yako.

Fikiria Yokebedi, mama ya Musa. Aliishi katika nyakati za taabu na hakuweza kumlea mwana wake jinsi alivyotaka. Hata hivyo, alitumia nafasi aliyokuwa nayo kumfundisha. Kwanza, alionyesha imani thabiti alipozuia Musa asiuawe. Mungu alibariki imani yake kwa kumwokoa mtoto huyo na vilevile kuongoza mambo ili Yokebedi awe mlezi wake—na mama yake.—Kutoka 1:15, 16; 2:1-10.

Ni wazi kwamba Yokebedi alisaidia kusitawisha utu wa mwana wake. Musa alipokuwa mtu mzima alijihusianisha pamoja na Waebrania na Mungu wao licha ya uhusiano wake na nyumba ya Farao. Bila shaka alifanya hivyo kwa sababu wazazi wake walimzoeza na kumfundisha alipokuwa mtoto.—Waebrania 11:24-26.

Ikiwa wewe ni mama, yaelekea una nafasi nyingi zaidi kumfundisha mtoto wako kuliko Yokebedi. Je, unatumia miaka michache ya utotoni kumfundisha mtoto wako mambo ya Mungu yatakayomsaidia maishani mwake daima? Au unaruhusu utamaduni uliopo kufinyanga utu wa mtoto wako?

[Picha katika ukurasa wa 10]

Wagawie wengine kazi za nyumbani, uwe na wakati wa kufanya mambo yako binafsi, na utangulize mambo ya kiroho