Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Chanzo cha Ulimwengu na Uhai Ni Nini?

Chanzo cha Ulimwengu na Uhai Ni Nini?

Chanzo cha Ulimwengu na Uhai Ni Nini?

‘Sayansi haina nguvu bila dini, dini bila sayansi imepungukiwa.’—Albert Einstein.

HIZI ni siku zenye kustaajabisha sana kuliko wakati mwingine wowote. Ugunduzi mpya huko angani unawalazimu wataalamu wa nyota kubadili maoni yao kuhusu chanzo cha ulimwengu wetu. Watu wengi wanastaajabishwa na ulimwengu na wanauliza maswali ambayo yameulizwa tangu zamani kuhusu kuwapo kwetu ndani yake: Ulimwengu na uhai ulitokeaje, na kwa nini ulitokea?

Hata tukichunguza miili yetu kupatana na uchunguzi uliofanywa hivi karibuni kuhusu chembe za urithi, maswali haya yanazuka: Viumbe wengi tofauti-tofauti waliumbwaje? Ikiwa kuna mtu aliyewaumba, mtu huyo ni nani? Rais mmoja wa Marekani alisema hivi kuhusu namna ambavyo chembe zetu za urithi zimeundwa kwa njia tata sana: ‘Tunajifunza jinsi Mungu alivyoumba viumbe.’ Mmojawapo wa wanasayansi wakuu waliohusika katika uchunguzi huo wa chembe za urithi alisema hivi kwa unyenyekevu: “Tumegundua habari chache kuhusu chembe zetu za urithi ambazo hapo awali ni Mungu tu aliyezijua.” Lakini maswali haya hayajajibiwa—uhai ulitokeaje, na kwa nini ulitokea?

“Madirisha Mawili”

Wanasayansi fulani wanasema kwamba utaratibu unaotumiwa kuendesha ulimwengu unaweza kuelezwa kwa kutumia akili, bila kutumia hekima ya Mungu. Lakini watu wengi, kutia ndani wanasayansi, wana mashaka kuhusu maoni hayo. Wanajaribu kuelewa ukweli wa mambo kwa kuchunguza sayansi na vilevile dini. Wanaonelea kwamba sayansi inaeleza jinsi ambavyo uhai na ulimwengu ulivyotokea, na dini inaeleza kwa nini vitu hivyo vilitokea.

Akizungumzia mbinu hiyo ya kuchunguza pande zote mbili, mwanafizikia Freeman Dyson alisema hivi: “Sayansi na dini ni kama madirisha mawili ambayo watu wanachungulia wanapojaribu kuelewa ule ulimwengu mkubwa huko nje.”

Mwandishi William Rees-Mogg alisema hivi: ‘Sayansi inashughulika na mambo yanayoweza kupimwa, na dini inashughulika na mambo yasiyoweza kupimwa. Sayansi haiwezi kuthibitisha kwamba kuna Mungu wala haiwezi kuthibitisha kwamba hakuna Mungu, sawa na jinsi ambavyo haiwezi kuthibitisha ubora wala ubaya wa maadili au sanaa. Hakuna sababu ya kisayansi ya kumpenda jirani au kuheshimu uhai wa mwanadamu. Ni kosa kubwa sana kusema kwamba ikiwa sayansi haiwezi kuthibitisha jambo fulani basi jambo hilo halipo. Hilo lingemaanisha kuwa karibu mambo yote muhimu maishani hayapo, kama vile Mungu, utu wa mwanadamu, upendo, ushairi, na muziki.’

Mafundisho ya Sayansi

Mara nyingi watu huamini nadharia za wanasayansi bila kuwa na uthibitisho wowote. Kwa mfano, kuhusiana na chanzo cha uhai, watu wengi wanaoamini mageuzi hushikilia maoni ambayo hayajathibitishwa na sayansi. Mambo yaliyothibitishwa huunganishwa na nadharia mbalimbali. Na wanasayansi wanapotumia mamlaka yao kuwalazimisha watu waamini nadharia ya mageuzi bila uthibitisho, wao humaanisha hivi: ‘Kwa kuwa wewe ulitokana na utendaji wa kibiolojia, wa kikemia, au wa kifizikia tu, huna wajibu wowote kuhusu mwenendo wako.’ Mwanabiolojia Richard Dawkins anasema kwamba katika ulimwengu ‘hakuna ubunifu, kusudi, uovu wala wema, hakuna chochote ila kutojali.’

Ili kudumisha maoni yao, wanasayansi fulani hupuuza uchunguzi mwingi ambao umefanywa na wanasayansi wengine wanaopinga mambo ya msingi kuhusu nadharia zao juu ya chanzo cha uhai. Hata mabilioni ya miaka ikipita, imethibitika wazi kwamba haiwezekani kwa molekuli tata kujifanyiza zenyewe kisha zitokeze chembe yenye uhai inayofanya kazi. * Hivyo, nadharia kuhusu chanzo cha uhai zinazopatikana katika vitabu vingi zinapasa kuonwa kuwa za uwongo.

Kuamini kwamba uhai ulijitokeza kunahitaji imani nyingi zaidi kuliko kuamini katika uumbaji. David Block, ambaye ni mtaalamu wa nyota, alisema hivi: ‘Mtu asiyemwamini Muumba anahitaji imani nyingi zaidi kuliko mtu anayemwamini. Mtu anaposema kwamba hakuna Mungu, anatoa taarifa isiyo na msingi wowote—kauli isiyothibitishwa ambayo inategemea imani tu.’

Uvumbuzi wa kisayansi unaweza kuwafanya wanasayansi fulani kuwa na kicho. Albert Einstein alikubali hivi: ‘Si rahisi kumpata mwanasayansi mwenye akili nyingi sana ambaye hana hisia fulani ya kidini. Hisia hiyo ya kidini yaweza kuonekana kwa jinsi anavyostaajabia sana upatano wa mambo ya asili, ambao unaonyesha kwamba ulifanyizwa kwa akili nyingi sana. Matendo ya mwanadamu na uwezo wake wote wa kufikiri ni mdogo sana unapolinganishwa na akili hiyo.’ Hata hivyo, jambo hilo haliwachochei wanasayansi kumwamini Muumba, Mungu mwenye utu.

Mipaka ya Sayansi

Inafaa kuheshimu kwa njia inayofaa maarifa na mafanikio ya sayansi. Hata hivyo, wengi watakubali kwamba ijapokuwa sayansi ni njia ya kupata maarifa, hiyo siyo njia pekee ya kupata maarifa. Kusudi la sayansi ni kueleza matukio ya asili na kusaidia kuonyesha jinsi matukio hayo yanavyotokea.

Sayansi hutuwezesha kuelewa kwa undani ulimwengu wa maumbile, yaani, kila kitu kinachoonekana. Lakini hata uchunguzi wa sayansi uwe wa hali ya juu jinsi gani, hauwezi kamwe kuonyesha kusudi la kuwepo kwa ulimwengu.

Mwandishi Tom Utley anasema hivi: ‘Kuna maswali fulani ambayo wanasayansi hawawezi kamwe kuyajibu. Huenda ikawa mlipuko mkubwa ulitukia miaka bilioni 12 iliyopita na hivyo ulimwengu ukaanza. Lakini kwa nini mlipuko huo ulitukia? Chembe zilizolipuka zilitoka wapi? Ni nini kilichokuwapo kabla ya tukio hilo?’ Utley amalizia hivi: “Inaonekana . . . wazi kwamba sayansi haitaweza kamwe kujibu maswali yote ya wanadamu.”

Badala ya kuthibitisha kwamba hakuna Mungu, maarifa ya sayansi ambayo yamepatikana kupitia uchunguzi kama huo yamethibitisha kwamba ulimwengu tunamoishi ni wa ajabu sana, una utata mwingi, na unatia kicho. Watu wengi wenye akili wanaona kwamba ni jambo linalofaa kukata kauli kuwa kanuni za mambo ya asili, utendaji wa kemikali, DNA, na unamna-namna wa viumbe unaonyesha wazi kwamba kuna Muumba. Hakuna uthibitisho unaopinga kauli hiyo.

“Imani Ni Halisi”

Iwapo kuna Muumba aliyeumba ulimwengu, basi hatuwezi kutazamia kumfahamu au kujua makusudi yake kwa kutumia darubini, hadubini, au vifaa vingine vya kisayansi. Hebu fikiria mfano wa mfinyanzi na chombo cha maua ambacho amefanyiza. Hata ukichunguza chombo hicho kadiri gani, hutaweza kamwe kujua kwa nini kilitengenezwa. Ili kupata jibu, ni lazima tumuulize mfinyanzi.

Mwanabiolojia wa molekuli Francis Collins anaeleza jinsi ambavyo imani na mambo ya kiroho yanavyoweza kujibu maswali yasiyoweza kujibiwa na sayansi: “Siwezi kutazamia dini ieleze muundo wa chembe za urithi za mwanadamu, na vilevile siwezi kutazamia sayansi ifundishe kuhusu mambo ya kiroho yasiyoonekana. Lakini ninaonelea kwamba sayansi haijibu kikamili maswali muhimu, kama vile ‘Ni nini kusudi la uhai?’ au ‘Kwa nini wanadamu wanapenda mambo ya kiroho?’ Mambo mengi ya ushirikina yametokea na kupotea. Imani imedumu, na hilo linaonyesha kwamba imani ni halisi.”

Sababu ya Kutokea kwa Ulimwengu na Uhai

Zaidi ya kuonyesha kusudi la uhai na kwa nini ulimwengu ulitokea, dini ya kweli hutoa pia kanuni za maadili, na vilevile mwongozo maishani. Mwanasayansi Allan Sandage alieleza jambo hilo hivi: “Sihitaji kusoma kitabu cha biolojia ili nijue jinsi ya kuishi.”

Mamilioni ya watu ulimwenguni pote wanahisi kwamba wamegundua namna wanavyoweza kujua jinsi ya kuishi vizuri. Pia, wanahisi kwamba wamepata majibu yenye kuridhisha kwa maswali haya: Kwa nini tuko hai? Na ni nini kitakachotokea wakati ujao? Majibu yapo. Yapo wapi? Katika kitabu kitakatifu na cha kale zaidi ambacho kimesambazwa zaidi ya kitabu kingine chochote, Biblia.

Biblia inatueleza kwamba Mungu aliumba dunia kwa ajili ya wanadamu hasa. Isaya 45:18 inasema hivi kuhusu dunia: “Mungu . . . hakuiumba ukiwa, [lakini] aliiumba ili ikaliwe na watu.” Na aliweka kila kitu ambacho wanadamu wangehitaji duniani, si ili waishi tu bali ili wafurahie maisha kabisa.

Wanadamu waliagizwa watunze dunia, ‘wailime na kuitunza.’ (Mwanzo 2:15) Biblia pia inaeleza kuwa ujuzi na hekima ni zawadi kutoka kwa Mungu na kwamba tunapaswa kuwatendea wengine kwa upendo na haki. (Ayubu 28:20, 25, 27; Danieli 2:20-23) Hivyo, maisha ya wanadamu yanaweza kuwa na kusudi iwapo tu watatambua na kukubali yale ambayo Mungu amekusudia kwa ajili yao. *

Mtu mwenye akili leo anaweza kufanya nini ili kukubali maoni ya kisayansi na vilevile ya kidini? Ni kanuni zipi zinazoweza kumsaidia mtu kufanya hivyo?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 11 Ona sura ya 3 yenye kichwa “Uhai Ulianzaje?” katika kitabu Je, Kuna Muumba Anayekujali?, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 26 Ili kupata habari kamili, ona broshua Ni Nini Lililo Kusudi la Uhai? Wewe Waweza Kulipataje?, iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 7]

Maoni ya Wanasayansi Fulani

Watu fulani hufikiri kwamba wanasayansi wengi huepuka kuzungumzia mambo ya kiroho na ya kidini kwa sababu wao si wanadini au hawapendi kujihusisha katika mjadala kati ya sayansi na dini. Naam, wanasayansi wengine wana maoni hayo, lakini si wote. Hebu ona maoni yafuatayo ya wanasayansi.

“Ulimwengu ulikuwa na mwanzo fulani lakini wanasayansi hawawezi kueleza kwa nini ulitokea. Mungu ndiye aliyeuumba.” “Mimi huiona Biblia kuwa kitabu cha kweli kutoka kwa Mungu. Bila shaka kuna mtu mwenye akili aliyeanzisha uhai.”—Ken Tanaka, mwanajiolojia wa mambo ya sayari kwenye Taasisi ya Uchunguzi wa Jiolojia ya Marekani.

“Wanadamu ndio wamesababisha tofauti kati ya ujuzi mbalimbali (wa kisayansi na wa kidini). . . . Ujuzi kumhusu Muumba na ujuzi kuhusu uumbaji unahusiana sana.”—Enrique Hernández, mtafiti na profesa kwenye Idara ya Fizikia na Nadharia ya Kemia ya Chuo Kikuu cha Kitaifa cha Mexico.

‘Tunapoendelea kujua zaidi juu ya habari hizi zote [kuhusu chembe za urithi za mwanadamu], tutaona utata uliopo na jinsi zote zinavyohusiana. Itaonyesha kwamba kuna muumba mwenye akili, yaani, nguvu fulani au mtu mwenye akili.’—Duane T. Gish, mtaalamu wa biokemia.

“Sayansi na dini zinapatana. Zote zinatafuta ukweli mmoja. Sayansi inaonyesha kwamba kuna Mungu.”—D.H.R. Barton, profesa wa kemia, Texas.

[Hisani]

NASA/U.S. Geological Survey

Picha: www.comstock.com

NASA and The Hubble Heritage Team (STScI/AURA)

[Picha katika ukurasa wa 5]

Je, uchunguzi wa kisayansi unaweza kutuonyesha kusudi la uhai?

[Hisani]

Courtesy Arecibo Observatory/David Parker/Science Photo Library

[Picha katika ukurasa wa 6]

Nyota kwenye ukurasa wa 2, 3, 5, na juu kwenye ukurasa wa 7: National Optical Astronomy Observatories