Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sikiliza Ili Ujifunze

Sikiliza Ili Ujifunze

Sikiliza Ili Ujifunze

RIPOTI moja katika gazeti la Toronto Star yasema hivi: “Tumejifunza asilimia 85 ya mambo tunayojua kupitia kusikiliza.” Ingawa sisi hutumia muda wetu mwingi tukisikiliza, sisi hukengeuka, hujishughulisha mno na mambo mengine au kusahau robo tatu ya mambo tunayosikia wakati huo. Tarakimu hizo zinazoamsha fikira zinaonyesha kwamba tunahitaji kuboresha uwezo wetu wa kusikiliza.

Kulingana na ripoti hiyo, “mazoea mabaya ya kusikiliza ndiyo kiini cha matatizo mengi katika jamii.” Rebecca Shafir, mtaalamu wa usemi na mawasiliano, anaamini kuwa jambo hilo ni mojawapo ya visababishi vya kujiua, jeuri shuleni, kuvunjika kwa familia, na matumizi ya dawa za kulevya.

Wanasayansi wa kijamii wamechunguza na kupata kwamba watu wanatofautiana katika njia zao za kusikiliza. Baadhi yao hupenda kusikiliza hadithi juu ya mambo ya watu na sehemu zote za hadithi zenye kuvutia kutia ndani mambo madogo-madogo. Wengine hupenda kusikiliza mambo yaliyotukia na hutaka msemaji aeleze jambo kuu haraka. “Kwa hiyo, mtu anayependa kusikiliza hadithi juu ya mambo ya watu anapozungumza na mtu anayependa kusikiliza mambo yaliyotukia, huenda mazungumzo yao yakakosa kufaulu,” lasema gazeti Star.

Basi Yesu alikuwa na sababu nzuri ya kukazia uhitaji wa ‘kukazia uangalifu jinsi msikilizavyo.’ (Luka 8:18) Kusikiliza kuzuri kwaonyesha una tabia nzuri. Hiyo ni sehemu muhimu ya maongezi yenye matokeo. Baadhi ya madokezo juu ya jinsi ya kusikiliza wakati wa maongezi yanahusisha kuepuka mambo yanayokengeusha fikira, kuegama mbele kidogo, na kutoa ishara ya kuonyesha unasikiliza kama vile kumwangalia msemaji kwenye macho na kutikisa kichwa ukionyesha kuwa unaitikia. Kwa sababu sisi hujifunza mambo mengi kwa kusikiliza vizuri, kukazia uangalifu jinsi tunavyosikiliza ni jambo ambalo sote tunapaswa kuendelea kuboresha.