Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mgogoro Kati ya Sayansi na Dini

Mgogoro Kati ya Sayansi na Dini

Mgogoro Kati ya Sayansi na Dini

“Je, dini ni ugonjwa wa akili ambao unaenea?”—Mwanabiolojia Richard Dawkins.

NYAKATI nyingine, watu huona kwamba dini na sayansi hazipatani kabisa. Wengine huonelea kwamba kuna mgogoro mkubwa sana kati ya mambo hayo mawili hivi kwamba huenda jambo moja litashinda endapo tu jambo lile jingine litatokomea.

Wanasayansi fulani, kama vile mtaalamu wa kemia Peter Atkins, wanaona kwamba “haiwezekani” kupatanisha dini na sayansi. Atkins anasema kwamba kuamini “kuwa kuwapo kwa Mungu kunajibu maswali (yoyote, sembuse maswali yote) ni jambo la upumbavu kabisa.”

Kwa upande mwingine wanadini wanalalamika kwamba sayansi imedhoofisha imani ya watu. Watu hao huamini kwamba sayansi ya kisasa ina udanganyifu; huenda maelezo ya kisayansi yakawa kweli, lakini imani ya wanadini hudhoofishwa wakati maelezo hayo yanapofafanuliwa kimakosa. Kwa mfano, mwanabiolojia William Provine anasema kuwa nadharia ya mageuzi huonyesha kwamba “hakuna msingi thabiti wa maadili; hakuna kusudi muhimu maishani.”

Hata hivyo, sehemu fulani ya mgogoro huo imesababishwa na madai ya uwongo au yasiyoweza kuthibitishwa kutoka pande hizo mbili. Kwa karne nyingi, viongozi wa dini wamefundisha hekaya na mafundisho ya uwongo ambayo hayapatani na ugunduzi wa kisasa wa sayansi wala na Maandiko yaliyoongozwa na Mungu. Kwa mfano, Kanisa Katoliki lilimshutumu Galileo kwa sababu alikata kauli, ya kweli, kwamba dunia inazunguka jua. Maoni ya Galileo hayakupinga Biblia, lakini yalikuwa tofauti na mafundisho ya kanisa ya wakati huo. Kwa upande mwingine, wanasayansi wanakosea wanapofundisha ile nadharia ambayo haijathibitishwa kuwa ya kweli inayosema kwamba uhai ulitokana na kitu kisichokuwa na uhai na si kutoka kwa Mungu. Wao hudhihaki mafundisho ya kidini wakisema kwamba hayapatani na sayansi.

Basi, je, inawezekana kupatanisha sayansi na dini? Naam, inawezekana. Kwa kweli, sayansi iliyothibitishwa kuwa ya kweli na dini ya kweli hukamilishana badala ya kupingana.

[Picha katika ukurasa wa 3]

Galileo alifundisha ukweli wa kisayansi, nayo dini ikamhukumu kwa sababu hiyo