Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unakaribishwa Kwenye Kusanyiko la Wilaya la “Watangazaji wa Ufalme Wenye Bidii”

Unakaribishwa Kwenye Kusanyiko la Wilaya la “Watangazaji wa Ufalme Wenye Bidii”

Unakaribishwa Kwenye Kusanyiko la Wilaya la “Watangazaji wa Ufalme Wenye Bidii”

MAKUSANYIKO 53 yamepangwa Afrika Mashariki na nchi za karibu. Kusanyiko la kwanza litafanywa Agosti 2-4 na la mwisho litafanywa katikati ya mwezi wa Septemba. Yaelekea mojawapo ya makusanyiko hayo ya siku tatu, ambayo kwa kawaida huanza Ijumaa na kumalizika Jumapili, yatafanywa karibu na eneo lenu.

Katika sehemu nyingi, programu itaanza saa 3:30 asubuhi kila siku. Siku ya kwanza, hotuba ya kukaribisha wasikilizaji itafuatwa na mahojiano ya watangazaji wa Ufalme. Kisha, hotuba “Furahi Sana Katika Yehova,” na “Jionyesheni Kuwa Wenye Shukrani” zitatolewa. Hotuba ya mwisho ya asubuhi itakuwa hotuba ya msingi yenye kichwa “Watangazaji wa Ufalme Wachochewa na Bidii.”

Ijumaa alasiri kutakuwa na mfululizo wa sehemu tatu wenye kichwa, “Unabii wa Mika Hutuimarisha Tutembee Katika Jina la Yehova,” na vilevile hotuba “Dumisha Usafi wa Maadili kwa Kulinda Moyo Wako” na “Jilinde Dhidi ya Udanganyifu.” Mwishowe, msaada bora utatolewa kuhusiana na huduma ya Kikristo katika hotuba ya mwisho ya siku hiyo, “Mwabudu Mungu wa Pekee wa Kweli.”

Jumamosi asubuhi kutakuwa na mfululizo wa sehemu tatu wenye kichwa, “Watangazaji wa Ufalme Ambao Huitukuza Huduma Yao.” Mfululizo huo utafuatwa na hotuba zenye kutia moyo, “Kwa Nini ‘Tusali Bila Kukoma’?” na “Maongezi ya Kiroho Hujenga.” Hotuba ya mwisho asubuhi hiyo itazungumzia kujiweka wakfu na ubatizo, na baadaye watu wanaostahili watabatizwa.

Jumamosi alasiri kutakuwa na mfululizo wa mwisho wenye sehemu tatu katika kusanyiko hili, “Ubora wa Imani Yetu Wajaribiwa na Magumu Mbalimbali.” Sehemu hizo tatu zitawasaidia Wakristo wasiunge mkono mambo yasiyofaa ya ulimwengu huu. Hotuba ya mwisho siku ya Jumamosi itakuwa yenye kuvutia na yenye kuchangamsha moyo. Ni hotuba yenye kichwa, “Mkaribie Yehova.”

Jumapili asubuhi, hotuba zitazungumzia vijana hasa. Hotuba ya kwanza itakuwa “Je, Unamfanya Yehova Kuwa Tumaini Lako?” ikifuatwa na “Vijana—Pangeni Maisha Yenu ya Wakati Ujao Katika Tengenezo la Yehova.” Sehemu ya mwisho ya hotuba hiyo itakuwa na mahojiano ya dakika 20. Baada ya hotuba hiyo kutakuwa na drama. kumhusu Yeremia aliyesema, “Mimi ni mtoto,” wakati alipowekwa kuwa nabii. Waigizaji watavalia nguo za nyakati za Biblia. (Yeremia 1:6) Baadaye kutakuwa na hotuba itakayoeleza waziwazi ujumbe wa drama hiyo. Katika kipindi cha alasiri, kutakuwa na hotuba ya watu wote yenye kichwa, “Mandhari ya Ulimwengu Huu Inabadilika.”

Bila shaka utafaidika kiroho ukiweza kuhudhuria siku zote tatu. Ili ujue kusanyiko litakalofanywa karibu na mahali unapoishi, wasiliana na Mashahidi wa Yehova katika eneo lenu au uwaandikie wachapishaji wa gazeti hili. Toleo la Februari 15, 2002, la gazeti letu la Mnara wa Mlinzi linaonyesha orodha ya makusanyiko yote yatakayofanywa Burundi, Kenya, Kongo (Kinshasa), Tanzania, na Uganda.