Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Utumwa Utakapokoma!

Utumwa Utakapokoma!

Utumwa Utakapokoma!

UHURU! Neno hilo ni mojawapo ya maneno yanayowafurahisha sana wanadamu. Watu wamepigana na kuteseka, kuishi na kufa, wakitafuta uhuru. Hata hivyo, inahuzunisha kwamba wengi wamefanya hivyo bila kufanikiwa sana. Je, kuna tumaini lolote kwamba utumwa utakoma—tumaini ambalo halitawafadhaisha wanadamu wala kuwakatisha tamaa? Naam, lipo.

Mtume Paulo aliongozwa na Mungu kuandika ahadi yake inayosema hivi: “Viumbe vyenyewe pia vitawekwa huru kutoka katika utumwa wa uharibifu na kuwa na uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.” (Waroma 8:21) Lakini tunawezaje kuwa na uhakika kwamba Mungu ataleta ‘uhuru huo wenye utukufu’? Njia moja ni kuchunguza jinsi ambavyo Mungu ameshughulika na wanadamu sikuzote.

Biblia inasema hivi: “Iliko roho ya Yehova, kuna uhuru.” (2 Wakorintho 3:17) Naam, roho ya Mungu, au nguvu yake ya utendaji, ina nguvu nyingi sana. Kwa muda mrefu, ameitumia kuwaweka watu huru kwa njia nyingi. Jinsi gani? Twapaswa kukumbuka kwamba kuna aina nyingi za utumwa. Tayari tumezungumzia aina moja yenye ukatili mwingi sana—jinsi ambavyo watu wenye uwezo huwatumikisha watu wasio na uwezo kwa nguvu au kwa ujeuri. Lakini hebu fikiria aina nyingine za utumwa.

Watu wanaweza kuwa watumwa wa mazoea mbalimbali ambayo ni vigumu sana kuyaacha. Na watu wanaweza kuwa watumwa wa uwongo na udanganyifu, wakidanganywa kuamini mafundisho ya uwongo sikuzote. Zaidi ya yote, kuna aina moja ya utumwa ambayo inatuathiri sote—iwe twajua au hatujui—na matokeo yake husababisha kifo. Hata hivyo, ni lazima tukazie kwamba ijapokuwa tunazungumzia aina mbalimbali za utumwa katika habari hii, hatumaanishi hata kidogo kwamba zote ziko sawa. Aina za utumwa zinatofautiana sana. Hata hivyo, zinafanana katika jambo moja. Hatimaye, Mungu wa uhuru atahakikisha kwamba wanadamu wamewekwa huru kutokana na aina zote hizo za utumwa.

Mazoea Yanapowafanya Watu Kuwa Watumwa

Ona jinsi kitabu When Luck Runs Out kinavyofafanua uchezaji sugu wa kamari: “Ni tatizo linalomchochea sana mtu kucheza kamari bila kuwa na uwezo wa kujidhibiti. Kichocheo hicho huendelea kwa muda mrefu, huongezeka na kuzidisha hamu . . . hadi, hatimaye, kinaingilia, kinadhoofisha na mara nyingi kuvuruga mambo yote ya maana katika maisha ya mtu huyo.” Hakuna ajuaye ni watu wangapi ambao ni watumwa wa kamari. Katika nchi moja tu, Marekani, inakadiriwa kwamba watu milioni sita ni watumwa wa kamari.

Kuwa mtumwa wa kileo kwaweza kusababisha madhara kama hayo, au hata mabaya zaidi, na watu wengi zaidi katika sehemu nyingi ni watumwa wa zoea hilo. Katika nchi moja kubwa, nusu ya idadi ya wanaume ni walevi sugu kwa kadiri fulani. Ricardo, aliyeanza kuwa mlevi sugu miaka 20 iliyopita, anaeleza hivi kuhusu zoea hilo: “Kuanzia wakati unapoamka, mwili wako unatamani kileo—ili utulie, usahau matatizo yako, au kujiamini vya kutosha kuweza kukabiliana na maisha. Mtu hutamani sana kunywa pombe, huku akijaribu kujisadikisha na kuwasadikisha watu wengine kwamba hana tatizo lolote.”

Mbali na kileo, kuna vitu vingine pia vinavyowafanya watu kuwa watumwa. Ulimwenguni pote, mamilioni ya watu hutumia dawa za kulevya. Isitoshe, watu bilioni 1.1 hivi hutumia tumbaku—ambayo ina mojawapo ya dawa za kulevya zinazowafanya watu kuwa watumiaji sugu sana. Watu wengi wangependa kuacha zoea hilo, lakini wanahisi kwamba hawawezi. Je, Yehova amewakomboa watu kutokana na aina hizo za utumwa zenye nguvu? *

Hebu fikiria mfano wa Ricardo. Anasema hivi: “Miaka kumi hivi iliyopita, nilitambua kwamba maisha yangu yaliongozwa na kileo. Jambo hilo lilikuwa likiharibu ndoa yangu, kazi yangu, na familia yangu, na nilijua kwamba singeweza kutatua matatizo yangu pasipo kuacha zoea hilo. Kupitia funzo la Biblia, nilijifunza kwamba umaskini—uwe ni halisi au wa kiroho—humkumba mlevi. (Mithali 23:20, 21) Nilitaka kuwa na uhusiano mzuri na Mungu, na nilipomwomba kwa moyo mnyofu, hilo lilinisaidia kujichunguza waziwazi. Mwanamume mmoja alijifunza Biblia pamoja nami, na akawa rafiki yangu mpendwa. Niliporudia zoea hilo, yeye hakuvunjika moyo, lakini kwa subira na uthabiti alinionyesha jinsi Mungu anavyotaka Wakristo wa kweli watende.”

Akilinganisha maisha yake ya awali na ya sasa, Ricardo anahisi kwamba amewekwa huru kutokana na utumwa huo. Anakubali waziwazi kwamba hapo mwanzoni alirudia zoea hilo mara kwa mara. Anasema hivi: “Lakini kujapokuwa vizuizi hivyo, tamaa yangu ya kumtumikia Yehova kwa uaminifu, na vilevile utegemezo wa mke wangu na Wakristo wenzangu, umenisaidia kukabiliana vema na hali hiyo. Ninatazamia kuona ahadi ya Mungu ikitimia, wakati ambapo ‘hakuna mtu atakayesema, Mimi mgonjwa’ na ulevi sugu utakoma. Kwa sasa, nitaendelea kujitahidi kila siku kutoa mwili wangu kuwa ‘dhabihu iliyo hai, takatifu, yenye kukubalika kwa Mungu.’”—Isaya 33:24; Waroma 12:1.

Maelfu ya watu ulimwenguni pote walisaidiwa na Mungu walipojitahidi kuacha mazoea mabaya. Ni kweli kwamba, wao wenyewe ndio waliojiingiza katika utumwa, labda kwa kujiruhusu washindwe na vishawishi. Hata hivyo, wametambua kwamba Yehova ni Mkombozi mwenye subira nyingi. Yu tayari kuwasaidia na kuwaimarisha wote wanaotaka sana kumtumikia.

“Kweli Itawaweka Nyinyi Huru”

Vipi juu ya utumwa wa uwongo na udanganyifu? Yesu Kristo anatuhakikishia kwamba inawezekana kuwekwa huru kutokana na utumwa huo. Alisema hivi: “Ikiwa nyinyi mwakaa katika neno langu, nyinyi kwa kweli ni wanafunzi wangu, nanyi mtajua kweli, na kweli itawaweka nyinyi huru.” (Yohana 8:31, 32) Wakati huo, watu wengi waliomsikiliza Yesu walikuwa watumwa wa sheria kali za mapokeo ya Mafarisayo. Ndiyo sababu Yesu alisema hivi kuhusu viongozi wa kidini wa wakati wake: “Wao hufunga mizigo mizito na kuiweka juu ya mabega ya watu, lakini wao wenyewe hawataki kuisogeza kwa kidole chao.” (Mathayo 23:4) Mafundisho ya Yesu yaliwaweka watu huru kutokana na utumwa huo. Alifichua uwongo wa kidini, na hata akataja waziwazi chanzo cha uwongo huo. (Yohana 8:44) Alifichua uwongo na kufundisha kweli, akieleza waziwazi matakwa rahisi ambayo Mungu anataka wanadamu watimize.—Mathayo 11:28-30.

Sawa na wanafunzi wa Yesu, maelfu ya watu leo wanaona kwamba kwa msaada wa Mungu wanaweza kuacha uwongo wa kidini na mapokeo ya uwongo ambayo yamewafanya kuwa watumwa. Baada ya kujifunza kweli za Biblia zenye kuburudisha, wao huwekwa huru kutokana na hofu ya wafu yenye kutisha, kutokana na hofu ya kuteketezwa milele motoni, na kutokana na kulazimishwa kulipa fedha wanazochuma kwa jasho eti ndiyo wapate msaada wa kidini kutoka kwa makasisi wanaodai kumwakilisha Kristo ambaye alisema hivi: “Mlipokea bure, toeni bure.” (Mathayo 10:8) Isitoshe, uhuru mkubwa zaidi u karibu.

Utumwa Hatari Zaidi Usioonekana Wazi

Hebu ona jinsi Yesu alivyofafanua utumwa mmoja hatari usioonekana wazi, ambao ulitajwa awali na unaathiri kila mwanamume, mwanamke, na mtoto hapa duniani: “Kwa kweli kabisa mimi nawaambia, Kila mtendaji wa dhambi ni mtumwa wa dhambi.” (Yohana 8:34) Ni nani anayeweza kudai kwamba yeye hatendi dhambi? Hata mtume Paulo alikubali hivi: “Lile jema nitakalo silifanyi, bali lile baya nisilotaka ndilo nazoea kulifanya.” (Waroma 7:19) Ijapokuwa hakuna mtu anayeweza kujiweka huru kutokana na dhambi, bado kuna tumaini.

Yesu aliwahakikishia wanafunzi wake hivi: “Mwana akiwaweka nyinyi huru, mtakuwa huru kikweli.” (Yohana 8:36) Utimizo wa ahadi hiyo utamaanisha uhuru wa kweli kutokana na ule utumwa hatari zaidi. Ili tuelewe namna ambavyo twaweza kuwekwa huru kutokana na utumwa huo, lazima kwanza tuone jinsi tulivyoingia utumwani.

Biblia inaeleza kwamba Mungu alimuumba mwanadamu akiwa na hiari, bila mwelekeo wa kutenda dhambi. Lakini mwana mmoja wa kiroho wa Mungu, asiyeonekana, alitaka kuwatawala wanadamu, bila kujali mateso ambayo yangewapata. Ili kufikia lengo hilo, malaika huyo mwasi, ambaye baadaye aliitwa Shetani Ibilisi, aliwafanya wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa, wamwache Mungu. Adamu alipoasi kimakusudi maagizo ya Mungu yaliyokuwa wazi, akawa mtendaji wa dhambi na akapitisha kutokamilika na kifo kwa wazao wake wote. (Waroma 5:12) Hatimaye, Shetani akawa “mtawala wa ulimwengu,” na ‘dhambi imewatawala wanadamu ikiwa mfalme pamoja na kifo.’—Yohana 12:31; Waroma 5:21; Ufunuo 12:9.

Twawezaje kuwekwa huru? Tunapokuwa wanafunzi wa Yesu, twaweza kufaidika kutokana na kifo cha Kristo cha kidhabihu, ambacho kina uwezo wa “kumfanya kuwa si kitu yule aliye na uwezo wa kusababisha kifo, yaani, Ibilisi” na “kuwaweka huru wale wote ambao kwa hofu ya kifo walitiishwa kwenye utumwa maisha zao zote.” (Waebrania 2:14, 15) Hebu wazia hilo—kuwekwa huru kutokana na dhambi na kifo! Je, uhuru wa aina hiyo haukufurahishi?

Lakini, vipi juu ya utumwa ambao tulizungumzia hapo mwanzoni? Je, kuna wakati ambapo watu hawatatumikishwa tena kwa nguvu?

Msingi Hakika wa Kuwa na Tumaini

Bila shaka, twaweza kuwa na uhakika kwamba utumwa huo wenye kuchukiza utakomeshwa. Kwa nini? Hebu fikiria jambo hili: Yehova Mungu alihusika moja kwa moja katika ukombozi mkubwa zaidi wa watumwa katika historia yote. Huenda ikawa unafahamu simulizi hilo.

Waisraeli walitumikishwa na Wamisri, wakalazimishwa kufanya kazi ngumu na kutendewa kwa ukatili. Wakamlilia Mungu awasaidie, naye, akisukumwa na huruma zake nyingi, akawasikia na kutenda. Yehova akawatumia Musa na Aroni kama wasemaji wake ili kumwamuru Farao Mmisri awaachilie huru Waisraeli. Mfalme huyo mwenye kiburi akakataa katakata, hata baada ya Yehova kuleta mapigo ambayo yaliharibu nchi hiyo. Hatimaye, Mungu akamnyenyekeza Farao. Waisraeli wakaachiliwa huru!—Kutoka 12:29-32.

Ni simulizi lenye kusisimua, sivyo? Hata hivyo, huenda ukajiuliza kwa nini Mungu hajafanya tendo kama hilo katika nyakati zetu. Mbona hajaingilia shughuli za wanadamu na kukomesha utumwa? Kumbuka, Shetani ndiye “mtawala wa ulimwengu” wala si Yehova. Kwa sababu ya masuala yaliyozushwa huko Edeni, Yehova amemruhusu Adui huyo mwovu kutawala kwa kipindi kifupi. Utumwa, uonevu, na ukatili ni ishara za utawala wa Shetani. Kwa sababu ya Shetani, utawala wa wanadamu umeshindwa kabisa. Biblia inaeleza vizuri utawala huo inaposema hivi: “Mtu mmoja anayo mamlaka juu ya mwenziwe kwa hasara yake.”—Mhubiri 8:9, Chapa ya 1989.

Lakini kwa muda gani? Biblia inaeleza kwamba tunaishi katika “siku za mwisho,” wakati ambapo ubinafsi na pupa zingeongezeka sana. (2 Timotheo 3:1, 2) Hiyo inamaanisha kwamba hivi karibuni Ufalme wa Mungu, ambao Yesu alitufundisha tusali juu yake, utaanzisha jamii yenye uadilifu na utumwa utapigwa marufuku. (Mathayo 6:9, 10) Yesu Kristo, Mfalme aliyewekwa rasmi na Mungu, atachukua hatua ya kukomesha utumwa wa aina zote hadi adui wa mwisho, kifo, atakapofanywa kuwa si kitu.—1 Wakorintho 15:25, 26.

Siku hiyo itakapofika, wanadamu waaminifu watatambua kwamba ule ukombozi ambao watu wa Mungu walipata kutoka utumwani huko Misri ulikuwa wonyesho mdogo tu wa ukombozi huo mkubwa zaidi. Naam, muda si muda, “viumbe vyenyewe pia vitawekwa huru kutoka katika utumwa wa uharibifu.” Hatimaye, kila mtu ataweza kufurahia kikamili “uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.”—Waroma 8:21.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Katika karne ya kwanza, ulafi ulikuwa jambo la kawaida kwenye karamu za Waroma. Hivyo, Wakristo walionywa wasiruhusu chakula au kitu kingine chochote kama hicho kiwafanye kuwa watumwa.—Waroma 6:16; 1 Wakorintho 6:12, 13; Tito 2:3.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Inakadiriwa kwamba watu milioni sita ni watumwa wa mchezo wa kamari huko Marekani peke yake

[Picha katika ukurasa wa 7]

Mamia ya mamilioni ya watu ni watumwa wa dawa za kulevya, kileo, na tumbaku

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Kama vile Ricardo, maelfu ya watu wamesaidiwa na Mungu kuacha mazoea mabaya

[Picha katika ukurasa wa 10]

Kama vile Waisraeli wa kale walivyokombolewa kutoka utumwani, hivi karibuni waabudu wa kweli wa Mungu watapata ukombozi mkubwa zaidi