Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Faraja kwa Waombolezao

Faraja kwa Waombolezao

Faraja kwa Waombolezao

MASHAMBULIZI ya kigaidi yaliyofanyika Septemba 11, 2001, katika New York City na Washington, D.C., yalishtua watu kotekote ulimwenguni. Kwa siku moja, maelfu ya watu walikufa, kutia ndani wazimamoto mashujaa, polisi, na wataalamu wa tiba.

Tangu tukio hilo, Mashahidi wa Yehova wamefanya jitihada ya pamoja ya kufariji waliofiwa na wapendwa wao wakati wa msiba huo. Wamefanya hivyo ili ‘kuwatibu waliovunjika moyo’ na ‘kuwafariji wote wanaoomboleza.’—Isaya 61:1, 2, Biblia Habari Njema.

Kwa miaka mingi, Mashahidi wa Yehova wametambua kwamba mara nyingi wale waliofiwa na wapendwa wao hujiuliza maswali yafuatayo. Biblia inatoa majibu yake. Kwa nini usichunguze Maandiko yaliyoonyeshwa hapa chini katika Biblia yako?

Je, kifo cha binadamu huwa kimepangiwa kimbele?

Katika Mhubiri 9:11, NW, Biblia inasema kuwa “wakati na tukio lisilotazamiwa” (“nasibu,” New English Bible) huwapata wanadamu wote. Ikiwa kifo huwa kimepangiwa kimbele, kwa nini Biblia inatusihi tuzingatie usalama?—Kwa mfano, ona Kumbukumbu la Torati 22:8.

Kwa nini sisi hufa?

Wanadamu wa kwanza wawili, Adamu na Hawa, waliwekwa katika dunia iliyokuwa paradiso. Iwapo hawangefanya dhambi, hawangekufa. Wanadamu wangekufa ikiwa tu wangekosa kumtii Mungu. (Mwanzo 1:28; 2:15-17) Kwa kuhuzunisha, Adamu na Hawa hawakumtii Muumba wao. Tokeo likawa adhabu ya kifo. Kwa sababu wanadamu wote wametoka kwa Adamu na Hawa, wote wamerithi dhambi na kifo. Biblia inaeleza hivi: “Kupitia mtu mmoja [Adamu] dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikasambaa kwa watu wote.”—Waroma 5:12.

Wafu wako katika hali gani?

Baada ya Adamu kuasi, Mungu alisema hivi: ‘Utairudia ardhi, ambayo katika hiyo ulitwaliwa; kwa maana u mavumbi wewe, nawe mavumbini utarudi.’ (Mwanzo 3:19) Kwa hiyo, kifo ni hali ya kuwa bila fahamu kabisa, yaani, kutokuwapo. Biblia inasema hivi: “Walio hai wanajua ya kwamba watakufa, lakini wafu hawajui neno lo lote.” (Mhubiri 9:5, italiki ni zetu.) Biblia pia inasema kwamba mtu akifa, yeye “huurudia udongo wake, siku hiyo mawazo yake yapotea.”Zaburi 146:3, 4, italiki ni zetu.

Je, tuna nafsi isiyoweza kufa?

Biblia inafundisha kuwa nafsi yako ni wewe, bali si kitu cha kuwaziwa tu kinachookoka wakati mtu anapokufa. (Mwanzo 2:7; Mithali 2:10) Kwa sababu hiyo, tunaweza kusema kwamba mtu anapokufa, nafsi imekufa. Biblia inasema hivi kwa wazi: “Nafsi [yaani, mtu] inayofanya zambi, itakufa.”—Ezekieli 18:4, Zaire Swahili Bible.

Kuna tumaini gani kwa wafu?

Biblia inafunua kwamba ni kusudi la Mungu kuwarudisha watu waliokufa kwenye uhai kwa kuwafufua waishi katika paradiso duniani, ambapo ugonjwa na kifo havitakuwapo tena. Yesu alisema: “Saa inakuja ambayo katika hiyo wote wale waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho watasikia sauti yake na kutoka.”—Yohana 5:28, 29; Ufunuo 21:1-4.

Wakati alipokuwa akizungumza kuhusu rafiki yake Lazaro aliyekuwa amekufa karibuni, Yesu alilinganisha kifo na usingizi. (Yohana 11:11-13) Na zaidi ya hilo, baada ya kufufuliwa na Yesu, Lazaro hakusema alikuwa mahali popote penye moto wa mateso au katika raha mstarehe kwa muda mfupi aliokuwa amekufa. (Yohana 11:37-44) Hilo linaeleweka, kwa kuwa wafu hawana fahamu. Wao hawapatwi na mateso lakini wanangoja “saa” ambayo watainuliwa. Uhakika wa kwamba Yesu alimfufua Lazaro unaonyesha kuwa wafu wanaweza kuishi tena. Kwa muujiza huo, Yesu alionyesha kwa kadiri ndogo yale yatakayofanyika duniani chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu. (Matendo 24:15) Ni faraja iliyoje kwa wale wanaofiwa na wapendwa wao katika wakati huu wenye magumu mengi!