Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Uhitaji wa Kila Mtu

Uhitaji wa Kila Mtu

Uhitaji wa Kila Mtu

Unahitaji chakula. Unahitaji maji. Unahitaji hewa. Unahitaji makao ili ujikinge na hali mbaya ya hewa. Hayo ni mahitaji ya kila mwanadamu na viumbe wengine wengi duniani. Hata hivyo, wanadamu wana uhitaji mmoja wa pekee sana. Ni upi huo?

Reginald W. Bibby, Mkanada ambaye ni mtaalamu wa elimu ya jamii, aliandika hivi: “Wanadamu wana mahitaji ambayo yanaweza kushughulikiwa tu na dini.” Na makala moja katika jarida la American Sociological Review la Februari 2000 ilisema hivi: “Huenda wanadamu watapendezwa na mambo ya kiroho sikuzote.”

Naam, katika historia yote wanadamu wamehitaji kuabudu. Kwa karne nyingi, wengi wamejiunga na dini ili kutosheleza uhitaji huo. Lakini hali zinabadilika. Katika nchi nyingi zilizoendelea kiviwanda—kama vile huko Amerika Kaskazini na Ulaya Kaskazini—watu wengi sana wanaacha makanisa. Je, hiyo inaonyesha kwamba dini inakwisha? La hasha!

Gazeti la Sweden la Svenska Dagbladet lasema kwamba “ripoti zinazoonyesha kuwa dini inakwisha si za kweli.” Basi watu huenda wapi wanapoacha makanisa? Gazeti hilo laendelea kusema hivi: ‘Siku hizi watu wana mwelekeo wa kutoshirikiana na kanisa lolote. Badala yake, wanaweza kuchagua na kubuni mambo wanayotaka kuamini kutoka kwa mafundisho ya dini mbalimbali zilizopo ulimwenguni. Wanaweza kuchagua chochote, kama vile kuamini vito vinavyotumiwa katika uponyaji na hata kuvalia joho la mtawa wa Kibudha. Wanapochoshwa na mambo hayo waliyochagua kuamini, wanaweza kuyatupilia mbali na kuanza kuamini mambo mengine.’

Watafiti wa mambo ya dini huita mwelekeo huo “dini ya mtu binafsi” au “dini ya kuwazia tu.” Bibby, yule mtaalamu wa elimu ya jamii aliyenukuliwa hapo awali, na watu wengine husema kwamba dini hizo huundwa ili zifaane na mapendezi ya watu. Sasa katika nchi fulani za Ukristo, idadi kubwa sana ya watu wanaofuata mambo ya dini imefanyizwa na wale ambao wamechagua kuamini mafundisho yale wanayoyapenda.

Hebu fikiria matokeo ya uchunguzi uliofanywa huko Sweden, mojawapo ya nchi zenye watu wengi walioacha dini. Uchunguzi huo ulionyesha kwamba watu 2 kati ya 3 walidai kwamba wao ni Wakristo ‘wanaoabudu jinsi wapendavyo.’ Wengine walisema hivi: “Ninafuata maoni yangu kuhusu Ukristo,” “Sifurahi ninapokuwa kanisani,” “Sipendi kwenda kanisani kuwasikiliza makasisi,” au “Naweza kujifungia katika chumba changu na kusali peke yangu.” Watu wengi walionyesha kwa kiasi fulani kwamba wanaamini kuzaliwa upya baada ya kifo au kwamba Mungu amewapangia mambo kimbele. Wengi walisema wanaamini kwamba kuna nguvu au uwezo fulani kama wa mungu lakini hawawezi kuufafanua.

Uchunguzi mwingine ulionyesha kwamba watu wengi hufuata mambo ya dini wanapokuwa tu nje, wakifurahia kutazama mandhari. Mwanamke mmoja mchanga ambaye ni mkulima alisema hivi: “Nadhani kwamba unapoenda msituni au mashambani ndipo unapokuwa karibu sana na Mungu.” Mtu mwingine aliyehojiwa, ambaye alidai kwamba hafuati mambo ya dini, alisema hivi: “Ninapoenda msituni, ninaona ni kana kwamba niko katika hekalu kubwa. . . . Hata hivyo sijui ni nani anayeongoza mambo huko, lakini ninahisi hivyo.” Watu wengine walisema kwamba sehemu za mashambani ni takatifu na zenye kutia kicho na kwamba kwenda katika maeneo hayo huwapa nguvu mpya, amani, na utulivu. Mtu mmoja aliyeshiriki katika uchunguzi huo alikamilisha ripoti yake kwa kutoa maelezo haya mafupi: “Mungu anaweza kupatikana msituni.”

Mwelekeo huo unaonekana katika sehemu nyingi za ulimwengu leo. Thomas Luckmann, Mmarekani ambaye ni mtaalamu wa mambo ya dini, alisema kwamba katika nchi zilizoendelea kiviwanda watu wameacha kufuata mambo ya dini katika makanisa na badala yake wanafuata ‘mapendezi yao binafsi ya kidini.’ Hivyo, watu hao hufanyiza imani zao kwa kuchagua maoni mbalimbali ya kidini na kuyajumlisha pamoja ili kuabudu jinsi wapendavyo.

Huenda ukajiuliza hivi, ‘Je, dini na makanisa mashuhuri yanapuuzwa na kutupiliwa mbali katika jamii? Ikiwa ndivyo, kwa nini?’ Maswali hayo yanajibiwa katika makala inayofuata.

[Picha katika ukurasa wa 3]

Mtafiti mmoja alikata kauli hii alipozungumzia jinsi ambavyo watu wameanza kutafuta mambo ya kiroho katika mazingira ya asili: “Mungu anaweza kupatikana msituni”