Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Amani ya Ulimwenguni Pote Si Ndoto Tu!

Amani ya Ulimwenguni Pote Si Ndoto Tu!

Amani ya Ulimwenguni Pote Si Ndoto Tu!

IWAPO Alfred Nobel angeona matukio ya karne iliyopita, je, angeendelea kutarajia amani ya ulimwenguni pote kwa hamu? Huenda angefurahi kujua kwamba watu wengi wamejitahidi sana kukomesha vita. Hata hivyo, angehuzunishwa na jambo fulani. Profesa Hugh Thomas anaeleza jambo hilo vizuri: ‘Ijapokuwa kwa ujumla kumekuwa na maendeleo ya kijamii katika karne ya 20 na serikali zimejitahidi hata zaidi kuwahangaikia maskini, karne hiyo imejulikana kwa bunduki za rashasha, vifaru, ndege za kurusha makombora za B-52, na mabomu ya nyuklia. Mapigano ambayo yalizuka katika karne hiyo yalisababisha umwagikaji mkubwa wa damu na uharibifu mkubwa kuliko katika kipindi kinginecho chote.’ Thomas anaendelea kusema kwamba “basi si watu wote wanaoweza kukubali kwamba maendeleo yalifanywa katika kipindi hicho.”

Je, mataraja ya kupata amani ya ulimwenguni pote yanaelekea kutimia katika karne hii ya 21? La hasha! Gazeti la Newsweek linasema hivi kuhusu yale mashambulizi ya kigaidi yaliyotokea huko New York City na Washington, D.C. mnamo Septemba 11, 2001: ‘Iwapo ndege aina ya 767 zaweza kutumiwa kama silaha, basi ni kana kwamba hakuna kitu kisichoweza kutokea, hakuna kitu kinachoweza kuwa cha kipumbavu, na jambo baya zaidi ni kwamba yaonekana hakuna kitu kinachoweza kuzuiwa.’

Watu fulani wanasema kwamba ili kuwepo na amani ulimwenguni pote, ni lazima mambo mawili yatukie: Kwanza, wanadamu wanapaswa kubadili sana maoni na tabia zao; na pili, mataifa yote yapasa kuungana ili kufanyiza serikali moja. Biblia inatabiri wakati ambapo amani itakuwepo—lakini si kupitia jitihada za wanadamu. Zaburi 46:9 inasema hivi kumhusu Muumba, Yehova Mungu: “Avikomesha vita hata mwisho wa dunia.” (Italiki ni zetu.) Mungu atatimizaje jambo hilo? Kwa kutumia Ufalme wake, ambao watu wengi wanyofu wamesali mara nyingi juu yake. Ufalme huo si hali ya moyoni isiyoeleweka bali ni serikali halisi ambayo Mungu atatumia ili kuleta amani kotekote duniani. Nabii Isaya alipuliziwa kutabiri kwamba raia wa serikali hiyo “hawatajifunza vita tena kamwe.” (Isaya 2:4) Kupitia programu ya elimu ya ulimwenguni pote, watu watajifunza kuishi kwa amani na ndiyo sababu “watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu.”

Mashahidi wa Yehova wanafanya hivyo hata sasa. Ijapokuwa wao hutoka katika makabila mbalimbali na wanaishi katika nchi zaidi ya 200, wao hukataa kupigana na wanadamu wenzao. Msimamo wao wa kutounga mkono upande wowote katika ulimwengu wenye vita nyingi unaonyesha kwamba amani si ndoto tu bali ni jambo linalowezekana.

Je, ungependa kujifunza zaidi juu ya tumaini hilo la amani ya kweli linalopatikana katika Biblia? Tafadhali waandikie wachapishaji wa gazeti hili, ukitumia anwani inayokufaa kati ya zile zilizoorodheshwa kwenye ukurasa wa 5, au uwasiliane na Mashahidi wa Yehova katika eneo lako.