Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wakristo Wanapaswa Kuwahubiria Wengine?

Je, Wakristo Wanapaswa Kuwahubiria Wengine?

Maoni ya Biblia

Je, Wakristo Wanapaswa Kuwahubiria Wengine?

HUENDA kulingana na malezi au utamaduni wako, haikupasi kuzungumzia mambo ya dini pamoja na watu wengine ila tu na watu wa familia yenu au kanisani. Hivyo, huenda ukaudhika wakati mtu ambaye hukutazamia anapokuja nyumbani kwako akiwa na Biblia. Watu wengine wana maoni hayo kwa sababu ya ujeuri uliofanywa na wanadini ambao walisingizia kwamba wanawaletea watu wokovu.

Katika nchi nyingi, watu wengi waligeuzwa imani kwa sababu walihofia kuuawa bali si kwa sababu ya kumpenda Kristo. Watu wengi walijificha, walihama makwao na nchi zao, au hata kufa—wengine wakiteketezwa kwenye mti—badala ya kukubali dini ya wanyanyasaji wao.

Maandiko ya Biblia yaliyotoka kwa Mungu hayaungi mkono matendo hayo ya kuwageuza watu imani kwa lazima. Basi, je, hiyo inamaanisha kwamba mtu hapaswi kuwaeleza wengine kuhusu imani yake ya kidini? Biblia inajibu.

Kufundisha kwa Mamlaka

Kwanza, hebu fikiria mfano wa Yesu Kristo. Alikuwa mwalimu stadi aliyekuwa na uvutano juu ya maisha ya watu waliomsikiliza. (Yohana 13:13, 15) Katika Mahubiri ya Mlimani, alifundisha kwa njia rahisi lakini yenye matokeo. Tokeo lilikuwa kwamba watu waliomsikiliza ‘walishangaa juu ya njia yake ya kufundisha; kwa maana alikuwa akiwafundisha kama mtu mwenye mamlaka.’ (Mathayo 7:28, 29) Miaka 2,000 hivi baadaye, watu wanaochunguza mafundisho yake wangali wanavutwa nayo. Profesa Hans Dieter Betz alitaja jambo linalopatana na hilo aliposema kwamba “uvutano wa Mahubiri ya Mlimani unazidi sana ule wa Dini ya Kiyahudi na Ukristo, au hata utamaduni wa Magharibi.”

Mara tu baada ya kupaa mbinguni, Yesu alitoa amri ambayo ilionyesha kwamba baada ya kifo chake kazi ya kufundisha aliyoanzisha ingeendelea na kuimarika. (Yohana 14:12) Aliwaagiza wanafunzi wake waende kwa watu wa mataifa yote, “kuwafundisha kushika mambo yote” ambayo aliwaamuru. Kusudi kuu la kazi hiyo lilionyeshwa wazi na maneno haya ya Yesu katika taarifa iyo hiyo: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi.”Mathayo 28:19, 20; Matendo 1:8.

Pia, fikiria mfano wa mtume Paulo. Baada ya kugeuka kuwa Mkristo, hakusita kuwatangazia wengine imani yake mpya. (Matendo 9:17-19, 22) Paulo alikuwa na desturi ya kufundisha kwenye masinagogi na kuthibitisha “kwa marejezo kwamba ilikuwa lazima Kristo kuteseka na kufufuliwa kutoka kwa wafu.” Kwa ustadi, ‘alitoa sababu kutokana na Maandiko’ ili ‘kuwashawishi Wayahudi na Wagiriki.’ Kulingana na kamusi moja neno la Kigiriki linalotafsiriwa “kushawishi” lamaanisha “kusababisha badiliko la maoni kwa kutoa sababu au kufikiria kanuni za maadili.” Kwa kuwa Paulo alitoa sababu kwa njia ya ushawishi ‘alishawishi umati mkubwa na kuwageuza kwenye kauli nyingine.’—Matendo 15:3; 17:1-4, 17; 18:4; 19:26.

Je, Inafaa Kulazimisha au Kushawishi?

Katika nyakati za kisasa, njia mbalimbali zimetumiwa kuwalazimisha watu kugeuza imani yao. Biblia haiungi mkono zoea hilo. Badala yake, inafundisha kwamba wanadamu waliumbwa wakiwa na hiari na vilevile haki na daraka la kuchagua jinsi wanavyotaka kuishi. Hiyo inatia ndani kuamua jinsi mtu anavyotaka kumwabudu Mungu.—Kumbukumbu la Torati 30:19, 20; Yoshua 24:15.

Yesu alionyesha kwamba aliheshimu haki hiyo kutoka kwa Mungu kwa kutotumia nguvu na mamlaka yake nyingi ili kumlazimisha mtu akubali mafundisho yake. (Yohana 6:66-69) Aliwachochea watu waliomsikiliza kwa kutoa sababu za kweli, kutumia mifano na maswali ya kutaka maoni, ili kufikia mioyo yao. (Mathayo 13:34; 22:41-46; Luka 10:36) Yesu aliwafundisha wanafunzi wake pia kuheshimu hiari ya wengine.—Mathayo 10:14.

Ni wazi kwamba Paulo alifuata mfano wa Yesu katika huduma yake. Paulo aliwashawishi watu waliomsikiliza kwa kutoa sababu za kweli kwa kutumia Maandiko, huku akiheshimu hisia na maoni yao. (Matendo 17:22, 23, 32) Alielewa kwamba ili tumtumikie Muumba wetu tunahitaji kuchochewa na upendo kwa Mungu na kwa Kristo. (Yohana 3:16; 21:15-17) Hivyo, uamuzi ni wetu binafsi.

Uamuzi wa Mtu Binafsi

Wakati wa kufanya maamuzi ya maana maishani kama vile kununua nyumba, kuchagua kazi, na kulea watoto, watu wenye akili hawafanyi maamuzi hayo bila kufikiri. Huenda wakachunguza uchaguzi mbalimbali walio nao, kutafakari juu ya mambo waliyochunguza na, hata labda, kuomba mashauri. Watafanya uamuzi baada tu ya kufikiria sana kuhusu mambo hayo.

Tunapofanya uamuzi kuhusu njia inayofaa ya kumwabudu Mungu tunahitaji kutumia wakati mwingi na jitihada nyingi kuliko tunapofanya uamuzi mwingine wowote maishani. Uamuzi huo utaathiri jinsi tunavyoishi sasa, na zaidi ya yote, utaathiri taraja letu la uhai wa milele wakati ujao. Wakristo wa karne ya kwanza huko Beroya walielewa jambo hilo waziwazi. Hata ingawa mtume Paulo mwenyewe aliwaeleza habari njema, bado walichunguza Maandiko kwa uangalifu kila siku ili kuhakikisha ikiwa mambo waliyofundishwa yalikuwa kweli. Hivyo, “wengi kati yao wakawa waamini.”—Matendo 17:11, 12.

Leo, Mashahidi wa Yehova huendelea na kazi ya kufundisha na kufanya wanafunzi ambayo ilianzishwa na Yesu. (Mathayo 24:14) Wanaheshimu haki ya watu wengine ya kuwa na dini yao. Lakini kwa habari ya kuwaeleza wengine kuhusu imani yao ya kidini, wao hufuata mfano unaopatikana katika Biblia. Naam, wao hutumia sababu za kweli kutoka kwenye Maandiko wanapofanya kazi ambayo kulingana na maoni yao, inaokoa uhai.—Yohana 17:3; 1 Timotheo 4:16.