Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Njia ya Kuunganisha Ulimwengu Ambayo Itakufaidi

Njia ya Kuunganisha Ulimwengu Ambayo Itakufaidi

Njia ya Kuunganisha Ulimwengu Ambayo Itakufaidi

“Ili utandaridhi ufaulu, ni lazima uwafaidi maskini na matajiri kwa usawa. Ni lazima watu wapate haki zao kama wanavyopata mali. Ni lazima utokeze haki na usawa katika jamii sawa na ufanisi wa kiuchumi na maendeleo ya mawasiliano.”—KOFI ANNAN, KATIBU-MKUU WA UMOJA WA MATAIFA.

KAMA vile Kofi Annan alivyosema, ili utandaridhi ufaulu, ni lazima uboreshe maisha ya watu wote ulimwenguni. Lakini hali ya maisha haijawa nzuri katika miaka ya hivi majuzi. Kumekuwa na ufanisi mwingi wa kiuchumi na maendeleo ya kitekinolojia kuliko maendeleo katika haki za binadamu na usawa katika jamii.

Tatizo kuu ni kwamba utandaridhi wa kiuchumi unachochewa hasa na tamaa ya kupata mali. Watu wanaoongozwa na tamaa hiyo hawawafikirii maskini wala kutilia maanani masilahi ya siku zijazo ya dunia. Dakt. David C. Korten anasema hivi: “Biashara ya ulimwenguni pote isiyodhibitiwa ambayo inaongozwa na mashirika ambayo yanazingatia tu kupata fedha haiwezi kuwa thabiti . . . na inawafanya wanadamu kuwa maskini katika njia nyingine.”

Je, serikali za ulimwengu zitaweza kudhibiti biashara ya ulimwenguni pote ili itokeze haki katika jamii? Inaonekana hilo haliwezekani. Kufikia sasa, serikali zimeshindwa kutatua matatizo yoyote ulimwenguni—iwe ni uhalifu wa kimataifa, ongezeko la joto duniani, au umaskini ulimwenguni pote. Annan anasema hivi: ‘Watu wanahitaji kushirikiana kutunza masilahi ya ulimwenguni pote, lakini katika ulimwengu huu wa utandaridhi mbinu za kufanya kazi hiyo ya ulimwenguni pote ni za hali ya chini sana.’

Licha ya mbinu za kushughulikia matatizo ya ulimwenguni pote, kuna mambo mengine yanayohitajiwa. Tume ya Usimamizi wa Ulimwengu * inasema kwamba maadili mazuri yanahitajiwa ulimwenguni. Ripoti ya tume hiyo inasema hivi: ‘Bila maadili ya ulimwenguni pote, migogoro itaongezeka ulimwenguni; bila mwongozo, hata mikakati na mashirika yaliyopangwa vizuri hayataweza kufaulu.’

Walipendekeza maadili gani kwa ajili ya ulimwengu wote? Ripoti hiyo ilisema hivi: “Watu wanapaswa kuwatendea wengine kama wanavyotaka kutendewa.” Yesu Kristo, kiongozi mkuu zaidi aliyewahi kuonekana ulimwenguni, alifundisha kanuni hiyo miaka elfu mbili hivi iliyopita. (Mathayo 7:12) Lakini kanuni hiyo bado inafaa hali za leo. Bila shaka, kuunganisha ulimwengu kwa kutumia kanuni hiyo kutafaidi kila mtu. Je, hilo linaweza kutukia?

Suluhisho Tofauti la Matatizo Ulimwenguni Pote

Biblia inatabiri kwamba hivi karibuni serikali ya ulimwenguni pote isiyokuwa na ubinafsi itawaunganisha wanadamu pasipo kutumia fedha wala tekinolojia. Serikali hiyo itafaulu kwa sababu ina uwezo na mbinu za kuwasaidia wanadamu wote ulimwenguni pote. Yesu Kristo alikazia serikali hiyo ya ulimwenguni pote alipowafundisha wafuasi wake kusali ‘Ufalme wa Mungu uje na mapenzi ya Mungu yatendeke duniani.’—Mathayo 6:10.

Ufalme wa Mungu, serikali ya mbinguni inayoongozwa na Yesu Kristo, utaleta maadili mapya ulimwenguni pote, maadili yaleyale ambayo Yesu alifundisha alipokuwa duniani. Kumpenda Mungu na jirani ndizo kanuni zitakazoongoza. (Mathayo 22:37-39) Unabii mwingi katika Biblia unaonyesha mambo ambayo yatafanywa na serikali hiyo mpya. Biblia inaahidi hivi kuhusu Mtawala wa serikali hiyo, Yesu Kristo: “Atawapatia haki watu maskini, atawaamulia sawasawa wanyonge nchini.” (Isaya 11:4, Biblia Habari Njema) Matajiri na watu wenye uwezo hawatawadhulumu watu wasio na uwezo. Yesu “atamhurumia aliye dhaifu na maskini . . . Atawakomboa nafsi zao na kuonewa na udhalimu.”—Zaburi 72:13, 14.

Matatizo yanayokumba mazingira yataondolewa haraka. Badala ya majangwa kuenea, “nyika na mahali palipo ukiwa patafurahi; jangwa litashangilia na kuchanua maua kama waridi.” (Isaya 35:1) Badala ya upungufu wa chakula, ‘kutakuwepo wingi wa nafaka.’—Zaburi 72:16.

Ufalme wa Mungu huwaunganisha watu wa jamii zote. ‘Nitawaleta pamoja kama kondoo katika zizi,’ Mungu anaahidi. ‘Nitawarudishia lugha iliyo safi, wanitumikie kwa nia moja.’ (Mika 2:12, BHN; Sefania 3:9) Hiyo ‘lugha safi,’ ambayo inatia ndani kanuni za kiadili na za kidini zinazowahusu wote, inawaunganisha watu hata sasa.

Kwa sababu ya vyombo vya usafiri ulimwenguni pote, Mashahidi wa Yehova hufanya makusanyiko makubwa ya kimataifa kwa ukawaida, ambayo huunganisha watu wa jamii, mataifa, na utamaduni mbalimbali. Makusanyiko hayo yanaonyesha wazi jinsi watu wanavyoweza kuunganishwa wawe na moyo mmoja na akili moja, badala ya kupitia tekinolojia na biashara. (Ona sanduku.) Mwanatheolojia mmoja Mhispania ambaye amehudhuria baadhi ya makusanyiko hayo aliandika hivi: ‘Nilitoka huko nikiwa nimejengwa, si tu kwa hotuba za Kimaandiko zenye kuelimisha bali pia kwa sababu ya umoja uliopo kati ya watu hao, maadili yao mazuri sana, na tabia yao njema.’

Mashahidi wa Yehova pia hutumia vizuri faida nyingine za utandaridhi ili kuendeleza kazi yao ya kuhubiri habari njema kuhusu Ufalme wa Mungu. Kwa mfano, gazeti la Amkeni! hutafsiriwa katika lugha zaidi ya 80 na watafsiri wengi ulimwenguni pote ambao wanatumia programu za kompyuta na njia za mawasiliano ya kompyuta. Vyombo hivyo huwasaidia Mashahidi wa Yehova kueneza programu yao ya elimu ya Biblia ulimwenguni pote. Kwa wazi, vifaa vya utandaridhi vyaweza kutumiwa kuleta faida au hasara.

Vivyo hivyo, badala ya kuleta matatizo kama vile njia ya wanadamu ya kuunganisha ulimwengu ilivyofanya, serikali ya ulimwenguni pote iliyosimamishwa na Mungu italeta masuluhisho. Tuna kila sababu ya kuwa na uhakika katika utawala huo wa mbinguni. Mungu anaahidi hivi: ‘Naumba nchi mpya, na mambo ya kwanza hayatakumbukwa. Furahini, mkashangilie daima, kwa ajili ya hivi niviumbavyo.’ (Isaya 65:17, 18) “Nchi mpya” ya Mungu itawafaidi watu kabisa ulimwenguni pote.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Tume hiyo, ambayo ina viongozi mashuhuri wa ulimwengu 28, ilitayarisha ripoti ndefu katika mwaka wa 1995, yenye kichwa “Our Global Neighbourhood.” Katika ripoti hiyo viongozi hao walitaja mapendekezo yao ya kuboresha usimamizi ulimwenguni.

[Sanduku katika ukurasa wa 12]

WAMEUNGANISHWA LAKINI BADO WAMEGAWANYIKA

Ijapokuwa tekinolojia imewaunganisha watu ulimwenguni pote, bado kuna migawanyiko. Televisheni, simu za mkononi, na Internet zimewawezesha watu kuwasiliana lakini hazijawawezesha kuwa kitu kimoja. Biashara ya ulimwenguni pote na kumalizika kwa uhasama kati ya mataifa yenye uwezo kumepunguza vita kati ya Nchi mbalimbali, lakini vita katili za wenyewe kwa wenyewe zinaendelea kuwaua na kuwalemaza mamia ya maelfu ya watu kila mwaka.

Kwa nini? Kwa sababu bado kuna chuki kati ya vikundi vya kikabila, vya kijamii, na vya kidini—kisababishi cha vita za wenyewe kwa wenyewe. Na biashara mbalimbali ulimwenguni pote na magenge ya wahalifu huuza silaha nyingi za bei rahisi kwa vikundi vinavyopigana. Umoja wa kweli hauwezi kutokezwa na mashine za elektroniki. Wala ongezeko la faida katika soko la hisa haliwezi kutokeza haki katika jamii.

Katika njia fulani, utandaridhi wa kiuchumi unaweza kusababisha mgawanyiko. Uchumi unapoanza kuzorota baada ya kuimarika sana, wanasiasa wakatili wanaweza kutumia nafasi hiyo ili kujifaidi na kuwanyanyasa maskini wasio na uwezo. Basi suluhisho ni nini? Kichapo cha Human Development Report 1999 kinasema hivi: “Ni lazima kuwe na usimamizi mpya katika mataifa na ulimwenguni pote—na hangaiko kuu liwe kuleta usawa na kuwawezesha watu kufanya maendeleo.” Ufalme wa Mungu utafanya hivyo hasa.

[Picha katika ukurasa wa 13]

Programu ya elimu ya Biblia ya ulimwenguni pote ya Mashahidi wa Yehova imewaunganisha watu wa jamii zote