Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Mungu Huunga Mkono Vita?

Je, Mungu Huunga Mkono Vita?

Maoni ya Biblia

Je, Mungu Huunga Mkono Vita?

MARA nyingi, watawala, majenerali, na hata makasisi wametangaza vita au kuiunga mkono katika jina la Mungu! Mnamo mwaka wa 1095, Krusedi ya Kwanza ambayo iliungwa mkono na Papa Urban wa Pili ilianzisha kampeni ya kulirudisha “Jiji Takatifu” la Yerusalemu liwe mkononi mwa Jumuiya ya Wakristo. Lakini kabla ya kufikia lengo lao, kikosi kimoja cha wapiganaji wa Vita Takatifu kiliangamizwa na Waturuki, ambao walikuwa na bidii nyingi kwa ajili ya Allah ambao ulifanana na bidii ya wale wapiganaji waliokuwa na imani thabiti katika Utatu.

Mnamo Agosti 1914, kijana mmoja Mjerumani aliandika hivi akiwa katika kambi yao wakati wa Vita ya Kwanza ya Ulimwengu: “Ikiwa kuna haki na ikiwa Mungu anaongoza matukio mbalimbali katika historia—jambo ambalo nina uhakika nalo—basi ni lazima tutashinda.” Mwezi huohuo Czar Nicholas wa Pili aliamuru majeshi ya Urusi yapigane na Ujerumani akisema: “Ninatuma salamu zangu changamfu kwa majeshi yangu yenye ujasiri na washirika wangu mashuhuri. Mungu yuko pamoja nasi!”

Wakiwa wamejasirishwa hivyo, wanajeshi wengi wameingia katika maeneo ya mapigano wakiwa na imani kwamba Mungu angewaunga mkono. Wengi hufikiri kuwa Mungu amewaruhusu kupigania uhuru, na wanasema kuwa vita zinazotajwa katika Maandiko ya Kiebrania (ambayo mara nyingi huitwa Agano la Kale) zinaunga mkono jambo hilo. Je, ufafanuzi wao wa Neno la Mungu ni sahihi?

Vita Katika Israeli ya Kale

Yehova Mungu aliamuru kwamba Waisraeli walipaswa wapigane vita ili kuwaondoa Wakanaani waliopotoka kutoka kwenye Bara Lililoahidiwa. (Mambo ya Walawi 18:1, 24-28; Kumbukumbu la Torati 20:16-18) Kama vile Mungu alivyotumia gharika ya siku za Noa na moto uliotumiwa wakati wa Sodoma na Gomora kuwaadhibu watenda mabaya, ndivyo alivyotumia taifa la Israeli ili kutekeleza adhabu ya kifo.—Mwanzo 6:12, 17; 19:13, 24, 25.

Kulingana na Biblia, wakati mwingine Mungu alielekeza Israeli kupigana vita, hata kabla ya kutishwa na maadui. Taifa hilo lilipomtii Yehova, lilipata ushindi. (Kutoka 34:24; 2 Samweli 5:17-25) Lakini taifa hilo la Israeli lilipojaribu kupigana kinyume cha maagizo ya Mungu, lilipatwa na maafa. Hebu fikiria mfano wa Mfalme Yeroboamu. Yeye alipuuza onyo la kiunabii la moja kwa moja na akatuma jeshi lake kubwa kufanya vita ya wenyewe kwa wenyewe dhidi ya Yuda. Mapigano yalipomalizika, wanajeshi 500,000 wa Yeroboamu walikuwa wamekufa. (2 Mambo ya Nyakati 13:12-18) Wakati mmoja hata Mfalme Yosia mwaminifu alipigana vita ambayo haikumhusu. Uamuzi huo wa haraka-haraka ulisababisha kifo chake.—2 Mambo ya Nyakati 35:20-24.

Matukio hayo yanaonyesha nini? Yanaonyesha kuwa katika Israeli ya kale, uamuzi wa kupigana vita ulifanywa na Mungu. (Kumbukumbu la Torati 32:35, 43) Aliwaamuru watu wake wapigane ili kutimiza makusudi fulani. Hata hivyo, makusudi hayo yalitimia kitambo sana. Zaidi ya hilo, Yehova alitabiri kwamba wale wanaomtumikia “katika siku za mwisho, . . . watafua panga zao ziwe majembe” na “hawatajifunza vita tena kamwe.” (Isaya 2:2-4) Ni wazi kwamba vita zinazotajwa katika Biblia haziungi mkono mapigano yoyote ya siku hizi. Mungu hajatoa amri wala kuelekeza mapigano hayo.

Matokeo ya Mafundisho ya Kristo

Alipokuwa duniani, Yesu alionyesha jinsi upendo usio na ubinafsi unavyoweza kuchukua mahali pa chuki, alipoamuru hivi: “Mpendane kama vile mimi nimewapenda nyinyi.” (Yohana 15:12) Pia, alisema hivi: “Wenye furaha ni wenye kufanya amani.” (Mathayo 5:9) Hapo neno la Kigiriki lililotafsiriwa “kufanya amani” linamaanisha zaidi ya kuwa na hali ya utulivu. Linatia ndani kusitawisha amani, kujitahidi kutokeza nia njema.

Wakati Yesu alipokamatwa, mtume Petro alijaribu kumtetea akitumia silaha ambayo ingesababisha kifo. Lakini Mwana wa Mungu alimkemea kwa kusema: “Rudisha upanga wako mahali pao, kwa maana wale wote wauchukuao upanga wataangamia kwa upanga.” (Mathayo 26:52) Wakristo wa karne ya kwanza walitumiaje shauri hilo? Ona manukuu yafuatayo.

“Kuchunguza kwa makini habari zote zinazopatikana [kwaonyesha] kwamba, kufikia wakati wa Marcus Aurelius [121-180 W.K.], hakuna Mkristo aliyejiandikisha katika jeshi; na hakuna mwanajeshi aliyeendelea katika utumishi wa kijeshi baada ya kuwa Mkristo.”—The Rise of Christianity.

“Mwenendo wa Wakristo [wa mapema] ulikuwa tofauti sana na ule wa Waroma. . . . Kwa kuwa Kristo alikuwa amehubiri amani, wao walikataa kuwa wanajeshi.”—Our World Through the Ages.

Kwa kuwa wafuasi wa Kristo walikataa kutumikia katika jeshi la maliki, wengi wao waliuawa na Waroma. Kwa nini Wakristo walidumisha msimamo huo ambao haukupendwa na wengi? Kwa sababu Yesu aliwafundisha kuwa watu wenye kufanya amani.

Vita za Siku Hizi

Hebu wazia hali yenye kuogopesha iwapo wafuasi wa Kristo wangehusika katika vita ya majeshi yanayopingana, wakijaribu kuuana. Hilo lingekuwa kinyume cha kanuni za Kikristo. Wale wanaomtii Mungu wa Biblia hawawezi kumwumiza mtu yeyote—hata maadui wao. *Mathayo 5:43-45.

Ni wazi kwamba Mungu hawezi kukubali vita za ukatili kati ya wanadamu siku hizi. Wakiwa watu wenye kufanya amani, Wakristo wa kweli wanahubiri amani ambayo Ufalme wa Mungu utaleta ulimwenguni kote.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 17 Biblia inataja “Har–Magedoni,” ambayo ni “vita ya siku kubwa ya Mungu Mweza-Yote.” Hiyo si vita ya wanadamu, bali ni uharibifu ambao Mungu atafanya kuelekea watu wanaotenda mabaya tu. Kwa hiyo, Har–Magedoni haiwezi kutumiwa kuunga mkono mapambano ya siku hizi au hata kufikiri kwamba Mungu anayakubali.—Ufunuo 16:14, 16; 21:8.

[Picha katika ukurasa wa 20]

Jenerali Francisco Franco wa Hispania, pamoja na baadhi ya makasisi Wakatoliki

[Hisani]

U.S. National Archives photo

[Picha katika ukurasa wa 21]

Makasisi wa Kanisa Othodoksi la Ugiriki wanawabariki wanajeshi kabla ya kwenda huko Kosovo, mnamo Juni 11, 1999

[Hisani]

AP Photo/Giorgos Nissiotis