Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ninawezaje Kupata Mtu Mzuri wa Kuishi Naye?

Ninawezaje Kupata Mtu Mzuri wa Kuishi Naye?

Vijana Huuliza . . .

Ninawezaje Kupata Mtu Mzuri wa Kuishi Naye?

“Singaliweza kuwa mhubiri wa wakati wote na kulipa kodi na kadhalika kama ningaliishi peke yangu.”—Lynn. *

MARA nyingi vijana wanaohama nyumbani hushtuka kuona gharama kubwa za mahitaji ya maisha. Kwa hiyo, wengi huamua kuishi pamoja na mtu mmoja au watu kadhaa ili wasaidiane kulipa gharama hizo.

Lakini kama vile makala moja katika mfululizo huu ilivyoonyesha, kuishi pamoja na mtu mwingine—hasa mtu ambaye hukumfahamu hapo awali—kunaweza kuwa vigumu sana. * Hata vijana Wakristo wanaoishi pamoja ili waweze kutumikia kama wahubiri wa wakati wote hupata matatizo mbalimbali. Hata hali yako iweje, ukiwa na mpango wa kuishi na mtu mwingine, ni jambo la akili kuchagua yule mtu utakayeishi naye kwa “hekima.” *Mithali 3:21.

Hatari ya Mashirika Mabaya

Vijana wengi hutafuta mtu wa kuishi naye kwa kusoma matangazo yanayobandikwa kwenye ubao wa matangazo, katika magazeti ya habari, na katika Internet. Lakini kwa vijana Wakristo, jambo hilo ni hatari sana. Kupitia njia hiyo, yamkini utapata watu wasiofuata imani, maadili, au kanuni unazofuata. Je, mtu anaonyesha ubaguzi au ubinafsi akitaka kuishi na mtu wa imani yake tu? La, ni jambo la hekima kufanya hivyo. Biblia yenyewe inaonya hivi: “Mashirika mabaya huharibu mazoea yenye mafaa.”—1 Wakorintho 15:33.

Fikiria kisa cha mwanamke mchanga anayeitwa Lee. Hakuwa Mkristo aliyebatizwa alipohamia kwenye bweni la chuo kikuu fulani. Anasema hivi: ‘Hali huko ilikuwa hatari. Nyakati nyingine, wasichana wengine walipata wenzao wakifanya ngono waliporudi chumbani mwao.’ Kuishi katika mazingira hayo kulianza kudhuru hali ya kiroho ya Lee mara moja. Anakiri hivi: “Nilikosa kuhudhuria karibu mikutano yote ya Kikristo.” Si ajabu kwamba mwenendo wake ulipotoka hatua kwa hatua. “Siku moja nilijikuta nikitumia matusi, na mmojawapo wa wasichana aliniuliza: ‘Je, Yehova anakubali jambo hilo?’” Lee aliaibika sana! Jambo la furaha ni kwamba Lee aliacha mazingira hayo mabaya na kuanza kufanya maendeleo ya kiroho. Lakini kisa chake kinaonyesha jinsi ilivyo hatari kuishi pamoja na watu wasiofuata kanuni unazofuata.

Kupata Mtu Mzuri wa Kuishi Naye

Basi, unaweza kupata wapi mtu wa kuishi naye? Anza kutafuta katika kutaniko lenu la Mashahidi wa Yehova. Mara nyingi, wahubiri wa wakati wote hukutana na vijana wanaotanguliza mambo ya kiroho kwenye shule na mikutano mbalimbali inayofanywa hasa kwa ajili ya wahubiri wa wakati wote. * Wazazi, wazee wa kutaniko, waangalizi wasafirio, na wengineo wanaweza kukusaidia pia; huenda wanawafahamu vijana fulani wanaofaa.

Kuwaambia watu kuhusu uhitaji wako kunaweza kusaidia pia. Yamkini utafanikiwa ikiwa watu wengi iwezekanavyo wanajua haja yako. (Mhubiri 11:6) Zaidi ya yote, omba Yehova akusaidie kupata mtu wa kuishi naye, na umtegemee abariki jitihada zako.—1 Yohana 5:14, 15.

Kufanya Uchunguzi

Baada ya kupata mtu ambaye unafikiri anafaa, huenda ukataka kuanza kuishi pamoja naye mara moja. Lakini ni jambo la hekima kufanya uchunguzi kwanza. Je, mtu huyo ‘anaripotiwa vema na akina ndugu’ katika kutaniko lao? (Matendo 16:1, 2) Huenda ikawa wewe na wazazi wako mnaweza kuongea moja kwa moja na watu waliokomaa kiroho wanaomjua mtu huyo. Unaweza kuuliza maswali haya: ‘Ana sifa gani? Je, mtu huyo ni thabiti kihisia na kiroho? Je, anashiriki katika kazi ya kuhubiri na kutoa maelezo mikutanoni? Je, mtu huyo anajulikana kwa mwenendo mzuri?’

Kumbuka kwamba “anayeandamana na wenye hekima hupata hekima.” (Mithali 13:20, Biblia Habari Njema) David anasema: ‘Mtu ninayeishi naye anapendezwa sana na mambo ya kiroho. Hilo hunisaidia kudumisha hali nzuri ya kiroho.’ Renee, ambaye ameishi pamoja na watu kadhaa, anasema hivi: “Wengine wao walidokeza tusome pamoja sura moja katika Biblia kila usiku. Kwa sababu watu wa familia yetu hawakuwa Mashahidi, hatukuwa na funzo la Biblia la familia kamwe. Kwa hiyo, nilifurahi sana nilipoweza kuwa na ‘funzo la familia’ pamoja na watu ambao niliishi nao.” Ndiyo, kuishi pamoja na mtu anayependa mambo ya kiroho kama wewe kunaweza kuwa baraka kwelikweli.

Kuzungumzia Mambo Waziwazi

Kisha, panga mkutane ili kuzungumzia mambo. Mazungumzo hayo yanaweza kukusaidia kujua ikiwa utapatana na mtu huyo. Jarida la Communication Research Reports liliripoti kuhusu uchunguzi mmoja ulioonyesha kwamba watu wanaoishi pamoja, ambao njia yao ya kuwasiliana inafanana, “walipendana na kuridhika na wenzao.” Kwa hiyo, ikiwa wewe unapenda kuongea na kushirikiana na watu, huenda ukapata matatizo ukiishi pamoja na mtu mnyamavu, au mtu anayependa kuwa peke yake.

Ijapokuwa si vizuri kufanya mazungumzo yenu yawe makali kama mahojiano ya polisi, ni vizuri kuzungumzia miradi na malengo ya yule unayetaka kuishi naye. Je, anataka kufanya maendeleo ya kiroho au anataka tu kuepuka hali ngumu nyumbani? Lynn anataja tatizo jingine linaloweza kuzuka: “Niliishi pamoja na msichana fulani aliyekuwa na rafiki wa kiume aliyemtembelea sikuzote na alikuwa akibaki hadi usiku wa manane.” Lynn aliudhika na vitendo vyao vya kimapenzi visivyofaa. Hata hivyo, nyakati nyingine matatizo hayo yataweza kuepukwa ikiwa watu wanaoishi pamoja watafanya mapatano kimbele kuhusu jinsi ya kushughulikia hali kama hizo. Kwa mfano, Renee anasema hivi: “Tulijiwekea sharti ya kwamba marafiki wa kiume wawe wameondoka kufikia saa fulani.” Ingefaa pia watu wanaoishi pamoja waamue kwamba hawatakubali kamwe kuwa peke yao na mtu wa jinsia tofauti nyumbani.

Pia ingefaa kuzungumzia mambo kama vile muziki na tafrija mnazopenda, na mapendezi mengine. Mark anasema hivi: “Ningependa kuishi pamoja na mtu anayependa vitu ninavyopenda, aliye na utu kama wangu, na anayependa kufanya mambo yale ninayopenda kufanya.” Bila shaka, jambo hilo halimaanishi kwamba watu walio na mapendezi yanayotofautiana hawataweza kuishi pamoja. Jambo muhimu ni kwamba nyote wawili mwe tayari kuvumilia sifa za yule mwingine, na kutanguliza mapendezi yake.

Lee anapendekeza: “Unapaswa pia kumwuliza yule mwingine kile anachotarajia kutoka kwako. Watu wengine hutarajia kwamba utakuwa rafiki yao wa karibu. Lakini mimi sina haja na jambo hilo.” David anasema hivi vilevile: “Ninataka kuishi pamoja na mtu ninayeweza kushirikiana naye lakini asiyehitaji kuambatana nami kila wakati ninapotaka kushirikiana na watu wengine.” Vilevile, mwulize ikiwa ananuia kuwa mwenzi wako katika kazi ya kuhubiri au ikiwa ana mpango mwingine, kama vile kutumikia katika kutaniko la lugha ya kigeni.

Jambo la mwisho, hakikisha kwamba mnakubaliana kuhusu upishi (je, nyote mnajua kupika?), kazi za nyumbani, utumizi wa vifaa na vyombo mbalimbali vya mtu binafsi, nafasi ya kila mmoja katika kabati na mahali pa kuwekea vitu vingine, na kama mtakuwa na mnyama-kipenzi. Mkizungumzia mambo hayo kimbele mnaweza kuepuka kutoelewana na kuumizana. Mithali 20:18 inasema hivi: “Kila kusudi huthibitika kwa kushauriana.”

“Kwa Adabu na kwa Mpango”

Kanuni nyingine inayoweza kusaidia inapatikana katika Luka 14:28. Andiko hilo linasema: ‘Piga hesabu ya gharama.’ Ndiyo, jaribu kukadiria gharama za mahitaji ya maisha. Kodi itagharimu kiasi gani? Vipi chakula? Vipi umeme na maji? Je, mtakuwa na simu moja? Ikiwa ndivyo, mtajuaje kiasi ambacho kila mmoja anapaswa kulipa? Lynn anasema hivi: “Mimi huhakikisha kwamba yule msichana ambaye ninataka kuishi naye anaweza kulipa sehemu yake ya gharama kabla sijakubali kuishi naye.” Gazeti The Next Step, linalopatikana kwenye Internet linasema hivi: ‘Ukiishi na mtu asiyelipa sehemu yake ya kodi wala chakula, au anayesababisha gharama nyingine zipande sana, utakuwa na mfadhaiko usio wa lazima.’

Renee anasema: ‘Nyakati nyingine tatizo si kiasi kinachotakiwa kulipwa, bali wakati wa kulipa.’ Anaeleza hivi: “Kodi yetu inapaswa kulipwa tarehe ya tatu kila mwezi. Lakini, nyakati nyingine yule ninayeishi naye husafiri mwishoni mwa juma kabla ya kulipa sehemu yake, na inanibidi kumwomba radhi mwenye nyumba.” Ni wazi kwamba kila kitu kinapaswa kufanywa “kwa adabu na kwa mpango.” Mambo muhimu hayapaswi kuachwa yafanyike kiholela. (1 Wakorintho 14:40) Mara nyingi inafaa mapatano yaandikwe.

Ukiwa mwangalifu na mwenye busara yamkini utafanikiwa kupata mtu wa kuishi naye atakayekufurahisha bali si kukufadhaisha. Hata hivyo, vipi ikiwa matatizo yanazuka au tabia fulani ya mwenzako inaanza kukuudhi? Matatizo hayo yatazungumziwa katika makala itakayofuata.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

^ fu. 5 Ona makala ya “Mbona Yule Ninayeishi Naye Ni Mgumu Sana?” katika toleo letu la Aprili 22, 2002.

^ fu. 5 Kwa kuwa watu wengi leo wanaishi pamoja na mtu wa jinsia tofauti na hivyo kufanya uasherati, tunataka kukazia kwamba makala hii inazungumzia watu wa jinsia moja wanaoishi pamoja ili wasaidiane kulipa gharama na mambo mengine.

^ fu. 10 Wahubiri wa wakati wote wana pendeleo la kuhudhuria Shule ya Utumishi wa Painia. Mikutano kwa ajili ya wahubiri wa wakati wote inafanywa pia kila mwaka wakati wa makusanyiko ya mzunguko.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Ni hatari kuishi na watu wasiofuata kanuni za Biblia

[Picha katika ukurasa wa 26]

Panga mkutane ili kuzungumzia mambo muhimu kabla ya kukubali kuishi pamoja na mtu fulani