Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Wanawake Wanaopigwa Ninashukuru sana kwa mfululizo wa makala wa “Msaada kwa Wanawake Wanaopigwa.” (Novemba 8, 2001) Mimi hupigwa na mume wangu, na hata niliporipoti hali hiyo kwa wenye mamlaka, bado sikuweza kuamini kwamba mtu yeyote anaweza kuelewa huzuni, uchungu wa moyoni, na maumivu niliyokuwa nayo ambayo sikuweza kuyatuliza kwa vyovyote. Mfululizo huo ulieleza hisia zangu kabisa.

N. L., Italia

Nilipofungua bahasha ya gazeti hilo na kuona jalada lake, nilitokwa na machozi. Mara moja nililifunga tena kwa kuwa gazeti hilo lilizungumzia magumu niliyopata maishani ambayo nilitaka kusahau. Nilisali ili nipate nguvu za kulisoma gazeti hilo. Ninafurahi sana kwamba nilifanya hivyo! Mfululizo huo wa makala ulinisaidia kutambua kwamba kuna wengine wanaoteseka kama mimi. Kusoma tu maneno, “kumpiga mwenzi wa ndoa ni dhambi nzito machoni pa Mungu” kulinifariji sana. Asanteni sana kwa habari kama hizo zinazozungumzia vile hali ilivyo.

D.G.M., Marekani

Nimepatwa na mambo yaleyale ambayo yaliwapata wanawake waliotajwa katika mfululizo huo. Nilikuwa nikijiambia kwamba kileo na malezi ya mume wangu ndiyo yaliyosababisha tabia hiyo. Lakini nilifarijika kujua kwamba ijapokuwa mambo hayo yanaweza kusababisha waume wapige wake zao, hayawezi kamwe kuwapa haki ya kufanya hivyo. Kwa moyo wangu wote ninataka mume wangu aanze kujifunza Biblia ili apendwe na Yehova.

S. I., Japani

Mfululizo huo wa makala ulinivutia kwa njia ya pekee, kwa kuwa mume wangu hunipiga. Nilijihisi kana kwamba nilikuwa Roxana. Inasaidia sana kujua kwamba watu wengine wanaelewa jinsi mwanamke anayepigwa anavyohisi. Nilijifunza kutokana na mfululizo huo wa makala kwamba sipaswi kujilaumu kwa sababu ya mwenendo wa mume wangu. Ulinisaidia pia kutambua kwamba Mungu ananithamini hata ingawa mume wangu ananiona kuwa mtu asiyefaa na asiye wa maana. Asanteni kwa kuchapisha habari hizo zenye faida. Habari kama hizo ni bora kuliko mali nyingi!

B. L., Ufilipino

Mlifaulu kueleza uchungu na hisia za kukata tamaa ambazo mimi nimeshindwa kueleza. Mfululizo huo wa makala ulinisaidia kuona kwamba Yehova anaelewa jinsi hali hiyo inavyovuruga akili na kumfadhaisha mtu. Tafadhali endeleeni kuandika habari kama hizo, kwa kuwa ni lazima tatizo hili lizungumziwe ili wengine walielewe. Ninajua kwamba wengi watafarijika kama mimi watakaposoma mfululizo huo wa makala.

K. E., Australia

Baba yangu alifoka kwa urahisi, nami humfokea mume wangu mara nyingi. Mara nyingi mimi humpiga. Mume wangu ni mwenye nguvu kuliko mimi, kwa hiyo sikufikiri nilimwumiza. Niliposoma makala hiyo—kwamba kumpiga mwenzi ni dhambi nzito machoni pa Mungu—nilishtuka sana. Mume wangu ni mtumishi mpole wa Yehova. Ninataka kumwomba msamaha kwa moyo wangu wote. Ninamshukuru Yehova kwa nidhamu hiyo.

T. I., Japani

Niliposoma gazeti hilo nilitokwa na machozi. Ni kana kwamba nilisoma kuhusu maisha yangu. Lakini, hivi majuzi mume wangu amekuwa akiuliza maswali kuhusu Biblia. Amehudhuria mikutano kadhaa katika Jumba la Ufalme, na sasa anajifunza Biblia. Ninakubaliana na maneno haya ya Lourde kwenye ukurasa wa 11: “Wakati mwingine mimi hufikiri ninaota ndoto!”

E. R., Marekani