Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kupatanisha Sayansi na Dini

Kupatanisha Sayansi na Dini

Kupatanisha Sayansi na Dini

“Siku hizi watu wanaonelea kwamba sayansi na dini zinaweza kupatanishwa.”—Gazeti la The Daily Telegraph la London la Mei 26, 1999.

SAYANSI na dini inayofaa hutafuta ukweli. Uvumbuzi wa sayansi hufunua ulimwengu wenye utaratibu wa hali ya juu, ulimwengu unaoonyesha wazi kwamba ulibuniwa na mtu mwenye akili. Dini ya kweli hufanya uvumbuzi huo uwe na maana kwa kufundisha kwamba Muumba mwenye akili ndiye aliyebuni ulimwengu.

Francis Collins, ambaye ni mwanabiolojia wa molekuli, anasema hivi: ‘Ninaona kwamba uelewevu wangu wa sayansi unaongezwa sana na dini. Ninapogundua jambo fulani kuhusu chembe za urithi za mwanadamu, ninahisi kicho kuhusu utata wa uhai, nami hujiambia hivi, “Lo! Ni Mungu tu aliyejua jambo hilo.” Hisia hiyo ni nzuri ajabu na inanichochea, nayo hunisaidia kumthamini Mungu na kufanya sayansi ipendeze hata zaidi.’

Ni nini kinachoweza kumsaidia mtu kupatanisha sayansi na dini?

Ni Jambo Linaloendelea

Kubali mipaka iliyopo: Yaonekana tutaendelea kujifunza kuhusu ulimwengu, anga, na wakati usio na kikomo. Mwanabiolojia Lewis Thomas alisema hivi: ‘Kujifunza hakutakoma, kwani wanadamu hupenda sana kujua, kupeleleza, kuchunguza na kujaribu kuelewa mambo. Hatutajua kamwe mambo yote. Sifikiri kutakuwa na wakati ambapo kila mtu ataweza kusema kwamba anajua kila kitu. Wanadamu hawataweza kamwe kuelewa mambo hayo.’

Vivyo hivyo, tamaa ya kufahamu kweli ya kidini haina kikomo. Paulo, mmoja wa waandikaji wa Biblia, alisema hivi: “Tunachoona sasa ni kama tu sura hafifu katika kioo . . . Sasa ninajua kiasi fulani tu.”—1 Wakorintho 13:12, Biblia Habari Njema.

Hata hivyo, ujuzi wa kiasi tu kuhusu sayansi na dini hauwezi kutuzuia kukata kauli zinazofaa ambazo zinategemea mambo ya kweli tunayofahamu. Hatuhitaji kujua mengi sana kuhusu chanzo cha jua ili tuwe na uhakika kabisa kwamba litachomoza kesho.

Fikiria ukweli wa mambo: Tunapotafuta majibu, tunahitaji kuongozwa na kanuni sahihi. Tusipoamini tu uthibitisho unaotegemeka kabisa, itakuwa rahisi kupotoshwa tunapotafuta ukweli wa kisayansi na wa kidini. Ni kweli kwamba hakuna mtu yeyote anayeweza kuanza kuchunguza dhana zote na maarifa yote ya kisayansi yanayopatikana katika maktaba kubwa-kubwa za leo. Kwa upande mwingine, Biblia ni kitabu ambacho kina mafundisho ya kiroho kwa ajili yetu na ni rahisi kukichunguza. Habari za Biblia zimethibitishwa kuwa za kweli. *

Hata hivyo, kuhusiana na ujuzi wa aina yoyote ile, mtu anahitaji kujitahidi sana kutofautisha kati ya ukweli wa mambo na mambo ya kukisia, kati ya mambo halisi na ya uwongo—iwe ni katika sayansi au dini. Kama vile Paulo, mwandikaji wa Biblia, alivyoshauri, tunahitaji kukataa “mapinganisho yenye kuitwa ‘ujuzi’ isivyo kweli.” (1 Timotheo 6:20) Ili kupatanisha sayansi na Biblia, ni lazima tuchunguze ukweli wa mambo na kuepuka makisio, na kuchunguza jinsi mambo ya kweli yanavyopatana.

Kwa mfano, tunapoelewa kwamba Biblia hutumia usemi “siku” ili kuwakilisha vipindi mbalimbali vya wakati, basi tunaona kwamba simulizi la Mwanzo kuhusu siku sita za uumbaji halipingani na maelezo ya kisayansi yanayosema kwamba dunia imekuwapo kwa miaka bilioni nne na nusu hivi iliyopita. Kulingana na Biblia, dunia ilikuwapo kwa muda usiojulikana kabla ya siku za uumbaji kuanza. (Ona sanduku “Je, Kila Siku ya Uumbaji Ilikuwa na Saa 24 Tu?”) Hata wanasayansi wakirekebisha maelezo yao na kuonyesha kwamba dunia iliumbwa katika kipindi tofauti na hicho, bado maelezo ya Biblia ni ya kweli. Katika visa vingi kama hivyo, sayansi haipingi Biblia bali inatoa habari nyingi za ziada kuhusu ulimwengu wa sasa na pia ule wa zamani.

Imani, si kuamini mambo bila uthibitisho: Biblia hutupatia ujuzi juu ya Mungu na makusudi yake ambayo hayapatikani mahali pengine popote. Kwa nini tuamini Biblia? Biblia yenyewe inatutia moyo tuichunguze ili tuone ikiwa ni sahihi. Hebu fikiria masimulizi yake ya kweli ya historia, jinsi inavyoweza kutusaidia maishani, unyoofu wa waandikaji wake, na jinsi ilivyoandikwa kwa usahihi. Mtu anapochunguza usahihi wa Biblia, kutia ndani taarifa zake zinazohusu mambo ya sayansi, na hata mamia ya unabii ambao umetimia kabisa zamani na katika wakati huu, anaweza kuiamini kwa uhakika kuwa Neno la Mungu. Kwa kuwa taarifa za Maandiko zimethibitishwa, kuamini Biblia si kuamini mambo bila uthibitisho bali ni kuwa na uhakika kwamba taarifa hizo ni sahihi.

Heshimu sayansi: tambua thamani ya imani ya kidini: Mashahidi wa Yehova wanawaomba watu wanaoweza kukubali maoni mapya, iwe ni wanasayansi au wanadini, kutafuta ukweli kwa bidii katika pande zote mbili. Katika makutaniko yao, Mashahidi huwatia watu moyo kuheshimu sayansi na uthibitisho wa kisayansi kwa njia inayofaa na pia kuamini kabisa kwamba ukweli wa kidini unaweza kupatikana tu katika Biblia, ambayo inasema waziwazi na kwa uthibitisho mwingi kwamba hiyo ni Neno la Mungu. Mtume Paulo alisema hivi: “Mlipopokea neno la Mungu, ambalo mlilisikia kutoka kwetu, mlilikubali, si kama neno la wanadamu, bali, kama vile lilivyo kwa kweli, kama neno la Mungu.”—1 Wathesalonike 2:13.

Kwa wazi, sawa na sayansi, uwongo na mazoea yenye kudhuru yameingizwa katika dini. Kwa hiyo, kuna dini ya kweli na dini ya uwongo. Hiyo ndiyo sababu watu wengi wameacha dini za kawaida na kuwa washiriki wa kutaniko la Kikristo la Mashahidi wa Yehova. Wamekata tamaa kwa sababu dini walizoshirikiana nazo hapo awali zilikataa kufuata ukweli na badala yake kufuata mapokeo na mafundisho ya uwongo ya wanadamu.

Zaidi ya hilo, Wakristo wa kweli hupata kusudi halisi maishani kwa kutegemea ujuzi mwingi kumhusu Muumba na makusudi yake kwa ajili ya wanadamu na dunia yetu, kama inavyoelezwa katika Biblia. Mashahidi wa Yehova wameridhika na majibu ya Biblia yenye kupatana na akili kuhusu maswali kama vile, Kwa nini tuko hai? Wakati ujao utakuwaje? Watafurahi sana kukueleza habari hizo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Ona kitabu BibliaNeno la Mungu au la Binadamu? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Sanduku katika ukurasa wa 10]

Je, Kila Siku ya Uumbaji Ilikuwa na Saa 24 Tu?

Watu fulani wenye imani kali ya kidini wanasema kwamba vitu vyote vinavyoonekana viliumbwa katika kipindi cha siku sita tu kati ya miaka 6,000 na 10,000 iliyopita, na kila siku ilikuwa na saa 24. Lakini kwa kufanya hivyo, wanaendeleza fundisho lisilopatana na Maandiko ambalo limewafanya watu wengi kuidharau Biblia.

Je, kila wakati ambapo Biblia inataja siku moja huwa inamaanisha kipindi cha saa 24? Mwanzo 2:4 inasema kuhusu “siku ile BWANA Mungu alipoziumba mbingu na nchi.” Siku hiyo moja inatia ndani siku zote sita za uumbaji zinazotajwa kwenye Mwanzo sura ya 1. Biblia hutumia neno siku kuonyesha kipindi cha wakati kilicho na urefu fulani na kinaweza kuwa cha miaka elfu moja au maelfu mengi ya miaka. Inawezekana kwamba kila siku ya uumbaji inayotajwa katika Biblia ilikuwa na maelfu ya miaka. Isitoshe, tayari dunia ilikuwepo hata kabla ya siku za uumbaji kuanza. (Mwanzo 1:1) Kwa hiyo, simulizi la Biblia linapatana na sayansi ya kweli katika jambo hilo.—2 Petro 3:8.

Akizungumzia kuhusu maoni ya kwamba siku za uumbaji zilikuwa saa 24 tu, mwanabiolojia wa molekuli Francis Collins anasema hivi: ‘Ile dhana ya kwamba kila siku ya uumbaji ilikuwa na saa 24 tu imepotosha sana imani ya watu wenye akili kuliko kitu kingine chochote hivi karibuni.’

[Sanduku katika ukurasa wa 11]

Je, Sayansi Ndiyo Yenye Maadili Bora Zaidi?

Inaeleweka ni kwa nini watu wengi wanaopenda sayansi wamekataa dini kwa sababu ya jinsi ambavyo imepinga maendeleo ya kisayansi, matendo yake mabaya, na unafiki na ukatili wake. Profesa wa elimu ya vijiumbe John Postgate anasema hivi: ‘Dini za ulimwengu zimesababisha uovu mwingi kupitia kuua wanadamu kama dhabihu, vita vitakatifu, maangamizi makubwa ya jamii mbalimbali, na mabaraza ya kuwahukumu waasi. Katika ulimwengu wa sasa, uovu huo wa dini umekuwa hatari. Kwani, dini si kama sayansi kwa sababu inaweza kuunga mkono upande wowote.’

Akilinganisha jambo hilo na vile ambavyo sayansi inaonekana kuwa yenye busara, isiyopendelea, na yenye utulivu, Postgate anasema kwamba “sasa sayansi ndiyo yenye maadili bora zaidi.”

Je, kweli sayansi ina maadili bora zaidi? La. Postgate mwenyewe anakubali kwamba ‘wanasayansi huwa na wivu, pupa, na ubaguzi.’ Anaongeza kwamba “wanasayansi wachache wamekuwa tayari kuua kwa sababu ya utafiti, kama ilivyotukia katika Ujerumani ya Nazi na katika kambi za magereza huko Japani.” Na wakati jarida la National Geographic lilipomtuma mwandishi wa habari kupeleleza jinsi habari za kisukuku bandia zilivyoingia katika jarida hilo, mwandishi huyo alitaja mambo kama vile “kuweka siri isivyofaa, kuamini watu wabaya, migogoro mikali kati ya watu walioshikilia kauli zao binafsi, watu waliojifanya kuwa wa maana sana, kuwazia mambo yasiyokuwapo, makisio ya kipumbavu, makosa, ukaidi, kubadili mambo kwa ujanja ili kujifaidi, kusengenyana, kusema uwongo, [na] ufisadi.”

Na ni wazi kwamba wanasayansi ndio wamewatengenezea wanadamu silaha hatari za vita, kama vile viini vya magonjwa vinavyotumiwa kama silaha, gesi yenye sumu, makombora, mabomu yanayoongozwa na miangaza maalumu, na mabomu ya nyuklia.

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Wingu la mavumbi la “Ant Nebula” (Menzel 3), kama lilivyoonekana kwenye Darubini ya Angani ya Hubble

[Hisani]

NASA, ESA and The Hubble Heritage Team (STScI/AURA)

[Picha katika ukurasa wa 9]

Uvumbuzi wa sayansi umeonyesha wazi kwamba ulimwengu ulibuniwa na mtu mwenye akili

[Picha katika ukurasa wa 10]

Mashahidi wa Yehova huwatia watu moyo waheshimu sayansi ya kweli na kuamini Biblia