Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mbona Yule Ninayeishi Naye Ni Mgumu Sana?

Mbona Yule Ninayeishi Naye Ni Mgumu Sana?

Vijana Huuliza . . .

Mbona Yule Ninayeishi Naye Ni Mgumu Sana?

‘Mimi ni mtu nadhifu sana. Lakini ninapofika nyumbani, mimi humpata yule ninayeishi naye amelala sakafuni akitazama televisheni, huku karatasi na mahindi yaliyokaangwa yakiwa yametapakaa kila mahala. Kila mara ninaporudi nyumbani, mimi hutarajia kupata hali hiyo, nami sipendi kuingia ndani ya nyumba hiyo.’—David.

“Msichana niliyekuwa nikiishi naye aliendekezwa sana na wazazi wake. Alitaka kufanyiwa kazi zote. Na kila mara alitaka mambo yafanywe jinsi alivyotaka.”—Renee. *

“GAZETI la U.S.News & World Report lilisema kwamba “kujifunza kuvumilia tabia za kiajabu za mtu usiyemfahamu kwaweza kukufunza . . . kubadilikana na kukubali maoni ya watu wengine. Lakini mara nyingi kuvumilia hali hiyo si rahisi.” Watu ambao wamewahi kuishi na mtu mwingine wanaweza kukubali kauli hiyo.

Wanafunzi wengi wa chuo kikuu huishi na mtu mwingine ili kupunguza gharama nyingi za masomo. Vijana wengine huhama nyumbani kwao na kuishi na mtu mwingine ili wajitegemee. Vijana wengi Wakristo wamekubali kuishi na mtu mwingine ili kushughulikia masilahi ya kiroho. (Mathayo 6:33) Vijana hao huona kwamba wakishirikiana na mtu mwingine kulipa gharama mbalimbali hiyo itawasaidia kutumikia kama waeneza-evanjeli wa wakati wote. Nyakati nyingine mishonari na wale wanaotumikia katika ofisi mbalimbali za tawi za Mashahidi wa Yehova huishi na mtu mwingine. *

Gazeti la Amkeni! liliwahoji wavulana na wasichana kadhaa ambao wamewahi kuishi na wengine. Wote walikubali kwamba mbali na kukusaidia kulipa kodi ya nyumba, yule unayeishi naye anaweza kuwa mwandamani wako, mnayeweza kuzungumza naye na kufanya mambo pamoja. Msichana anayeitwa Lynn anasema hivi: “Tulikuwa tukizungumza kuhusu mambo ya wanawake au kutazama filamu pamoja.” Naye Renee anasema hivi: “Yule unayeishi naye anaweza pia kukutia moyo. Ni jambo zuri kutiwa moyo na yule unayeishi naye wakati unapojaribu kufanya kazi, kulipa gharama zako, na kuhubiri.”

Hata hivyo, kuishi na mtu mwingine—hasa ambaye humjui hata kidogo—kwaweza kuwa vigumu sana. Gazeti la U.S.News & World Report lilisema hivi kuhusu hali katika vyuo: ‘Ijapokuwa vyuo vingi hujitahidi sana kuchagua vizuri watu ambao wataishi pamoja, mara nyingi watu hao hawafurahii uchaguzi huo.’ Kwa kweli, kutoelewana kati ya wanafunzi wanaoishi pamoja vyuoni kumesababisha ujeuri! Vituo vya Internet vimeanzishwa ili kuwaruhusu wanafunzi kueleza waziwazi malalamiko yao mengi kuhusu watu ambao wanaishi nao. Kwa nini mara nyingi ni vigumu kuishi pamoja na mtu mwingine?

Kuishi na Mtu Usiyemjua

Mark anasema hivi: “Kuanza kuishi na mtu usiyemjua ni jambo lenye kupendeza kwa njia fulani. Hujui tabia yake.” Kwa kweli, mtu anaweza kuwa na wasiwasi sana anapofikiria juu ya kuishi na mtu mwingine ambaye labda ana mapendezi tofauti. Ni kweli kwamba Wakristo wanapaswa kuwa na mapendezi mengi yenye kupatana na mambo mengi ya kuzungumzia. Hata hivyo, David anakubali hivi: “Niliogopa sana kuishi na mtu mwingine.”

Hata hivyo, baadaye David aligundua kwamba mtu aliyeambiwa aishi naye alikuwa pia amelelewa katika mazingira sawa na yake. Lakini nyakati nyingine watu wanaochaguliwa kuishi pamoja hawafanikiwi sana. Mark anasema hivi: “Mtu niliyeishi naye mara ya kwanza alikuwa mnyamavu. Mnapoishi na mtu mwingine katika chumba kimoja, mnahitaji kuzungumza. Lakini hakuwa akizungumza sana. Niliudhika sana.”

Tofauti za malezi zaweza kusababisha mfadhaiko na mikwaruzano mingine. Lynn asema hivi: “Unapoanza kuishi peke yako, unataka kufanya mambo jinsi upendavyo. Lakini muda si muda unatambua kwamba unahitaji kuwafikiria watu wengine.” Kwa kweli, unapohama kutoka kwenye mazingira mazuri ya kwenu, unaweza kushangaa sana unapoona jinsi maoni ya watu wengine yalivyo tofauti.

Malezi Tofauti Hutokeza Maoni Tofauti

Mambo mengi hutegemea iwapo mtu alizoezwa ama hakuzoezwa na wazazi wake. (Mithali 22:6) Kijana anayeitwa Fernando anasema hivi: “Mimi ni nadhifu, na yule niliyeishi naye alikuwa akifanya mambo shaghalabaghala. Kwa mfano alikuwa akitupa vitu ovyoovyo kwenye kabati ya nguo. Mimi nilikuwa nikipanga nguo zangu vizuri.” Nyakati nyingine watu hutofautiana sana.

Renee anakumbuka jambo hili: “Chumba cha kulala cha mtu fulani niliyeishi naye kilikuwa kichafu sana! Nimewahi pia kuishi pamoja na watu ambao hawapangusi meza baada ya kula wala kuosha vyombo kwa muda wa siku mbili au tatu.” Naam, kuhusu kazi za nyumba, maneno ya Mithali 26:14 yanawafaa watu fulani: “Kama vile mlango ugeukavyo katika bawaba zake; kadhalika mtu mvivu katika kitanda chake.”

Kwa upande mwingine, huwezi kufurahia kuishi pamoja na mtu anayependa usafi kupita kiasi. Msichana mmoja anayeitwa Lee alisema hivi kuhusu msichana aliyekuwa akiishi naye: “Alitaka kusafisha nyumba kila wakati. Mimi si mchafu, lakini nyakati nyingine niliacha vitu, kama vile vitabu, juu ya kitanda changu. Na aliona kwamba ni lazima arekebishe hali hiyo.”

Yule unayeishi naye anaweza kuwa na maoni tofauti na yako kuhusu usafi wa mwili. Mark anasema hivi: “Yule ninayeishi naye huamka akiwa amechelewa mno. Yeye hukimbia kwenye beseni, halafu anajitupia maji kidogo kichwani, kisha anaondoka.”

Tofauti za malezi na nyutu zaweza kuathiri uchaguzi wa burudani na tafrija. Mark anasema hivi kuhusu mtu anayeishi naye: “Mimi hupenda muziki tofauti na ule ambao anapenda.” Hata hivyo, watu wanaoishi pamoja wakiheshimiana, tofauti hizo zaweza kuleta faida, labda zikiwasaidia wote wawili kupenda mambo mengi zaidi. Lakini mara nyingi, tofauti hizo husababisha kutoelewana. Fernando anasema hivi: “Mimi hupenda muziki wa Kihispania, lakini yule ninayeishi naye huuchambua kila wakati.”

Tatizo la Simu

Kisababishi kikuu cha kutoelewana kinaweza kuwa matumizi ya simu. Mark anasema hivi: “Ninapotaka kulala, yule ninayeishi naye huzungumza kwa muda mrefu kwa simu. Baada ya muda jambo hilo laweza kuudhi.” Lynn anakumbuka jambo hili pia: “Nyakati nyingine marafiki wa msichana niliyekuwa ninaishi naye walikuwa wakipiga simu saa tisa au saa kumi usiku. Wakati ambapo hakuwepo, ilinibidi niamke ili kupokea simu hizo.” Walitatuaje jambo hilo? “Ilibidi kila mmoja wetu awe na simu yake.”

Hata hivyo, sio vijana wote wanaweza kununua simu, na wengine hulazimika kutumia simu pamoja. Hilo laweza kusababisha mikwaruzano. Renee anakumbuka jambo hili: “Mmojawapo wa wasichana niliyekuwa nikiishi nao alikuwa na mchumba, na mara nyingi alizungumza kwa muda mrefu kwa simu. Mwezi mmoja alipata bili ya simu ya dola 90 za Marekani. Alitazamia sote tumsaidie kulipa pesa hizo kwa sababu sote tulikubali kushirikiana kulipa gharama ya simu kwa usawa.”

Tatizo jingine laweza kutokea unapotaka kutumia simu. Lee anasema hivi: ‘Yule niliyeishi naye alinizidi umri. Na tulikuwa na simu moja tu. Nilitumia simu mara nyingi kwa sababu nilikuwa na marafiki wengi. Lakini yeye hakulalamika. Nilidhani kwamba iwapo angetaka kutumia simu angeniambia. Sasa ninatambua kwamba sikumjali.’

Kukosa Faragha

David asema hivi: ‘Kila mtu anahitaji kuwa peke yake wakati mwingine. Nyakati nyingine, mimi huhitaji kupumzika bila kufanya lolote.’ Hata hivyo, kupata wakati wa kuwa peke yako kwaweza kuwa jambo gumu iwapo unaishi na mtu mwingine. Mark anasema hivi: ‘Mimi hupenda kuwa peke yangu wakati fulani. Kwa hiyo jambo gumu zaidi limekuwa kukosa faragha. Ratiba yangu inafanana na ya yule ninayeishi naye. Kwa hiyo ni vigumu kuwa na faragha.’

Hata Yesu Kristo alihitaji kuwa peke yake wakati mwingine. (Mathayo 14:13) Kwa hiyo, mtu anaweza kuudhika wakati anaposhindwa kusoma, kujifunza, au kutafakari kwa sababu yule mwingine yupo. Mark anasema hivi: ‘Ni vigumu kujifunza kwa sababu yule ninayeishi naye anakuwa na shughuli zake kila wakati nyumbani. Mara kuna wageni, mara anazungumza kwa simu, mara anatazama televisheni au kusikiliza redio.’

Hata hivyo, japo ni vigumu kumvumilia yule unayeishi naye, maelfu ya vijana wamefaulu. Makala nyingine katika mfululizo huu zitazungumzia njia kadhaa za kufaulu kuishi na mwingine.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

^ fu. 6 Japo shauri hili limeandikwa kwa ajili ya vijana, huenda pia likawasaidia watu wenye umri mkubwa ambao wamelazimika kuishi na mtu mwingine baada ya hali zao kubadilika, kama vile kifo cha mwenzi wa ndoa.

[Picha katika ukurasa wa 16, 17]

Mapendezi tofauti ya muziki yaweza kusababisha magumu

[Picha katika ukurasa wa 18]

Kutojali mwingine kwaweza kusababisha kutoelewana