Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuutazama Ulimwengu

Kuutazama Ulimwengu

Kuutazama Ulimwengu

Wanyama-Vipenzi Wanono

“Unono ndio ugonjwa unaoathiri zaidi mbwa na paka,” kulingana na ripoti ya gazeti la The Globe and Mail la Kanada. “Visababishi vya unene ni sawa kwa binadamu na wanyama: mazoea mabaya ya kula na kukosa mazoezi.” Berney Pukay, wa baraza la Shirika la Madaktari wa Mifugo wa Kanada, analaumu mtindo wa maisha wa wale walio na wanyama-vipenzi akisema: “Hatupati mazoezi ya kutosha kwa sababu tuna shughuli nyingi. Mbwa hapati mazoezi ya kutosha kwa sababu mwenye mbwa ana shughuli nyingi. Kwa kuwa tunahitaji chakula cha kuburudisha, wanyama wetu pia hupata chakula cha kuburudisha.” Gazeti la Globe linaonya kwamba “wanyama-vipenzi wana hatari kubwa zaidi ya kupata ugonjwa wa sukari, ugonjwa wa moyo, kupanda kwa shinikizo la damu na yabisi-kavu. . . . Wao hufa mapema kuliko wanyama wengine wenye afya.” Kwa kawaida, matibabu ya wanyama-vipenzi wanono hutia ndani kuwapunguzia chakula, na mbwa hufanyishwa mazoezi zaidi.

Matatizo Wakati wa Likizo

“Iwapo unafunga mizigo yako ili uende likizo, basi uwe mwangalifu!” laonya gazeti la Hamburg Die Welt. Zogo na mabishano huharibu likizo katika jamaa nyingi. Kulingana na uchunguzi mmoja uliofanywa nchini Ujerumani, “talaka moja kati ya tatu ilianza kujadiliwa baada ya kutoka likizo.” Kwa nini? Sababu moja ni kule kukaribiana na kushirikiana ambako watu hawajazoea, kunakofanya washiriki wa familia kuchokozana. Ili kuepuka matatizo, wanasaikolojia wanapendekeza kwamba likizo ipangwe mapema, na mambo ya kufanya pamoja yaratibiwe kwa njia ya kwamba yatawawezesha watu mmoja-mmoja kufanya mambo wanayopenda. Gazeti hilo la Die Welt linasema kwamba “kutarajia mambo mengi kupita kiasi huchangia [matatizo wakati wa likizo]. Kwa sababu mwaka una miezi kumi na moja ya kufanya kazi na mambo mengine ya kila siku, majuma matatu au manne ya likizo yanapaswa kutumiwa kufanya mambo ambayo hayakufanywa katika mwaka huo.”

Watoto Wengi Zaidi Wanazaliwa Nje ya Ndoa

Gazeti la Ujerumani la Westdeutsche Allgemeine Zeitung laripoti kwamba kulingana na shirika la utafiti huko Ulaya linaloitwa Eurostat, sasa mtoto 1 kati ya watoto 4 wanaozaliwa katika nchi zilizo katika Umoja wa Nchi za Ulaya anazaliwa na wazazi ambao hawajafunga ndoa. Katika mwaka wa 1980 idadi hiyo ilikuwa chini ya asilimia 10. Nchi ya Ugiriki ndiyo ina idadi ya chini zaidi ya watoto wanaozaliwa nje ya ndoa—asilimia 4. Kwa upande mwingine, huko Sweden zaidi ya nusu ya watoto wote wanazaliwa nje ya ndoa. Kumekuwa na badiliko kubwa zaidi huko Ireland. Watoto ambao walizaliwa nje ya ndoa waliongezeka kutoka asilimia 5 tu katika mwaka wa 1980 hadi asilimia 31.8 katika mwaka wa 2000. Maongezeko hayo makubwa “yanaonyesha kwamba Wazungu wamebadili sana mtazamo wao kuelekea ndoa na jamaa,” yasema ripoti hiyo.

Nyigu Wanaojenga kwa Sumaku

Gazeti la The Daily Telegraph la London lasema hivi: “Nyigu ni wajenzi stadi wanaotumia kifaa kinachofanana na pima-maji kuhakikisha kwamba viota vyao vimenyooka.” Kikundi cha watafiti kutoka Chuo Kikuu cha Tel Aviv, nchini Israel, kilichochunguza nyigu wa aina fulani kiligundua kwamba wadudu hao hutia sumaku ndogo kwenye paa ya kila sehemu ya kiota yenye pande sita. Sumaku hiyo huwa na urefu wa milimeta 0.1 na ina titani, chuma, na oksijeni. Ripoti hiyo yasema hivi: “Kiota cha nyigu hutengenezwa kwa vipande vya vidude vilivyolala ambavyo vimetegemezwa na nguzo zilizo wima.” Haijulikani jinsi sumaku hizo zinavyofanya kazi, lakini yaonekana “vipande vya sumaku humsaidia mdudu huyo kujua njia wakati wa giza na kuhakikisha kwamba kiota hakiegemei upande mmoja kwa njia yenye kuhatarisha. Kwa sasa utafiti unafanywa ili kujua kama aina nyingine za nyigu, au hata nyuki, hutumia mbinu hiyo.

Wanawake Wachanga na Ugonjwa wa Mifupa

Gazeti la Asahi Shimbun la Japani linaonya kwamba wanawake wengi zaidi wachanga wanajitia katika hatari ya kupata ugonjwa wa mifupa wa osteoporosis baadaye maishani mwao kwa sababu ya kujinyima chakula kupita kiasi. Ugonjwa huo wa mifupa, unaowapata wanawake wengi wenye umri mkubwa, hupunguza uzito wa mifupa na hivyo kufanya mifupa ivunjike kwa urahisi. Kufanyizwa kwa mifupa ya wanawake kunahusiana sana na utendaji wa homoni za kike. Tangu wakati wanapoingia mwezini, uzito wa mifupa huanza kuongezeka haraka na kufikia kilele wanapokuwa na umri wa miaka 20, kabla ya kuanza kushuka wanapokuwa na umri wa miaka 40 hivi. Profesa Ikuko Ezawa wa Chuo Kikuu cha Wanawake huko Japani anaeleza hivi: “Iwapo anafikia kilele cha uzito wa mifupa baada ya muda mrefu, hata kama uzito huo utapungua baadaye, mifupa yake itaanza kuvunjika baada ya muda mrefu zaidi.” Kwa hiyo, yeye anaongeza kusema hivi: “Ni muhimu sana kuwa na mifupa mizito sana kufikia umri wa miaka 20.” Hata hivyo, wanawake wachanga hawajishughulishi sana na ugonjwa huo wa mifupa. Ezawa anasema hivi: ‘Kwa ujumla, wao hawali chakula cha kutosha, na ukosefu wa kalisi na kutofanya mazoezi kunaathiri mifupa yao moja kwa moja.’

Wenye Furaha na Wenye Afya Katika Umri wa Miaka 100

Kulingana na ripoti katika gazeti la Yomiuri Shimbun, “asilimia 80 ya watu wenye umri wa zaidi ya miaka 100 wanahisi wana afya na wako katika hali nzuri kila siku.” Idadi ya watu wenye umri wa zaidi ya miaka 100 nchini Japani ilipita 1,000 kwa mara ya kwanza katika mwaka wa 1981, na kufikia 13,000 katika mwaka wa 2000. Hivi majuzi, Shirika la Afya na Nishati nchini Japani lilichunguza zaidi ya watu 1,900 wenye umri wa zaidi ya miaka 100, na yaelekea huo ndio uchunguzi mkubwa zaidi uliowahi kufanywa kuhusu “hali ya maisha” ya wazee hao. Kulingana na gazeti hilo “idadi kubwa ya wanaume, yaani asilimia 43.6, ikilinganishwa na asilimia 25.8 ya wanawake, walisema ‘wana kusudi maishani.’” Wengi wa hao waliohojiwa walisema kwamba “jamaa,” “maisha marefu,” na “kuwa na afya bora na kuishi kwa furaha” yalikuwa baadhi ya makusudi yao maishani. Kwa hiyo, gazeti la Yomiuri Shimbun lilidokeza kwamba “kuwa na kusudi maishani hutokeza maisha marefu.”

Watu Wanaoishi Peke Yao

Sensa moja iliyofanywa hivi majuzi ilionyesha kwamba huko Ufaransa mtu 1 kati ya watu 8 sasa anaishi peke yake. Gazeti la kila siku nchini Ufaransa la Le Monde lasema kwamba idadi hiyo ni mara mbili ya ilivyokuwa miaka 30 iliyopita. Takwimu hizo zinatia ndani vijana waseja na vilevile watu wazee. Wanawake wanaoishi peke yao ni wengi kuliko wanaume wanaoishi peke yao, na makala hiyo inaonyesha kwamba “mwanamke anapokuwa na cheo cha juu katika jamii, kuna uwezekano mkubwa zaidi kwamba ataishi peke yake.” Sensa hiyo pia inafunua kwamba tangu mwaka wa 1990, kumekuwa na ongezeko la asilimia 22 la idadi ya familia za mzazi mmoja na ongezeko la asilimia 16 la idadi ya wenzi wa ndoa wasio na watoto. Makala hiyo inamalizia kusema kwamba “kwa ujumla, sasa idadi ya wenzi wa ndoa wasio na watoto na ya watu wanaoishi peke yao ni kubwa kuliko ya jamaa zenye watoto.”

Vijana Waliobalehe Wanaofanya Ngono

Ripoti ya Taasisi ya Masuala ya Familia ya Uingereza inaonyesha kwamba uwezekano wa vijana waliobalehe “kufanya ngono ikiwa wazazi wao wametengana ama wanaishi bila kufunga ndoa ni mara mbili ya uwezekano wa kufanya hivyo kama wamefunga ndoa,” kulingana na gazeti la The Guardian la London. Robo ya vijana wenye umri wa miaka 13 wanaofanya ngono, wamefanya ngono na angalau watu wanne, na kijana 1 kati ya vijana 5 alikuwa mlevi alipofanya ngono kwa mara ya kwanza. Ripoti hiyo inakazia uhitaji wa “watu kuhimizwa kuona ndoa kuwa mpango wa jamaa unaofaa wa kulea watoto.” Matatizo huzuka wakati ‘hakuna uhusiano wa karibu kati ya wazazi na vijana wanaobalehe, wakati wanapoonana mara chache, na kukosa kusimamiwa.’ Ripoti hiyo inamalizia kwa kusema hivi: “Wazazi wa vijana waliobalehe wasipochukua daraka la kuangalia tabia ya watoto wao kwa uzito zaidi, idadi ya vijana waliobalehe wanaofanya ngono haitapungua na mimba miongoni mwa vijana waliobalehe na magonjwa ya kuambukizwa kingono yataendelea kuongezeka.”

Madereva Wenye Usingizi

Wataalamu wa usingizi, pamoja na watetezi wa usalama, wanashauri wenye magari wasiendeshe magari wakiwa wamechoka sana, charipoti kichapo Fleet Maintenance & Safety Report. Ingawa wachunguzi wa usingizi wanapendekeza watu walale kwa muda wa angalau saa nane kila usiku, uchunguzi unaonyesha kwamba watu wengi wanaendelea kupunguza muda wao wa kulala. Uchunguzi pia unaonyesha kwamba madereva wenye umri wa kati ya miaka 19 na 29 ndio hasa wanaoelekea kuendesha gari wakiwa na usingizi na kuendesha kwa kasi zaidi wanaposinzia. Ripoti hiyo inasema kwamba “kileo pia huongeza hatari ya kulala wakati wa kuendesha gari.” David Willis, msimamizi wa Shirika la Magari la Marekani la Usalama Barabarani, anasema kwamba kusikiliza redio au kufungua kioo hakutakufanya ukae macho, lakini kulala kwa muda mfupi ndiko kunakoweza kukusaidia uache kusinzia. Willis anakazia kwamba: “Usingizi huisha tu wakati mtu anapolala.”