Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa mhariri: Wasomaji wengi wametuandikia kuhusu mfululizo wa makala wenye kichwa “Uhai Una Thamani” (Oktoba 22, 2001). Jambo hilo linatufurahisha sana kwa sababu kupitia gazeti la “Amkeni!” tunajitahidi kutoa habari za Biblia zinazoweza kuwasaidia watu wa kila taifa, rangi, na dini kutatua matatizo ya siku hizi.

Nimesoma gazeti la Amkeni! kwa muda mrefu, lakini sijawahi kuguswa kama nilivyoguswa na mfululizo wa “Uhai Una Thamani.” Mwaka mmoja uliopita nilikuwa nimekata tamaa kabisa na nilitaka kufa. Mfululizo huo ulinihakikishia kwamba Mungu anaelewa udhaifu wetu.

S. H., Japani

Nilikuwa nimekufa moyo kwa sababu ya shambulizi la majengo ya Twin Towers huko New York. Nyakati nyingine nimefikiria kujiua, lakini sikuwa nimetambua kwamba nina shida fulani. Nitakwenda kupata msaada ninaohitaji na kufuata mapendekezo yaliyotolewa katika mfululizo huo.

M. M., Marekani

Nimefikiria kujiua kwa sababu ya afya yangu mbaya. Nilikuwa nikiongea na wengine kuhusu jambo hilo, nyakati nyingine kama mzaha tu, ili nijue maoni yao. Nilitokwa na machozi niliposoma kwamba Mungu hutusikiliza sikuzote na kutujali. Gazeti hili limebadili maoni yangu kabisa.

T.E.J., Kanada

Nimekuwa na mfadhaiko kwa miaka kadhaa, na hivi majuzi nilikuwa nimeamua kujiua. Nilipotaka kutoka nje, nilikumbuka kwamba ile makala ya mwisho ya mfululizo huo wa Amkeni! ilipendekeza kuongea na mtu. Kwa hiyo, nilimwambia mume wangu kuhusu nia yangu. Jambo hilo lilinizuia nisifanye vile nilivyokuwa nimeamua. Mfululizo huo uliokoa maisha yangu!

M. B., Marekani

Majuma machache kabla ya gazeti hilo kuchapishwa, nilikuwa nikitazama kikombe kilichojaa tembe za dawa ya usingizi na kujiuliza swali lilelile lililoonyeshwa kwenye makala hiyo: “Je, nizimeze au nisizimeze?” Gazeti lenu limenipa tamaa ya kuishi. Magonjwa mengine yanaathiri akili kiasi cha kwamba tunapoteza tamaa ya kuishi, lakini inafurahisha kuona kwamba Mungu anapendezwa hata na watu ambao hawaonekani kuthamini tena zawadi ya uhai.

E. S., Italia

Nilizungumzia habari zilizokuwa katika mfululizo huo pamoja na daktari wangu. Nilimwambia kwamba habari hizo zilikuwa zimenisaidia sana. Kujua kwamba Mungu ananithamini kunanitia moyo nitamani kuendelea kuishi. Ninaomba Mungu daima kwamba mwendelee kuandika makala kama hizo!

J. S., Marekani

Nilidhani kwamba hakukuwa na mtu yeyote anayenielewa, na nikaanza kufikiri kwamba kifo kingekuwa suluhisho rahisi. Lakini niliposoma makala hizo, nilikumbuka jambo muhimu zaidi maishani. Sitafikiria tena kujiua!

M. M., Japani

Wanawake Wanaopigwa Asanteni kwa mfululizo wa makala “Msaada kwa Wanawake Wanaopigwa.” (Novemba 8, 2001) Nilipokuwa mtoto nilimwona baba yangu akimpiga mama yangu kila siku. Kisha, alianza kunipiga mimi na dada zangu. Niliwachukia sana wanaume wote nilipokuwa mtoto. Hata hivyo, hatimaye tulianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Haikuwa rahisi kwa Baba kubadili mwenendo wake, lakini kwa msaada wa Yehova alianza kutambua kwamba hawezi kumpendeza Mungu ikiwa anawaumiza wengine. Alifanya mabadiliko polepole, lakini sasa baba yangu ni mpole sana. Ninampenda kwa moyo wote.

G. B., Marekani