Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ninawezaje Kuishi Vizuri na Yule Ninayeishi Naye?

Ninawezaje Kuishi Vizuri na Yule Ninayeishi Naye?

Vijana Huuliza . . .

Ninawezaje Kuishi Vizuri na Yule Ninayeishi Naye?

“Nilitaka eneo la jikoni liwe safi. Lakini wasichana nilioishi nao waliacha vyombo ovyoovyo au sufuria juu ya jiko. Hawakujali.”—Lynn. *

WATU wanaoishi pamoja “wanaweza kuwa marafiki wakubwa au maadui wakubwa,” asema mwandishi Kevin Scoleri. Huenda maoni yako yasiwe makali hivyo, lakini ni wazi kwamba kuishi na mtu mwingine kwaweza kuwa jambo gumu. * Kuna migogoro mingi kati ya wanafunzi wa chuo kikuu wanaoishi pamoja hivi kwamba jarida la U.S.News & World Report linasema kuwa vyuo vingi “vinajitahidi sana” kuwasaidia wanafunzi wanaokaa pamoja waweze kuishi vizuri. Pia, vyuo hivyo hufanya mikutano na ‘mipango ya kusuluhisha matatizo baina ya wanafunzi.’

Hata vijana Wakristo ambao wamehama makwao ili kufanya kazi ya kuhubiri wakati wote wanaweza kuona ni vigumu kuishi na mtu mwingine. Ni vizuri kukumbuka kwamba mara nyingi hali za kutoelewana zinaweza kutatuliwa kwa kutumia kanuni za Biblia na kuwa na “hekima.”—Mithali 2:7.

Mjue Vizuri Yule Mtu Mwingine

Msisimko wa kuhama unapokwisha, unaweza kuanza kutamani maisha uliyokuwa nayo nyumbani. (Hesabu 11:4, 5) Hata hivyo, kufikiria sana kuhusu yaliyopita kutafanya iwe vigumu zaidi kuzoea maisha mapya. Andiko la Mhubiri 7:10, linatoa shauri hili kulingana na Biblia Habari Njema: “Usiulize, ‘Kwa nini nyakati za kale zilikuwa bora kuliko za sasa?’ Huulizi hivyo kwa kutumia hekima.” Naam, jaribu kufurahia hali yako ya sasa.

Anza kwa kujitahidi kumjua vizuri yule unayeishi naye. Ni kweli kwamba si lazima watu wanaoishi pamoja wawe marafiki wa karibu sana. Na huenda usivutiwe na mtu unayeishi naye. Hata hivyo, iwapo ni lazima uishi naye, je, huoni kwamba ni jambo la akili kuwa na uhusiano mwema naye?

Andiko la Wafilipi 2:4 linatuambia tuangalie, ‘si masilahi ya kibinafsi ya mambo yetu wenyewe tu, bali pia masilahi ya kibinafsi yale ya wengine.’ Bila kufanya mazungumzo yawe kama mahojiano, unaweza kumuuliza yule unayeishi naye kuhusu familia yao, mapendezi yake, na miradi yake. Mweleze kuhusu maisha yako. Kadiri mnavyojuana zaidi, ndivyo mtakavyoelewana zaidi.

Mara kwa mara, pangeni kufanya mambo pamoja. Lee anasema hivi: “Nyakati nyingine mimi huenda kwenye mikahawa au kwenye majumba ya sanaa pamoja na watu ninaoishi nao.” Njia bora kwa Wakristo wanaoishi pamoja kusitawisha urafiki ni kushiriki katika utendaji wa kiroho pamoja, kama vile kutayarisha mikutano ya kutaniko au kuhubiri.

David anasema hivi: “Wakati ambapo yule ninayeishi naye alikuwa na hotuba ya Biblia, nilienda kwenye kutaniko lake ili kumtia moyo.” Japo David na yule anayeishi naye wana mapendezi tofauti ya michezo na muziki, upendo wao kwa mambo ya kiroho umefanya wawe marafiki. David anasema hivi: ‘Sisi huzungumza sana kuhusu mambo ya kiroho. Twaweza kutumia saa nyingi sana kuzungumzia mambo ya kiroho.’

Tahadhari: Uhusiano wako na yule unayeishi naye haupaswi kuwa wa karibu sana kiasi cha kukuzuia usiwe na marafiki wengine. Ikiwa yule unayeishi naye anahisi kuwa ni lazima uandamane naye kila anapoenda mahali fulani, huenda akaanza kuhisi kwamba amebanwa sana. Biblia inakushauri ‘upanue’ urafiki wako.—2 Wakorintho 6:13.

Kufuata Ile Kanuni Bora

Bila shaka, mnapozidi kujuana vizuri, mtatambua pia jinsi tabia, mapendezi, na maoni yenu yanavyotofautiana. Kama vile kijana anayeitwa Mark anavyoonya, “mwapaswa kutazamia kasoro.” Kushikilia sana mapendezi yako au kujifikiria sana husababisha kutoelewana. Kutoelewana hutokea pia unapomtazamia yule unayeishi naye afanye mabadiliko makubwa ili kukupendeza.

Fernando amejifunza somo hili kwa kuishi na mtu mwingine: “Unapaswa kuwafikiria wengine bali si kujifikiria sana.” Maneno yake yanapatana na ile Kanuni Bora inayojulikana sana, inayosema hivi: “Kwa hiyo, mambo yote mtakayo watu wawafanyie nyinyi, lazima mwafanyie wao pia hivyohivyo.” (Mathayo 7:12) Kwa mfano, baada ya muda Fernando na yule aliyekuwa akiishi naye walizozana kuhusu hali ya joto chumbani mwao. Fernando alitaka chumba kiwe na joto, lakini yule aliyeishi naye alipenda kulala katika chumba kisichokuwa na joto. Suluhisho likawa nini? Fernando anasema hivi: “Nilinunua blanketi.” Naam, kama vile Mark anavyosema, “badilika kulingana na hali. Si lazima utupilie mbali mapendezi yako yote, lakini huenda ukahitaji kuachilia mapendezi kadhaa.”

Unaweza pia kutumia ile Kanuni Bora kwa njia hii: Jifunze kukubali mapendezi ya mtu unayeishi naye. Kwa mfano, labda hupendi muziki ambao anapenda. Lakini huenda ikawa yeye pia hapendi muziki ambao unapenda. Kwa hiyo, iwapo yule unayeishi naye anapenda muziki ambao hauvunji kanuni za maadili, unaweza kujaribu kuvumilia. Fernando anasema hivi: “Ingekuwa afadhali kama yule ninayeishi naye angependa muziki tofauti. Lakini nimeanza kuzoea.” Kwa upande mwingine, mtu anaweza kusikiliza muziki kwa kutumia vidude vinavyovaliwa masikioni ili asimsumbue mwenzake, ambaye labda anasoma.

Kutumia ile Kanuni Bora kwaweza pia kuzuia migogoro isiyo ya lazima kuhusu vitu mbalimbali. Kwa mfano, ikiwa una tabia ya kula vyakula vyovyote vinavyopatikana nyumbani bila ruhusa na bila kununua vingine, hilo linaweza kutokeza chuki. Kwa upande mwingine, kukasirika au kumkodolea macho yule unayeishi naye eti kwa sababu ametumia kitu ambacho umenunua hakuwezi kuzidisha urafiki wenu. Biblia inatutia moyo “kuwa wakarimu, tayari kushiriki.” (1 Timotheo 6:18) Ukihisi kwamba mwenzako anatumia vitu vyako kupita kiasi, usinyamaze tu. Taja malalamiko yako kwa upole na fadhili.

Heshimu mali za yule unayeishi naye. Kuchukua kitu bila ruhusa ni kuwa na kimbelembele. (Mithali 11:2) Pia, elewa kwamba yule unayeishi naye anahitaji kuwa na faragha. Onyesha adabu kwa kupiga hodi kabla ya kuingia chumbani mwake. Ukimheshimu, yaelekea atakuheshimu. David anasema hivi: ‘Mimi na yule ninayeishi naye twaweza kusomea nyumbani. Kila mmoja wetu anaheshimu kabisa jambo hilo nasi hatupigi kelele wakati yule mwingine anaposoma. Lakini nyakati nyingine mimi huenda kusomea kwenye maktaba iwapo yule ninayeishi naye anataka kufanya mambo mengine.’

Kufuata ile Kanuni Bora pia kunatia ndani kutimiza wajibu wako kama vile kulipa sehemu yako ya kodi kwa wakati au kufanya kazi za nyumba ulizogawiwa.

Kushughulikia Hali za Kutoelewana

Katika nyakati za Biblia, kulitokea “mfoko mkali wa hasira” kati ya Paulo na Barnaba, wanaume wawili Wakristo walioheshimiwa sana. (Matendo 15:39) Vipi jambo kama hilo likitokea kati yenu? Huenda ikawa nyutu zenu hazipatani au unashindwa kuvumilia tabia fulani yenye kuudhi. Je, inafaa kuacha kuishi pamoja mnapokosa kuelewana juu ya jambo moja au ugomvi mkali unapotokea mara moja? Si lazima. Ni wazi kwamba Paulo na Barnaba walitatua hali hiyo ya kutoelewana. Labda wewe pia unaweza kufanya hivyo kabla ya kuamua haraka-haraka kuhama. Kanuni za Biblia zifuatazo zinaweza kusaidia.

‘Usifanye jambo lolote kwa ugomvi au kwa majisifu ya bure, bali kwa hali ya akili ya kujishusha chini, ukifikiria kwamba wengine ni wakubwa kuliko wewe.’—Wafilipi 2:3.

“Acheni uchungu wote wenye nia ya kudhuru na hasira na hasira ya kisasi na kupiga kelele na usemi wenye kuudhi viondolewe mbali kutoka kwenu pamoja na ubaya wote. Bali iweni wenye fadhili nyinyi kwa nyinyi, wenye huruma kwa njia nyororo, mkisameheana kwa hiari mtu na mwenzake kama vile Mungu pia kupitia Kristo alivyowasamehe nyinyi kwa hiari.”—Waefeso 4:31, 32.

“Basi, ikiwa wewe unaleta zawadi yako kwenye madhabahu na huko wakumbuka kwamba ndugu yako ana jambo fulani dhidi yako, acha zawadi yako hapo mbele ya madhabahu, na uende zako; kwanza fanya amani yako na ndugu yako, na ndipo, ukiisha kurudi, toa zawadi yako.”—Mathayo 5:23, 24; Waefeso 4:26.

Faida

Vijana wengi Wakristo (na pia watu wenye umri mkubwa) ambao wanaishi na mtu mwingine wamejionea ukweli wa maneno haya ya Mfalme Solomoni mwenye hekima: “Afadhali kuwa wawili kuliko mmoja.” (Mhubiri 4:9) Kwa kweli, wengi wamefaidika kwa kuishi na mtu mwingine. Mark anasema hivi: “Nimejifunza jinsi ya kushughulika na watu vizuri na kubadilika kulingana na hali.” Renee aongeza hivi: “Unajifahamu vizuri zaidi. Na vilevile, mtu unayeishi naye anaweza kukutia moyo kuwa na tabia njema.” Lynn anakubali hivi: “Nilikuwa nikijifikiria sana nilipoanza kuishi na watu wengine. Lakini nimejifunza kubadilika kulingana na hali. Sasa ninatambua kwamba mtu anapofanya mambo kwa njia tofauti na jinsi ninavyopenda, hiyo haimaanishi kwamba amekosea.”

Naam, kuishi vizuri na mtu mwingine kwahitaji jitihada na kujinyima. Lakini ukijitahidi kutumia kanuni za Biblia, zaidi ya kuishi tu kwa amani, huenda ukaona kwamba inafurahisha kuwa na mtu wa kuishi naye.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

^ fu. 4 Ona makala “Mbona Yule Ninayeishi Naye Ni Mgumu Sana?” katika toleo la Aprili 22, 2002.

[Picha katika ukurasa wa 16]

Kula vyakula vya mtu mwingine bila ruhusa kwaweza kusababisha kutoelewana

[Picha katika ukurasa wa 17]

Mjali mwenzako